Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Furahia Kumngojea Yehova

Furahia Kumngojea Yehova

Furahia Kumngojea Yehova

JE, UMEWAHI kula tunda bichi? Haikosi kwamba hukupendezwa na ladha yake. Matunda yanachukua wakati ili kuiva, na bila shaka kuna faida ya kungojea yaive. Kuna faida ya kungojea katika hali nyinginezo pia. Biblia inasema: “Ni jambo jema kwa mtu kuungojea, ndiyo, kimyakimya, wokovu wa Yehova.” (Maombolezo 3:26; Tito 2:13) Wakristo wanapaswa kumngojea Yehova katika njia gani? Tutapata faida gani tukimngojea Yehova?

Kumngojea Mungu—Kunahusisha Nini?

Tukiwa Wakristo ‘tunangojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.’ Tunatarajia kupata kitulizo wakati atakaposababisha “kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.” (2 Petro 3:7, 12) Yehova mwenyewe anatamani sana kukomesha uovu wote, lakini anajizuia ili awaokoe Wakristo kwa njia ambayo itatukuza jina lake. Biblia inasema: “Mungu, ingawa alikuwa na nia ya kuonyesha ghadhabu yake na kujulisha nguvu zake, alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya ghadhabu vilivyofanywa kuwa vyenye kufaa kwa ajili ya uharibifu, ili ajulishe utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema.” (Waroma 9:22, 23) Kama alivyofanya katika siku za Noa, Yehova anajua wakati unaofaa wa kuwaokoa watu wake leo. (1 Petro 3:20) Hivyo, kumngojea Mungu kunatia ndani kungojea wakati wake wa kuchukua hatua.

Tunapongojea siku ya Yehova, huenda nyakati nyingine tukahuzunika kuona viwango vya maadili vya ulimwengu tunamoishi vikishuka zaidi na zaidi. Tunapohisi hivyo, inatia moyo kufikiria maneno ya Mika, nabii wa Mungu, ambaye aliandika: “Mshikamanifu ameangamia kutoka duniani, na kati ya wanadamu hakuna mnyoofu.” Kisha akaongeza hivi: “Lakini mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu.” (Mika 7:2, 7) Ni nini ‘mtazamo wa kungojea’ tunaopaswa kusitawisha? Kwa kuwa mara nyingi kungojea kunachosha, tunaweza jinsi gani kupata shangwe kwa kumngojea Mungu?

Wenye Furaha Tunapongojea

Tunaweza kujua mtazamo unaofaa kwa kumfikiria Yehova. Hajakosa kamwe kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Yeye ni mwenye furaha huku akingojea kwa sababu anaendelea kujitahidi kutimiza kusudi lake la kuwawezesha watu wanaompenda wawe wakamilifu kama alivyokusudia alipowaumba wanadamu. (Waroma 5:12; 6:23) Anaona matokeo mazuri ya kazi yake—mamilioni ya watu wamevutwa kwenye ibada ya kweli. Yesu alisema: “Baba yangu anaendelea kufanya kazi mpaka sasa, na mimi ninaendelea kufanya kazi.” (Yohana 5:17) Ili tuwe na furaha ni muhimu tuwatumikie wengine. (Matendo 20:35) Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli hawaketi kitako tu na kungojea. Badala yake, wanaendelea kuwasaidia wengine kujifunza kuhusu kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu.

Nyakati zote, watu waaminifu wamekuwa wakimsifu Mungu huku wakingojea wakati wake wa kuchukua hatua. Kwa mfano, mfikirie mtunga-zaburi Daudi. Daudi aliteswa na mfalme wake, akasalitiwa na rafiki yake wa karibu, na kusalitiwa na mwana wake. Katika kila moja ya hali hizo, je, Daudi angeweza kuwa mwenye furaha huku akimngojea Yehova amwokoe kwa wakati Wake? Zaburi ya 71, ambayo inaelekea iliandikwa na Daudi, inasema: “Lakini mimi, nitangoja daima, nami nitaongezea sifa zako zote. Kinywa changu mwenyewe kitasimulia uadilifu wako, wokovu wako mchana kutwa.” (Zaburi 71:14, 15) Badala ya kungojea akiwa ameudhika, Daudi alishangilia kwa sababu aliendelea kumsifu Yehova kwa bidii na kuwaimarisha wengine katika ibada ya kweli.—Zaburi 71:23.

Kumngojea Yehova si kama kungojea kwa hasira basi lililochelewa. Kunalingana sana na jinsi wazazi wanavyongojea kwa shangwe mtoto wao akue na kuwa mtu mzima ambaye wanaweza kujivunia. Wanakuwa na shughuli nyingi katika miaka hiyo ya kungojea. Ili watimize mradi wao, wanamzoeza, wanamfundisha, na kumtia mtoto nidhamu. Vivyo hivyo, sisi ambao tunamngojea Yehova tunapata furaha kwa kuwasaidia wengine wamkaribie Mungu. Sisi pia tunataka kupata kibali cha Mungu na mwishowe, kupata wokovu.

Bila Kupoteza Tumaini

Kumngojea Yehova kunamaanisha kuendelea kumpenda na kumtumikia bila kupoteza tumaini letu. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo. Watumishi wengi wa Mungu leo wanaishi miongoni mwa watu wanaowadhihaki wale wanaoishi maisha yanayotegemea imani katika ahadi za Mungu. Hata hivyo, fikiria mfano wa Waisraeli waaminifu waliodumisha tumaini lao katika ile miaka 70 ya uhamisho huko Babiloni. Ni nini kilichowasaidia kudumisha tumaini lao? Hapana shaka kwamba kusoma Zaburi kuliwaimarisha. Zaburi moja yenye kutia moyo ambayo huenda ilikuwa imeandikwa kufikia wakati huo inasema: “Neno lake nimelingojea. Nafsi yangu imemngojea Yehova kuliko walinzi wanavyoingojea asubuhi, ambao wanaingojea asubuhi. Israeli na aendelee kumngojea Yehova.”—Zaburi 130:5-7.

Wayahudi waliodumisha tumaini lao kwa kusoma na kuzungumza kuhusu tumaini hilo walithawabishwa Babiloni liliposhindwa na wavamizi. Upesi, maelfu ya Wayahudi waaminifu walifunga safari kwenda Yerusalemu. Kuhusu wakati huo, imeandikwa hivi: “Yehova alipowakusanya tena mateka wa Sayuni, . . . kinywa chetu kilijaa kicheko.” (Zaburi 126:1, 2) Wayahudi hao hawakupoteza tumaini lao. Badala yake waliendelea kuimarisha imani yao. Na hawakuacha kamwe kuimba sifa za Yehova.

Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli wanaomngojea Mungu katika “umalizio wa mfumo wa mambo” wanajitahidi daima kudumisha imani yao. Wanajifunza Neno la Mungu, wanatiana moyo, na wanaendelea kumsifu Yehova kwa kuhubiri habari njema ya Ufalme wake.—Mathayo 24:3, 14.

Kungojea Ili Kufaidika na Nidhamu

Yeremia, nabii wa Mungu aliandika: “Ni jambo jema kwa mtu kuungojea, ndiyo, kimyakimya, wokovu wa Yehova.” (Maombolezo 3:26) Yeremia alimaanisha kwamba haingefaa watumishi wa Mungu walalamike kuhusu jinsi Yehova alivyowatia nidhamu alipoacha jiji la Yerusalemu liharibiwe. Badala yake, walipaswa kufaidika kutokana na mambo yaliyowapata kwa kufikiria kutotii kwao na uhitaji wa kubadili mtazamo wao.—Maombolezo 3:40, 42.

Faida tunayopata tunapotiwa nidhamu na Yehova inaweza kulinganishwa na jinsi tunda linavyokua na kukomaa. Biblia inasema hivi kuhusu nidhamu kutoka kwa Mungu: “Kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Kama vile tunda linavyohitaji wakati ili liive, ndivyo tunavyohitaji wakati ili kubadili mitazamo yetu na kuipatanisha na mazoezi yanayotolewa na Mungu. Kwa mfano, tukipoteza mapendeleo kutanikoni kwa sababu ya mwenendo fulani usiofaa, kumngojea Mungu kwa kupenda kutatuzuia tusivunjike moyo au kukata tamaa. Chini ya hali kama hizo, maneno haya ya Daudi ambayo yaliongozwa na roho yanatia moyo: “Kuwa chini ya hasira yake [Mungu] ni kwa muda kidogo tu, kuwa chini ya nia yake njema ni kwa muda wote wa maisha. Huenda kilio kikakaa wakati wa jioni, lakini asubuhi kuna vigelegele vya shangwe.” (Zaburi 30:5) Tukisitawisha mtazamo wa kungojea na tukifuata mashauri tunayopata kutoka katika Neno la Mungu na tengenezo lake, wakati wetu wa kupiga “vigelegele vya shangwe” utafika.

Kukomaa Kunachukua Wakati

Ikiwa wewe ni mdogo kwa umri au umebatizwa hivi karibuni, huenda ukatamani sana kupata mapendeleo katika kutaniko la Kikristo. Lakini wakati unahitajiwa ili mtu akomae kiroho na kuweza kutimiza mapendeleo kama hayo. Hivyo, tumia miaka yako ya kwanza ili kukua kiroho. Kwa mfano, miaka yako ya ujana ni kipindi kizuri cha kuisoma Biblia nzima, kusitawisha sifa za Kikristo, na kujifunza ustadi wa kufanya wanafunzi. (Mhubiri 12:1) Ukionyesha kwa unyenyekevu mtazamo wa kungojea, wakati wa Yehova wa kukupa mapendeleo zaidi utafika.

Kazi ya kufanya wanafunzi inahitaji subira pia. Kama vile mkulima anavyoendelea kutilia mbegu maji hadi Mungu anapoikuza, ndivyo ilivyo na kazi ya kufanya wanafunzi. (1 Wakorintho 3:7; Yakobo 5:7) Ili tuwasaidie wengine wawe na imani na wamthamini Yehova kutoka moyoni tunahitaji kujifunza nao Biblia kwa subira kwa miezi au hata miaka. Kumngojea Yehova kunatia ndani kustahimili, hata kama mwanzoni wanafunzi hawatendi kupatana na yale wanayojifunza. Ikiwa wanathamini hata kwa kadiri ndogo, huenda hilo likaonyesha kwamba wanakubali roho ya Yehova iwaongoze. Ukiwa na subira, huenda ukashangilia kuona Yehova akimsaidia mwanafunzi wako akue na kuwa mwanafunzi wa Kristo.—Mathayo 28:20.

Kuonyesha Upendo kwa Kungojea

Ili kuonyesha jinsi kungojea kunavyoweza kuwa tendo la upendo na la uhakika, fikiria hali ya dada mmoja Shahidi aliyezeeka ambaye anaishi katika jangwa la Andes, huko Amerika ya Kusini. Yeye na dada mwingine ndio Mashahidi pekee wa Yehova katika kijiji chao. Je, unaweza kuwazia jinsi wanavyongojea kwa hamu kutembelewa na Wakristo wenzao? Pindi moja, mwangalizi fulani wa mzunguko alipotea njia alipokuwa akienda kuwatembelea kwa mara ya kwanza. Ilimbidi arudi alikoanzia safari yake, na hivyo akachelewa kwa saa kadhaa. Usiku ulikuwa umesonga sana alipoona kijiji hicho kwa mbali. Kwa kuwa eneo hilo halikuwa na umeme, alishangaa kuona nuru fulani ikiangaza. Alifurahi kama nini alipofika kwenye kijiji hicho na kugundua kwamba nuru hiyo ilikuwa ya taa ya mafuta iliyoinuliwa na yule dada mzee! Dada huyo alikuwa na uhakika kwamba mwangalizi angekuja, na hivyo akaendelea kumngojea.

Tukiwa na subira kama dada huyo, tutafurahia kumngojea Yehova. Tuna hakika kwamba atatimiza ahadi zake. Na kama yule mwangalizi anayesafiri, tunawathamini wale wanaotungojea kwa upendo. Basi, haishangazi kwamba Mungu anawathamini wale wanaomngojea. Biblia inasema: “Yehova anawafurahia . . . wale wanaozingojea fadhili zake zenye upendo.”—Zaburi 147:11.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Watu wanaomsifu Mungu kwa bidii wanafurahia kumngojea Yehova