Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza ‘Kuifanikisha Njia Yako’ Jinsi Gani?

Unaweza ‘Kuifanikisha Njia Yako’ Jinsi Gani?

Unaweza ‘Kuifanikisha Njia Yako’ Jinsi Gani?

“KUFANIKIWA” ni neno linalovutia kama nini! Watu fulani wamepandishwa cheo kazini na kufanikiwa kabisa kuwa matajiri na kujijengea jina wenyewe. Wengine wamekuwa wakiota ndoto kwamba watafanikiwa lakini hawajafanikiwa.

Kwa kadiri kubwa, mafanikio yanategemea jambo ambalo unakazia fikira katika maisha yako. Mambo mengine mawili ya maana ni jinsi unavyotumia wakati wako na nguvu, na ikiwa unajitahidi kabisa kufikia miradi yako.

Wakristo wengi wamegundua kwamba kushiriki kwa ukamili katika huduma kumewaletea furaha nyingi. Kufuatilia utumishi wa wakati wote maishani kumewasaidia vijana na wazee kufanikiwa. Hata hivyo, huenda wengine wakahisi kwamba huduma inachosha na hivyo wanafuatia miradi mingine badala ya kutanguliza huduma katika maisha yao. Ni nini kinachoweza kusababisha hali hiyo? Unaweza kufanya nini ili usipuuze mambo yenye thamani kikweli? Na unaweza ‘kuifanikisha njia yako’ jinsi gani?—Yos. 1:8.

Michezo na Utendaji wa Baada ya Masomo

Vijana Wakristo wanahitaji kuendelea kuwa na usawaziko unaofaa katika kumtumikia Mungu wa kweli na kushiriki katika utendaji mwingine. Wale ambao wanafanya hivyo watafanikiwa maishani na wanastahili kupongezwa kwa uchangamfu.

Hata hivyo, vijana fulani Wakristo wanajihusisha sana na michezo na utendaji wa baada ya masomo. Huenda utendaji huo si mbaya. Hata hivyo, vijana Wakristo wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Nitahitaji kutumia muda gani katika utendaji huo? Namna gani kuhusu mashirika? Watu ninaoshirikiana nao katika utendaji huo wana roho ya aina gani? Na huenda nikaanza kutumia maisha yangu kufuatia nini?’ Inaelekea unatambua kwamba mtu anaweza kujiingiza sana katika utendaji huo hivi kwamba anakosa wakati au nguvu za kutosha za kuendelea kuwa na uhusiano pamoja na Mungu. Basi, unaweza kuona ni kwa nini ni jambo la maana kupanga mambo tunayohitaji kutanguliza maishani.—Efe. 5:15-17.

Fikiria mfano wa Wiktor. * Anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilijiunga na timu ya kucheza mpira wa wavu (volleyball). Baada ya muda, nilishinda tuzo na zawadi nyingi. Nilikuwa na nafasi ya kuwa mchezaji maarufu.” Baada ya muda, Wiktor alisumbuka kwa sababu kufuatia mchezo huo kulimfanya apoteze usawaziko wake wa kiroho. Siku moja, alilala usingizi alipokuwa akijaribu kusoma Biblia. Pia, alitambua kwamba hakuwa akipata shangwe nyingi katika huduma ya shambani. “Nilitumia nguvu zangu zote katika mchezo huo, na muda si muda niligundua kwamba ulikuwa pia ukipunguza bidii yangu ya kiroho. Nilijua kwamba sikuwa nikifanya mambo yote ambayo ningeweza kufanya.”

Je, Nifuatie Elimu ya Juu?

Mkristo ana wajibu wa Kimaandiko wa kuitunza familia yake, na hilo linatia ndani kutimiza mahitaji yao ya kimwili. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, je, kweli tunahitaji digrii ya chuo kikuu au chuo cha mafunzo ili kufanya hivyo?

Ni vizuri mtu afikirie kufuatia elimu ya juu kutakuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wake pamoja na Yehova. Acheni tuchunguze mfano wa Kimaandiko ambao utatusaidia kuelewa jambo hilo.

Baruku alikuwa mwandishi wa nabii Yeremia. Wakati fulani, badala ya kukazia fikira mapendeleo ambayo alikuwa nayo ya kumtumikia Yehova, Baruku alianza kujitafutia mambo makuu. Yehova aliona jambo hilo na akamwonya hivi kupitia Yeremia: “Wewe unaendelea kujitafutia makuu. Usiendelee kuyatafuta.”—Yer. 45:5.

Ni ‘mambo gani makuu’ ambayo Baruku alikuwa akiendelea kutafuta? Huenda alishawishiwa kujitafutia umashuhuri katika mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Au huenda mambo hayo makuu yalikuwa utajiri wa kimwili. Kwa vyovyote vile, aliacha kukazia fikira mambo ya maana zaidi, mambo yenye thamani kiroho. (Flp. 1:10) Hata hivyo, bila shaka Baruku alisikiliza onyo ambalo Yehova alitoa kupitia Yeremia na hivyo akaiokoa nafsi yake kama nyara.—Yer. 43:6.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na simulizi hilo? Shauri ambalo Baruku alipewa linaonyesha kwamba kulikuwa na tatizo. Alikuwa akijitafutia mwenyewe mambo makuu. Ikiwa una njia ya kujitegemeza mwenyewe, je, kweli unahitaji kutumia wakati, pesa, na nguvu kupata elimu ya juu ili tu kutimiza miradi ya kibinafsi au kwa sababu wazazi au watu wengine wa ukoo wanataka ufanye hivyo?

Mfikirie Grzegorz, anayefanya kazi ya kutayarisha programu za kompyuta. Alishawishiwa na wafanyakazi wenzake, akaamua kupata elimu ya ziada ya pekee inayochukua muda mrefu. Baada ya muda hakuwa na wakati wa kufuatia mambo ya kiroho. Anakumbuka hivi: “Sikuzote dhamiri ilinisumbua. Dhamiri yangu ilinisumbua kwa sababu singeweza kufikia miradi yangu ya kiroho ambayo nilikuwa nimejiwekea.”

Kujishughulisha Sana na Kazi ya Kimwili

Neno la Mungu linawatia moyo Wakristo wa kweli wafanye kazi kwa bidii kuwa wafanyakazi na wasimamizi wanaochukua madaraka yao kwa uzito. Mtume Paulo aliandika hivi: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.” (Kol. 3:22, 23) Hata hivyo, ingawa kufanya kazi kwa bidii ni jambo linalostahili pongezi, kuna jambo lingine linalohitajiwa, kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Muumba wetu. (Mhu. 12:13) Ikiwa Mkristo atajishughulisha sana na kazi yake ya kimwili, ni rahisi sana kuacha kutanguliza mambo ya kiroho.

Kujishughulisha sana na kazi ya kimwili kunaweza kumfanya Mkristo ahisi kwamba amechoka sana na hivyo hawezi kudumisha usawaziko wake wa kiroho na kuisaidia familia yake. Mfalme Sulemani alisema kwamba “konzi mbili za kazi ngumu” mara nyingi zinaambatana na “kufuatilia upepo.” Ikiwa Mkristo anajishughulisha na kazi ya kimwili kupita kasi, mwishowe atakuwa na mkazo mkali sana kwa muda mrefu. Mtu kama huyo anaweza hata kuwa mtumwa wa kazi na mwishowe anachoka kabisa. Ikiwa ndivyo ilivyo, je, kweli anaweza ‘kufurahi na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu’? (Mhu. 3:12, 13; 4:6) Jambo la maana zaidi ni kwamba je, atakuwa na nguvu za kutosha za kimwili na za kihisia za kutimiza madaraka yake katika familia na kushiriki katika utendaji wa kiroho?

Janusz, ambaye anaishi Ulaya Mashariki, alijishughulisha sana na kazi yake ya kutunza mabustani. Anakumbuka hivi: “Watu wa ulimwengu walinipenda kwa sababu nilikuwa mwenye juhudi sana na nilimaliza kila kazi niliyopewa. Lakini hali yangu ya kiroho ilidhoofika, na nikaacha kushiriki katika huduma ya shambani. Muda si muda niliacha kuhudhuria mikutano. Nilikuwa mwenye kiburi sana hivi kwamba nilikataa mashauri ya wazee na nikajitenga na kutaniko.”

Unaweza Kufanikisha Maisha Yako

Tumezungumzia mambo matatu ambayo Mkristo anaweza kujishughulisha nayo sana mpaka afikie hatua ya kufa kiroho. Je, unahusika katika jambo lolote kati ya mambo hayo? Ikiwa ndivyo, maandiko, maelezo na maswali au maulizo yafuatayo yanaweza kukusaidia kujua ikiwa kwa kweli unafanikisha maisha yako.

Michezo na utendaji wa baada ya masomo: Unashiriki kwa kadiri gani katika utendaji huo? Je, wakati ambao hapo mwanzoni ulitumia kufuatia mambo ya kiroho unautumia kufuatia utendaji wa baada ya masomo? Je, umeanza kukosa kufurahia ushirika pamoja na waamini wenzako? Ikiwa ndivyo, kwa nini usimwige Mfalme Daudi, ambaye alimsihi Yehova hivi: “Unijulishe njia ninayopaswa kuitembea.”—Zab. 143:8.

Mwangalizi mmoja anayesafiri alimsaidia Wiktor, aliyetajwa mwanzoni. Mwangalizi huyo alimwambia hivi: “Unazungumza kwa shauku sana kuhusu mchezo wa wavu ambao unapenda.” Wiktor anasema hivi: “Maelezo hayo yalinishtua sana. Nilitambua kwamba nilikuwa nimepita mipaka. Baada ya muda, niliacha kushirikiana na marafiki walimwengu katika timu yetu nikaanza kutafuta marafiki katika kutaniko.” Leo, Wiktor anamtumikia Yehova kwa bidii katika kutaniko lao. Anapendekeza hivi: “Waulize marafiki wako, wazazi wako, au wazee wa kutaniko ikiwa wameona kwamba utendaji wako wa shuleni umekusaidia kumkaribia Yehova zaidi au kujitenga naye.”

Kwa nini usiwaambie wazee wa kutaniko lenu kwamba ungependa kujitahidi kufikia mapendeleo zaidi katika utumishi wa Mungu? Je, unaweza kuwasaidia waliozeeka ambao wanahitaji msaada au rafiki, labda unaweza kuwasaidia kununua vitu au kufanya kazi katika nyumba zao? Hata uwe na umri gani, unaweza kushiriki katika huduma ya wakati wote, na kuwaeleza wengine mambo yanayokuletea shangwe.

Elimu ya juu: Yesu alionya kuhusu ‘kutafuta utukufu wako mwenyewe.’ (Yoh. 7:18) Unapofanya uamuzi wowote kuhusu kiwango cha elimu ya kilimwengu ambacho utapata, je, ‘umehakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi’?—Flp. 1:9, 10.

Grzegorz, ambaye anafanya kazi ya kutayarisha programu za kompyuta, alifanya mabadiliko fulani katika maisha yake. Alisema hivi: “Nilichukua kwa uzito mashauri ya wazee, nikarahisisha maisha yangu. Nilitambua kwamba sikuhitaji kupata elimu zaidi ya kilimwengu. Ningetumia wakati na nguvu zangu zote kupata elimu hiyo.” Grzegorz alishiriki zaidi katika utendaji wa kutaniko. Baada ya muda, alihitimu katika shule ambayo sasa inaitwa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja. Ndiyo, ‘alinunua wakati’ ili kuongeza elimu yake ya kimungu.—Efe. 5:16.

Kazi ya kimwili: Je, unajishughulisha sana na kazi yako ya kimwili hivi kwamba umeanza kupuuza mambo ya kiroho? Je, unapata wakati wa kutosha wa kuzungumza na familia yako? Je, unaboresha migawo yako ya hotuba katika kutaniko? Je, unashiriki katika mazungumzo yenye kujenga pamoja na wengine? “Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake,” nawe utapata baraka nyingi za Yehova na ‘utaona mema kwa sababu ya kazi yako ngumu.’—Mhu. 2:24; 12:13.

Janusz, aliyetajwa mwanzoni, hakufanikiwa sana katika biashara yake ya kutunza mabustani; badala yake, alishindwa. Hakupata pesa na alikuwa na madeni makubwa sana, akamgeukia Yehova. Janusz alipanga utendaji wake na sasa anatumika akiwa painia wa kawaida na mzee wa kutaniko. Anasema hivi: “Ninapotosheka na mambo ya msingi na wakati huohuo kujitoa kabisa kiroho, ninapata amani ya akili na utulivu katika moyo.”—Flp. 4:6, 7.

Chukua wakati fulani kuchunguza kwa unyoofu nia yako na mambo unayotanguliza. Kumtumikia Yehova ni njia ambayo inaleta mafanikio ya kudumu maishani. Uwe na mradi wa kumtumikia Yehova maishani.

Huenda ukahitaji kufanya marekebisho fulani, hata kuondoa kabisa mambo fulani yasiyo ya lazima ili ujihakikishie mwenyewe “mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Rom. 12:2) Lakini unaweza ‘kuifanikisha njia yako’ kwa kumtumikia kwa nafsi yote.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 31]

Unaweza Kuifanikisha Njia Yako Jinsi Gani?

Kwa kuwa kuna mambo mengi sana unayohitaji kutimiza, unaweza namna gani kuepuka kukengeushwa kutoka kwa mambo ambayo kwa kweli ni yenye thamani? Chukua wakati fulani kuchunguza nia yako na mambo unayotanguliza kwa kufikiria maswali au maulizo yafuatayo:

MICHEZO NA UTENDAJI WA BAADA YA MASOMO

▪ Watu unaoshirikiana nao katika utendaji huo wana mitazamo ya aina gani?

▪ Unatumia muda mwingi kadiri gani katika utendaji huo?

▪ Je, utaanza kutanguliza mambo hayo katika maisha yako?

▪ Je, unatumia wakati ambao mwanzoni ulitumia kufuatia mambo ya kiroho kufuatia utendaji huo?

▪ Namna gani watu unaoshirikiana nao?

▪ Je, unafurahia kushirikiana na watu hao kuliko waamini wenzako?

ELIMU YA JUU

▪ Ikiwa una njia ya kupata riziki, je, kweli unahitaji kutumia wakati, pesa, na nguvu zako kupata elimu zaidi ya kilimwengu?

▪ Je, kweli ni lazima uwe na digrii ya chuo fulani cha mafunzo au chuo kikuu ili kupata riziki?

▪ Je, hilo litakuzuia kuhudhuria mikutano?

▪ Je, ‘umehakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi’?

▪ Je, unahitaji kutia nguvu uhakika wako katika uwezo wa Yehova wa kutimiza mahitaji yako?

KAZI YA KIMWILI

▪ Je, uamuzi wako unakuruhusu ‘ufurahie na kuona mema kwa ajili ya kazi yako yote iliyo ngumu’?

▪ Je, una nguvu za kutosha za kimwili na kihisia za kutimiza madaraka yako katika familia na kushiriki katika utendaji wa kiroho?

▪ Je, unatumia wakati wa kutosha kuzungumza na familia yako?

▪ Je, unajishughulisha sana na kazi hivi kwamba unasukuma kando mambo ya kiroho?

▪ Je, kazi ya kimwili imekuwa na matokeo mabaya kwa migawo yako ya hotuba?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Yehova alimwonya Baruku kuhusu kujitafutia mambo makuu