Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

Mambo Makuu Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Barua ya Yakobo na ya Petro

KARIBU miaka 30 baada ya Pentekoste ya 33 W.K., mwanafunzi Yakobo—ndugu wa kambo wa Yesu—anaandika barua kwa “makabila kumi na mawili” ya Israeli la kiroho. (Yak. 1:1) Kusudi lake: kuwahimiza wawe wenye nguvu katika imani na kuvumilia majaribu. Pia, anatoa mashauri ili kurekebisha hali zenye kusumbua ambazo zimesitawi katika makutaniko.

Kabla tu ya kampeni ya kuwatesa Wakristo ya Maliki Mroma Nero mwaka wa 64 W.K., mtume Petro anawaandikia Wakristo barua yake ya kwanza ili kuwatia moyo wasimame imara katika imani. Katika barua yake ya pili, iliyoandikwa muda mfupi tu baada ya ile ya kwanza, Petro anawatia moyo waamini wenzake wakazie uangalifu neno la Mungu na anawaonya kuhusu kuja kwa siku ya Yehova. Kwa kweli, tunaweza kufaidika kwa kukazia uangalifu ujumbe wa barua ya Yakobo na ya Petro.—Ebr. 4:12.

MUNGU ANAWAPA HEKIMA WALE ‘WANAOMWOMBA KWA IMANI’

(Yak. 1:1–5:20)

Yakobo anaandika: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.” Yehova anawapa hekima wale ‘wanaoendelea kuomba kwa imani’ ili wavumilie majaribu.—Yak. 1:5-8, 12.

Pia, wale ambao ni “walimu” katika kutaniko wanahitaji imani na hekima. Baada ya kusema kwamba ulimi ni “kiungo kidogo” ambacho kinaweza ‘kuutia doa mwili wote,’ Yakobo anaonya kuhusu mielekeo ya kilimwengu ambayo inaweza kuharibu uhusiano wa mtu pamoja na Mungu. Pia, anataja hatua ambazo mtu aliye mgonjwa kiroho anapaswa kuchukua ili apone.—Yak. 3:1, 5, 6; 5:14, 15.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:13—Ni katika maana gani “rehema hufurahi kwa njia ya ushindi juu ya hukumu”? Mungu anapotutoza hesabu, anafikiria pia rehema ambayo tumewaonyesha wengine naye anatusamehe kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Mwana wake. (Rom. 14:12) Hiyo ni sababu moja inayopaswa kutuchochea kufanya rehema kuwa sifa kuu katika maisha yetu.

4:5—Ni andiko gani ambalo Yakobo ananukuu hapa? Yakobo hanukuu andiko lolote. Hata hivyo, inawezekana kwamba maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanategemea mawazo ya ujumla ya maandiko kama Mwanzo 6:5; 8:21; Methali 21:10; na Wagalatia 5:17.

5:20—“Yeye anayemrudisha mtenda-dhambi kutoka kwenye kosa la njia yake” ataiokoa nafsi ya nani kutoka kwenye kifo? Mkristo anayemrudisha mkosaji kutoka kwenye njia ya dhambi anaiokoa nafsi ya mtu huyo anayetubu kutokana na kifo cha kiroho na pengine kutokana na uharibifu wa milele. Mtu anayemsaidia mtenda-dhambi katika njia hiyo “atafunika dhambi nyingi” za mtenda-dhambi huyo.

Mambo Tunayojifunza:

1:14, 15. Dhambi inatokana na tamaa zisizofaa. Kwa hiyo, hatupaswi kusitawisha tamaa mbaya kwa kuendelea kuzifikiria. Badala yake, tunahitaji ‘kuendelea kufikiria’ mambo yenye kujenga na kuyajaza katika akili na mioyo yetu.—Flp. 4:8.

2:8, 9“Kuonyesha upendeleo” ni kinyume cha “sheria ya kifalme” ya upendo. Hivyo, Wakristo wa kweli hawaonyeshi upendeleo.

2:14-26. ‘Tunaokolewa kupitia imani,’ na “si kutokana na matendo” ya Sheria ya Musa au yale tunayotenda tukiwa Wakristo. Hatupaswi tu kudai kwamba tuna imani. (Efe. 2:8, 9; Yoh. 3:16) Imani inapaswa kutuchochea kuwa na matendo ya kimungu.

3:13-17. “Hekima inayotoka juu” bila shaka ni bora zaidi kuliko hekima ya “kidunia, ya kinyama, ya roho waovu”! Tunapaswa ‘kuendelea kuitafuta hekima ya kimungu kama hazina zilizofichika.’—Met. 2:1-5.

3:18. Mbegu ya habari njema ya Ufalme inapaswa ‘kupandwa kwa amani na wale wanaofanya amani.’ Ni jambo la maana sana kwetu kuwa watu wanaofanya amani na si wenye majivuno, wagomvi, au watu wa fujo.

‘SIMAMA IMARA KATIKA IMANI’

(1 Pet. 1:1–5:14)

Petro anawakumbusha waamini wenzake kuhusu “tumaini lililo hai” la urithi mbinguni. Petro anawaambia hivi: “Ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu.’” Baada ya kutoa mashauri hususa kuhusu kujitiisha, anawahimiza wote kuwa na ‘akili zinazopatana, wakionyesha hisia-mwenzi, wakiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili.’—1 Pet. 1:3, 4; 2:9; 3:8.

Kwa kuwa “mwisho wa [mfumo wa Kiyahudi wa] mambo umekaribia,” Petro anawashauri ndugu ‘wawe na utimamu wa akili, na kukesha kuhusiana na sala.’ Anawaambia hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. . . . Chukueni msimamo mkampinge [Shetani], mkiwa imara katika imani.”—1 Pet. 4:7; 5:8, 9.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:20-22—Ubatizo unatuokoa jinsi gani? Ubatizo ni takwa kwa wale wanaotafuta wokovu. Hata hivyo, ubatizo peke yake hautuokoi. Wokovu ni “kupitia ufufuo wa Yesu Kristo.” Mtu anayebatizwa anapaswa kuamini kwamba wokovu unawezekana tu kwa sababu Yesu alikufa kifo cha kidhabihu, akafufuliwa, na ‘yuko kwenye mkono wa kuume wa Mungu,’ akiwa na mamlaka juu ya watu walio hai na wafu. Ubatizo unaotegemea imani kama hiyo ndio ambao unalingana na ‘nafsi nane, waliochukuliwa salama kupitia maji.’

4:6—Ni nani “wafu” ambao ‘walitangaziwa habari njema’? Hao ni wale ambao walikuwa ‘wafu katika makosa yao na dhambi zao,’ au wale ambao walikuwa wafu kiroho, kabla ya kusikia habari njema. (Efe. 2:1) Hata hivyo, baada ya kuamini habari njema, walianza kuwa “hai” kiroho.

Mambo Tunayojifunza:

1:7. Ili imani yetu iwe na thamani kubwa, ubora wake unapaswa kujaribiwa. Imani kama hiyo yenye nguvu ndiyo kwa kweli ‘inayohifadhi hai nafsi.’ (Ebr. 10:39) Hatupaswi kurudi nyuma imani yetu inapojaribiwa kwa njia mbalimbali.

1:10-12. Malaika walitamani sana kuchunguza na kuelewa kweli nzito za kiroho ambazo manabii wa Mungu wa zamani waliandika kuhusu kutaniko la Kikristo la watiwa-mafuta. Hata hivyo, mambo hayo yalieleweka waziwazi Yehova alipoanza kushughulika na kutaniko. (Efe. 3:10) Je, hatupaswi kufuata mfano wa malaika na kujitahidi kuchunguza ndani ya “mambo mazito ya Mungu”?—1 Kor. 2:10.

2:21. Kwa kumwiga Yesu Kristo, ambaye ndiye Kielelezo chetu, tunapaswa kuwa tayari kuteseka hata kufikia kifo ili kuunga mkono enzi kuu ya Yehova.

5:6, 7Tunapomtupia Yehova mahangaiko yetu, anatusaidia tuendelee kutanguliza ibada ya kweli katika maisha yetu badala ya kuhangaikia sana mambo ya kesho.—Mt. 6:33, 34.

“SIKU YA YEHOVA ITAKUJA”

(2 Pet. 1:1–3:18)

Petro anaandika hivi: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” Kukazia uangalifu neno la unabii kunaweza kutulinda tusidanganywe na “walimu wa uwongo” na watu wengine wapotovu.—2 Pet. 1:21; 2:1-3.

Petro anaonya hivi: “Katika siku za mwisho watakuja wadhihaki na dhihaka zao.” Lakini “siku ya Yehova itakuja kama mwizi.” Petro anamalizia barua yake kwa kutoa mashauri mazuri kwa wale ‘wanaongojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’—2 Pet. 3:3, 10-12.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:19—Ni nani aliye “nyota ya mchana,” anachomoza wakati gani, na tunajua jinsi gani kwamba jambo hilo tayari limetukia? “Nyota ya mchana” ni Yesu Kristo akiwa katika mamlaka ya Ufalme. (Ufu. 22:16) Katika mwaka wa 1914, Yesu alichomoza mbele ya uumbaji wote akiwa Mfalme wa Kimasihi, na hivyo kutangaza mapambazuko ya siku mpya. Kugeuka sura kulionyesha kimbele utukufu wa Yesu na mamlaka ya Ufalme, na hivyo kukazia kwamba neno la Mungu la kinabii linategemeka. Kukazia uangalifu neno hilo kunatia mwangaza katika mioyo yetu, na hivyo tunajua kwamba Nyota ya Mchana amechomoza.

2:4—“Tartaro” ni nini, na malaika waasi walitupwa humo wakati gani? Tartaro ni hali kama ya gereza ambamo ni viumbe wa roho tu wanazuiliwa, bali si wanadamu. Ni hali ya giza tititi la akili kuhusiana na makusudi matukufu ya Mungu. Wale walio katika Tartaro hawana tumaini lolote la wakati ujao. Mungu aliwatupa malaika waasi ndani ya Tartaro katika siku za Noa, na watabaki katika hali hiyo ya kushushwa mpaka watakapoharibiwa.

3:17—Petro alimaanisha nini alipotaja ‘ujuzi wa kimbele’? Petro alikuwa akizungumza kuhusu ujuzi wa kimbele wa matukio ya wakati ujao, ambao yeye na waandikaji wengine wa Biblia walipewa kwa mwongozo wa roho ya Mungu. Kwa kuwa ujuzi huo haukuwa na mipaka, Wakristo wa mapema waliokuwa nao hawakujua mambo yote kuhusu matukio ya wakati ujao. Walijua tu mambo ya jumla ambayo yalitarajiwa.

Mambo Tunayojifunza:

1:2, 5-7. Zaidi ya kutusaidia kuongeza “ujuzi sahihi juu ya Mungu na Yesu,” kujitahidi sana kusitawisha sifa kama vile imani, uvumilivu, na ujitoaji-kimungu kunaweza ‘kutuzuia kuwa ama wasiotenda au wasiozaa matunda’ kuhusiana na ujuzi huo.—2 Pet. 1:8.

1:12-15. Ili tubaki tukiwa ‘tumewekwa imara katika kweli,’ kila mara tunahitaji vikumbusho, kama vile tunavyopokea kupitia mikutano yetu ya kutaniko, funzo la kibinafsi, na usomaji wa Biblia.

2:2. Tunapaswa kuwa waangalifu ili mwenendo wetu usimletee suto Yehova na tengenezo lake.—Rom. 2:24.

2:4-9. Kwa sababu ya mambo ambayo alifanya wakati uliopita, tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, lakini kuwaweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya ile siku ya hukumu ili wakatiliwe mbali.”

2:10-13. Ingawa “watukufu,” yaani, wazee Wakristo, wana kasoro na huenda nyakati nyingine wakakosea, hatupaswi kuwatukana.—Ebr. 13:7, 17.

3:2-4, 12. Kukazia karibu akilini “maneno yaliyosemwa hapo zamani na manabii watakatifu na amri ya Bwana na Mwokozi” kutatusaidia kukumbuka kwamba siku ya Yehova imekaribia sana.

3:11-14. Tukiwa watu ambao ‘wanangojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova,’ ni lazima (1) ‘tuwe watakatifu katika mwenendo,’ tukidumisha usafi wa kimwili, kiakili, kiadili, na kiroho; (2) tuwe na matendo mengi ya “ujitoaji-kimungu,” kama yale yanayohusiana na kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi; (3) tuwe na mwenendo na utu ‘usio na doa,’ usiochafuliwa na ulimwengu; (4) tuwe “bila dosari,” kwa kufanya mambo yote kwa nia nzuri; na (5) tuwe “katika amani”—amani pamoja na Mungu, pamoja na ndugu zetu Wakristo, na pamoja na wanadamu wenzetu.