Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Anapendekeza Upendo Wake Kwetu

Mungu Anapendekeza Upendo Wake Kwetu

Mungu Anapendekeza Upendo Wake Kwetu

“Fadhili zisizostahiliwa [zitatawala] kama mfalme kupitia uadilifu kwa tazamio la uzima wa milele.”—ROM. 5:21.

1, 2. Tunaweza kufikiria zawadi gani mbili, lakini ni zawadi gani ambayo ina thamani kubwa zaidi?

“ZAWADI kubwa zaidi ambayo Waroma . . . waliwapatia wale waliotawala baada yao ni sheria yao na wazo la kwamba watu wanapaswa kuishi kulingana na sheria.” (Dakt. David J. Williams wa Chuo Kikuu cha Melbourne, Australia) Hata iwe jambo hilo ni la kweli kadiri gani, kuna zawadi ambayo ina thamani kubwa hata zaidi. Zawadi hiyo ni mpango wa Mungu wa kutuwezesha kuwa na msimamo unaokubalika na wenye uadilifu mbele zake na tumaini la kuokolewa na kupata uzima wa milele.

2 Katika njia fulani, kulikuwa na mambo ya kisheria ambayo yalihusu jinsi Mungu alivyotoa zawadi hiyo. Katika Waroma sura ya 5, mtume Paulo hakutaja mambo hayo kana kwamba ni makubaliano ya kisheria ambayo hayategemei hisia zozote. Badala yake alianza kwa kutoa uhakikisho huu wenye kusisimua: “Tumetangazwa kuwa waadilifu kutokana na imani, [basi] na tufurahie amani pamoja na Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo.” Wale wanaopokea zawadi hiyo kutoka kwa Mungu wanachochewa kumpenda pia. Paulo alikuwa mmoja wa watu hao. Aliandika hivi: “Upendo wa Mungu umemiminwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu.”—Rom. 5:1, 5.

3. Ni maswali au maulizo gani ambayo yanajitokeza?

3 Hata hivyo, kwa nini zawadi hiyo ya upendo ilihitajiwa? Mungu angeweza kuitoa jinsi gani kwa njia ya haki, na kwa usawaziko? Na watu wanapaswa kufanya nini ili wastahili kuipokea? Acheni tutafute majibu yenye kuridhisha na tuone jinsi yanavyokazia upendo wa Mungu.

Upendo wa Mungu Unashinda Dhambi

4, 5. (a) Yehova alionyesha upendo wake katika njia gani kubwa? (b) Ni ujuzi kuhusu mambo gani ambao unatuwezesha kuelewa Waroma 5:12?

4 Katika tendo ambalo lilionyesha upendo mkubwa, Yehova alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee ili kuwasaidia wanadamu. Paulo alieleza jambo hilo hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Fikiria jambo moja la hakika ambalo limetajwa hapo: “Tulipokuwa tungali watenda-dhambi.” Wote wanapaswa kujua jinsi hali hiyo ilivyotokea.

5 Paulo alieleza hali hiyo, alipoanza kwa kutaja jambo hili: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Rom. 5:12) Tunaweza kuelewa jambo hilo kwa sababu Mungu aliongoza mambo ili masimulizi yaandikwe ambayo yanaonyesha jinsi maisha ya mwanadamu yalivyoanza. Yehova aliwaumba wanadamu wawili, Adamu na Hawa. Muumba ni mkamilifu, na wanadamu hao wa kwanza ambao ni wazazi wetu, walikuwa pia wakamilifu. Mungu aliwapa sheria moja tu ambayo walipaswa kufuata na akawaambia kwamba kutotii sheria hiyo kungeleta adhabu ya kifo. (Mwa. 2:17) Hata hivyo, walichagua kuasi, huku wakipuuza mwongozo wa Mungu uliokuwa wenye usawaziko, na hivyo wakamkataa Mungu kuwa Mpaji-Sheria na Mwenye Enzi Kuu.—Kum. 32:4, 5.

6. (a) Kwa nini wazao wa Adamu walikufa kabla Mungu hajatoa Sheria ya Musa na baada ya hapo? (b) Ni hali gani ambayo inaweza kulinganishwa na ugonjwa kama wa damu kutoganda?

6 Adamu alipata watoto baada ya kutenda dhambi, na hivyo akawapitishia wote dhambi na matokeo yake mabaya. Bila shaka, watoto hao hawakuwa wamevunja sheria ya Mungu kama Adamu alivyofanya, kwa hiyo hawakushtakiwa kwa dhambi hiyohiyo; na pia hakukuwa na sheria yoyote iliyokuwa imeandikwa wakati huo. (Mwa. 2:17) Hata hivyo, bado wazao wa Adamu walirithi dhambi. Hivyo, dhambi na kifo vilitawala mpaka wakati Mungu alipowapa Waisraeli sheria iliyoandikwa, ambayo ilionyesha wazi kwamba walikuwa watenda-dhambi. (Soma Waroma 5:13, 14.) Matokeo mabaya ya dhambi tuliyorithi yanaweza kufananishwa na magonjwa na kasoro fulani zinazorithiwa kama vile upungufu wa damu, au hemofilia yaani, ugonjwa wa damu kutoganda. Huenda umewahi kusoma kwamba Alexis, mwana wa Alexandra na Nicholas wa Pili mtawala wa Urusi, alirithi ugonjwa wa damu kutoganda unaoitwa hemofilia. Ni kweli kwamba katika familia kama hiyo, watoto fulani hawasumbuliwi na magonjwa kama hayo, lakini huenda wakawa na magonjwa hayo mwilini. Lakini hali ni tofauti kabisa kuhusu dhambi. Matokeo mabaya ya dhambi ya Adamu hayangeweza kuepukika. Wote wanapatwa na matokeo hayo. Sikuzote yanasababisha kifo. Na watoto wote wanarithi matokeo hayo. Je, matokeo hayo mabaya yangeweza kuondolewa?

Mpango Ambao Mungu Alifanya Kupitia Yesu Kristo

7, 8. Maisha ya wanaume wawili wakamilifu yalileta jinsi gani matokeo tofauti?

7 Kwa upendo, Mungu alifanya mpango ili wanadamu wawe huru kutokana na dhambi waliyorithi. Paulo alieleza kwamba hilo liliwezekana kupitia mwanadamu mwingine, mwanamume mkamilifu aliyeishi baadaye, yaani, Adamu wa pili. (1 Kor. 15:45) Lakini maisha ya kila mmoja wa wanaume hao wawili wakamilifu yameleta matokeo yaliyo tofauti kabisa. Jinsi gani?—Soma Waroma 5:15, 16.

8 Paulo aliandika hivi: “Sivyo ilivyo kwa ile zawadi kama ilivyokuwa kwa lile kosa.” Adamu alikuwa na hatia ya kosa hilo, na kwa haki alipokea adhabu kali, alikufa. Hata hivyo, hangekufa peke yake. Tunasoma hivi: “Kwa kosa la mtu [huyo] mmoja wengi walikufa.” Hukumu ya haki iliyotolewa kwa Adamu ilitaka kwamba wazao wake wote wasio wakamilifu wapate adhabu hiyohiyo, kutia ndani sisi. Lakini bado tunaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba mwanamume mkamilifu, Yesu, angeweza kuleta matokeo yaliyo kinyume kabisa. Matokeo gani? Tunapata jibu katika maneno haya ya Paulo: “Kutangazwa [kwa watu wa namna zote] kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.”Rom. 5:18.

9. Mungu alikuwa akifanya nini alipotangaza wanadamu kuwa waadilifu, kama inavyotajwa katika Waroma 5:16, 18?

9 Ni nini maana ya maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa kuwa “tangazo la uadilifu” na “kutangazwa kuwa waadilifu”? Mtafsiri mmoja wa Biblia aliandika hivi kuhusu wazo hilo: “Ni maneno ya mfano ya kisheria ambayo yanaonyesha jambo halali kisheria. Yanaonyesha badiliko la msimamo wa mtu mbele za Mungu, si badiliko linalofanyika ndani ya mtu . . . Maneno hayo ya mfano yanaonyesha kwamba Mungu ni hakimu au mwamuzi ambaye amefanya uamuzi ambao unampendelea mshtakiwa, ambaye ameletwa mbele ya mahakama ya Mungu, kwa njia ya mfano, akiwa ameshtakiwa kwa kosa la kutokuwa mwadilifu. Lakini Mungu anamwondolea mshtakiwa huyo hatia.”

10. Yesu alifanya jambo gani ambalo liliweka msingi wa wanadamu kutangazwa kuwa waadilifu?

10 Ni kwa msingi gani ‘Mwamuzi mwadilifu wa dunia yote’ angeweza kumtangaza mtu asiye mwadilifu kuwa mwadilifu? (Mwa. 18:25) Kwa upendo, Mungu aliweka msingi kwa kumtuma duniani Mwana wake mzaliwa-pekee. Yesu alifanya mapenzi ya Baba yake kikamili, ingawa alishawishiwa, alitukanwa, na kudhihakiwa vikali sana. Alishika utimilifu wake mpaka kufikia hatua ya kufa kwenye mti wa mateso. (Ebr. 2:10) Kwa kuudhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu, Yesu alitoa fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo ingewaachilia huru, au kuwakomboa, wazao wa Adamu kutoka katika dhambi na kifo.—Mt. 20:28; Rom. 5:6-8.

11. Fidia au dhabihu ya ukombozi inategemea ulinganifu gani?

11 Katika andiko lingine Paulo alisema hiyo ni “fidia inayolingana.” (1 Tim. 2:6) Ililingana katika maana gani? Adamu aliwaletea mabilioni ya wazao wake hali ya kutokamilika na kifo. Ni kweli kwamba Yesu, akiwa mwanadamu mkamilifu, angetokeza mabilioni ya wazao wakamilifu. * Hivyo, ilieleweka kwamba maisha ya Yesu pamoja na maisha ya wale wote ambao wangekuwa wazao wake wakamilifu yangetokeza dhabihu inayolingana na maisha ya Adamu na wazao wake wasio wakamilifu. Hata hivyo, Biblia haisemi kwamba wote ambao wangeweza kuwa wazao wa Yesu walikuwa sehemu ya dhabihu ya ukombozi. Andiko la Waroma 5:15-19 linaonyesha kwamba kifo cha “mtu mmoja” tu ndicho kilichowawezesha wanadamu wawekwe huru. Ndiyo, uhai mkamilifu wa Yesu ulilingana na uhai wa Adamu. Jambo ambalo linakaziwa, na ambalo linapaswa kukaziwa ni, Yesu Kristo peke yake. Sasa iliwezekana kwa watu wa namna zote kupokea zawadi ya bure na uzima kwa sababu ya “tendo moja la kutetewa kuwa haki” la Yesu, maisha yake ya utii na kushika utimilifu mpaka kifo. (2 Kor. 5:14, 15; 1 Pet. 3:18) Jambo hilo liliwezekana jinsi gani?

Kuwekwa Huru kwa Msingi wa Fidia

12, 13. Kwa nini wale ambao wanatangazwa kuwa waadilifu wanahitaji rehema na upendo wa Mungu?

12 Yehova Mungu alikubali fidia au dhabihu ya ukombozi ambayo Mwana wake alitoa. (Ebr. 9:24; 10:10, 12) Lakini wanafunzi wa Yesu waliokuwa duniani, kutia ndani mitume wake waaminifu waliendelea kuwa na hali ya kutokamilika. Ingawa walijitahidi kuepuka makosa, nyakati nyingine hawakufaulu. Kwa nini? Kwa sababu walikuwa wamerithi dhambi. (Rom. 7:18-20) Lakini Mungu angeweza na alifanya jambo fulani kuhusiana na hilo. Aliikubali “fidia inayolingana” na alikuwa tayari kuitumia kwa ajili ya watumishi wake wa kibinadamu.

13 Si kwamba Mungu alikuwa chini ya wajibu wa kutumia dhabihu ya ukombozi kwa ajili ya mitume na wengine kwa sababu walikuwa wamefanya mambo fulani mazuri. Badala yake, Mungu alitumia dhabihu ya ukombozi kwa ajili yao kwa sababu ya rehema na upendo wake mwingi sana. Alichagua kuwaweka huru mitume na wengine kutoka kwa hukumu waliyopewa, na kuwaona kuwa wameondolewa hatia ambayo walikuwa wamerithi. Paulo alieleza hilo waziwazi hivi: “Kwa fadhili hizi zisizostahiliwa, kwa kweli, ninyi mmeokolewa kupitia imani; na hiyo si kutokana na ninyi, ni zawadi ya Mungu.”—Efe. 2:8.

14, 15. Ni thawabu gani ambayo wale wanaotangazwa na Mungu kuwa waadilifu waliahidiwa, lakini bado walihitaji kufanya nini?

14 Hebu fikiria zawadi kubwa ajabu kutoka kwa Mweza-Yote ya kusamehe dhambi ambazo mtu alirithi kutia ndani makosa aliyofanya! Huwezi kuhesabu dhambi ambazo watu mmoja-mmoja walitenda kabla ya kuwa Wakristo; hata hivyo, kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi, Mungu anaweza kusamehe dhambi hizo. Paulo aliandika hivi: “Zawadi ilitokana na makosa mengi katika tangazo la uadilifu.” (Rom. 5:16) Mitume na watu wengine ambao walipokea zawadi hiyo yenye upendo (kutangazwa kuwa waadilifu) walipaswa kuendelea kumwabudu Mungu wa kweli wakiwa na imani. Wangepata thawabu gani wakati ujao? ‘Wale wanaopokea wingi wa fadhili zisizostahiliwa na zawadi ya bure ya uadilifu watatawala wakiwa wafalme katika uzima kupitia mtu mmoja, Yesu Kristo.’ Kwa kweli, zawadi ya uadilifu ina matokeo yaliyo tofauti kabisa. Zawadi hiyo inatokeza uzima.—Rom. 5:17; soma Luka 22:28-30.

15 Wale wanaopokea zawadi hiyo, yaani, kutangazwa kuwa waadilifu, wanakuwa wana wa kiroho wa Mungu. Wakiwa warithi wenzi pamoja na Kristo, wana tumaini la kufufuliwa na kwenda mbinguni ili kuwa wana halisi wa kiroho na ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Yesu Kristo.—Soma Waroma 8:15-17, 23.

Watu Wengine Wanaonyeshwa Upendo wa Mungu

16. Wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza kupokea zawadi jinsi gani?

16 Si wote wanaomwamini Mungu na kumtumikia kwa ushikamanifu wana tumaini la ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni. Wengi wao wana tumaini linalotegemea Biblia kama lile la watumishi wa Mungu walioishi kabla ya Ukristo. Wanatumaini kuishi milele katika paradiso duniani. Je, wanaweza hata sasa kupokea zawadi ya upendo kutoka kwa Mungu na kuonwa kuwa waadilifu wakiwa na tumaini la kuishi duniani? Kulingana na yale ambayo Paulo aliwaandikia Waroma, bila shaka jibu ni ndiyo!

17, 18. (a) Mungu alimwona Abrahamu jinsi gani kwa sababu ya imani yake? (b) Ni kwa njia gani Yehova angeweza kumwona Abrahamu kuwa mwadilifu?

17 Paulo alizungumza kuhusu mfano mkuu zaidi, Abrahamu, mwanamume mwenye imani aliyeishi kabla Yehova hajawapa Waisraeli sheria iliyoandikwa na muda mrefu kabla Kristo hajafungua njia ya kupata uzima mbinguni. (Ebr. 10:19, 20) Tunasoma hivi: “Kwa maana ahadi ile kwamba awe mrithi wa ulimwengu hakuipata Abrahamu au uzao wake kupitia sheria, bali ilikuwa kupitia uadilifu kwa njia ya imani.” (Rom. 4:13; Yak. 2:23, 24) Kwa hiyo, Mungu alimhesabu Abrahamu ambaye alikuwa mwaminifu kuwa mwadilifu.—Soma Waroma 4:20-22.

18 Hilo halimaanishi kwamba Abrahamu hakuwa na dhambi alipokuwa akimtumikia Yehova kwa makumi mengi ya miaka. Hapana, hakuwa mwadilifu katika njia hiyo. (Rom. 3:10, 23) Hata hivyo, kwa sababu ya hekima yake isiyo na mipaka, Yehova alifikiria kuhusu imani ya Abrahamu iliyokuwa ya pekee na matendo yake yaliyotegemea imani hiyo. Abrahamu aliweka imani hasa katika “uzao” ulioahidiwa ambao ungekuja kupitia ukoo wake. Uzao huo ulithibitika kuwa yule Masihi, au Kristo. (Mwa. 15:6; 22:15-18) Kwa kufaa, kwa msingi wa “fidia ambayo Kristo Yesu alilipa,” Mungu ambaye ni Hakimu anaweza kusamehe dhambi ambazo zilifanywa zamani. Hivyo, Abrahamu na watu wengine wenye imani walioishi kabla ya Ukristo wana tumaini la kufufuliwa.—Soma Waroma 3:24, 25; Zab. 32:1, 2.

Furahia Msimamo wa Uadilifu Leo

19. Kwa nini maoni ya Mungu kuhusu Abrahamu yanapaswa kuwatia moyo watu wengi leo?

19 Ukweli wa kwamba Mungu mwenye upendo alimhesabu Abrahamu kuwa mwadilifu unapaswa kuwachochea Wakristo wa kweli leo. Yehova hakumtangaza kuwa mwadilifu kama anavyowatangaza kuwa waadilifu wale anaowatia mafuta kuwa “warithi pamoja na Kristo.” Washiriki wa kikundi hicho kidogo ‘wanaitwa wawe watakatifu’ na wanakubaliwa kuwa “wana wa Mungu.” (Rom. 1:7; 8:14, 17, 33) Kinyume na hilo, Abrahamu alikuja kuwa “rafiki ya Yehova,” na jambo hilo lilitukia kabla ya kutolewa kwa dhabihu ya ukombozi. (Yak. 2:23; Isa. 41:8) Basi, namna gani kuhusu Wakristo wa kweli ambao wana tumaini la kuishi katika dunia iliyorudishwa kuwa Paradiso?

20. Leo Mungu anawatazamia wale anaowaona kuwa waadilifu kama Abrahamu wafanye nini?

20 Watu hao hawapokei “zawadi ya bure ya uadilifu” wakiwa na tumaini la kuishi mbinguni “kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.” (Rom. 3:24; 5:15, 17) Hata hivyo, wanamwamini kabisa Mungu na maandalizi yake, na wanaonyesha imani yao kupitia matendo mazuri. Moja kati ya matendo hayo ni ‘kuhubiri kuhusu ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:31) Hivyo, Yehova anaweza kuwaona watu hao kuwa waadilifu kama vile alivyomwona Abrahamu. Zawadi ambayo watu hao wanapokea, yaani, urafiki pamoja na Mungu, ni tofauti na “zawadi ya bure” ambayo watiwa mafuta wanapokea. Hata hivyo, bila shaka wanapokea zawadi hiyo kwa shukrani nyingi.

21. Ni faida gani ambazo tunaweza kupata kwa sababu ya upendo na haki ya Yehova?

21 Ikiwa unatazamia kufurahia uzima wa milele duniani, unapaswa kutambua kwamba umepata nafasi hiyo si kwa sababu ya tendo la mtawala fulani wa kibinadamu. Badala yake, mpango huo unaonyesha kusudi lenye hekima la Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Yehova anatimiza kusudi lake hatua kwa hatua. Hatua hizo zinalingana na haki ya kweli. Zaidi ya hilo, hatua hizo zimeonyesha upendo mkubwa wa Mungu. Ndiyo sababu Paulo alisema: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”—Rom. 5:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kwa mfano, maoni hayo kuhusu wazao yalitiwa ndani ya Insight on the Scriptures, Buku la 2, ukurasa wa 736, fungu la 4 na 5 (Étude perspicace des Écritures, Buku la 2, ukurasa wa 728 fungu la 1 na 2).

Je, Unakumbuka?

• Wazao wa Adamu walipokea urithi gani, na matokeo yalikuwa nini?

• Fidia inayolingana ilitolewa jinsi gani, na ililingana katika maana gani?

• Umepata tumaini gani kwa sababu ya zawadi ya kutangazwa kuwa mwadilifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Mwanamume mkamilifu Adamu alifanya dhambi. Mwanamume mkamilifu Yesu alitoa “fidia inayolingana”

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ni habari njema kama nini kwamba kupitia Yesu tunaweza kutangazwa kuwa waadilifu!