Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu Jinsi ya Kumfuata Kristo

Kuhusu Jinsi ya Kumfuata Kristo

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu Jinsi ya Kumfuata Kristo

Mara nyingi Yesu aliwaambia hivi watu waliomwamini: “Uwe mfuasi wangu.” (Mathayo 9:9; 19:21) Mtu anahitaji kufanya nini ili awe mfuasi wa Yesu, yaani, Mkristo? Chunguza majibu ya maswali matatu ya maana.

Unapaswa kuwatendea wengine jinsi gani?

▪ Mwanafunzi wa Yesu anapaswa kufuata maagizo yanayohusu jinsi ya kuwatendea wengine. Kwa mfano, Yesu alisema: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” Namna gani mtu akikukosea? Yesu alisema: “Uwe tayari kusuluhisha mambo upesi pamoja na mtu anayekushtaki mahakamani.” Pia, aliwaambia wafuasi wake hivi: “Ikiwa hamtawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.”—Mathayo 5:25; 6:15; 7:12.

Yesu aliwashauri hivi watu waliofunga ndoa: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” Mkristo wa kweli anaruhusu mafundisho ya Yesu yaongoze akili na moyo wake.—Mathayo 5:27, 28.

Wakristo wa kweli wanajidhabihu ili wawasaidie wengine. Yesu alijidhabihu. Kwa mfano, walipokuwa kwenye safari yenye kuchosha ya kuhubiri, Yesu na mitume wake hawakuwa hata na wakati wa kula chakula. Hivyo, Yesu akawapeleka kwa mashua mahali pasipo na watu ili wapumzike. Lakini watu wakasikia kuhusu mahali alipokuwa anaenda, wakakimbia na kufika mbele yake. Simulizi hilo la Biblia linasema: “Aliposhuka, akaona umati mkubwa, lakini akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:30-34) Unaweza kumwiga Yesu kwa kufanya mambo ambayo Mungu anataka ufanye, hata ingawa huenda ukakabiliana na hali ngumu.

Kwa nini unapaswa kuwahubiria wengine habari njema?

▪ Yesu aliwafundisha wafuasi wake kuwahubiria wengine habari njema. Aliwaambia hivi mitume: “Mnapoenda, hubirini, mkisema, ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’” (Mathayo 10:7) Wafuasi wa Yesu wana ujumbe wenye thamani sana. Yesu alisali hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli.”—Yohana 17:3.

Yesu alitabiri kuhusu kazi ambayo mamilioni ya wafuasi wake wangeshiriki. Alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mathayo 24:14) Ikiwa umejifunza kuhusu Ufalme wa Mungu na unaamini yale ambayo Biblia inasema, bila shaka, utafurahi kuwaambia wengine mambo unayojua. Wafuasi wengi wa Yesu wanaanza kwa kuwaambia watu wao wa ukoo kuhusu Ufalme wa Mungu.—Yohana 1:40, 41.

Kwa nini unapaswa kubatizwa?

▪ Yesu alipobatizwa katika mto Yordani, inaelekea alisema hivi katika sala: ‘Nimekuja ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.’ (Waebrania 10:7) Ikiwa unataka kufanya mapenzi ya Mungu, wewe pia unapaswa kubatizwa. Yesu aliamuru hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza.”—Mathayo 28:19.

Ni majukumu na faida gani ambazo mtu anapata anapobatizwa? Wafuasi wa Yesu waliobatizwa wanamtumikia Mungu kwa nafsi yao yote. Yesu alitaja Sheria ya Mungu inayosema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote.” (Mathayo 22:37) Pia alisema hivi: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe.” (Mathayo 16:24) Ubatizo unaonyesha kwamba mtu ameamua kujikana mwenyewe na kuwa mali ya Mungu. Watu walio katika uhusiano huo wa pekee wanaweza kumwomba Mungu awape dhamiri safi.—1 Petro 3:21.

Ili upate habari zaidi, ona sura ya 18 ya kitabu hiki kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.