Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

NYONGEZA

Maneno “Nafsi” na “Roho” Yanamaanisha Nini Hasa?

Maneno “Nafsi” na “Roho” Yanamaanisha Nini Hasa?

MANENO “nafsi” na “roho” yanamaanisha nini kwako? Wengi huamini kwamba maneno hayo yanamaanisha kitu fulani kisichoonekana na kisichoweza kufa kilicho ndani yetu. Wao hufikiri kwamba mtu anapokufa kitu hicho kisichoonekana hutoka ndani ya mwili wa binadamu na kuendelea kuishi. Kwa kuwa fundisho hilo limeenea sana, watu wengi hushangaa wanapogundua kwamba si fundisho la Biblia. Basi, Neno la Mungu linasema nafsi na roho ni nini?

FUNDISHO LA BIBLIA KUHUSU “NAFSI”

Kwanza, tuzungumzie nafsi. Huenda unakumbuka kwamba mwanzoni Biblia iliandikwa katika Kiebrania na Kigiriki. Waandishi wa Biblia walitumia neno neʹphesh la Kiebrania au psy·kheʹ la Kigiriki walipoandika kuhusu nafsi. Maneno hayo mawili yanapatikana zaidi ya mara 800 katika Maandiko, na Tafsiri ya Ulimwengu Mpya huyatafsiri yote kuwa “nafsi.” Unapochunguza jinsi neno “nafsi” linavyotumiwa katika Biblia, utaona kwa wazi kwamba neno hilo humaanisha (1) watu, (2) wanyama, au (3) uhai wa mtu au mnyama. Na tuzungumzie baadhi ya Maandiko yanayoonyesha mambo hayo matatu.

Watu. “Katika siku za Noa . . . watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Kwa wazi neno “nafsi” katika andiko hilo linamaanisha watu, yaani, Noa, mkewe, wanawe watatu, na wake zao. Andiko la Kutoka 16:16 lina maagizo kwa Waisraeli kuhusu kuokota mana. Waliambiwa: “Okoteni kiasi chake . . . kulingana na hesabu ya nafsi ambazo kila mmoja wenu anazo katika hema lake.” Kwa hiyo, kiasi cha mana kilichookotwa kilitegemea kiasi cha watu katika kila familia. Maandiko yafuatayo ya Biblia yanaonyesha matumizi ya neno “nafsi” kumaanisha watu, Mwanzo 46:18; Yoshua 11:11; Matendo 27:37; na Waroma 13:1.

Wanyama. Tunasoma hivi katika masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji: “Mungu akaendelea kusema: ‘Maji na yajawe na nafsi hai na viumbe vinavyoruka viruke juu ya dunia kwenye uso wa anga la mbingu.’ Mungu akaendelea kusema: ‘Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake, mnyama wa kufugwa na mnyama anayetambaa na mnyama-mwitu wa dunia kulingana na aina yake.’ Ikawa hivyo.” (Mwanzo 1:20, 24) Katika andiko hilo, samaki, wanyama wa kufugwa, na wanyama-mwitu wote wanaitwa kwa neno lilelile—“nafsi.” Ndege na wanyama wengine wanaitwa nafsi kwenye Mwanzo 9:10; Mambo ya Walawi 11:46; na Hesabu 31:28.

Uhai wa mtu. Wakati mwingine neno “nafsi” humaanisha uhai wa mtu. Yehova alimwambia Musa: “Watu wote waliokuwa wakiiwinda nafsi yako wamekufa.” (Kutoka 4:19) Adui za Musa walikuwa wakiwinda nini? Walitaka kumuua Musa. Raheli alipokuwa akimzaa mwanawe Benyamini, ‘nafsi yake ilitoka (kwa sababu alikufa).’ (Mwanzo 35:16-19) Wakati huo Raheli alipoteza uhai wake. Fikiria pia maneno ya Yesu: “Mimi ndiye mchungaji mwema; mchungaji mwema huitoa nafsi yake kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:11) Yesu alitoa nafsi au uhai wake kwa ajili ya wanadamu. Katika maandiko hayo ya Biblia, ni wazi kwamba neno “nafsi” linamaanisha mtu. Utapata mifano mingine yenye maana hiyo ya neno “nafsi” kwenye 1 Wafalme 17:17-23; Mathayo 10:39; Yohana 15:13; na Matendo 20:10.

Unapoendelea kujifunza Neno la Mungu utaona kwamba hakuna popote katika Biblia ambapo neno “nafsi” linahusianishwa na “kutoweza kufa” au “kuishi milele.” Badala yake, Maandiko yanasema kwamba nafsi inaweza kufa. (Ezekieli 18:4, 20) Kwa hiyo, katika Biblia mtu ambaye amekufa huitwa ‘nafsi iliyokufa.’—Mambo ya Walawi 21:11.

MAANA YA “ROHO”

Hebu tuzungumzie jinsi Biblia inavyotumia neno “roho.” Watu fulani hufikiri kwamba “roho” ni neno lingine linalomaanisha “nafsi.” Lakini, si kweli. Biblia inaonyesha wazi kwamba “roho” na “nafsi” ni vitu viwili tofauti. Vinatofautianaje?

Waandishi wa Biblia walitumia neno la Kiebrania ruʹach au neno la Kigiriki, pneuʹma waliporejelea “roho.” Maandiko yenyewe yanaonyesha maana ya maneno hayo. Kwa mfano, andiko la Zaburi 104:29 linasema: “[Yehova] ukiiondoa roho [ruʹach] yao, wanakata pumzi, na kurudi katika mavumbi yao.” Andiko la Yakobo 2:26 linasema kwamba “mwili bila roho [pneuʹma] umekufa.” Katika andiko hilo “roho” inamaanisha kile ambacho huupa mwili uhai. Bila roho, mwili umekufa. Kwa hiyo, katika Biblia neno ruʹach halitafsiriwi tu “roho” bali pia “nguvu” au kani ya uhai. Kwa mfano, Mungu alisema hivi kuhusu Mafuriko ya siku ya Noa: “Ninaleta gharika ya maji duniani ili kuharibu kutoka chini ya mbingu wote wenye mwili walio na nguvu [ruʹach] za uhai ndani yao.” (Mwanzo 6:17; 7:15, 22) Hivyo, “roho” inarejelea nguvu isiyoonekana, inayotendesha viumbe vyote vilivyo hai.

Nafsi na roho hutofautiana. Mwili unahitaji roho kama vile redio inavyohitaji umeme ili kufanya kazi. Kwa mfano, unapotia betri katika redio na kuiwasha, nguvu zilizo katika betri huiwezesha redio kufanya kazi. Hata hivyo, redio haiwezi kufanya kazi bila betri. Hali kadhalika, redio ambayo imeondolewa kwenye umeme haiwezi kufanya kazi. Vivyo hivyo, roho ni nguvu ambayo hutendesha mwili wetu. Kama umeme, roho haiwezi kuhisi wala kufikiri. Ni nguvu isiyo na utu. Lakini bila roho au kani ya uhai, “tunakata pumzi na kurudi kwenye udongo,” kama mtunga-zaburi alivyosema.

Andiko la Mhubiri 12:7 linasema hivi linapozungumzia kifo cha mwanadamu: “Mavumbi [mwili wake] huirudia nchi kama yalivyokuwa, nayo roho yenyewe humrudia Mungu wa kweli aliyeitoa.” Roho au kani ya uhai inapoondoka mwilini, mwili hufa na kurudi ulipotoka, yaani, kwenye udongo. Vivyo hivyo, nguvu ya uhai hurudi ilipotoka, yaani, kwa Mungu. (Ayubu 34:14, 15; Zaburi 36:9) Hiyo haimaanishi kwamba nguvu ya uhai huenda mbinguni kihalisi. Badala yake, inamaanisha kwamba mtu akifa, tumaini lolote la kuishi tena linamtegemea Yehova Mungu. Ni kana kwamba uhai wake uko mikononi mwa Mungu. Ni kupitia nguvu za Mungu tu ndipo roho au nguvu ya uhai inaweza kurudishwa ili mtu aweze kuishi tena.

Inafariji kama nini kujua kwamba hivyo ndivyo Mungu atakavyofanya kwa wote wanaopumzika ndani ya “makaburi ya ukumbusho!” (Yohana 5:28, 29) Wakati wa ufufuo, Yehova atamfanyizia mwili mpya yule anayelala katika kifo na kuuhuisha kwa kutia roho, au nguvu ya uhai ndani yake. Itakuwa siku ya shangwe sana.

Ikiwa ungependa kupata habari zaidi kuhusu maneno “nafsi” na “roho” kama yanavyotumiwa katika Biblia, ona broshua Ni Nini Hutupata Tunapokufa? na ukurasa wa 221-226 katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko, Chapa ya 2004, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.