Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuelewa Kusudi la Nidhamu

Kuelewa Kusudi la Nidhamu

Kuelewa Kusudi la Nidhamu

NI NINI huja akilini unaposikia neno “nidhamu”? Neno nidhamu hufafanuliwa kuwa desturi ya kuwafanya watu watii sheria au kanuni za mwenendo, na kuwaadhibu wasipofanya hivyo. Ingawa huu sio ufafanuzi pekee wa neno nidhamu, leo watu wengi wana maoni yasiyofaa kuelekea jambo lolote linalohusu nidhamu.

Hata hivyo, Biblia ina maoni tofauti kuhusu nidhamu. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika: “Ewe mwanangu, usikatae nidhamu ya Yehova.” (Mithali 3:11, NW) Maneno hayo hayamaanishi nidhamu kwa ujumla, bali “nidhamu ya Yehova,” yaani, nidhamu inayotegemea kanuni za juu za Mungu. Nidhamu hiyo tu ndiyo yenye matokeo, yenye kunufaisha kiroho, na hata yenye kupendeza. Tofauti na hilo, mara nyingi nidhamu inayotegemea maoni ya wanadamu ambayo inapingana na kanuni za juu za Yehova huwa kali na yenye kudhuru. Jambo hilo linaonyesha kwa nini wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu nidhamu.

Kwa nini tunahimizwa tukubali nidhamu ya Yehova? Katika Maandiko, nidhamu ya Mungu inafafanuliwa kuwa wonyesho wa upendo wa Mungu kwa ajili ya wanadamu ambao ni viumbe vyake. Kwa hiyo, Sulemani aliendelea kusema: “Yeye ambaye Yehova anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.”—Mithali 3:12, NW.

Kuna Tofauti Gani Kati ya Nidhamu na Adhabu?

Nidhamu inayotajwa katika Biblia inatia ndani mambo mengi—mwongozo, maagizo, mafundisho, karipio, rekebisho, na hata adhabu. Hata hivyo, katika kila kisa, nidhamu ya Yehova hutolewa kwa upendo, na lengo lake huwa ni kumnufaisha mtu anayepewa nidhamu. Nidhamu ambayo Yehova hutoa ili kurekebisha, haitolewi kamwe kwa kusudi la kuadhibu tu.

Kwa upande mwingine, sikuzote adhabu ya Mungu haikusudiwi kurekebisha au kuelimisha mtu anayeadhibiwa. Kwa mfano, mara tu Adamu na Hawa walipotenda dhambi, walianza kuteseka kutokana na kutotii kwao. Yehova aliwafukuza kutoka katika bustani ya Edeni iliyokuwa paradiso, nao wakapatwa na matokeo mabaya ya kutokamilika, ugonjwa, na kuzeeka. Baada ya kuteseka kwa mamia ya miaka, mwishowe waliangamia milele. Kwa kweli, yote hayo yalikuwa adhabu ya Mungu, bali si nidhamu iliyokusudiwa kurekebisha. Kwa kuwa Adamu na Hawa walitenda dhambi kimakusudi na hawakutubu, haikuwezekana kuwarekebisha.

Masimulizi mengine kuhusu adhabu ya Yehova yanatia ndani Gharika ya siku za Noa, uharibifu wa Sodoma na Gomora, na kuangamizwa kwa jeshi la Misri katika Bahari Nyekundu. Adhabu hiyo ya Yehova haikukusudiwa kutoa mwongozo, maagizo, au mafundisho kwa watu hao waliohusika. Mtume Petro aliandika hivi kuhusu adhabu hiyo ya Mungu: “Hakuacha kuadhibu ulimwengu wa kale, bali alitunza salama Noa, mhubiri wa uadilifu, pamoja na wengine saba alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasioogopa Mungu; na kwa kugeuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu aliyahukumia adhabu, akiweka kiolezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yajayo.”—2 Petro 2:5, 6.

Ni katika maana gani adhabu hiyo ‘iliweka kiolezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yajayo’? Katika barua yake kwa Wathesalonike, Paulo anataja siku zetu kuwa wakati ambao Mungu, kupitia Mwana wake Yesu Kristo, ataleta “kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” Paulo anaongeza kusema: “Hawahawa watapatwa na adhabu ya kihukumu ya uharibifu udumuo milele.” (2 Wathesalonike 1:8, 9) Ni wazi kwamba adhabu hiyo haikukusudiwa kufundisha wala kurekebisha wenye kuipokea. Hata hivyo, Yehova anapowasihi waabudu wake waikubali nidhamu yake, yeye hamaanishi wakubali adhabu ya watenda dhambi wasiotubu.

Ni jambo la maana kutambua kwamba Biblia haimtaji Yehova kuwa mtoa-adhabu tu. Badala yake, mara nyingi inamtaja kuwa mwalimu mwenye upendo na mfundishaji mwenye subira. (Ayubu 36:22; Zaburi 71:17; Isaya 54:13) Naam, nidhamu ya Mungu inayotolewa kwa kusudi la kurekebisha, sikuzote huambatana na upendo na subira. Wakristo wanapoelewa kusudi la nidhamu, wataweza kuikubali na kuitoa wakiwa na mtazamo unaofaa.

Nidhamu ya Wazazi Wenye Upendo

Katika familia na katika kutaniko la Kikristo, wote wanahitaji kuelewa kusudi la nidhamu, hasa wale wenye madaraka, kama vile wazazi. Andiko la Mithali 13:24, NW, linasema: “Anayezuia fimbo yake anamchukia mwana wake, lakini anayempenda ni yule anayemwangalia kwa nidhamu.”

Wazazi wanapaswa kutoa nidhamu kwa njia gani? Biblia inasema: “Nanyi, akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Shauri hilo linarudiwa katika maneno haya: “Nyinyi akina baba, msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.”—Wakolosai 3:21.

Wazazi Wakristo wanaoelewa kusudi la nidhamu hawatakuwa wakali. Kanuni inayotajwa katika 2 Timotheo 2:24 inaweza kutumiwa kuhusiana na jinsi wazazi wanavyotoa nidhamu. Paulo aliandika: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali ahitaji kuwa mwanana kuelekea wote, mwenye sifa za ustahili kufundisha.” Bila shaka, hasira nyingi isiyozuiwa, kusema kwa sauti kubwa, na matusi au maneno yenye kutia aibu si nidhamu ya upendo, nao Wakristo hawapaswi kuyatumia kamwe.—Waefeso 4:31; Wakolosai 3:8.

Rekebisho la wazazi linahusisha mengi zaidi ya adhabu inayotolewa haraka-haraka pasipo kusita. Watoto wengi wanahitaji kushauriwa mara kadhaa kabla ya kurekebisha maoni yao. Hivyo, wazazi wanapaswa kutumia wakati, kuwa wenye subira, na kufikiria kwa makini jinsi wanavyotoa nidhamu. Ni lazima wakumbuke kwamba watoto wanapaswa kulelewa katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” Mafundisho hayo huendelea kwa miaka mingi.

Wachungaji Wakristo Hutoa Nidhamu kwa Upole

Kanuni hizohizo zinawahusu pia wazee Wakristo. Wakiwa wachungaji wenye upendo wao hujitahidi kuliimarisha kundi kwa kutoa maagizo, mwongozo, na karipio inapohitajika. Wanapotoa nidhamu wanakumbuka kusudi hasa la nidhamu. (Waefeso 4:11, 12) Ikiwa watakazia tu fikira kutoa adhabu, watakuwa wamemwadhibu tu mkosaji bila kumsaidia. Nidhamu ya Mungu inahusisha mengi zaidi. Kwa kuchochewa na upendo, wazee huendelea kumsaidia mkosaji. Kwa kuwa wanalijali kundi kikweli, mara nyingi wao hutumia pindi mbalimbali kuwatia moyo na kuwafundisha wakosaji.

Kulingana na shauri linalopatikana katika 2 Timotheo 2:25, 26, hata wanaposhughulika na wale wasiokubali nidhamu kwa urahisi, wazee wanapaswa kufundisha “kwa upole.” Kisha andiko hilo linataja kusudi la nidhamu: “Huenda Mungu akawapa toba inayoongoza kwenye ujuzi sahihi juu ya kweli, nao wapate kurudiwa na fahamu zao nzuri kutoka katika mtego wa Ibilisi.”

Wakati mwingine, inakuwa lazima kuwatenga na ushirika wa kutaniko wakosaji wasiotubu. (1 Timotheo 1:18-20) Hata hatua hiyo kali inapaswa kuonwa kuwa nidhamu, wala si adhabu tu. Mara kwa mara, wazee hujitahidi kuwatembelea watu waliotengwa na ushirika ambao hawaendelei kutenda mambo mabaya. Wanapowatembelea, wazee hutenda kulingana na kusudi hasa la nidhamu kwa kuonyesha hatua ambazo mtu huyo anapaswa kuchukua ili kurudi katika kutaniko la Kikristo.

Yehova Ndiye Hakimu Mkamilifu

Wazazi, wachungaji Wakristo, na wengine walio na mamlaka ya Kimaandiko ya kutoa nidhamu wanapaswa kuchukua daraka hilo kwa uzito. Hawapaswi kukata kauli kimbele kwamba wengine hawawezi kurekebika. Kwa hiyo, nidhamu wanayotoa haipaswi kamwe kuwa adhabu kali au ya kulipiza kisasi.

Naam, Biblia humtaja Yehova kuwa ndiye atakayetoa adhabu kali na ya mwisho. Kwa kweli, Biblia husema kwamba “ni jambo lenye kuhofisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai.” (Waebrania 10:31) Lakini hakuna mwanadamu yeyote anayepaswa kujaribu kujilinganisha na Yehova kwa kutoa adhabu kali au katika njia nyingine yoyote. Na hakuna mtu yeyote anayepaswa kuhisi kwamba ni jambo lenye kuhofisha kuanguka katika mikono ya mzazi au mzee fulani kutanikoni.

Yehova ana uwezo wa kuonyesha usawaziko kwa njia kamilifu anapotoa nidhamu. Wanadamu hawawezi. Mungu anaweza kusoma mioyo na kutambua wakati mtu amefikia hatua ya kutoweza kurekebishwa na hivyo kustahili kupata adhabu ya mwisho kabisa. Kwa upande mwingine, wanadamu hawana uwezo wa kutoa hukumu kama hiyo. Kwa sababu hiyo, inapokuwa lazima kutoa nidhamu, sikuzote wale walio na mamlaka wanapaswa kufanya hivyo wakiwa na kusudi la kumrekebisha mkosaji.

Kukubali Nidhamu ya Yehova

Sote tunahitaji nidhamu ya Yehova. (Mithali 8:33) Kwa kweli, tunapaswa kutamani nidhamu inayotegemea Neno la Mungu. Tunapojifunza Neno la Mungu, tunaweza kukubali nidhamu inayotoka moja kwa moja kwa Yehova kupitia Maandiko. (2 Timotheo 3:16, 17) Hata hivyo, nyakati nyingine, tutapokea nidhamu kutoka kwa Wakristo wenzetu. Tunapotambua kusudi hasa la kutolewa kwa nidhamu hiyo, itakuwa rahisi kwetu kuikubali.

Mtume Paulo alikiri hivi: “Kweli, hakuna nidhamu ionekanayo kwa wakati wa sasa kuwa yenye shangwe, bali yenye kihoro.” Kisha akaongeza kusema: “Lakini baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo hutoa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Waebrania 12:11) Nidhamu ya Yehova ni wonyesho wa upendo wake mwingi kwetu. Iwe tunapokea au tunatoa nidhamu, na tukumbuke kusudi la nidhamu ya Mungu na kutii shauri hili la Biblia la hekima: “Shika nidhamu; usiiache. Ilinde, kwa maana hiyo ndiyo uzima wako.”—Mithali 4:13, NW.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Watenda dhambi wasiotubu hupokea hukumu ya adhabu ya Mungu, wala si nidhamu ya kuwarekebisha

[Picha katika ukurasa wa 22]

Kwa kuchochewa na upendo, wazee hutumia wakati mwingi kufanya utafiti na kusaidia wakosaji

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa subira na upendo wazazi hutoa “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”