Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” Wakusanyika kwa Shangwe

“Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” Wakusanyika kwa Shangwe

“Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii” Wakusanyika kwa Shangwe

MISUKOSUKO ya kiadili, kiuchumi, na kisiasa inautikisa ulimwengu. Hata hivyo, licha ya misukosuko yote hiyo, Mashahidi wa Yehova walikusanyika kwa amani kwa ajili ya Makusanyiko ya Wilaya ya “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii.” Makusanyiko hayo yalifanywa ulimwenguni pote kuanzia Mei 2002.

Makusanyiko hayo yalikuwa pindi zenye shangwe kwelikweli. Na tuangalie kwa ufupi programu hiyo yenye kujenga inayohusu Biblia.

Siku ya Kwanza Ilikazia Bidii ya Yesu

Kichwa cha habari cha siku ya kwanza ya kusanyiko kilikuwa “Iga Bidii ya Bwana Wetu, Yesu.” (Yohana 2:17) Hotuba “Shangilieni Kukusanyika Pamoja Mkiwa Watangazaji wa Ufalme” iliwakaribisha kwa uchangamfu wote waliohudhuria washiriki katika shangwe ambayo sikuzote imeonyeshwa katika makusanyiko ya watu wa Mungu. (Kumbukumbu la Torati 16:15) Baada ya hotuba hiyo, watangazaji wa habari njema wenye bidii walihojiwa.

Hotuba “Furahi Sana Katika Yehova” ilizungumzia Zaburi 37:1-11 mstari kwa mstari. Tulihimizwa ‘tusikasirike’ kwa sababu ya yale yanayoonekana eti kuwa mafanikio ya waovu. Ijapokuwa waovu huenda wakatusema vibaya, hatimaye Yehova ataonyesha ni nani hasa walio watu wake waaminifu. Hotuba “Jionyesheni Kuwa Wenye Shukrani” ilizungumzia jinsi tunavyoweza kumshukuru Mungu. Wakristo wote lazima wamtolee Yehova “dhabihu ya sifa.” (Waebrania 13:15) Ni dhahiri kwamba, kiwango cha wakati tunachotumia katika utumishi wa Yehova kinategemea shukrani zetu na hali zetu.

Hotuba ya msingi ilikuwa na kichwa “Watangazaji wa Ufalme Wachochewa na Bidii.” Ilikazia kuwa Yesu Kristo ndiye kielelezo chetu bora cha bidii. Baada ya Ufalme wa mbinguni kusimamishwa mwaka wa 1914, Wakristo wa kweli walihitaji bidii ili kutangaza hizo habari njema. Msemaji alitaja kusanyiko lililofanywa huko Cedar Point, Ohio, Marekani, mwaka wa 1922 na akatukumbusha ule mwito wa pekee: “Tangazeni Mfalme na Ufalme wake”! Hatimaye, bidii ya watumishi wa Mungu waaminifu iliwachochea kutangazia mataifa yote kweli za ajabu za Ufalme.

Hotuba “Msiogope kwa Maana Yehova Yu Pamoja Nasi,” iliyotolewa alasiri siku ya kwanza, ilionyesha kwamba Shetani hushambulia hasa watu wa Mungu. Hata hivyo, tujapopatwa na upinzani, kufikiria mifano mingi ya imani ya nyakati za Biblia na ya siku hizi hutupa ujasiri wa kukabiliana na majaribu tunayopata bila hofu.—Isaya 41:10.

Kisha programu hiyo ilifuata kwa mfululizo wa hotuba tatu chini ya kichwa “Unabii wa Mika Hutuimarisha Tutembee Katika Jina la Yehova.” Msemaji wa kwanza alilinganisha ukosefu wa maadili, uasi wa kidini, na ufuatiaji wa vitu vya kimwili katika siku za Mika na siku zetu. Alisema hivi: “Tutakuwa na tumaini hakika la wakati ujao iwapo tutasitawisha moyo mtiifu na kuhakikisha kwamba mwenendo wetu ni mtakatifu na tuna vitendo vya ujitoaji-kimungu—na tusiposahau kamwe kwamba siku ya Yehova itakuja.”2 Petro 3: 11, 12.

Msemaji wa pili katika mfululizo wa hotuba hizo alizungumzia hukumu aliyotangaza Mika kwa viongozi wa Yuda. Waliwaonea maskini, watu wasioweza kujitetea. Lakini Mika pia alitabiri ushindi wa ibada ya kweli. (Mika 4:1-5) Tukiwa tumetiwa nguvu na roho takatifu ya Yehova, tunaazimia kutangaza ujumbe huu wa tumaini na wenye kuburudisha. Lakini vipi tukihisi kwamba tumepungukiwa kwa sababu ya magonjwa au udhaifu fulani? Msemaji wa hotuba ya tatu alisema hivi: “Matakwa ya Yehova si ya kupita kiasi hata kidogo na vilevile wanadamu wanaweza kuyatimiza.” Aliendelea kuzungumzia sehemu mbalimbali za Mika 6:8, ambapo tunasoma hivi: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako?”

Kwa kuwa upotovu wa maadili katika ulimwengu huu unaweza kuathiri Wakristo, sisi sote tulinufaika na hotuba yenye kichwa “Dumisha Usafi wa Maadili kwa Kulinda Moyo Wako.” Kwa mfano, tukiendelea kuwa safi kiadili tutakuwa na ndoa yenye furaha. Tukiwa Wakristo, tusiwazie kamwe jinsi tunavyoweza kujiingiza katika mwenendo mchafu kingono.—1 Wakorintho 6:18.

Hotuba “Jilinde Dhidi ya Udanganyifu” ilionyesha kwamba tuwe na hekima na kuona kuwa sumu udanganyifu unaoenezwa na waasi-imani ambao hupotosha mambo, huwa na kweli nusu-nusu na uwongo wa waziwazi. (Wakolosai 2:8) Vivyo hivyo, tusijidanganye kamwe kwa kufikiria kwamba tunaweza kutosheleza tamaa zetu zenye dhambi bila matokeo mabaya.

Kichwa cha hotuba ya mwisho ya siku ya kwanza kilikuwa “Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli.” Hali ulimwenguni ziendeleapo kuwa mbaya zaidi, inachangamsha moyo kama nini kujua kwamba hivi karibuni Yehova ataleta ulimwengu wake mpya wenye uadilifu! Ni nani watakaoishi humo? Ni wale tu wanaomwabudu Yehova. Msemaji alitoa kitabu kipya cha kujifunza Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli ili kutusaidia sisi, pamoja na watoto wetu, na wanafunzi wetu wa Biblia kufikia mradi huo. Tulifurahi kama nini kukipokea!

Siku ya Pili Ilikazia Umaana wa Kuwa na Bidii kwa Lililo Jema

Kichwa cha habari cha siku ya pili kilikuwa “Iweni Wenye Bidii kwa Lililo Jema.” (1 Petro 3:13) Msemaji wa kwanza alizungumzia andiko la Biblia la siku hiyo. Alikazia kwamba kuyachunguza maandiko kila siku kwa makini na kwa ukawaida, huongeza bidii yetu.

Kisha ukafuata mfululizo wa hotuba “Watangazaji wa Ufalme Ambao Huitukuza Huduma Yao.” Sehemu ya kwanza ilikazia uhitaji wa kulitumia Neno la Mungu sawasawa. (2 Timotheo 2:15) Tunapotumia Biblia kwa matokeo, ‘nguvu’ yake inaweza kupenya katika maisha ya watu. (Waebrania 4:12) Twapaswa kuelekeza fikira kwenye Biblia na kuitumia kutoa sababu zenye kusadikisha. Hotuba ya pili katika mfululizo huo ilituhimiza tuwarudie tena na tena watu wenye kupendezwa. (1 Wakorintho 3:6) Kujitayarisha na ujasiri wahitajiwa ili kuwarudia bila kukawia watu wote wenye kupendezwa. Sehemu ya tatu ilipendekeza tumwone kila mtu tunayekutana naye kuwa anaweza kujifunza na ikaonyesha kwamba tunaweza kupata shangwe ya kuwasaidia watu wawe wanafunzi wa Biblia ikiwa tutawaeleza juu ya mpango wa funzo la Biblia katika ziara ya kwanza.

Kichwa cha hotuba iliyofuata kilikuwa “Kwa Nini ‘Tusali Bila Kukoma’?” Biblia huhimiza Wakristo watafute mwongozo wa Mungu katika maisha yao yote. Tunahitaji kupanga wakati wa kusali faraghani. Zaidi ya hilo, lazima tudumu katika sala, kwa kuwa huenda Yehova akaacha twendelee kusali kwa muda fulani kabla hajatujibu.—Yakobo 4:8.

Hotuba “Maongezi ya Kiroho Hujenga” ilituhimiza tutumie zawadi yetu ya usemi kujinufaisha wenyewe na wengine pia. (Wafilipi 4:8) Wenzi wa ndoa na watoto wanahitaji kuwa na maongezi ya kiroho kila siku. Ili wafanikiwe kuwa na mazungumzo yenye kujenga, familia zapaswa kujaribu kula angalau mlo mmoja pamoja kila siku.

Programu ya asubuhi ilimalizika kwa hotuba yenye kutia moyo “Jinsi ambavyo Wakfu na Ubatizo Huongoza Kwenye Wokovu.” Wale waliostahili kubatizwa walikuwa wamepata ujuzi, wakadhihirisha imani, wakatubu, wakageuka na kuacha njia mbaya, na kujiweka wakfu kwa Mungu. Msemaji aliwaambia kwamba walipaswa kuendelea kukua kiroho, kudumisha bidii yao, na mwenendo mzuri hata baada ya kubatizwa. —Wafilipi 2:15, 16.

Alasiri hiyo, mambo mawili makuu yalikaziwa katika hotuba “Uwe na Kiasi, na Kudumisha Jicho Lako Likiwa Sahili.” Kuwa na kiasi humaanisha kuwa na maoni yaliyosawazika kuhusu mambo tusiyoweza kufanya kwa sababu ya kupungukiwa au msimamo wetu mbele za Mungu. Kiasi hutusaidia tuweke jicho letu likiwa “sahili”—tukazie Ufalme wa Mungu, na si vitu vya kimwili. Tukifanya hivyo, hatuhitaji kuwa na wasiwasi, kwa kuwa Yehova atatimiza mahitaji yetu.—Mathayo 6:22-24, 33, 34.

Msemaji aliyefuata alionyesha ni kwa nini tunapaswa “[Ku]mtumaini Yehova Kikamili Katika Nyakati za Taabu.” Twaweza kukabilianaje na mambo kama vile udhaifu wetu na matatizo ya kiuchumi na ya kiafya? Na tumwombe Yehova atupatie hekima inayofaa na kuomba wengine msaada. Badala ya kuhofu au kukata tamaa, twapaswa kuimarisha tumaini letu katika Mungu kwa kusoma Neno lake.—Waroma 8:35-39.

Mfululizo wa hotuba wa mwisho katika kusanyiko hilo ulikuwa na kichwa “Ubora wa Imani yetu Wajaribiwa na Magumu Mbalimbali.” Sehemu ya kwanza ilitukumbusha kwamba Wakristo wote wa kweli hunyanyaswa. Mnyanyaso huo huwa ushahidi kwa wengine, huimarisha imani yetu, na hutupatia fursa ya kuonyesha uaminifu wetu kwa Mungu. Hata ingawa hatutaki kuhatarisha maisha yetu, hatungetumia njia isiyo ya Kimaandiko ili kuepuka mnyanyaso.—1 Petro 3:16.

Msemaji wa pili katika mfululizo wa hotuba hizo alizungumzia maswali yanayohusiana na msimamo wetu wa kutokuwamo. Wakristo wa awali hawakuwa wapinga-vita, lakini walitambua kwamba walipaswa kuwa waaminifu kwa Mungu. Vivyo hivyo leo, Mashahidi wa Yehova hushikilia kabisa kanuni hii: “Nyinyi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 15:19) Kwa kuwa majaribu ya kutokuwamo yanaweza kutokea upesi, familia zapaswa kupanga wakati wa kuchunguza mwongozo ambao Biblia inatoa kuhusu habari hiyo. Kama vile hotuba ya tatu ya mfululizo huo ilivyoonyesha, lengo la Shetani si kutuua, bali ni kutusonga ili tuache kuwa waaminifu kwa Mungu. Tutamletea Yehova sifa tukivumilia kwa uaminifu dhihaka, misongo ya kufanya mambo yasiyo ya adili, maumivu ya kihisia, na magonjwa.

Hotuba ya mwisho siku hiyo ilikuwa na mwaliko mchangamfu “Mkaribie Yehova.” Kuelewa sifa kuu za Yehova hutuvuta kwake. Yeye hutumia nguvu yake isiyo na kifani kulinda watu wake, hasa kiroho. Yeye haonyeshi sifa yake ya haki kwa ukali bali sifa hiyo humchochea kuwapa uhai wa milele wote wafuatao uadilifu. Hekima ya Mungu ni dhahiri katika njia ambayo alitumia wanadamu wasio wakamilifu kuandika Biblia. Upendo wake ambao ni wenye kuvutia zaidi, ulimchochea awape wanadamu wokovu kupitia Yesu Kristo. (Yohana 3:16) Msemaji alimalizia kwa kutoa kitabu kipya chenye kutia moyo Mkaribie Yehova.

Siku ya Tatu Ilikazia Bidii kwa Kazi Zilizo Bora

Kichwa cha habari cha siku ya tatu kilikuwa “Watu Wenye Bidii kwa Kazi Zilizo Bora.” (Tito 2:14) Kipindi cha asubuhi kilianza na familia moja ikizungumzia andiko la siku. Kisha ikafuata hotuba “Je, Unamfanya Yehova Kuwa Tumaini Lako?” Mataifa yamekosea kwa kutumaini hekima na nguvu zao wenyewe. Hata hivyo, tofauti na mataifa, watumishi wa Yehova humtegemea kwa ujasiri na shangwe licha ya misiba mbalimbali.—Zaburi 46:1-3, 7-11.

Hotuba yenye kichwa “Vijana—Pangeni Maisha Yenu ya Wakati Ujao Katika Tengenezo la Yehova” ilijibu swali hili: Kijana anawezaje kufaidika kabisa maishani? Hiyo haiwezekani kwa kutafuta fedha, mali, na umaarufu. Muumba wetu huwasihi vijana kwa upendo wamkumbuke wakiwa wangali vijana. Msemaji alihoji baadhi ya vijana ambao wamejitahidi katika utumishi wa Kikristo, na tuliweza kuona shangwe yao. Na ilinufaisha kama nini kupokea trakti mpya, Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu?, iliyokusudiwa kusaidia vijana Mashahidi waweke msingi wa wakati ujao wa milele katika tengenezo la Yehova!

Kisha ikafuata drama ya Biblia yenye kuvuta fikira “Simama Imara Katika Nyakati za Taabu.” Ilizungumzia kwa ufupi kazi ya muda mrefu ya Yeremia tangu ujana wake hadi wakati wa uharibifu wa Yerusalemu, ambao alikuwa ameutabiri kwa bidii. Yeremia alihisi kwamba hawezi kutimiza mgao wake, lakini aliutimiza ajapopingwa, naye Yehova alimwokoa.—Yeremia 1:8, 18, 19.

Drama hiyo ilifuatiwa na hotuba “Uwe Kama Yeremia—Tangaza Neno la Mungu Bila Woga.” Watangazaji wa Ufalme wa siku hizi hushambuliwa mara nyingi kupitia habari za uwongo zenye kudhuru. (Zaburi 109:1-3) Ingawa hivyo, kama Yeremia tunaweza kukabiliana na kivunja-moyo kwa kufurahia kusoma Neno la Yehova. Na tuna uhakika kwamba wale ambao wanapigana nasi hawatashinda.

Kwa kweli, hotuba ya watu wote ilitolewa kwa wakati unaofaa kabisa. Hotuba hiyo ilikuwa na kichwa “Mandhari ya Ulimwengu Huu Inabadilika.” Siku zetu zimekuwa na mabadiliko makubwa mno. Biblia ilitabiri kwamba hali kama hizo, kutia ndani kile kilio cha “amani na usalama,” zingeelekeza kwenye siku ya Mungu ya hukumu yenye kutisha. (1 Wathesalonike 5:3) Siku hiyo italeta mabadiliko mazuri ajabu—mwisho wa vita vyote, uhalifu, jeuri, na hata magonjwa. Badala ya kutumaini ulimwengu huu, sasa ndio wakati wa kufuatia ujitoaji-kimungu na kudumisha mwenendo safi.

Muhtasari wa funzo la Mnara wa Mlinzi la juma hilo ulifuatiwa na hotuba ya mwisho ya kusanyiko, yenye kichwa “Zidisheni Kazi Zilizo Bora Mkiwa Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii.” Msemaji alionyesha jinsi programu ilivyotuchochea kiroho na kututia moyo tumtegemee Yehova. Kwa kumalizia, tulihimizwa tuwe safi, wenye upendo, na watangazaji wa Ufalme wa Mungu wenye bidii.—1 Petro 2:12.

Kwa kweli tulirudi nyumbani tukiwa na roho kama ile ya watumishi wa Mungu katika siku za Nehemia, tukiwa na shangwe kwa sababu ya baraka za kiroho tulizopokea kwenye Makusanyiko ya Wilaya ya “Watangazaji wa Ufalme Wenye Bidii.” (Nehemia 8:12) Je, si kweli kwamba kusanyiko hilo lenye kuchochea limekujaza shangwe na azimio la kuendelea mbele ukiwa mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

Msaada Mpya wa Kujifunzia!

Kwenye umalizio wa siku ya kwanza ya kusanyiko, wahudhuriaji walifurahia kutolewa kwa kitabu kipya Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli. Kimekusudiwa kuwa kitabu cha kujifunza na wale ambao wamemaliza kujifunza kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kwa kweli kitaimarisha imani ya wale ‘walio na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele.’—Matendo 13:48.

[Hisani]

Image on book cover: U.S. Navy photo

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

Msaada wa Kumkaribia Mungu Zaidi

Msemaji wa mwisho katika siku ya pili ya kusanyiko alitangaza kutolewa kwa kitabu kipya Mkaribie Yehova. Kitabu hicho kina sehemu nne, na kila sehemu inazungumzia mojawapo ya sifa kuu za Yehova, yaani, nguvu, haki, hekima, na upendo. Kila sehemu ya kitabu hicho ina sura inayoonyesha jinsi ambavyo Yesu Kristo alionyesha waziwazi sifa za Mungu. Kusudi kuu la kitabu hiki ni kutusaidia sisi na wanafunzi wetu wa Biblia kuwa na uhusiano wa karibu na wenye nguvu zaidi pamoja na Yehova Mungu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26]

Mwongozo wa Kiroho kwa Vijana

Katika siku ya tatu ya kusanyiko, trakti ya pekee yenye kichwa Vijana—Mtatumiaje Maisha Yenu? ilitolewa. Trakti hii mpya inayokusudiwa kusaidia vijana Mashahidi wafanye maamuzi yanayofaa kuhusu wakati wao ujao, inawapa mashauri ya Kimaandiko kuhusu jinsi ya kufanya utumishi wa Yehova uwe kazi yao ya maisha.