Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ni Nani kwa Kweli Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara? ”

“Ni Nani kwa Kweli Mtumwa Mwaminifu na Mwenye Busara? ”

“Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani?”—MT. 24:45.

1, 2. Yesu anatulisha leo kupitia nani, na kwa nini ni muhimu tutambue njia hiyo ya ulishaji?

“AKINA ndugu, siwezi kuhesabu ni mara ngapi nimepokea kutoka kwenu makala zenye habari ninazohitaji kwa wakati unaofaa.” Maneno hayo ya uthamini yalisemwa na dada mmoja katika barua aliyowaandikia ndugu wanaotumikia katika makao yetu makuu ya ulimwenguni pote. Je, umewahi kuhisi hivyo? Wengi wetu tumehisi hivyo. Je, hilo litushangaze? Hapana.

2 Chakula cha kiroho tunachopokea kwa wakati unaofaa ni uthibitisho wa kwamba Yesu, akiwa Kichwa cha kutaniko, anatulisha kama alivyoahidi. Anatulisha kupitia nani? Alipokuwa akitaja ishara ya kuwapo kwake, Yesu alisema kwamba angemtumia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kuwapa watumishi wake wa nyumbani ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ * (Soma Mathayo 24:45-47.) Yesu anamtumia mtumwa huyo mwaminifu kuwalisha wafuasi wake wa kweli katika siku hizi za mwisho. Ni muhimu kwetu kumtambua mtumwa huyo mwaminifu. Afya yetu ya kiroho na uhusiano wetu pamoja na Mungu unategemea njia hiyo ya ulishaji.—Mt. 4:4; Yoh. 17:3.

3. Machapisho yetu yamesema nini kuhusu mfano wa yule mtumwa mwaminifu?

3 Basi, tueleweje mfano wa Yesu kuhusu mtumwa mwaminifu? Zamani, machapisho yetu yalisema yafuatayo. Katika Pentekoste ya 33 W.K., Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani. Mtumwa huyo anafananisha Wakristo wote watiwa-mafuta wakiwa kikundi hapa duniani wakati wowote ule tangu siku hiyo. Watumishi wa nyumbani wanarejelea watiwa-mafuta hao wakiwa mtu mmoja-mmoja. Katika mwaka wa 1919, Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu “juu ya mali zake zote,” yaani, masilahi yake yote ya Ufalme duniani. Hata hivyo, baada ya kuchunguza zaidi kwa makini, kusali na kutafakari kuhusu suala hilo, inaonekana kwamba uelewaji wetu wa maneno ya Yesu kuhusu mtumwa mwaminifu na mwenye busara unahitaji  kurekebishwa. (Met. 4:18) Acheni tuchunguze mfano huo na kuona jinsi unavyotuhusu, iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au la kuishi duniani.

MFANO HUO UNATIMIZWA WAKATI GANI?

4-6. Kwa nini tunaweza kufikia mkataa kwamba mfano wa Yesu kuhusu mtumwa mwaminifu ulianza kutimizwa baada tu ya mwaka wa 1914?

4 Muktadha wa mfano wa mtumwa mwaminifu na mwenye busara unaonyesha kwamba ulianza kutimizwa katika siku hizi za mwisho na wala si wakati wa Pentekoste ya 33 W.K. Acheni tuone jinsi Maandiko yanavyotusaidia kufikia mkataa huo.

5 Mfano huo wa mtumwa mwaminifu ni sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 24:3) Sehemu ya kwanza ya unabii huo ulioandikwa katika Mathayo 24:4-22, inatimizwa kwa njia mbili—kwanza, kuanzia mwaka wa 33 W.K. hadi mwaka wa 70 W.K., na pili, inatimizwa kwa njia kubwa zaidi katika siku zetu. Je, hilo linamaanisha kwamba maneno ya Yesu kuhusu mtumwa mwaminifu yangetimizwa pia kwa njia mbili? Hapana.

6 Tukianza na maneno yaliyo katika Mathayo 24:29, Yesu alikazia hasa mambo ambayo yangetukia katika siku zetu. (Soma Mathayo 24:30, 42, 44.) Akizungumzia mambo yatakayotukia wakati wa dhiki kuu, alisema kwamba watu ‘watamwona Mwana wa binadamu akija juu ya mawingu ya mbinguni.’ Kisha, akiwahimiza watu wanaoishi katika siku za mwisho kuendelea kukesha, alisema hivi: “Hamjui ni siku gani Bwana yenu atakuja” na, “Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” * Katika muktadha huo, Yesu alipokuwa akizungumzia mambo ambayo yangetukia katika siku za mwisho, alisimulia mfano kuhusu mtumwa mwaminifu. Hivyo, tunaweza kufikia mkataa kwamba maneno yake kuhusu mtumwa huyo mwaminifu yalianza kutimizwa baada tu ya siku za mwisho kuanza katika mwaka wa 1914. Mkataa huo unapatana na akili. Kwa nini?

7. Ni swali gani muhimu lililozuka majira ya mavuno yalipoanza, na kwa nini?

7 Fikiria swali hili: “Ni nani kwa kweli mtumwa mwaminifu na mwenye busara?” Katika karne ya kwanza, hakukuwa na sababu yoyote ya kuuliza swali hilo. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, mitume walifanya miujiza na hata kutoa zawadi za kimuujiza, jambo lililothibitisha kwamba walitegemezwa na Mungu. (Mdo. 5:12) Hivyo hakukuwa na sababu ya mtu yeyote kuuliza ni nani kwa kweli aliyewekwa rasmi na Kristo kuongoza. Hata hivyo, hali ilikuwa tofauti sana katika mwaka wa 1914. Majira ya mavuno yalianza mwaka huo. Hatimaye wakati ulikuwa umefika wa kutenganisha magugu na ngano. (Mt. 13:36-43) Majira ya mavuno yalipoanza, swali muhimu lilizuka: Kwa kuwa Wakristo wengi wa uwongo walidai kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu, Wakristo watiwa-mafuta, yaani, ngano, wangetambuliwaje? Mfano kuhusu mtumwa mwaminifu ulijibu swali hilo. Wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wangelishwa vizuri kiroho.

MTUMWA MWAMINIFU NA MWENYE BUSARA NI NANI?

8. Kwa nini inafaa mtumwa mwaminifu afanyizwe na Wakristo watiwa-mafuta?

8 Ni lazima mtumwa mwaminifu afanyizwe na Wakristo watiwa-mafuta walio duniani. Wakristo hao huitwa “ukuhani wa kifalme” na wameagizwa “ ‘watangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:9) Basi inafaa kwamba washiriki wa ‘ukuhani huo wa kifalme’ wahusike moja kwa moja katika kuwafundisha kweli waamini wenzao.—Mal. 2:7; Ufu. 12:17.

9. Je, mtumwa mwaminifu anatia ndani Wakristo wote watiwa-mafuta? Eleza.

9 Je, mtumwa mwaminifu anatia ndani watiwa-mafuta wote walio duniani? Hapana.  Ukweli ni kwamba, si watiwa-mafuta wote wanaoshiriki katika kuwaandalia chakula cha kiroho waamini wenzao ulimwenguni pote. Ngano inatia ndani ndugu watiwa-mafuta ambao huenda wanatumikia wakiwa watumishi wa huduma au wazee katika kutaniko lao. Wanafundisha nyumba kwa nyumba na katika kutaniko, na wanaunga mkono kwa ushikamanifu mwongozo kutoka makao makuu. Hata hivyo, hawashiriki katika kuandaa chakula cha kiroho kwa ajili ya undugu wa ulimwengu pote. Pia, kuna dada wanyenyekevu watiwa-mafuta ambao kamwe hawana nia ya kuchukua madaraka ya kufundisha kutanikoni.—1 Kor. 11:3; 14:34.

10. Mtumwa mwaminifu na mwenye busara ni nani?

10 Basi, ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara? Yesu aliweka kielelezo alipowatumia watu wachache kuwalisha wengi, vivyo hivyo, mtumwa huyo ni kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta wanaohusika moja kwa moja katika kutayarisha na kuandaa chakula cha kiroho wakati wa kuwapo kwa Kristo. Katika kipindi chote cha siku za mwisho, ndugu watiwa-mafuta ambao ni yule mtumwa mwaminifu wametumika pamoja katika makao makuu. Katika miaka ya karibuni, mtumwa huyo amehusianishwa kwa ukaribu na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, zingatia kwamba neno “mtumwa” katika mfano wa Yesu liko katika hali ya umoja, kuonyesha kwamba ni jamii ya mtumwa. Maamuzi ya Baraza Linaloongoza hufanywa na washiriki wote kwa pamoja.

WATUMISHI WA NYUMBANI NI NANI?

11, 12. (a) Mtumwa mwaminifu na mwenye busara anapokea migawo gani miwili? (b) Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani wakati gani, naye alichagua nani?

11 Ni muhimu kukumbuka kwamba katika mfano wa Yesu, yule mtumwa mwaminifu na mwenye busara anawekwa rasmi juu ya mambo mawili tofauti. Kwanza, anawekwa rasmi juu ya watumishi wa nyumbani; na pili anawekwa rasmi juu ya mali zote za bwana. Kwa kuwa mfano huo unatimizwa tu katika siku hizi za mwisho, mtumwa huyo angepewa migawo yote miwili baada ya kuanza kwa kipindi cha kuwapo kwa Yesu katika mamlaka ya kifalme mwaka wa 1914.

12 Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya watumishi wake wa nyumbani wakati gani? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kurudi nyuma hadi mwaka wa 1914, majira ya mavuno yalipoanza. Kama tulivyojifunza mwanzoni, wakati huo vikundi vingi vilidai  kumfuata Kristo. Yesu angemchagua na kumweka rasmi mtumwa mwaminifu kutoka katika kikundi gani? Swali hilo lilijibiwa baada ya yeye na Baba yake kuja na kulikagua hekalu, au mpango wa kiroho wa ibada, kuanzia mwaka wa 1914 hadi mwanzoni mwa 1919. * (Mal. 3:1) Walipendezwa na kikundi kidogo cha Wanafunzi washikamanifu wa Biblia walioonyesha kwamba walimpenda Yehova na Neno lake kutoka moyoni. Bila shaka, walihitaji kutakaswa, lakini waliitikia kwa unyenyekevu walipojaribiwa na kusafishwa kwa kipindi kifupi. (Mal. 3:2-4) Wanafunzi hao waaminifu wa Biblia walikuwa Wakristo wa kweli ambao ni ngano. Mwaka wa 1919, katika kipindi cha kuamka kiroho, Yesu alichagua ndugu watiwa-mafuta wenye uwezo kutoka miongoni mwao ili wawe mtumwa mwaminifu na mwenye busara na kuwaweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani.

13. Watumishi wa nyumbani wanatia ndani nani, na kwa nini?

13 Basi ni nani walio watumishi wa nyumbani? Kwa ufupi, ni wale wanaolishwa. Mwanzoni mwa siku za mwisho, watumishi wote wa nyumbani walikuwa watiwa-mafuta. Baadaye, watumishi wa nyumbani wakaja kutia ndani umati mkubwa wa kondoo wengine. Leo, idadi kubwa ya washiriki wa “kundi moja” ambalo liko chini ya uongozi wa Kristo, ni kondoo wengine. (Yoh. 10:16) Vikundi vyote viwili vinafaidika na chakula kilekile cha kiroho kinachotolewa kwa wakati unaofaa na mtumwa mwaminifu. Namna gani washiriki wa Baraza Linaloongoza ambao leo wanafanyiza mtumwa mwaminifu na mwenye busara? Ndugu hao wanahitaji pia kulishwa kiroho. Hivyo, wanatambua kwa unyenyekevu kwamba wakiwa mtu mmoja-mmoja wao pia ni watumishi wa nyumbani kama wafuasi wengine wote wa kweli wa Yesu.

Tuwe na tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani, sisi sote ni watumishi wa nyumbani na tunahitaji chakula kilekile cha kiroho kwa wakati unaofaa

14. (a) Mtumwa mwaminifu amekabidhiwa jukumu gani, nalo linatia ndani nini? (b) Ni onyo gani ambalo Yesu alimpa mtumwa mwaminifu na mwenye busara? (Tazama sanduku lenye kichwa “Mtumwa Huyo Mwovu Akisema . . . ”)

14 Yesu alimkabidhi mtumwa mwaminifu na mwenye busara jukumu zito. Katika nyakati za Biblia, mtumwa aliyeaminika, au msimamizi-nyumba, alisimamia nyumba. (Luka 12:42) Hivyo, mtumwa mwaminifu na mwenye busara amepewa jukumu la kusimamia watu wa nyumba ya imani. Jukumu hilo linatia ndani kusimamia mali halisi, kazi ya kuhubiri, programu za makusanyiko, na kazi ya kutayarisha machapisho ya Biblia yanayotumiwa katika huduma ya shambani, funzo la kibinafsi na la kutaniko. Watumishi  wa nyumbani wanategemea maandalizi yote ya kiroho yanayotayarishwa na jamii ya mtumwa.

ALIWEKWA RASMI JUU YA MALI ZOTE ZA BWANA—WAKATI GANI?

15, 16. Yesu anamweka rasmi mtumwa mwaminifu juu ya mali zake zote wakati gani?

15 Yesu anamweka rasmi juu ya mgawo wa pili, yaani, “juu ya mali zake zote” wakati gani? Yesu alisema hivi: “Mtumwa huyo atakuwa mwenye furaha ikiwa bwana wake atakapofika atamkuta akifanya hivyo! Kwa kweli ninawaambia ninyi, Atamweka juu ya mali zake zote.” (Mt. 24:46, 47) Ona kwamba Yesu anamweka rasmi juu ya mgawo huo wa pili baada ya kufika na kumkuta mtumwa huyo “akifanya hivyo,” yaani, akiandaa kwa uaminifu chakula cha kiroho. Kwa hiyo, wakati fulani ungepita kabla hajapewa mgawo wa pili. Ili kuelewa ni jinsi gani na wakati gani Yesu anapomweka mtumwa juu ya mali zake zote, tunapaswa kujua mambo mawili: anafika wakati gani na mali zake zote zinatia ndani nini.

16 Yesu anafika wakati gani? Muktadha unatoa jibu. Kumbuka kwamba mistari inayotangulia inaposema kwamba Yesu ‘anakuja,’ neno hilo linarejelea wakati anapokuja kutangaza na kutekeleza hukumu mwisho wa mfumo huu. * (Mt. 24:30, 42, 44) Hivyo, katika mfano huo wa mtumwa mwaminifu, Yesu ‘anafika,’ au ‘anakuja’ katika dhiki kuu.

17. Mali za Yesu zinatia ndani nini?

17 ‘Mali zote za Yesu’ zinatia ndani nini? Yesu hakusema kwamba hizo mali “zote” ni mali zake zilizo duniani tu. Kwa kweli, Yesu ana mamlaka kubwa mbinguni. Alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18; Efe. 1:20-23) Mali zake sasa zinatia ndani Ufalme wa Kimasihi, ambao umekuwa wake tangu mwaka wa 1914 na ambao atashiriki pamoja na wafuasi wake watiwa-mafuta.—Ufu. 11:15.

18. Kwa nini Yesu atafurahia kumweka rasmi mtumwa huyo juu ya mali zake zote?

 18 Tunapofikiria mambo hayo yaliyotajwa, tufikie mkataa gani? Yesu atakapokuja kutekeleza hukumu katika dhiki kuu, atapata kwamba mtumwa mwaminifu amekuwa akiwaandalia watumishi wa nyumbani chakula cha kiroho kwa ushikamanifu na kwa wakati unaofaa. Ndipo Yesu atakapofurahia kumweka juu ya mgawo wa pili, yaani, juu ya mali zake zote. Washiriki wa mtumwa mwaminifu watapata pendeleo hilo watakapopokea thawabu yao ya kimbingu ya kutawala pamoja na Kristo.

19. Je, mtumwa mwaminifu anapokea thawabu kubwa zaidi mbinguni kuliko watiwa-mafuta wengine? Eleza.

19 Je, mtumwa mwaminifu anapokea thawabu kubwa zaidi mbinguni kuliko watiwa-mafuta wengine? Hapana. Watu wengine wanaweza kushiriki thawabu ambayo kikundi kidogo kiliahidiwa katika kikao fulani. Kwa mfano, fikiria yale ambayo Yesu aliwaambia mitume wake 11 waaminifu usiku uliotangulia kifo chake. (Soma Luka 22:28-30.) Yesu aliahidi kikundi hicho kidogo cha wanaume kwamba wangepokea thawabu nzuri kwa sababu ya uaminifu wao. Wangeshiriki na Yesu kiti chake cha mamlaka ya kifalme. Lakini miaka mingi baadaye, alisema kwamba wale 144,000 wangeketi wote katika viti vya ufalme na kutawala pamoja naye. (Ufu. 1:1; 3:21) Vivyo hivyo, kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 24:47, aliahidi kwamba kikundi kidogo cha wanaume, yaani, ndugu watiwa-mafuta wa jamii ya mtumwa mwaminifu, watawekwa rasmi juu ya mali zake zote. Ukweli ni kwamba wale 144,000 watashiriki wote katika mamlaka yake kubwa ya kimbingu.—Ufu. 20:4, 6.

Wale 144,000 watashiriki wote katika mamlaka kubwa ya Yesu ya kimbingu (Tazama fungu la 19)

20. Kwa nini Yesu alimweka rasmi mtumwa mwaminifu, na umeazimia kufanya nini?

20 Kupitia mtumwa mwaminifu na mwenye busara, Yesu anafuata kielelezo alichoweka katika karne ya kwanza, yaani, anawatumia watu wachache kuwalisha wengi. Alimweka rasmi mtumwa huyo mwaminifu ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake wa kweli, iwe ni watiwa-mafuta au kondoo wengine, wanapokea kwa ukawaida chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa katika kipindi chote cha siku za mwisho. Acheni tuazimie kuonyesha uthamini wetu kwa kuwaunga mkono kwa ushikamanifu ndugu watiwa-mafuta wa jamii hiyo ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.—Ebr. 13:7, 17.

 

^ fu. 2 Fungu la 2: Pindi moja, Yesu alisimulia mfano kama huo akimrejelea “mtumwa” huyo kuwa “msimamizi-nyumba” na ‘watumishi wa nyumbani’ kuwa “watumishi.”—Luka 12:42-44.

^ fu. 6 Fungu la 6: ‘Kuja’ kwa Kristo (Kigiriki, er′kho·mai) ni tofauti na “kuwapo” kwake (pa·rou·si′a). Kuwapo kwake kusikoonekana kunaanza kabla ya kuja kwake kutekeleza hukumu.

^ fu. 12 Fungu la 12: Tazama makala yenye kichwa “Tazama! Mimi Nipo Pamoja Nanyi Siku Zote,” katika toleo hili, ukurasa wa 10-12, fungu la 5-8.

^ fu. 16 Fungu la 16: Tazama makala yenye kichwa “Tuambie, Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?” katika toleo hili, ukurasa wa 7-8, fungu la 14-18.