Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hatua Saba za Kufaidika na Usomaji wa Biblia

Hatua Saba za Kufaidika na Usomaji wa Biblia

Hatua Saba za Kufaidika na Usomaji wa Biblia

“Biblia ndicho kitabu ambacho kimeuzwa sana katika historia yote, na bado kila mwaka kinaendelea kuuzwa kwa wingi kuliko vitabu vingine.”—TIME MAGAZINE.

“Nyakati nyingine mimi husoma Biblia, lakini nakiona kuwa kitabu chenye kuchosha sana.”—KEITH, MWANAMUZIKI MASHUHURI KUTOKA UINGEREZA.

INASHANGAZA kwamba watu wengi wana Biblia, lakini hawafaidiki sana kwa kuisoma. Hata hivyo, wengine huthamini sana mambo wanayosoma katika Biblia. Kwa mfano, mwanamke mmoja anayeitwa Nancy anasema hivi: “Tangu nianze kusoma na kutafakari Biblia mapema kila asubuhi, ninahisi kwamba niko tayari kukabiliana na matatizo yoyote yatakayotokea katika siku. Kati ya mambo yote ambayo nimejaribu kufanya kwa miaka 35 iliyopita, zoea hilo ndilo limenisaidia sana kushinda tatizo la kushuka moyo.”

Hata kama hujawahi kusoma Biblia, je, huvutiwi kuona kwamba imewasaidia watu fulani? Ikiwa tayari wewe husoma Biblia, je, ungependa kufaidika zaidi kutokana na usomaji wako? Ikiwa ndivyo, jaribu kufuata hatua saba zilizoelezwa katika habari hii.

Hatua ya 1—Soma ukiwa na nia nzuri

▪ Unaweza kusoma Biblia kama kitabu kizuri au kwa sababu umeamriwa kufanya hivyo au ili tu kupata mwongozo katika ulimwengu huu wenye matatizo. Hata hivyo, utafaidika zaidi ikiwa lengo lako ni kujua ukweli kumhusu Mungu. Kwa kuongezea, utapata baraka nyingi ikiwa nia yako ni kujifunza jinsi ambavyo ujumbe wa Biblia unaweza kukusaidia maishani.

Maandiko yanakazia umuhimu wa kusoma Biblia ukiwa na nia nzuri kwa kulinganisha Biblia na kioo: “Ikiwa yeyote ni msikiaji wa neno, na si mtendaji, huyo ni kama mtu anayeutazama uso wake wa asili katika kioo. Kwa maana yeye hujitazama, naye huenda zake na kusahau mara moja yeye ni mtu wa namna gani. Lakini yeye anayechunguza ndani ya sheria kamilifu iliyo ya uhuru na ambaye hudumu katika hiyo, mtu huyo, kwa sababu amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.”—Yakobo 1:23-25.

Mtu anayetajwa katika mfano huu huutazama uso wake katika kioo lakini harekebishi jinsi anavyoonekana. Labda alijitazama haraka, au huenda hataki kufanya mabadiliko. Vivyo hivyo, hatutafaidika sana ikiwa tutasoma Biblia kijuujuu tu au hatutafuata yale tunayosoma. Tofauti na hilo, tunaweza kupata furaha ya kweli ikiwa tutaichunguza Biblia kwa undani tukiwa na lengo la kuwa “mtendaji,” kwa kuacha mawazo ya Mungu yafinyange mawazo na matendo yetu.

Hatua ya 2—Chagua tafsiri inayoeleweka kwa urahisi

▪ Huenda kukawa na tafsiri nyingi katika lugha yako. Ingawa tafsiri yoyote ya Neno la Mungu itakufaidi, nyingine hutumia lugha ya kale au lugha ngumu ambayo ni wasomi tu wanayoweza kuielewa. (Matendo 4:13) Tafsiri nyingine hata hubadili ujumbe safi wa Biblia kwa sababu ya mapokeo. Kwa mfano, kama tulivyoona katika habari iliyotajwa mwanzoni mwa gazeti hili, tafsiri nyingine zimeondoa jina la Mungu, Yehova, na badala yake kuweka majina ya cheo kama vile “Mungu” au “Bwana.” Hivyo, unapochagua tafsiri, tafuta iliyo sahihi, rahisi kueleweka, na itayokuchochea kuendelea kuisoma.

Mamilioni ya wasomaji ulimwenguni pote wamegundua kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni sahihi, rahisi kueleweka, na inakuchochea kusoma. * Fikiria kisa cha mwanamume mmoja mzee huko Bulgaria. Alipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova, alipewa Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Baada ya mkutano, alisema hivi: “Nimesoma Biblia kwa miaka mingi, lakini sijawahi kuona tafsiri inayoeleweka kwa urahisi na inayonigusa moyo sana.”

Hatua ya 3—Sali

▪ Unaweza kuielewa Biblia vizuri zaidi kwa kumwomba Mtungaji wake akusaidie, kama vile mtunga zaburi alivyofanya aliposema hivi: “Ufunue macho yangu, ili nipate kutazama mambo ya ajabu kutoka katika sheria yako.” (Zaburi 119:18) Sali kwa Mungu kila mara unaposoma Maandiko, ukimwomba akusaidie kuelewa Neno lake. Pia unaweza kumshukuru kwa kutupa Biblia, kwa kuwa bila hiyo hatuwezi kumjua Mungu.—Zaburi 119:62.

Je, Mungu husikia sala hizo za kumwomba msaada? Fikiria yale yaliyotukia huko Uruguai kwa dada wawili. Hawakuelewa kile ambacho Biblia inasema kwenye Danieli 2:44 na wakamwomba Mungu atume mtu wa kuwasaidia kuelewa andiko hilo. Huku Biblia zao zikiwa bado zimefunguliwa, Mashahidi wawili wa Yehova waliwatembelea na kusoma mstari uleule ambao wasichana hao walikuwa wamesali juu yake. Mashahidi hao waliwaambia kwamba mstari huo unaonyesha jinsi ambavyo serikali za wanadamu zitaondolewa na mahali pake pachukuliwe na Ufalme wa Mungu. * Wasichana hao walisadiki kwamba Mungu alikuwa amejibu sala yao za kuomba msaada.

Hatua ya 4—Isome kila siku

▪ Mchapishaji mmoja alisema kwamba baada ya yale mashambulizi ya kigaidi huko Marekani Septemba 11, 2001 (11/09/2001), “Biblia nyingi sana zilinunuliwa.” Watu wengi husoma Neno la Mungu wakati wa taabu peke yake. Hata hivyo, Biblia inatutia moyo tuisome kila siku. Inasema hivi: “Kitabu hiki cha sheria kisiondoke katika kinywa chako, nawe ukisome kwa sauti ya chini mchana na usiku, upate kuangalia kufanya kulingana na yote ambayo yameandikwa ndani yake; kwa maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha utatenda kwa hekima.”—Yoshua 1:8.

Umuhimu wa kusoma Biblia kwa ukawaida unaweza kulinganishwa na mtu ambaye alipatwa na mshtuko wa moyo na sasa ameamua kula vyakula vyenye lishe. Je, vyakula hivyo vitamsaidia ikiwa atavikula wakati tu anahisi maumivu makali kifuani? Hapana. Ili afaidike zaidi, lazima ale vyakula vyenye lishe kwa ukawaida. Vivyo hivyo, kusoma Biblia kila siku kutakusaidia ‘kuifanikisha njia yako.’

Hatua ya 5—Fuata utaratibu mbalimbali

▪ Kusoma Biblia kuanzia Mwanzo hadi Ufunuo kunafaa, lakini huenda kutumia njia nyingine kukaburudisha. Yafuatayo ni madokezo machache.

Soma kuhusu mtu fulani hususa. Soma sura au vitabu vyote vinavyozungumzia mwabudu fulani wa Mungu, kwa mfano:

Yosefu: Mwanzo 37-50.

Ruthu: Ruthu 1-3.

Yesu: Mathayo 1-28; Marko 1-16; Luka 1-24; Yohana 1-21. *

Soma habari fulani hususa. Soma maandiko yanayohusiana na habari hiyo. Kwa mfano, fanya utafiti kuhusu sala, kisha usome mashauri ya Biblia kuhusu sala na pia baadhi ya sala nyingi zinazotajwa katika Biblia. *

Soma kwa sauti. Unaweza kufaidika sana ukisoma Biblia kwa sauti. (Ufunuo 1:3) Hata mnaweza kusoma kwa sauti mkiwa familia, kila mmoja akigawiwa kusoma fungu fulani au sehemu za watu mbalimbali wanaotajwa katika simulizi fulani. Wengine hufurahia kusikiliza usomaji wa Biblia uliorekodiwa. Mwanamke mmoja alisema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kwangu kuanza kusoma Biblia, kwa hiyo nilianza kwa kusikiliza usomaji wa Biblia uliorekodiwa. Sasa ninaona kwamba Biblia ni kitabu chenye kusisimua sana kuliko kitabu cha hadithi.”

Hatua ya 6—Tafakari

▪ Hekaheka na vikengeusha-fikira vya maisha ya kisasa humzuia mtu kutafakari. Hata hivyo, kama vile tu tunavyohitaji kumeng’enya chakula ili tupate lishe, lazima tutafakari yale tunayosoma katika Biblia ili tufaidike. Tunafanya hivyo kwa kurudia akilini yale ambayo tumesoma na kwa kujiuliza maswali kama vile: ‘Nimejifunza nini kumhusu Yehova Mungu? Ninaweza kutumia habari hii jinsi gani maishani mwangu? Ninaweza kuitumia kwa njia gani kuwasaidia wengine?’

Kutafakari hufanya ujumbe wa Biblia uguse mioyo yetu na kuongeza shangwe ya kusoma Neno la Mungu. Zaburi 119:97 inasema: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.” Kutafakari kulimsaidia mtunga zaburi ahangaikie Maandiko mchana kutwa. Na hilo lilifanya apende sana mambo aliyojifunza.

Hatua ya 7—Tafuta msaada ili uielewe

▪ Mungu hatazamii tuelewe Neno lake bila msaada wowote. Hata Biblia yenyewe inasema kwamba ina “mambo fulani yaliyo magumu kuelewa.” (2 Petro 3:16) Kitabu cha Matendo kinasimulia kuhusu ofisa Mwethiopia ambaye hakuelewa fungu fulani alilosoma katika Biblia. Mungu alimtuma mtumishi Wake ili amsaidie, na matokeo yakawa kwamba Mwethiopia huyo “aliendelea kwenda zake akishangilia.”—Matendo 8:26-39.

Wewe pia unaweza kufaidika zaidi na usomaji wa Biblia kwa kutafuta msaada ili uelewe unachosoma. Wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu, au waandikie barua ukitumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 4 wa gazeti hili ili ujifunze Biblia nyumbani bila malipo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inachapishwa na Mashahidi wa Yehova, na imechapishwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 83 na pia inapatikana katika Tovuti ya www.watchtower.org katika lugha 11.

^ fu. 15 Kwa habari zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na mambo ambayo utatimiza, ona sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 24 Ikiwa ni mara yako ya kwanza kusoma Biblia, anza kwa kusoma kitabu cha Marko chenye matukio yenye kusisimua kuhusu huduma ya Yesu.

^ fu. 25 Kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kimewasaidia wengi wajifunze Biblia kwa kutegemea vichwa hususa. Kwa mfano, sura ya 17, inazungumzia kile ambacho Maandiko yanafundisha kuhusu sala.