Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wessel Gansfort—“Mrekebishaji Aliyetangulia Marekebisho”

Wessel Gansfort—“Mrekebishaji Aliyetangulia Marekebisho”

Wessel Gansfort—“Mrekebishaji Aliyetangulia Marekebisho”

Luther, Tyndale, na Calvin ni majina yanayojulikana sana na wanafunzi wote wa yale Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti ambayo yalianza katika mwaka wa 1517. Lakini ni watu wachache tu wanaojua jina Wessel Gansfort. Wessel ameitwa “Mrekebishaji aliyetangulia Marekebisho.” Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu mwanamume huyo?

WESSEL alizaliwa mnamo 1419 katika mji wa Groningen huko Uholanzi. Katika karne ya 15, watu wachache tu ndio waliopata nafasi ya kwenda shule, lakini Wessel alienda shule. Ijapokuwa alifaulu sana katika masomo yake, ilimbidi kuacha shule akiwa na umri wa miaka tisa kwa sababu wazazi wake walikuwa maskini sana. Mambo yalimwendea vema mjane mmoja tajiri aliposikia kwamba Wessel ni mtoto mwenye akili, akajitolea kumlipia pesa za shule na kuwa mlezi wake. Hivyo, Wessel aliweza kuendelea na masomo yake. Baada ya muda, alipata Digrii ya Pili. Inaelekea kwamba baadaye alipata cheo cha kuwa mtaalamu wa theolojia.

Wessel alikuwa na hamu kubwa ya kupata ujuzi. Hata hivyo, katika siku zake kulikuwa na maktaba chache. Ijapokuwa mashini ya kuchapishia yenye herufi zinazopangwa ilivumbuliwa katika siku zake, bado vitabu vingi viliandikwa kwa mkono navyo viliuzwa kwa bei ya juu. Wessel alikuwa mmoja wa wasomi walioenda maktaba kwa maktaba na makao ya watawa kwa makao ya watawa, wakitafuta hati na vitabu vya zamani vilivyosahauliwa. Kisha, walizungumza pamoja kuhusu mambo waliyokuwa wamejifunza katika hati na vitabu hivyo. Alipata ujuzi mwingi na kujaza kitabu chake cha mfukoni habari nyingi sana alizonukuu kutoka katika vitabu vya zamani vya Kilatini na Kigiriki. Mara nyingi, wanatheolojia wengine walikuwa na mashaka kwa kuwa Wessel alijua mambo mengi sana ambayo hawakuwa wamewahi kusikia. Wessel aliitwa Magister Contradictionis, yaani, Bingwa wa Kupinga.

“Mbona Huniongozi kwa Kristo?”

Miaka 50 hivi kabla ya yale Marekebisho Makubwa, Wessel alikutana na Thomas à Kempis (karibu 1379-1471), ambaye anakubaliwa na wengi kuwa mtungaji wa kitabu maarufu kinachoitwa Kumwiga Kristo (De Imitatione Christi). Thomas à Kempis alikuwa mshiriki wa kikundi kilichoitwa Brethren of the Common Life, ambacho kilikazia uhitaji wa kuishi maisha ya kumcha Mungu. Kitabu cha masimulizi ya maisha ya Wessel kinasema kwamba Thomas à Kempis alimhimiza Wessel mara kadhaa amwombe msaada Maria mama ya Yesu. Wessel alimjibu hivi: “Mbona huniongozi kwa Kristo, ambaye kwa fadhili anawaalika watu wote ambao wamelemewa na mizigo waje kwake?”

Inasemekana kwamba Wessel alipinga wazo la kuwatawaza makasisi. Alipoulizwa kwa nini alikataa zoea la kunyolewa kabisa sehemu fulani ya nywele ili kutambuliwa kuwa kasisi, alijibu kwamba haogopi kunyongwa mradi tu nguvu zake za kufikiri ziwe timamu. Alikuwa akizungumzia uhakika wa kwamba makasisi waliotawazwa hawangeweza kushtakiwa mahakamani, na inaelekea kwamba kunyolewa huko kuliwaokoa makasisi wengi wasinyongwe! Wessel alipinga pia mazoea fulani ya kawaida ya kidini. Kwa mfano, alishutumiwa kwa kukataa kuamini miujiza ambayo ilielezwa katika kitabu kimoja maarufu cha siku zake, (Dialogus Miraculorum). Aliitikia kwa kusema hivi: “Ingekuwa afadhali kusoma Maandiko Matakatifu.”

“Tunajua Tu Kadiri Tunavyouliza”

Wessel alijifunza Kiebrania na Kigiriki na akawa na ujuzi mwingi wa maandishi ya Mababa wa mapema wa Kanisa. Inashangaza sana jinsi alivyopenda lugha za awali za Biblia kwa kuwa aliishi kabla ya Erasmus na Reuchlin. * Kabla ya Marekebisho Makubwa, si watu wengi waliojua Kigiriki: Huko Ujerumani, wasomi wachache tu ndio waliofahamu Kigiriki, na hakukuwa na vifaa vyovyote vya kujifunzia lugha hiyo. Baada ya jiji la Constantinople kuanguka mwaka wa 1453, inaelekea Wessel alikutana na watawa Wagiriki waliokimbilia Magharibi, na akajifunza kanuni za msingi za Kigiriki. Nyakati hizo, Kiebrania kilizungumzwa hasa na Wayahudi, na inaelekea kwamba Wessel alijifunza kanuni za msingi za Kiebrania kutoka kwa wageuzwa-imani Wayahudi.

Wessel aliipenda sana Biblia. Aliiona kuwa kitabu kilichoongozwa na roho ya Mungu naye aliamini kwamba vitabu vyote vilivyo katika Biblia vinapatana kabisa. Wessel aliamini kwamba ufafanuzi wowote wa mistari ya Biblia ulipaswa kupatana kabisa na mistari mingine na haungeweza kupotoshwa. Ufafanuzi wowote uliopotoshwa ungepaswa kuonwa kuwa uzushi. Mojawapo ya mistari aliyopenda ya Biblia ni Mathayo 7:7, unaosema: “Endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.” Kwa msingi wa mstari huo, Wessel alisadiki kabisa kwamba kuna faida ya kuuliza maswali, na akasema kuwa “tunajua tu kadiri tunavyouliza.”

Ombi Lenye Kushangaza

Mwaka wa 1473, Wessel alitembelea Roma. Akiwa huko, alikubaliwa kuongea na Papa Sixtus wa Nne, ambaye alikuwa papa wa kwanza kati ya mapapa sita ambao mwenendo wao mchafu sana mwishowe uliongoza kwenye Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti. Mwanahistoria Barbara W. Tuchman anasema kwamba Sixtus wa Nne alianzisha kipindi cha “kufuatia waziwazi na bila aibu faida za kibinafsi na mamlaka ya kisiasa.” Aliwashtua watu wote kwa kuwapendelea waziwazi watu wa jamaa yake. Mwanahistoria mmoja anaandika kwamba huenda Sixtus alitaka kufanya cheo cha papa kiwe cha kifamilia. Ni watu wachache tu waliothubutu kupinga matumizi hayo mabaya ya mamlaka.

Hata hivyo, Wessel Gansfort alikuwa tofauti. Siku moja Sixtus alimwambia Wessel hivi: “Mwanangu, omba chochote unachotaka nasi tutakupa.” Papo hapo Wessel akaomba hivi: “Baba mtakatifu, . . . kwa kuwa hapa duniani wewe ndiye uliye na cheo cha kuhani na mchungaji mkuu zaidi, naomba . . . utimize wajibu wako uliokwezwa sana kwa njia ambayo itamfanya Mchungaji Mkuu wa kondoo . . . atakapokuja, akuambie: ‘Vema, mtumwa mwema, ingia katika shangwe ya Bwana wako.’” Sixtus alimjibu kwamba huo ni wajibu wake na hivyo Wessel aombe jambo linalomhusu yeye mwenyewe. Wessel akajibu: “Ikiwa ndivyo, nipe Biblia ya Kigiriki na ya Kiebrania kutoka katika Maktaba ya Vatikani.” Papa alikubali ombi lake lakini akasema kuwa Wessel alitenda kwa upumbavu na kwamba angeomba afanywe kuwa askofu!

“Uwongo na Kosa”

Kwa kuwa kulikuwa na uhitaji mkubwa wa fedha za kujenga Kanisa la Sistine ambalo sasa linajulikana sana, Papa Sixtus alianzisha mpango wa kutoa msamaha kwa ajili ya wafu kwa watu ambao walikuwa tayari kulipia huduma hizo. Huduma hizo zilipendwa na wengi. Kitabu kimoja (Vicars of Christ—The Dark Side of the Papacy) kinasema: “Wajane na wazazi waliofiwa na watoto wao walitumia pesa zao zote wakijaribu kuwaondoa wapendwa wao Toharani.” Watu wa kawaida walifurahia kwa kuwa walisadiki kabisa kwamba papa anaweza kuhakikisha kuwa wapendwa wao ambao walikufa wanaenda mbinguni.

Hata hivyo, Wessel alisadiki kwamba Kanisa Katoliki, kutia ndani papa, halina uwezo wa kusamehe dhambi. Wessel alisema waziwazi kwamba msamaha uliotolewa na papa kwa pesa ni “uwongo na kosa.” Naye hakuamini kwamba ni lazima mtu aungame kwa kasisi ili asamehewe dhambi.

Wessel alitilia shaka pia wazo la kwamba papa ni mkamilifu. Alisema kwamba kwa kuwa mapapa wanafanya makosa, misingi ya imani ingekuwa dhaifu ikiwa watu wangetazamiwa kuwaamini mapapa sikuzote. Wessel aliandika: “Ikiwa makasisi wanakataa amri za Mungu na kuweka amri zao wenyewe zilizotungwa na wanadamu, . . . mambo wanayofanya na kuamuru ni ya ubatili.”

Wessel Atayarisha Njia kwa Ajili ya Yale Marekebisho Makubwa

Wessel alikufa mwaka wa 1489. Ingawa alipinga makosa fulani ya kanisa, aliendelea kuwa Mkatoliki. Hata hivyo, kanisa halikuwahi kumshutumu kuwa mzushi. Lakini, baada ya kifo chake, watawa fulani Wakatoliki wenye msimamo mkali walijaribu kuharibu maandishi yake kwa kuwa yalionekana hayapatani na mafundisho ya kanisa. Kufikia siku za Luther, jina la Wessel lilikuwa karibu kusahauliwa, hakuna hata moja ya maandishi yake yaliyokuwa yamechapishwa, na ni hati chache tu ambazo bado zilikuwapo. Maandishi ya kwanza ya Wessel yalichapishwa mwishowe kati ya mwaka wa 1520 na 1522. Yalitia ndani barua iliyoandikwa na Luther ambamo yeye mwenyewe alipendekeza maandishi ya Wessel.

Ingawa hakuwa mwanaharakati wa Marekebisho kama Luther, Wessel alipinga waziwazi makosa fulani yaliyoongoza kwenye Marekebisho Makubwa. Kwa kweli, katika kitabu kimoja (Cyclopedia cha McClintock na Strong), Wessel anasemwa kuwa “mtu muhimu zaidi kati ya Wajerumani waliotayarisha njia kwa ajili ya yale Marekebisho Makubwa.”

Luther alimwona Wessel kuwa mtu aliyemuunga mkono. Mtungaji wa vitabu C. Augustijn, anaandika hivi: “Luther analinganisha siku zake na mambo yaliyompata na kisa cha Eliya. Kama vile nabii huyo alivyofikiri kwamba ni yeye tu aliyebaki ili kupigana vita vya Mungu, ndivyo Luther alivyohisi kwamba yuko peke yake katika mapambano dhidi ya kanisa. Baada ya kusoma maandishi ya Wessel, aligundua kwamba Bwana aliokoa ‘mabaki katika Israeli.’” “Luther hata anasema hivi waziwazi: ‘Ikiwa ningesoma maandishi yake mapema, maadui wangu wangefikiri kwamba nilijifunza mambo yote kutoka kwa Wessel, maoni yake yanafanana sana na yangu.’” *

“Mtapata”

Marekebisho Makubwa hayakutokea ghafula tu. Kwa muda fulani mawazo yaliyoongoza kwenye marekebisho hayo yalikuwa yakitolewa. Wessel alitambua kwamba mwishowe kushuka kwa maadili ya mapapa kungewafanya watu watake marekebisho. Wakati fulani alimwambia mwanafunzi mmoja hivi: “Mvulana mwenye bidii ya kujifunza, wakati utafika ambapo utaona mafundisho ya . . . wanatheolojia wabishi yakikataliwa na wasomi wote walio Wakristo wa kweli.”

Ingawa Wessel alitambua makosa fulani na mazoea ya ufisadi katika siku zake, hakuweza kufunua nuru kamili ya kweli ya Biblia. Lakini kulingana na maoni yake, Biblia ni kitabu ambacho watu wanapaswa kusoma na kujifunza. Kulingana na kitabu kimoja (A History of Christianity), Wessel “aliamini kwamba, kwa kuwa Biblia imeongozwa na Roho Takatifu, ndiyo inayotoa kauli ya mwisho katika masuala ya imani.” Katika ulimwengu wa leo, Wakristo wa kweli wanaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Timotheo 3:16) Hata hivyo, kweli za Biblia zinapatikana kwa urahisi leo na hazijafichika. Leo, zaidi ya wakati mwingine wowote, kanuni hii ya Biblia imethibitika kuwa ya kweli: “Endeleeni kutafuta, nanyi mtapata.”—Mathayo 7:7; Methali 2:1-6.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Wanaume hawa walisaidia sana katika uchunguzi wa lugha za awali za Biblia. Mwaka wa 1506, Reuchlin alichapisha sarufi yake ya Kiebrania, ambayo iliongoza kwenye uchunguzi wa ndani zaidi wa Maandiko ya Kiebrania. Erasmus alichapisha maandishi yaliyochunguzwa kwa makini ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika mwaka wa 1516.

^ fu. 21 Wessel Gansfort (1419-1489) and Northern Humanism, ukurasa wa 9, 15.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

WESSEL NA JINA LA MUNGU

Kwa ujumla, jina la Mungu limetafsiriwa kuwa “Johavah” katika maandishi ya Wessel. Hata hivyo, Wessel alitumia “Jehovah” angalau mara mbili. Akizungumzia maoni ya Wessel, mtungaji wa vitabu H. A. Oberman anakata kauli kwamba Wessel alihisi kwamba ikiwa Thomas Aquinas na wengine wangejua Kiebrania, “wangegundua kwamba jina la Mungu lililofunuliwa kwa Musa halimaanishi ‘Mimi ndimi niliye,’ lakini ‘Nitakuwa kile nitakachokuwa.’” * Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatoa maana sahihi “Nitakuwa kile nitakachokuwa.”—Kutoka 3:13, 14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 30 Wessel Gansfort (1419-1489) and Northern Humanism, ukurasa wa 105.

[Hisani]

Manuscript: Universiteitsbibliotheek, Utrecht

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wessel alishutumu zoea lililokubaliwa na Papa Sixtus wa Nne la kutoa msamaha kwa ajili ya wafu kwa malipo