Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Lichungeni Kundi la Mungu Lililo Chini ya Uangalizi Wenu”

“Lichungeni Kundi la Mungu Lililo Chini ya Uangalizi Wenu”

“Lichungeni Kundi la Mungu Lililo Chini ya Uangalizi Wenu”

“Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda.”—1 PET. 5:2.

1. Ni hali gani ambazo Wakristo walikuwa wakipambana nazo Petro alipoandika barua yake ya kwanza?

MUDA fulani kabla ya Nero kuanza kuwatesa Wakristo huko Roma, mtume Petro aliandika barua yake ya kwanza. Alitaka kuwatia nguvu waamini wenzake. Ibilisi alikuwa ‘akitembea huku na huku,’ akitafuta kuwameza Wakristo. Ili kusimama imara na kumpinga, Wakristo walihitaji ‘kutunza akili zao’ na ‘kujinyenyekeza wenyewe chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu.’ (1 Pet. 5:6, 8) Walihitaji pia kuendelea kuwa na umoja. Hawangepaswa kuendelea “kuumana na kulana,” kwa sababu hilo lingefanya ‘waangamizane.’—Gal. 5:15.

2, 3. Tunapaswa kupigana na nani, na tutachunguza nini katika mfululizo huu?

2 Leo, tunapambana na hali kama hizo. Ibilisi anatafuta nafasi ili atumeze. (Ufu. 12:12) Na hivi karibuni kutakuwa na “dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu.” (Mt. 24:21) Kama vile tu Wakristo wa karne ya kwanza walivyopaswa kuepuka kuzozana wenyewe, tunapaswa pia kuepuka kuzozana. Ili kufanya hivyo, nyakati nyingine tunahitaji msaada kutoka kwa wanaume wazee wenye sifa za kustahili.

3 Acheni tuchunguze jinsi wazee wanavyoweza kuthamini zaidi pendeleo lao la kulichunga ‘kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao.’ (1 Pet. 5:2) Baadaye, tutazungumzia njia inayofaa ya kutimiza kazi ya uchungaji. Katika habari inayofuata, tutachunguza jinsi kutaniko linavyoweza ‘kuwatilia maanani wale wanaofanya kazi kwa bidii na kusimamia’ kundi. (1 The. 5:12) Kuchunguza mambo hayo kutatusaidia kusimama imara ili kumpinga Adui yetu mkuu, tukitambua kwamba yeye ndiye tunayepigana naye mweleka.—Efe. 6:12.

Lichungeni Kundi la Mungu

4, 5. Wanaume wazee wanapaswa kuliona kundi jinsi gani? Toa mfano.

4 Petro aliwatia moyo wanaume wazee kati ya Wakristo wa karne ya kwanza kuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu kundi ambalo aliwakabidhi. (Soma 1 Petro 5:1, 2.) Ingawa alionwa kuwa nguzo katika kutaniko, Petro hakuzungumza na wazee kwa njia ya kuwadharau. Badala yake, aliwaonya kama wazee wenzake. (Gal. 2:9) Kama Petro, Baraza Linaloongoza leo linawatia moyo wazee wa makutaniko wajitahidi kutimiza daraka lao zito la kulichunga kundi la Mungu.

5 Mtume huyo aliandika kwamba wanaume wazee walipaswa ‘kulichunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao.’ Lilikuwa jambo la maana sana kwao kutambua kwamba kundi ni la Yehova na Yesu Kristo. Wazee walipaswa kutoa hesabu kuhusu jinsi walivyotunza kondoo wa Mungu. Tuseme kwamba rafiki yako wa karibu anakuomba umtunzie watoto wake wakati anapoondoka. Je, hungewatunza vizuri na kuwalisha? Ikiwa mtoto mmoja angekuwa mgonjwa, je, hungehakikisha kwamba amepata msaada wowote wa matibabu ambao anahitaji? Vivyo hivyo, wazee katika kutaniko ‘wanalichunga kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Mdo. 20:28) Wanajua kwamba kila kondoo alinunuliwa kwa damu yenye thamani ya Kristo Yesu. Kwa kuwa watatoa hesabu, wazee wanalisha, kulinda, na kulitunza kundi.

6. Wachungaji wa kale walikuwa na daraka gani?

6 Fikiria madaraka ambayo wachungaji halisi walikuwa nayo katika nyakati za Biblia. Walilazimika kuvumilia joto la mchana na baridi ya usiku ili kulichunga kundi. (Mwa. 31:40) Hata walihatarisha maisha yao kwa ajili ya kondoo. Mchungaji kijana Daudi aliokoa kundi lake kutokana na wanyama wa mwitu, kutia ndani simba na dubu. Kuhusiana na kila mmoja wa wanyama hao, Daudi alisema kwamba ‘alizikamata ndevu zake, akampiga, na kumuua.’ (1 Sam. 17:34, 35) Ujasiri kama nini! Kwa kweli, alikaribia sana mataya, yaani, kinywa kilicho wazi cha mnyama huyo. Hata hivyo, hakuogopa kumwokoa kondoo huyo.

7. Wazee wanaweza jinsi gani kumnyakua kondoo kutoka katika kichwa cha mfano cha Shetani?

7 Leo, wazee wanahitaji kuwa macho ili kuona mashambulizi ya Ibilisi ambayo ni kama ya simba. Huenda wakahitaji kutenda kwa ujasiri ili kumnyakua kondoo kutoka katika kinywa cha mfano cha Ibilisi. Kwa kukamata kwa njia ya mfano ndevu za mnyama mwitu huyo, wazee wanaweza kumwokoa kondoo. Wazee wanaweza kuzungumza na ndugu wasiokuwa waangalifu ambao wanashawishiwa na mitego ya Shetani ili kuwasaidia kufikiri. (Soma Yuda 22, 23.) Bila shaka, wazee hawatimizi hilo bila msaada wa Yehova. Wanamshughulikia kwa wororo kondoo aliyeumia, huku wakimfunga vidonda na kumpaka mafuta yenye kutuliza ya Neno la Mungu.

8. Wazee wanawaelekeza kondoo wapi, na jinsi gani?

8 Mchungaji halisi pia aliongoza kondoo kwenye malisho mazuri na mahali penye maji. Vivyo hivyo, wazee wanaelekeza kondoo kwenye kutaniko, wakiwatia moyo kuhudhuria mikutano kwa ukawaida ili kondoo waweze kulishwa vizuri na kupata “chakula chao kwa wakati unaofaa.” (Mt. 24:45) Huenda wazee wakahitaji kutumia wakati wa ziada kuwasaidia wale walio wagonjwa kiroho ili wakubali kulishwa Neno la Mungu. Huenda kondoo aliyepotea anajaribu kurudi kwenye kundi. Badala ya kumwogopesha ndugu yao, wazee wanamweleza kwa wororo kanuni za Kimaandiko na kumwonyesha jinsi anavyoweza kuzitumia katika maisha yake.

9, 10. Wazee wanapaswa kuwatunza jinsi gani wale walio wagonjwa kiroho?

9 Unapokuwa mgonjwa, wewe unapendelea daktari wa aina gani? Je, unapendelea daktari ambaye anatumia muda mfupi kukusikiliza na kisha anafanya haraka kukuandikia dawa ili awe huru kumwona mgonjwa anayefuata? Au badala yake ungependa kumwona daktari ambaye anakusikiliza, anakueleza tatizo lako, na ikiwezekana anapendekeza matibabu yanayofaa?

10 Vivyo hivyo, wazee wanaweza kumsikiliza mtu ambaye ni mgonjwa kiroho na kumsaidia kupona vidonda vyake, na hivyo ‘kumpaka mafuta kwa njia ya mfano katika jina la Yehova.’ (Soma Yakobo 5:14, 15.) Kama mafuta ya zeri ya Gileadi, Neno la Mungu linaweza kumtuliza mgonjwa. (Yer. 8:22; Eze. 34:16) Kanuni za Biblia zinapotumiwa, zinaweza kumsaidia mtu ambaye anayumba-yumba kupata tena usawaziko wa kiroho. Ndiyo, wazee wanasaidia sana mara tu wanaposikia mahangaiko ya kondoo aliye mgonjwa na kusali pamoja naye.

Si kwa Kulazimishwa Bali kwa Kupenda

11. Ni nini kinachowachochea wazee kulichunga kundi la Mungu kwa kupenda?

11 Kisha Petro aliwakumbusha wanaume wazee jinsi kazi ya uchungaji inavyopaswa kufanywa na jinsi ambavyo haipaswi kufanywa. Wazee wanapaswa kulichunga kundi la Mungu, “si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda.” Ni nini kinachowachochea wazee kuwatumikia ndugu zao kwa kupenda? Ni nini kilichomchochea Petro kuchunga na kulisha kondoo wa Yesu? Jambo kuu ni kwamba alimpenda sana Bwana. (Yoh. 21:15-17) Kwa sababu ya upendo, wazee ‘hawaishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao.’ (2 Kor. 5:14, 15) Upendo huo, pamoja na upendo wao kwa ajili ya Mungu na ndugu zao, unawalazimisha wazee kutumikia kondoo, huku wakitumia nguvu, mali, na wakati wao kufanya hivyo. (Mt. 22:37-39) Wanajitoa, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda.

12. Mtume Paulo alijitoa mwenyewe kwa kadiri gani?

12 Wazee wanapaswa kujitoa kwa kadiri gani? Katika kuwatunza kondoo, wazee wanamwiga mtume Paulo, kama alivyomwiga Yesu. (1 Kor. 11:1) Kwa kuwa walikuwa na upendo mwororo kwa ndugu zao wa Thesalonike, Paulo na wenzake walipendezwa sana kuwapa ‘si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zao wenyewe.’ Walipokuwa wakifanya hivyo, walikuwa wapole “kama mama mwenye kunyonyesha anavyowatunza kwa upendo watoto wake mwenyewe.” (1 The. 2:7, 8) Paulo alielewa jinsi mama mwenye kunyonyesha anavyohisi kuhusu watoto wake. Anafanya yote anayoweza kwa ajili yao, kutia ndani kuamka usiku wa manane ili kuwalisha.

13. Wazee wanahitaji kuwa na usawaziko gani?

13 Wazee wanahitaji kuwa waangalifu ili wawe na usawaziko wanapotimiza madaraka yao ya uchungaji na wajibu mbalimbali kuelekea familia zao. (1 Tim. 5:8) Wakati ambao wazee wanatumia kuwa pamoja na kutaniko ni wakati wenye thamani ambao wangetumia kuwa pamoja na familia zao. Njia moja ya kusawazisha madaraka hayo mawili ni kuwaalika wengine mara kwa mara kwenye jioni ya Ibada yao ya Familia. Kwa miaka mingi, Masanao, ambaye ni mzee wa kutaniko huko Japani, aliwaalika kwenye funzo la familia yake waseja na familia ambazo hazina baba kiroho. Baada ya muda, wengine wao ambao walisaidiwa walikuja kuwa wazee na wakaiga mfano mzuri wa Masanao.

Kataeni Pato Lisilo la Haki—Lichungeni Kundi kwa Hamu

1415. Kwa nini wazee wanapaswa kuepuka “kupenda pato lisilo la haki,” na wanaweza kumwiga Paulo jinsi gani katika jambo hilo?

14 Pia, Petro aliwatia moyo wazee walichunge kundi, “si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” Kazi ya wazee inachukua wakati mwingi, hata hivyo hawatazamii walipwe mshahara wowote. Petro aliona uhitaji wa kuwaonya wanaume wenzake wazee kuhusu hatari ya kulichunga kundi kwa “kupenda pato lisilo la haki.” Hatari hiyo inaonekana wazi katika maisha ya anasa ya viongozi wa kidini wa “Babiloni Mkubwa” huku watu wengi wakilazimika kuishi maisha ya umaskini. (Ufu. 18:2, 3) Leo, wazee wana sababu nzuri ya kujilinda ili wasiwe na mwelekeo wowote kama huo.

15 Paulo aliwawekea wazee Wakristo mfano mzuri. Ingawa alikuwa mtume na angeweza kuwa “mzigo wenye gharama” kwa Wakristo wa huko Thesalonike, Paulo ‘hakula chakula kwa yeyote bure.’ Badala yake, alifanya “kazi ya jasho na kutaabika usiku na mchana.” (2 The. 3:8) Wazee wengi leo, kutia ndani wale ambao ni waangalizi wanaosafiri, wanaweka mfano mzuri katika jambo hilo. Ingawa wanakubali wakati wanapokaribishwa na waamini wenzao, ‘hawamtwiki mtu yeyote mzigo wenye gharama.’—1 The. 2:9.

16. Inamaanisha nini kulichunga kundi “kwa hamu”?

16 Wazee wanalichunga kundi “kwa hamu.” Hamu yao inaonekana wazi kupitia mtazamo wao wa kujidhabihu ili kulisaidia kundi. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wanalilazimisha kundi kumtumikia Yehova; wala wazee wenye upendo hawawachochei wengine wamtumikie Mungu kwa roho ya kushindana. (Gal. 5:26) Wazee wanatambua kwamba kila kondoo ni tofauti na mwingine. Wana hamu ya kuwasaidia ndugu zao wamtumikie Yehova kwa furaha.

Si kwa Kupiga Ubwana Juu ya Kundi Bali Kuwa Vielelezo

17, 18. (a) Kwa nini nyakati nyingine mitume walikuwa na tatizo la kuelewa fundisho la Yesu kuhusu unyenyekevu? (b) Sisi tunaweza kujikuta katika hali gani inayofanana na hiyo?

17 Kama tulivyozungumza, wazee wanapaswa kukumbuka kwamba kundi ambalo wanachunga ni la Mungu, bali si lao. Wanakuwa waangalifu ili kuepuka “kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu.” (Soma 1 Petro 5:3.) Nyakati nyingine, mitume wa Yesu walitafuta mapendeleo wakiwa na nia mbaya. Mitume walitaka kupata vyeo vikubwa kama viongozi ambao walikuwa wakitawala mataifa.—Soma Marko 10:42-45.

18 Leo, ndugu ambao wanajitahidi “kufikia cheo cha mwangalizi” wanapaswa kujichunguza wenyewe ili kujua kwa nini wanajitahidi kufikia pendeleo hilo. (1 Tim. 3:1) Wale ambao sasa ni wazee wanapaswa kujiuliza wenyewe kwa unyoofu ikiwa wana tamaa ya kupata mamlaka au ukubwa kama mitume fulani walivyofanya. Ikiwa mitume walikuwa na tatizo hilo, basi wazee wanaweza kuona wazi kwamba wanahitaji kufanya bidii ili kuepuka mtazamo wowote wa ulimwengu wa kutaka kuwatawala wengine.

19. Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapochukua hatua ya kulinda kundi?

19 Ni kweli kwamba nyakati nyingine wazee wanahitaji kuwa thabiti, kama wakati wanapolinda kundi kutokana na “mbwa-mwitu wenye kukandamiza.” (Mdo. 20:28-30) Paulo alimwambia Tito aendelee “kuhimiza na kukaripia kwa mamlaka kamili.” (Tito 2:15) Lakini, hata wanapolazimika kuchukua hatua kama hiyo, wazee wanajitahidi kuwaheshimu wale ambao wanahusika. Wanatambua kwamba badala ya kumchambua mtu kwa ukali, kwa kawaida kumshawishi kwa upole kunagusa moyo wake zaidi na kumchochea kufuata njia iliyo sawa.

20. Wazee wanaweza kumwiga jinsi gani Yesu katika kuweka mfano mzuri?

20 Mfano mzuri wa Kristo unawachochea wazee kulipenda kundi. (Yoh. 13:12-15) Mioyo yetu inachochewa tunaposoma jinsi Yesu alivyowafundisha wanafunzi wake katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Mfano wake wa unyenyekevu uligusa mioyo ya wanafunzi wake, ukawachochea kufuata njia inayoonyesha ‘unyenyekevu wa akili wakiwaona wengine kuwa ni bora kuliko wao.’ (Flp. 2:3) Leo, wazee wanachochewa vivyo hivyo kufuata mfano wa Yesu, na hivyo, wanapaswa kuwa “vielelezo kwa kundi.”

21. Wazee wanaweza kutazamia thawabu gani?

21 Petro alimalizia shauri lake kwa wanaume wazee kwa kuzungumza kuhusu ahadi ya wakati ujao. (Soma 1 Petro 5:4.) Waangalizi watiwa-mafuta ‘watapokea taji la utukufu lisiloweza kufifia’ pamoja na Kristo huko mbinguni. Wachungaji wadogo ambao ni washiriki wa “kondoo wengine” watakuwa na pendeleo la kulichunga kundi la Mungu duniani chini ya utawala wa yule “mchungaji mkuu.” (Yoh. 10:16) Habari inayofuata itazungumzia njia mbalimbali ambazo washiriki wa kutaniko wanaweza kuwaunga mkono wale ambao wamewekwa rasmi ili kuongoza.

Kwa Kupitia

• Kwa nini lilikuwa jambo linalofaa kwa Petro kuwaonya wazee wenzake walichunge kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao?

• Wazee wanapaswa kuwachunga jinsi gani wale walio wagonjwa kiroho?

• Ni nini kinachowachochea wazee kulichunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Leo, wazee wanapaswa kulinda “kondoo” walio chini ya uangalizi wao kama wachungaji walivyofanya katika nyakati za kale