Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwavuta Wanyenyekevu Kuijua Kweli

Yehova Huwavuta Wanyenyekevu Kuijua Kweli

Simulizi la Maisha

Yehova Huwavuta Wanyenyekevu Kuijua Kweli

LIMESIMULIWA NA ASANO KOSHINO

Katika mwaka wa 1949, miaka michache tu baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kwisha, mtu mmoja kutoka nchi ya kigeni, aliyekuwa mrefu na mwenye urafiki, alitembelea familia iliyokuwa imeniajiri kazi huko Kobe City. Alikuwa mishonari wa kwanza kabisa wa Mashahidi wa Yehova kuja Japani. Ziara yake ilinisaidia kusikia kweli ya Biblia. Acheni kwanza niwaeleze kuhusu malezi yangu.

NILIZALIWA mwaka wa 1926 katika kijiji kidogo huko kaskazini mwa Wilaya ya Okayama. Nilikuwa wa tano kati ya watoto wanane. Baba alikuwa muumini mwenye kujitoa kwa mungu wa hekalu la Shinto. Kwa hiyo tukiwa watoto tulifurahia miadhimisho na mikutano ya familia kwenye sherehe za kidini zilizofanywa kila mwaka.

Nilipokuwa nikikua, nilikuwa na maswali mengi kuhusu maisha, lakini nilitaka kujua sana kuhusu kifo. Kulingana na desturi ilikuwa lazima watu wafie nyumbani na watoto wawe karibu na kitanda cha mshiriki wa familia aliyekuwa karibu kufa. Nilihuzunika sana nyanya yangu alipokufa na wakati ndugu yangu alipokufa hata kabla hajafikisha umri wa mwaka mmoja. Nilivunjika moyo sana nilipofikiria kifo cha wazazi wangu. ‘Je, kweli kifo ndio mwisho wa mambo yote? Je, maisha yanaweza kuwa na maana zaidi?’ Nilitaka sana kujua mambo hayo.

Katika mwaka wa 1937, nilipokuwa darasa la sita kwenye shule ya msingi, vita kati ya Japani na China vilianza. Wanaume waliitwa jeshini na kupelekwa kwenye uwanja wa mapigano huko China. Watoto wa shule waliwaaga baba au ndugu zao, huku wakisema kwa sauti kubwa “banzai!” (yaani, maisha marefu) kwa maliki. Watu waliamini kwamba Japani, taifa lililotawaliwa na mungu, halingeweza kushindwa. Pia waliamini kwamba maliki wake, aliyekuwa mungu hai, hangeweza kushindwa.

Baada ya muda mfupi, familia zilianza kupokea habari kuhusu vifo kutoka uwanja wa mapigano. Watu wa familia zilizofiwa walikuwa na huzuni nyingi sana. Walianza kusitawisha chuki mioyoni mwao, na walifurahi waliposikia kwamba maadui wengi wameuawa au kuumizwa vibaya. Lakini wakati huohuo, nikawaza hivi, ‘Bila shaka maadui wetu wanateseka kama tunavyoteseka wapendwa wetu wanapokufa.’ Nilipomaliza shule ya msingi, vita vilikuwa vimeenea ndani kabisa katika nchi ya China.

Nakutana na Mtu Kutoka Nchi ya Kigeni Bila Kutarajia

Kwa kuwa tulikuwa wakulima, sikuzote familia yetu ilikuwa maskini, lakini baba aliniruhusu niendelee na masomo maadamu masomo hayo yangekuwa bila malipo. Kwa hiyo, katika mwaka wa 1941, nilijiunga na shule ya wasichana huko Okayama City, iliyoko umbali wa kilometa 100 hivi. Shule hiyo iliwaelimisha wasichana kuhusu jinsi ya kuwa wanawake na akina mama wema, nayo iliwapeleka wanafunzi kuishi na familia tajiri jijini ili wazoezwe kazi za nyumbani. Asubuhi wanafunzi walijifunza kwa kufanya kazi katika nyumba hizo, na alasiri wakaenda shuleni.

Baada ya sherehe ya kuwakaribisha wanafunzi wapya kumalizika, mwalimu wangu aliyekuwa amevaa kimono, alinipeleka kwenye nyumba fulani kubwa. Lakini kwa sababu fulani isiyojulikana, mke wa nyumba hiyo hakukubali nikae naye. “Je, twende nyumbani kwa Bi. Koda?” mwalimu huyo akauliza. Alinipeleka kwenye nyumba fulani iliyojengwa kwa mtindo wa nchi za magharibi na kufinya kengele ya mlango. Baada ya muda mfupi, mwanamke mrefu mwenye nywele za rangi ya fedha alitokea. Nilishangaa sana! Hakuwa Mjapani, na sikuwa nimewahi kuona Mzungu maishani. Mwalimu huyo alinijulisha kwa Bi. Maud Koda na kuondoka haraka. Nilikokota mifuko yangu, na kuingia ndani ya nyumba hiyo nikiwa na wasiwasi. Baadaye nilifahamu kwamba Bi. Maud Koda alikuwa Mmarekani aliyeolewa na mwanamume Mjapani ambaye alisomea Marekani. Alifundisha Kiingereza katika shule zinazofundisha mambo ya kibiashara.

Nilianza maisha yenye shughuli nyingi asubuhi iliyofuata. Mume wa Bi. Koda alikuwa na ugonjwa wa kifafa, na nilipaswa kusaidia kumtunza. Kwa kuwa sikujua Kiingereza chochote, nilikuwa na wasiwasi kidogo. Nilitulia sana wakati Bi. Koda alipozungumza nami kwa Kijapani. Kila siku niliwasikia wakizungumza Kiingereza, na hatua kwa hatua masikio yangu yakaanza kuzoea lugha hiyo. Nilifurahia hali nzuri katika nyumba hiyo.

Nilivutiwa na jinsi Maud alivyojitoa kumtunza mume wake mgonjwa ambaye alipenda kusoma Biblia. Baadaye nilipata kujua kwamba Maud na mume wake walikuwa wamepata chapa ya Kijapani ya kitabu The Divine Plan of the Ages kwenye duka la vitabu vilivyotumika na kwamba walikuwa wameandikisha gazeti la Kiingereza la Mnara wa Mlinzi kwa miaka kadhaa.

Siku moja nilipewa Biblia kama zawadi. Nilifurahi kwa sababu hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya kwanza kuwa na Biblia yangu mwenyewe maishani. Niliisoma nilipoenda na kurudi kutoka shuleni lakini sikuielewa sana. Kwa kuwa nililelewa katika dini ya Kijapani ya Shinto, sikumjua Yesu Kristo. Sikujua kwamba huo ulikuwa mwanzo wa matukio ambayo mwishowe yangeniongoza kuikubali kweli ya Biblia, ambayo ingejibu maswali yangu kuhusu maisha na kifo.

Matukio Matatu Yenye Kuhuzunisha

Miaka miwili niliyokuwa nikizoezwa kazi za nyumbani iliisha upesi na ikanibidi kuiaga familia hiyo. Baada ya kumaliza shule, nilijiunga na kikosi cha wasichana wa kujitolea nami nilishiriki kushona mavazi ya jeshi la wanamaji. Mashambulizi ya angani yaliyofanywa na ndege za Marekani aina ya B-29 yalianza, na Agosti 6, 1945, bomu la atomu likaangushwa huko Hiroshima. Siku chache baadaye, nilipokea ujumbe wa telegramu uliosema kwamba Mama alikuwa mgonjwa sana. Nilisafiri nyumbani kwa gari-moshi la kwanza kuondoka. Niliposhuka kutoka gari-moshi hilo, mtu mmoja wa ukoo alinilaki na kuniambia kwamba Mama alikuwa amekufa. Alikufa Agosti tarehe 11. Jambo nililokuwa nimeogopa kwa miaka mingi lilitukia! Mama hangeweza kutabasamu wala kuzungumza nami tena.

Agosti tarehe 15, Japani ilishindwa. Kwa hiyo, nilikabili matukio matatu yenye kuhuzunisha, yote katika muda mfupi wa siku kumi: la kwanza lilikuwa kulipuliwa kwa bomu la kwanza la atomu, kifo cha Mama, na kushindwa kwa Japani kulikokuwa muhimu kihistoria. Angalau nilifarijika kujua kwamba watu hawataendelea kufa vitani. Nikiwa na huzuni nyingi, niliacha kushona mavazi ya kijeshi na kurudi nyumbani kwetu mashambani.

Navutwa Kujifunza Kweli

Siku moja, nilipokea barua bila kutarajia kutoka kwa Maud Koda aliyekuwa anaishi Okayama. Aliniomba niende kwake nikamsaidie kazi za nyumbani, kwa kuwa alitaka kuanzisha shule ya kufundisha Kiingereza. Sikujua nifanyeje, lakini nilikubali mwaliko wake. Miaka michache baadaye, nilihamia Kobe pamoja na familia ya Koda.

Mapema mwaka wa 1949, mwanamume mmoja mrefu mwenye urafiki aliitembelea familia ya Koda. Aliitwa Donald Haslett, naye alikuwa amekuja Kobe kutoka Tokyo ili kutafutia mishonari nyumba. Yeye alikuwa mishonari wa kwanza kabisa wa Mashahidi wa Yehova kuja Japani. Alipata nyumba, na mnamo Novemba 1949, mishonari kadhaa wakaja Kobe. Siku moja, mishonari watano walikuja kuitembelea familia ya Koda. Wawili kati yao, Lloyd Barry na Percy Iszlaub, walitumia muda wa dakika kumi hivi kila mmoja wakizungumza kwa Kiingereza na wale waliokuwa katika nyumba hiyo. Mishonari hao walimwita Maud dada Mkristo na yaonekana alitiwa moyo na ushirika huo. Wakati huo ndipo nilipochochewa kujifunza Kiingereza.

Mishonari hao wenye bidii walinisaidia, na hatua kwa hatua nikaelewa kweli za msingi za Biblia. Nilipata majibu kwa maswali niliyokuwa nayo tangu utotoni. Naam, Biblia inatoa tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani na ahadi ya kufufuliwa kwa “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho.” (Yohana 5:28, 29; Ufunuo 21:1, 4) Nilimshukuru Yehova kwa kufanya iwezekane kuwa na tumaini hilo kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake Yesu Kristo.

Utendaji wa Kiroho Wenye Kufurahisha

Kuanzia Desemba 30, 1949, mpaka Januari 1, 1950, kusanyiko la kwanza nchini Japani lilifanywa kwenye makao ya mishonari ya Kobe. Nilienda huko pamoja na Maud. Ukiwa kwenye nyumba hiyo kubwa iliyokuwa ya askari mmoja wa Nazi, ungeweza kuona vizuri Kisiwa cha Awaji na Bahari Iliyo Katikati ya Visiwa. Kwa kuwa sikuifahamu sana Biblia, nilielewa mambo machache sana yaliyosemwa. Hata hivyo, nilivutiwa sana na mishonari waliochangamana kwa uhuru na Wajapani. Watu 101 walihudhuria hotuba ya watu wote kwenye kusanyiko hilo.

Muda mfupi baada ya hapo, niliamua kushiriki katika mahubiri. Nilihitaji ujasiri ili kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kuwa nilikuwa mwenye haya. Asubuhi moja, Ndugu Lloyd Barry alikuja nyumbani kwetu kunichukua ili twende kuhubiri pamoja. Alianza kuhubiri nyumba iliyokuwa karibu na ya Dada Koda. Nilikuwa karibu nimejificha kabisa nyuma yake huku nikisikiliza alipokuwa akihubiri. Mara ya pili nilienda kuhubiri na mishonari wengine wawili. Mwanamke mmoja Mjapani aliyekuwa mzee alitukaribisha na kutusikiliza, na baadaye akatupatia kila mmoja wetu glasi ya maziwa. Alikubali funzo la Biblia la nyumbani na mwishowe akabatizwa na kuwa Mkristo. Ilitia moyo kuona maendeleo aliyofanya.

Mnamo Aprili 1951, Ndugu Nathan H. Knorr, kutoka makao makuu ya Brooklyn alitembelea Japani kwa mara ya kwanza. Watu wapatao 700 walikuja kusikiliza hotuba ya watu wote aliyotoa kwenye Jumba la Kyoritsu huko Kanda, Tokyo. Kwenye mkutano huo wa pekee, wote waliohudhuria walifurahia kutolewa kwa chapa ya Kijapani ya gazeti Mnara wa Mlinzi. Mwezi uliofuata, Ndugu Knorr alitembelea Kobe, na kwenye mkutano huo wa pekee nilibatizwa ili kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova.

Mwaka mmoja hivi baadaye, nilitiwa moyo kuanza huduma ya wakati wote, yaani, utumishi wa painia. Wakati huo kulikuwa na mapainia wachache nchini Japani, na sikujua ningejitegemeza jinsi gani kifedha. Nilifikiria pia jinsi ambavyo mambo yangekuwa kuhusu matumaini yangu ya kuolewa. Lakini nilikuja kutambua kwamba jambo linalopaswa kutangulizwa maishani ni kumtumikia Yehova, kwa hiyo nikaanza upainia mwaka wa 1952. Jambo la kufurahisha ni kwamba niliweza kufanya kazi ya muda kwa Dada Koda huku nikifanya upainia.

Karibu wakati huo, ndugu yangu, ambaye nilifikiri alikuwa ameuawa vitani, alirudi nyumbani na familia yake kutoka Taiwan. Watu wa familia yetu hawakuwa wamewahi kupendezwa na Ukristo, lakini nikiwa na bidii wanayokuwa nayo mapainia, nilianza kuwatumia magazeti na vijitabu. Baadaye, ndugu yangu pamoja na familia yake walihamia Kobe kwa sababu ya kazi yake. “Je, umesoma magazeti niliyokutumia?” nikamwuliza mke wa ndugu yangu. Nilishangaa aliposema, “Ni magazeti mazuri.” Alianza kujifunza Biblia pamoja na mishonari mmoja, naye dada yangu mdogo aliyekuwa akiishi pamoja nao akajiunga na funzo hilo. Baada ya muda, wote wawili walibatizwa wakawa Wakristo.

Navutiwa na Undugu wa Ulimwenguni Pote

Baada ya muda mfupi, nilishangaa kupokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 22 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Mimi na Ndugu Tsutomu Fukase tulikuwa Wajapani wa kwanza kualikwa katika shule hiyo. Katika mwaka wa 1953, kabla ya darasa kuanza, tuliweza kuhudhuria Kusanyiko la Jamii ya Ulimwengu Mpya katika Uwanja wa Yankee huko New York. Nilivutiwa sana na undugu wa ulimwenguni pote wa watu wa Yehova.

Siku ya tano ya kusanyiko hilo, wajumbe kutoka Japani, hasa mishonari, walipaswa kuvaa kimono. Kwa kuwa kimono nilichokuwa nimetuma mapema hakikuwa kimefika, niliazima kimoja kutoka kwa Dada Knorr. Kusanyiko lilipokuwa likiendelea kulianza kunyesha, na nikawa na wasiwasi kwamba kimono kingelowa maji. Wakati huo, mtu fulani alinifunika kwa koti la mvua kutoka nyuma. Dada mmoja aliyekuwa amesimama kando yangu aliniuliza, “Je, unajua mtu huyo ni nani?” Baadaye niliambiwa kwamba alikuwa Ndugu Frederick W. Franz, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Nilihisi jinsi tengenezo la Yehova lilivyo na upendo!

Darasa la 22 la Gileadi lilikuwa la kimataifa kwelikweli kwa kuwa lilikuwa na wanafunzi 120 kutoka nchi 37. Ingawa nyakati nyingine haikuwa rahisi kuwasiliana kwa sababu tulizungumza lugha mbalimbali, tulifurahia kikamili undugu wa ulimwenguni pote. Siku moja yenye theluji mnamo Februari 1954, nilihitimu na kupokea mgawo wa kurudi Japani. Mwanadarasa mwenzangu, Inger Brandt, dada kutoka Sweden, ndiye angekuwa mwenzi wangu huko Nagoya City. Huko, tulijiunga na kikundi cha mishonari waliokuwa wamehamishwa kutoka Korea kwa sababu ya vita. Nilithamini sana miaka michache niliyotumikia nikiwa mishonari.

Kufurahia Utumishi Tukiwa Wenzi wa Ndoa

Mnamo Septemba 1957, nilialikwa kutumikia kwenye Betheli ya Tokyo. Ofisi ya tawi ya Japani ilikuwa nyumba ya mbao ya orofa mbili. Tulikuwa wanne tu katika ofisi hiyo ya tawi, kutia ndani Ndugu Barry, aliyekuwa mwangalizi wa tawi. Washiriki wale wengine wa Betheli walikuwa mishonari. Nilipewa mgawo wa kutafsiri na kusahihisha tafsiri, na pia kazi ya usafi, kufua nguo, kupika na kadhalika.

Kazi nchini Japani ilikuwa inapanuka, na ndugu zaidi walialikwa Betheli. Mmoja wao alikuwa mzee katika kutaniko langu. Katika mwaka wa 1966, mimi na ndugu huyo anayeitwa Junji Koshino, tulioana. Baada ya kuoana, Junji alipewa mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko. Tulifurahi kuwajua ndugu na dada wengi sana tulipotembelea makutaniko mbalimbali. Kwa kuwa nilikuwa nimepewa kazi ya kutafsiri, niliifanyia mahali tulipokuwa tukikaa kila juma. Tulipokuwa tukisafiri, ilitubidi kubeba kamusi nzito pamoja na sanduku letu na mifuko mingine.

Tulifurahia kazi ya kutembelea makutaniko kwa zaidi ya miaka minne na kuona tengenezo likizidi kukua. Ofisi ya tawi ilihamishiwa Numazu, na miaka kadhaa baadaye ikahamishiwa Ebina, mahali ilipo leo. Mimi na Junji tumefurahia utumishi wa Betheli kwa muda mrefu, na sasa tunafanya kazi pamoja na Wanabetheli wapatao 600. Mnamo Mei 2002, marafiki wangu wa Betheli walionyesha fadhili kwa kusherehekea mwaka wangu wa 50 katika utumishi wa wakati wote.

Nafurahi Kuona Ongezeko

Nilipoanza kumtumikia Yehova mwaka wa 1950, kulikuwa na wahubiri wachache tu nchini Japani. Sasa kuna watangazaji wa Ufalme zaidi ya 210,000. Kwa kweli, maelfu ya watu walio mfano wa kondoo wamevutwa kwa Yehova, kama nilivyovutwa.

Wale ndugu wanne mishonari na yule dada aliyetutembelea nyumbani kwa Dada Koda mwaka wa 1949, na vilevile Dada Maud Koda, wote walikufa wakiwa waaminifu. Ndugu yangu, aliyekuwa mtumishi wa huduma, na mke wa ndugu yangu aliyekuwa painia kwa miaka 15 hivi, wamekufa pia. Wakati ujao utakuwa na matumaini gani kwa wazazi wangu, ambao niliogopa kifo chao nilipokuwa mtoto? Ahadi ya Biblia ya ufufuo hunipa tumaini na faraja.—Matendo 24:15.

Ninapofikiria wakati uliopita, ninahisi kwamba badiliko muhimu lilitokea maishani mwangu nilipokutana na Maud mwaka wa 1941. Kama singalikutana naye wakati huo na kama singalikubali ombi lake kumfanyia kazi tena baada ya vita, labda ningaliendelea kuishi kwenye shamba letu katika kijiji cha mbali na singalikutana na mishonari siku hizo za mapema. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunivuta niijue kweli kupitia Maud na mishonari waliokuwa wa kwanza kuja Japani.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa pamoja na Maud Koda na mume wake. Mimi niko mbele upande wa kushoto

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikiwa pamoja na mishonari kutoka Japani kwenye Uwanja wa Yankee mwaka wa 1953. Mimi niko kushoto kabisa

[Picha katika ukurasa wa 28]

Nikiwa Betheli pamoja na mume wangu, Junji