Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mtu Mzuri Hukubaliwa na Mungu’

“Mtu Mzuri Hukubaliwa na Mungu’

“Mtu Mzuri Hukubaliwa na Mungu’

YEHOVA Mungu ndiye chanzo cha uhai wote. (Zaburi 36:9) Naam, “kwa njia yake tuna uhai na twaenda na kuwako.” (Matendo 17:28) Je, mioyo yetu haijawi na shukrani tunapoona thawabu ambayo Yehova huwapa wale walio na uhusiano wa karibu pamoja naye? Kwa kweli, “zawadi ambayo Mungu hutoa ni uhai udumuo milele.” (Waroma 6:23) Ni muhimu kama nini kutafuta kibali cha Yehova!

Mtunga-zaburi anatuhakikishia kwamba ‘Mungu hutoa kibali.’ (Zaburi 84:11, NW) Lakini yeye humkubali nani? Leo, mara nyingi watu huwapendelea wengine kwa sababu ya elimu, utajiri, rangi ya ngozi, kabila, na kadhalika. Mungu humkubali nani? Mfalme Sulemani wa Israeli la kale anajibu: “Mutu mzuri atakubaliwa na BWANA; lakini atahukumu mutu mwenye mashauri maovu.”Mezali 12:2, Zaire Swahili Bible.

Bila shaka, Yehova hupendezwa na mtu mzuri—mtu mwenye wema wa adili. Mtu mzuri hudhihirisha wema wa adili kwa kujitia nidhamu, kutobagua wengine, kwa kuwa mnyenyekevu, mwenye huruma, na busara. Mawazo yake ni ya uadilifu, maneno yake yanatia moyo, nayo matendo yake ni ya haki na yenye kunufaisha. Sehemu ya kwanza ya sura ya 12 ya kitabu cha Biblia cha Mithali inatuonyesha jinsi wema unavyopaswa kutuathiri kila siku na manufaa ya kudhihirisha sifa hiyo. Kwa kuzingatia mambo yanayotajwa humo tutapata “akili na kutenda mema.” (Zaburi 36:3) Tutapata kibali cha Mungu kwa kufuata shauri hilo la hekima.

Nidhamu Ni Muhimu

“Kila apendaye mafundisho [“nidhamu,” “NW”] hupenda maarifa; bali yeye achukiaye kulaumiwa ni kama mnyama,” asema Sulemani. (Mithali 12:1) Mtu mwema hutamani kutiwa nidhamu kwa sababu anataka kujirekebisha. Yeye hutumia mara moja shauri analopata kwenye mikutano ya Kikristo au kutoka kwa wengine. Maandiko ya Biblia na maneno yaliyo katika vichapo vinavyozungumzia Biblia ni kama michokoo ambayo humwelekeza kwenye njia iliyonyooka. Yeye hutafuta ujuzi na kuutumia ili kunyoosha njia zake. Naam, mtu anayependa nidhamu, hupenda ujuzi pia.

Nidhamu ni muhimu kwa waabudu wa kweli—hasa tunapojitia nidhamu sisi wenyewe! Huenda tukatamani kuwa na ujuzi zaidi wa Neno la Mungu, kupata matokeo katika huduma yetu ya Kikristo, na kuwa walimu bora wa Neno la Mungu. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Lakini ili tutimize mambo hayo, tunahitaji kujitia nidhamu. Kujitia nidhamu kunahitajiwa pia katika maeneo fulani maishani. Kwa mfano, leo kuna habari nyingi sana zinazochochea tamaa mbaya. Je, hatuhitaji kujitia nidhamu ili tusitazame picha zisizofaa? Zaidi ya hayo, kwa kuwa “mawazo ya moyo wa mwanadamu ni mabaya tangu ujana wake,” basi mawazo machafu yanaweza kutoka katika sehemu ya ndani kabisa ya akili yetu. (Mwanzo 8:21) Kujitia nidhamu kunahitajiwa ili tusiendelee kufikiria mambo hayo.

Kwa upande mwingine, mtu anayechukia kukaripiwa, hapendi nidhamu wala ujuzi. Akiwa na mwelekeo wa kibinadamu wa kuchukia karipio, atafanana na mnyama asiyefikiri—asiyeweza kutofautisha mema na mabaya. Lazima tukatae kabisa mwelekeo huo.

“Mizizi Isiyoweza Kung’olewa”

Bila shaka, mtu mwema ni mwadilifu na hufuatia haki. Kwa hiyo sifa ya uadilifu ni muhimu ili kukubaliwa na Yehova. Mfalme Daudi aliimba hivi: “Maana Wewe utambariki mwenye haki; BWANA, utamzungushia radhi kama ngao.” (Zaburi 5:12) Akitofautisha hali ya mtu mwadilifu na mwovu, Sulemani asema: “Mtu hatathibitika kwa njia ya mwovu; shina la mwenye haki halitaondolewa kamwe.”Mithali 12:3.

Huenda waovu wakaonekana kana kwamba wamefanikiwa. Fikiria mfano wa mtunga-zaburi Asafu. Anasema: “Nami miguu yangu ilikuwa karibu na kupotoka, hatua zangu zilikuwa karibu na kuteleza.” Kwa nini? Asafu anajibu: “Niliwaonea wivu wenye kujivuna, nilipoona hali ya amani ya wasio haki.” (Zaburi 73:2, 3) Lakini alipokaribia patakatifu pa hekalu la Mungu, alitambua kwamba Yehova amewaweka mahali penye utelezi. (Zaburi 73:17, 18) Mafanikio ambayo huenda waovu wakapata ni ya muda tu. Hivyo basi, mbona tuwaonee wivu?

Kwa upande mwingine, mtu ambaye anakubaliwa na Mungu, yu imara. Akitumia mfano wa mti wenye mizizi imara, Sulemani anasema: “Watu wema wana mizizi isiyoweza kung’olewa.” (Mithali 12:3, The New English Bible) Mizizi isiyoonekana ya mti mkubwa sana kama ule uitwao sequoia ambao unapatikana huko California inaweza kusambaa kwa ekari kadhaa na kuwa ngome wakati wa mafuriko na pepo kali. Mti huo mkubwa hata unaweza kustahimili tetemeko kubwa la ardhi.

Kama mizizi hiyo inayopenya kwenye udongo ulio na rutuba, akili na mioyo yetu inapaswa kupenya katika Neno la Mungu na kutwaa maji ya uhai. Kwa hiyo imani yetu inakuwa thabiti na yenye nguvu, nalo tumaini letu linakuwa hakika na imara. (Waebrania 6:19) ‘Hatutachukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho lisilo la kweli.’ (Waefeso 4:14) Bila shaka, tutahisi matokeo ya majaribu makali na hata kuogopa wakati kunapotokea janga. Lakini ‘shina letu halitaondolewa.’

“Mwanamke Mwema Ni Taji ya Mumewe”

Inasemekana kwamba wanawake huchangia sana mafanikio ya waume zao. Akitaja thamani ya mke ambaye humwunga mkono mumewe, Sulemani anasema: “Mwanamke mwema [“mwenye uwezo,” “NW”] ni taji ya mumewe; bali aaibishaye ni kama kuoza mifupani mwake.” (Mithali 12:4) Usemi “mwenye uwezo” unajumlisha sifa nyingi nzuri. Sifa za mke mwema, kama zinavyofafanuliwa katika Mithali sura ya 31, zinatia ndani bidii, uaminifu, na hekima. Mke mwenye sifa hizo ni taji kwa mumewe kwa sababu mwenendo wake mzuri humletea mume wake heshima na sifa. Hashindani na mumewe kamwe ili apate umashuhuri. Badala yake, mke huyo anakuwa kikamilisho na msaidizi wa mumewe.

Mwanamke anawezaje kutenda kwa aibu, na matokeo yanakuwa nini? Mwenendo huo wa aibu huenda ukahusisha ugomvi na uzinzi. (Mithali 7:10-23; 19:13) Mwanamke anayetenda hivyo anamwangamiza tu mumewe. Yeye ni kama “kuoza mifupani mwake” katika maana ya kwamba “anamwangamiza, kama ugonjwa unaodhoofisha mifupa,” chasema kichapo fulani cha kitaalamu. “Tunaweza kutumia mfano wa kisasa wenye maana sawa na huo—‘ugonjwa wa kansa’—ambao humdhoofisha mtu polepole,” chasema kichapo kingine. Wake Wakristo na wajitahidi kupata kibali cha Mungu kwa kudhihirisha sifa za mke mwema.

Mawazo Huongoza Kwenye Matendo, Kisha Matokeo

Mawazo huongoza kwenye matendo, nayo matendo huongoza kwenye matokeo. Sulemani sasa anaonyesha jinsi mawazo huongoza kwenye matendo, akitofautisha wenye haki na waovu. Anasema: “Mawazo ya mwenye haki ni adili; bali mashauri ya mtu mwovu ni hadaa. Maneno ya waovu huotea damu; bali kinywa cha wanyofu kitawaokoa.”Mithali 12:5, 6.

Mawazo ya watu wema ni ya uadilifu nayo huwaongoza kutenda kwa njia ya haki bila ubaguzi. Nia ya wenye haki ni njema kwa kuwa wao huchochewa na upendo wao kwa Mungu na wanadamu wenzao. Kwa upande mwingine, waovu huchochewa na ubinafsi. Kwa hiyo, mbinu zao—njia wanazotumia kutimiza malengo yao—ni za udanganyifu. Matendo yao ni yenye hila. Hawasiti kuwawekea mtego watu wasio na hatia, labda mahakamani, kwa kuwasilisha mashtaka bandia. Maneno yao “huotea damu” kwa sababu wanataka kuwadhuru watu wasio na hatia. Wenye haki huepuka hatari hiyo kwa sababu wanafahamu mbinu za waovu na wana hekima ambayo huwasaidia kuwa chonjo. Hata wanaweza kuwaonya watu wasio waangalifu na kuwaokoa kutokana na mbinu za waovu.

Ni nini kitakachowapata wenye haki na waovu? “Waovu huangamia, hata hawako tena; bali nyumba ya mwenye haki itasimama,” ajibu Sulemani. (Mithali 12:7) Kichapo fulani cha kitaalamu kinasema kwamba nyumba “inamaanisha familia na kitu chochote chenye thamani cha mtu huyo, ambacho humwezesha kuishi.” Inaweza kumaanisha wazao wa mwenye haki. Vyovyote iwavyo, jambo linalotajwa na methali hiyo ni wazi: Mwenye haki atasimama imara wakati wa magumu.

Mtu Mnyenyekevu Atafanikiwa

Akikazia umuhimu wa ufahamu, mfalme wa Israeli anasema: “Mtu atasifiwa kwa kadiri ya akili zake [“kinywa chake cha busara,” “NW”]; bali mwenye moyo wa ukaidi atadharauliwa.” (Mithali 12:8) Mtu mwenye ufahamu hazungumzi haraka-haraka. Yeye hufikiri kabla ya kunena naye huwa na uhusiano mzuri na wengine kwa sababu “kinywa cha busara” hufanya achague maneno yake kwa uangalifu. Anapokabili mambo ya upuuzi au yenye kutilika shaka, mtu mwenye ufahamu anaweza ‘kuzuia maneno yake.’ (Mithali 17:27) Mtu huyo husifiwa naye humpendeza Yehova. Anatofautiana kama nini na mtu mwenye maoni yaliyopotoka ambayo hutoka katika ‘moyo uliopotoka’!

Naam, mtu mwenye busara husifiwa, lakini methali inayofuata inatufundisha umuhimu wa kuwa wanyenyekevu. Inasema: “Afadhali mtu anayedharauliwa, ikiwa ana mtumwa, kuliko ajisifuye, ikiwa anahitaji chakula.” (Mithali 12:9) Inaonekana Sulemani anasema kwamba ni afadhali kuwa na mali chache, kuwa na mtumishi mmoja tu, badala ya kujaribu kuishi maisha ya hali ya juu. Tunapata shauri zuri kama nini kwamba tuishi kulingana na uwezo wetu!

Maisha ya Mashambani Yanatufunza Wema

Kwa kutumia mfano wa maisha ya mashambani, Sulemani anatufunza mambo mawili kuhusu wema. “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake; bali huruma za mtu mwovu ni ukatili,” asema Sulemani. (Mithali 12:10) Mwenye haki hutendea wanyama wake kwa fadhili. Anafahamu mahitaji yao, naye hujali usalama wao. Huenda mtu mwovu akadai kwamba anajali wanyama, lakini hajali kikweli mahitaji yao. Ana nia ya ubinafsi, naye huwatendea vyema iwapo tu watamletea faida. Huenda mtu huyo akadhani kwamba anawatunza wanyama wake lakini kwa kweli anawatendea kikatili.

Kanuni ya kutendea wanyama kwa fadhili inatumika pia kuhusiana na utunzaji wa mnyama-kipenzi. Lingekuwa jambo la ukatili kama nini kuwa na mnyama-kipenzi na kumtesa isivyo lazima kwa kutomtimizia mahitaji yake au kumtesa! Iwapo mnyama anateseka sana kwa sababu ya ugonjwa au jeraha, lingekuwa jambo la fadhili kumwua mnyama huyo.

Akitumia mfano mwingine tena unaohusiana na maisha ya mashambani—Sulemani asema: “Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele.” Kwa kweli, kazi ngumu inayofaa huleta faida. “Bali afuataye mambo ya upuzi hana ufahamu.” (Mithali 12:11) Mtu asiye na busara au ufahamu, yaani ‘asiye na akili’ hufuatia biashara hatari lakini zinazoweza kuleta faida. Mistari hii inatufunza mambo mawili yaliyo wazi: Uwe mwenye rehema na mwenye bidii.

Mwenye Haki Husitawi

“Asiye haki hutamani nyavu za wabaya,” asema mfalme mwenye hekima. (Mithali 12:12a) Asiye haki hufanya hivyo jinsi gani? Hufanya hivyo kwa kutamani nyara iliyopatikana kwa njia isiyofaa.

Tunaweza kusema nini kuhusu mtu mwema? Anapenda nidhamu na ana imani yenye nguvu. Ni mwadilifu, mwenye busara, mnyenyekevu, mwenye huruma na bidii. Na “shina lao wenye haki huleta matunda,” au “husitawi” asema Sulemani. (Mithali 12:12b) “Mzizi wa mwenye haki utadumu milele,” yasema tafsiri ya An American Translation. Mtu wa namna hiyo ni imara na salama. Kwa kweli ‘mtu mzuri atakubaliwa na BWANA.’ Hivyo basi, na ‘tumtumaini BWANA tukatende mema.’—Zaburi 37:3.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kama mti imara, imani ya wenye haki ni yenye nguvu