Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hilo Ni Jambo Jipya!”

“Hilo Ni Jambo Jipya!”

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

“Hilo Ni Jambo Jipya!”

DOROTA, ambaye ni mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova nchini Poland, alimpeleka mwanawe mwenye umri wa miaka 14 kwenye kliniki ya shule ambapo wanafunzi hupimwa kwa ukawaida. Daktari, anayeitwa, Janina alipokuwa anampima, * alimwuliza Dorota kazi ambazo mwanawe hufanya nyumbani.

“Mwanangu hupika chakula kwa ajili ya familia yetu ya watu sita wakati ninaposhindwa kufanya hivyo,” Dorota akajibu. “Pia yeye husafisha nyumba na kusaidia kurekebisha vitu vilivyoharibika nyumbani. Anapenda kusoma naye ni mwanafunzi mwenye bidii.”

“Siamini,” akasema Janina. “Nimefanya kazi hapa kwa miaka 12, na sijawahi kusikia jambo kama hilo.”

Alipoona kwamba nafasi ya kutoa ushahidi ilikuwa imejitokeza, Dorota alisema: “Leo wazazi wengi hawawazoezi watoto wao ifaavyo. Ndiyo sababu mara nyingi watoto hao hukosa kujiheshimu.”

“Unajuaje mambo hayo yote?” Janina akauliza. “Wazazi wengi hawajui lolote kuhusu mambo hayo.”

“Biblia ni chanzo kizuri sana cha habari hizo,” Dorota akajibu. “Kwa mfano, andiko la Kumbukumbu la Torati 6:6-9, linaonyesha kwamba tunapaswa kujifundisha kwanza ili tuweze kuwafundisha watoto wetu. Je, haitupasi kwanza kukazia moyoni na akilini mwetu maadili tunayotaka kuwafundisha watoto wetu?”

“Siamini,” Janina akasema. Kisha akamwuliza Dorota jinsi Biblia ilivyomsaidia kuwalea na kuwafundisha watoto wake.

“Sisi hujifunza Biblia kila juma pamoja na watoto wetu,” Dorota akaeleza. “Tunatumia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.” * Kisha akamweleza kuhusu kitabu hicho na kutaja mambo mbalimbali kinachozungumzia.

“Hilo ni jambo jipya!” Janina akasema. “Ninaweza kukiona kitabu hicho?”

Muda wa saa moja baadaye, Dorota alimletea kitabu hicho.

“Wewe ni wa dini gani?” Janina akauliza, huku akichunguza kitabu hicho.

“Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”

“Mashahidi wa Yehova huwatendeaje watu wa dini nyingine?”

“Kwa heshima kama vile tu ninavyokutendea,” Dorota akajibu, kisha akaongeza kusema: “Bila shaka, tungependa wajue kweli ya Biblia.”

“Tayari mimi najihisi vizuri sana,” Janina akakiri.

Mwishoni mwa ziara yake, Dorota alimtia moyo Janina aisome Biblia. “Itafanya maisha yako yawe na kusudi na kukusaidia katika kazi yako.”

“Kwa kweli umenichochea kufanya hivyo,” Janina akakiri.

Kwa busara na ujasiri Dorota alitumia vizuri ziara ya kawaida kwa daktari kutoa ushahidi kwa njia inayofaa.—1 Petro 3:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Jina lake limebadilishwa.

^ fu. 10 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.