Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Tayari Kumtumikia Yehova—Popote Pale

Tayari Kumtumikia Yehova—Popote Pale

Sikuwahi kamwe kuhubiri nikiwa peke yangu. Nilikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba miguu yangu ilitetemeka kila mara nilipoenda kuhubiri. Mambo yalikuwa magumu hata zaidi kwa sababu watu hawakutaka kamwe kusikiliza ujumbe wetu. Baadhi yao walikuwa wakali sana na hata walitaka kunipiga. Mwezi wa kwanza wa utumishi wangu wa upainia, nilitoa kijitabu kimoja tu!—Markus.

HUO ulikuwa mwaka 1949, zaidi ya miaka 60 iliyopita, lakini simulizi langu linaanza miaka mingi mapema. Baba yangu, Hendrik, alikuwa mshona-viatu na mtunza-bustani huko Donderen, kijiji kidogo kilicho kaskazini mwa Drenthe, Uholanzi. Nilizaliwa huko katika mwaka 1927, nikiwa mtoto wa nne katika familia ya watoto saba. Nyumba yetu ilikuwa karibu na barabara ya vumbi katika eneo la mashambani. Jirani zetu walikuwa wakulima, nami nilifurahia sana maisha ya mashambani. Mwaka wa 1947, nikiwa na umri wa miaka 19, nilijifunza kweli kupitia mmoja wa jirani zetu aliyeitwa Theunis Been. Ninakumbuka kwamba mwanzoni sikumpenda Theunis, hata hivyo muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, Theunis akawa Shahidi wa Yehova, na niligundua kwamba alikuwa mwenye urafiki zaidi kuliko zamani. Nilivutiwa na badiliko hilo la utu wake, nami nilimsikiliza aliponiambia kuhusu ahadi ya Mungu ya dunia paradiso. Nilikubali kweli haraka, nasi tukawa marafiki muda wote wa maisha yetu. *

Nilianza kuhubiri mnamo Mei 1948, na mwezi uliofuata, yaani, Juni 20, nilibatizwa katika kusanyiko la wilaya huko Utrecht. Januari 1, 1949, nilianza kufanya upainia, nami nilitumwa katika kutaniko dogo huko Borculo, mashariki mwa Uholanzi. Kwa kuwa nilihitaji kusafiri kilomita 130 ili kufika huko, niliamua kutumia baiskeli yangu. Nilifikiri kwamba  ningesafiri kwa saa 6 hivi, hata hivyo, kwa sababu ya mvua nyingi na upepo mkali, ilinichukua saa 12, ijapokuwa nilipanda gari-moshi ili kumalizia kilomita 90 zilizobaki! Hatimaye, nilifika usiku huo katika nyumba ya familia moja ya Mashahidi, na niliishi pamoja nao nilipokuwa nikifanya upainia katika eneo hilo.

Katika miaka hiyo ya baada ya vita, watu hawakuwa na mali nyingi. Nilikuwa na suti moja na suruali moja ndefu, suti hiyo ilikuwa kubwa sana nayo suruali ilikuwa fupi sana! Kama nilivyotaja mwanzoni, mwezi wa kwanza huko Borculo haukuwa rahisi, hata hivyo Yehova alinibariki na nikapata mafunzo kadhaa ya Biblia. Baada ya miezi tisa, nilitumwa Amsterdam.

KUTOKA MASHAMBANI KWENDA JIJINI

Nililelewa katika eneo la wakulima lakini sasa nilijikuta Amsterdam, jiji kubwa zaidi nchini Uholanzi. Huduma ilikuwa yenye matokeo sana. Mwezi wa kwanza, niliwaachia watu machapisho mengi zaidi ya yale niliyotoa katika kipindi cha miezi tisa iliyopita. Punde si punde, nilikuwa nikiongoza mafunzo ya Biblia yasiyopungua manane. Baada ya kuwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko (sasa anaitwa mratibu wa baraza la wazee), nilipewa mgawo wa kutoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote. Niliogopa sana kufanya hivyo, kwa hiyo nilifarijika sana nilipohamishiwa kutaniko lingine kabla tu ya kutoa hotuba hiyo. Hata hivyo, sikujua kwamba kwa miaka mingi iliyofuata, ningetoa hotuba zaidi ya 5,000!

Markus akihubiri barabarani karibu na Amsterdam mwaka wa 1950

Katika Mei 1950, nilipewa mgawo wa kutumikia huko Haarlem. Kisha nikaalikwa kufanya kazi ya mzunguko. Sikuweza kulala kwa siku tatu. Nilimweleza Robert Winkler, ndugu aliyetumikia katika ofisi ya tawi, kwamba nilihisi sistahili, lakini akasema hivi: “Jaza tu fomu. Utajifunza.” Muda mfupi baadaye, nilizoezwa kwa mwezi mmoja kisha nikaanza kutumikia nikiwa mtumishi (mwangalizi) wa mzunguko. Nilipotembelea kutaniko moja, nilikutana na Janny Taatgen, dada kijana painia mchangamfu mwenye roho ya kujidhabihu na aliyempenda sana Yehova. Tulifunga ndoa mwaka wa 1955. Hata hivyo kabla sijaendelea na simulizi langu, Janny ataeleza jinsi alivyoanza kufanya upainia na jinsi tulivyotumikia pamoja baada ya kufunga ndoa.

KUTUMIKIA TUKIWA WENZI WA NDOA

Janny: Mama yangu alikuwa Shahidi mwaka wa 1945 nilipokuwa na umri wa miaka 11. Mara moja aliona umuhimu wa kujifunza Biblia na watoto wake watatu, lakini baba yangu alipinga kweli, kwa hiyo tulifundishwa na mama wakati ambapo baba hakuwa nyumbani.

Mkutano wa kwanza niliohudhuria ulikuwa kusanyiko la wilaya huko The Hague mwaka wa 1950. Juma moja baadaye, nilihudhuria mkutano wangu wa kwanza katika Jumba la Ufalme huko Assen (Drenthe). Baba yangu alikasirika sana hivi kwamba akanifukuza nyumbani. Hata hivyo, mama aliniambia hivi: “Unajua mahali pa kuishi.” Nilijua alikuwa anarejelea ndugu na dada zangu wa kiroho.  Kwanza, niliishi na familia moja ya Mashahidi waliokuwa jirani zetu, hata hivyo, Baba hakupendezwa na hilo, kwa hiyo nilihamia kutaniko lililo Deven-ter (Overijssel), umbali wa kilomita 95 hivi. Lakini nilikuwa na umri mdogo, kwa hiyo wenye mamlaka walitaka kumchukulia baba hatua kwa sababu ya kunifukuza nyumbani. Kwa sababu hiyo, aliniambia nirudi nyumbani. Ingawa baba yangu hakukubali kweli kamwe, hatimaye aliniruhusu nihudhurie mikutano yote na kuhubiri.

Janny akifanya upainia wa likizo mwaka wa 1952

Muda mfupi baada ya kurudi nyumbani, mama yangu akawa mgonjwa sana na hivyo ilinibidi kufanya kazi zote za nyumbani. Licha ya hilo, niliendelea kufanya maendeleo ya kiroho na nikabatizwa katika mwaka wa 1951 nikiwa na umri wa miaka 17. Katika mwaka wa 1952, baada ya Mama kupona, nilitumikia kwa miezi miwili nikiwa painia wa likizo (msaidizi) pamoja na dada watatu mapainia. Tuliishi katika mashua na tulihubiri katika miji miwili huko Drenthe. Niliwekwa rasmi kuwa painia wa kawaida katika mwaka wa 1953. Mwaka mmoja baadaye mwangalizi wa mzunguko aliyekuwa kijana alitembelea kutaniko letu. Aliitwa Markus. Tulifunga ndoa mwezi wa Mei 1955, kwa kuwa tuliona kwamba tungeweza kumtumikia Yehova vizuri zaidi tukiwa wenzi wa ndoa.—Mhu. 4:9-12.

Siku yetu ya harusi katika mwaka wa 1955

Markus: Baada ya harusi yetu, tulipewa kwanza mgawo wa kuwa mapainia huko Veendam (Gro-ningen). Tuliishi katika chumba kidogo kilichokuwa na upana wa mita 2 kwa mita 3. Hata hivyo, Janny alikifanya chumba hicho kipendeze na kuvutia. Kila usiku, ilitubidi kuondoa meza na viti vyetu viwili vidogo ili tupate nafasi ya kitanda chetu kilichokuwa ukutani.

Baada ya miezi sita, tulipewa mgawo wa kufanya kazi ya kusafiri nchini Ubelgiji. Mwaka wa 1955, kulikuwa na wahubiri wapatao 4,000 tu katika nchi hiyo. Sasa idadi hiyo imeongezeka mara sita! Huko Flanders, kaskazini mwa Ubelgiji, watu huzungumza lugha ileile inayozungumzwa nchini Uholanzi. Hata hivyo, matamshi ya Kibelgiji ni tofauti sana, kwa hiyo mwanzoni tulihitaji kushinda kizuizi hicho cha lugha.

Janny: Kazi ya kusafiri inahitaji roho ya kujidhabihu kikweli. Tulitumia baiskeli zetu kutembelea makutaniko na tuliishi na ndugu na dada. Kwa kuwa hatukuwa na nyumba yetu, wakati wa ziara tulikaa na ndugu na dada mpaka Jumatatu, kisha tulisafiri Jumanne asubuhi ili kutembelea kutaniko linalofuata. Lakini sikuzote tuliona utumishi wetu kuwa baraka kutoka kwa Yehova.

Markus: Mwanzoni hatukumjua ndugu au dada yeyote katika makutaniko tuliyotembelea, hata hivyo walikuwa wakarimu na wenye fadhili sana. (Ebr. 13:2) Kwa miaka mingi, tulitembelea mara kadhaa makutaniko yote yanayozungumza Kiholanzi, nchini Ubelgiji. Hilo limetuletea baraka nyingi. Kwa mfano, tulipata kuwajua karibu ndugu na dada wote katika wilaya ya lugha ya Kiholanzi, nao wamekuwa rafiki zetu sana. Tumewaona mamia ya vijana wakikua kimwili na kiroho kufikia ukomavu na kujiweka  wakfu wenyewe kwa Yehova, wakitanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao. Ni shangwe kama nini kuona wengi wao wakimtumikia Yehova kwa uaminifu katika utumishi wa wakati wote! (3 Yoh. 4) ‘Badilishano hilo la kitia-moyo’ limefanya iwe rahisi kwetu kuendelea kutumikia katika mgawo wetu kwa moyo wote.—Rom. 1:12.

JARIBU KUBWA NA BARAKA KUBWA

Markus: Tangu tulipofunga ndoa, tulitamani sana kuhudhuria Shule ya Gileadi. Kila siku kwa muda wa saa moja, tulijifunza Kiingereza. Hata hivyo, haikuwa rahisi kujifunza lugha hiyo kupitia vitabu tu, kwa hiyo tukaamua kwenda nchini Uingereza wakati wa likizo yetu ili kufanya mazoezi ya lugha hiyo huku tukihubiri. Hatimaye, katika mwaka wa 1963, tulipokea bahasha kutoka makao makuu ya ulimwenguni pote huko Brooklyn. Ilikuwa na barua mbili, moja yangu na nyingine ya Janny. Barua yangu ilikuwa mwaliko wa kuhudhuria darasa maalumu la miezi kumi la Gileadi. Shule hiyo ingekazia hasa kuzoeza ndugu na kuwapa maagizo ya tengenezo. Kwa hiyo, wanafunzi 82 kati ya 100 waliohudhuria darasa hilo walikuwa ndugu.

Janny: Barua niliyopokea siku hiyo, iliniomba nisali na kufikiria ikiwa nitakuwa tayari kubaki Ubelgiji Markus akienda kuhudhuria Gileadi. Kusema kweli, nilivunjika moyo mwanzoni. Ilionekana kwamba jitihada zangu za kufanya maendeleo hazikubarikiwa na Yehova. Hata hivyo, nilijikumbusha lengo la Shule ya Gileadi, yaani, kuwasaidia wale wanaohudhuria kutimiza kazi ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote. Kwa hiyo nilikubali kubaki, nami nikapewa mgawo wa kutumikia nikiwa painia wa pekee katika jiji la Ubelgiji lililoitwa Ghent, pamoja na Anna na Maria Colpaert, mapainia wa pekee wenye uzoefu.

Markus: Kwa kuwa nilihitaji kuboresha Kiingereza changu, nilialikwa kwenda Brooklyn miezi mitano kabla ya shule kuanza. Nilifanya kazi katika idara ya Upakizi na ya Utumishi. Kutumikia katika makao makuu na kusaidia kupakia machapisho ili yasafirishwe mpaka Asia, Ulaya, na Amerika Kusini, kulinisaidia kujua zaidi undugu wetu wa ulimwenguni pote. Ninamkumbuka hasa Ndugu A. H. Macmillan, aliyefanya kazi ya upilgrimu (mwangalizi anayesafiri) katika siku za Ndugu Russell. Kufikia wakati huo alikuwa amezeeka na hivyo hakuweza kusikia vizuri, hata hivyo bado alihudhuria kwa uaminifu mikutano yote ya kutaniko. Jambo hilo lilinitia moyo sana na kunifundisha kwamba hatupaswi kamwe kupuuza ushirika wetu wa Kikristo.—Ebr. 10:24, 25.

Janny: Niliandikiana barua na Markus mara kadhaa kwa juma. Nilimkosa sana Markus, naye pia alinikosa sana! Hata hivyo, Markus alifurahia sana mazoezi aliyokuwa akipata Gileadi, nami nilipata shangwe ya kweli katika huduma yangu. Mark-us aliporudi kutoka Marekani, nilikuwa nikiongoza mafunzo 17 ya Biblia! Bila shaka, haikuwa rahisi kuishi mbali na Markus kwa miezi 15, lakini niliona kwamba Yehova alitubariki kwa sababu ya kujidhabihu kwetu. Siku ambayo Markus alirudi, ndege aliyopanda ilichelewa kwa saa kadhaa, alipofika hatimaye, tulikumbatiana na kulia kwa furaha. Tangu pindi hiyo na kuendelea, mimi na Markus hatujaachana.

TUNASHUKURU KWA KILA PENDELEO LA UTUMISHI

Markus: Niliporudi kutoka Gileadi mnamo Desemba 1964, tulipewa mgawo wa kutumikia Betheli. Hatukujua wakati huo kwamba huo haungekuwa  mgawo wetu wa kudumu. Miezi mitatu tu baadaye, tulipewa mgawo wa kuzungukia wilaya huko Flanders. Aalzen na Els Wiegersma walipotumwa kuwa wamishonari nchini Ubelgiji, walipewa mgawo wa kuzungukia wilaya, nasi tulirudi tena Betheli ambako nilitumikia katika Idara ya Utumishi. Kuanzia 1968 hadi 1980, migawo yetu ilibadilika mara kadhaa, tulitumika Betheli na kufanya kazi ya kusafiri. Mwishowe, kuanzia mwaka wa 1980 mpaka 2005, nilitumikia tena nikiwa mwangalizi wa wilaya.

Ingawa mgawo wetu ulibadilika-badilika mara kadhaa, hatukusahau uhakika wa kwamba tuliweka maisha yetu wakfu ili kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. Tulifurahia sana kila mgawo tuliopewa, tukiwa na hakika kwamba kila badiliko katika utumishi wetu lilikusudiwa kuendeleza masilahi ya Ufalme.

Janny: Nilifurahia hasa pendeleo lenye kusisimua la kwenda pamoja na Markus huko Brooklyn mwaka wa 1977 na Patterson mnamo 1997, wakati Mar-kus alipoenda kupata mazoezi zaidi akiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.

YEHOVA ANAJUA MAHITAJI YETU

Markus: Mwaka wa 1982, Janny alifanyiwa upasuaji, naye akapona. Miaka mitatu baadaye, kutaniko lililo huko Louvain, kwa fadhili lilitupatia chumba kilicho juu ya Jumba la Ufalme. Kwa mara ya kwanza baada ya miaka 30, tukawa na nyumba yetu ndogo. Jumanne, tulipokuwa tukijitayarisha kutembelea kutaniko, mara kadhaa nilishuka na kupanda ngazi 54 zinazotoka katika chumba chetu ili kupeleka chini mizigo yetu! Tulifurahi mnamo mwaka wa 2002 mipango ilipofanywa ili tuishi katika chumba kilicho chini. Nilipofikisha umri wa miaka 78, tulipewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee katika mji wa Lokeren. Tunafurahi kwamba tunaweza kutumikia tukiwa mapainia wa pekee na kuhubiri kila siku.

“Tuna hakika kabisa kwamba jambo la muhimu si wapi tunapotumikia au pendeleo tulilo nalo, bali ni nani tunayemtumikia”

Janny: Mimi na Markus tumeshiriki katika utumishi wa wakati wote kwa jumla ya miaka zaidi ya 120! Tumejionea ukweli wa ahadi ya Yehova ya kwamba ‘hatatuacha hata kidogo,’ na ikiwa tutamtumikia kwa uaminifu, ‘hatutakosa kitu chochote.’—Ebr. 13:5; Kum. 2:7.

Markus: Tulipokuwa vijana, tulijiweka wakfu kwa Yehova. Hatukujitafutia kamwe mambo makuu. Tumekubali kwa hiari mgawo wowote tunaopewa kwa kuwa tuna hakika kabisa kwamba jambo la muhimu si wapi tunapotumikia au pendeleo tulilo nalo, bali ni nani tunayemtumikia.

^ fu. 5 Kadiri miaka ilivyopita, baba, mama, dada yangu mkubwa, pamoja na ndugu zangu wawili wadogo wamekuwa pia Mashahidi.