Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kataa Maoni ya Ulimwengu

Kataa Maoni ya Ulimwengu

“Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu . . . [wa] ulimwengu.”—KOL. 2:8.

NYIMBO: 38, 31

1. Mtume Paulo aliwapa Wakristo wenzake shauri gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

HUENDA mtume Paulo aliandika barua yake kwa Wakristo Wakolosai mwishoni mwa kifungo chake cha kwanza jijini Roma katika mwaka wa 60-61 W.K. Aliwaeleza umuhimu wa kuwa na “utambuzi wa kiroho.” (Kol. 1:9) Paulo aliwaeleza hivi pia: “Ninasema jambo hili ili mtu yeyote asiwadanganye ninyi kwa hoja zenye kushawishi. Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.” (Kol. 2: 4, 8) Kisha Paulo akaeleza kwa nini baadhi ya maoni yanayopendwa na watu wengi si sahihi na kwa nini huenda maoni ya ulimwengu yakawavutia wanadamu wasio wakamilifu. Kwa mfano, huenda maoni hayo yakafanya mtu ajione kuwa mwenye hekima na bora kuliko wengine. Barua hiyo ilikusudiwa kuwasaidia akina ndugu kukataa maoni ya ulimwengu na mazoea mabaya.—Kol. 2:16, 17, 23.

2. Kwa nini tutazungumzia mifano inayoonyesha maoni ya ulimwengu?

2 Maoni ya ulimwengu hufanya watu wapuuze au kudharau miongozo ya Yehova, nayo yanaweza kudhoofisha imani yetu hatua kwa hatua. Leo, sote tumezungukwa na maoni ya ulimwengu. Maoni hayo yanaenezwa kwenye televisheni na Intaneti, kazini, au shuleni. Katika makala hii, tutachunguza mambo tunayoweza kufanya ili kuzuia maoni hayo yasipotoshe akili zetu. Tutachunguza mifano mitano inayoonyesha maoni ya ulimwengu na tutazungumzia jinsi tunavyoweza kukataa maoni hayo.

JE, TUNAHITAJI KUAMINI KWAMBA KUNA MUNGU?

3. Watu wengi wanavutiwa na maoni gani, na kwa nini?

3 “Ninaweza kuwa mtu mzuri bila kuamini kwamba kuna Mungu.” Katika nchi nyingi, ni jambo la kawaida kusikia watu wakisema hawaamini kuna Mungu; wanasema kwamba wao si wafuasi wa dini yoyote. Huenda hawajachunguza kwa makini ikiwa kweli Mungu yupo, lakini wanapendezwa na wazo la kuwa na uhuru wa kufanya wanachotaka. (Soma Zaburi 10:4.) Wengine wanaweza kufikiri kwamba wataonekana wenye akili nyingi wakisema: “Ninaweza kuwa na viwango vya juu vya maadili bila kuamini kwamba kuna Mungu.”

4. Tunaweza kutumia hoja gani kumsadikisha mtu anayedai kwamba hakuna Muumba?

4 Je, madai ya watu wanaoamini kwamba hakuna Muumba yanategemea hoja zenye kusadikisha? Mtu anapotegemea sayansi imsaidie kujua chanzo cha uhai, anaweza kutatanishwa na habari nyingi sana zilizopo. Lakini ukweli wa mambo ni kwamba jibu ni rahisi. Ikiwa nyumba ilijengwa na mtu fulani, sembuse vitu vilivyo hai! Kwa kweli, chembe hai za msingi duniani ni tata sana kuliko nyumba yoyote kwa sababu zinaweza kufanya mambo ambayo nyumba haiwezi kufanya, yaani, zinaweza kujigawanya. Chembe hizo zina uwezo wa kuhifadhi na kunakili habari zitakazoziwezesha kujigawanya. Ni nani aliyebuni chembe hai? Biblia inajibu hivi: “Kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.”—Ebr. 3:4.

5. Tunaweza kusema nini kuhusu wazo la kwamba mtu ana uwezo wa kujiamulia yaliyo mema pasipo kuamini kwamba kuna Mungu?

5 Unaweza kusema nini kuhusu wazo la kwamba wanadamu wana uwezo wa kujiamulia yaliyo mema pasipo kuamini kwamba kuna Mungu? Neno la Mungu linakubali kwamba watu wasiomwamini Mungu wanaweza kuwa na sifa fulani nzuri. (Rom. 2:14, 15) Kwa mfano, huenda wanawaheshimu na kuwapenda wazazi wao. Lakini viwango vyao vya maadili vinategemea msingi gani ikiwa hawaamini kwamba kuna Muumba mwenye upendo ambaye ndiye ameweka viwango vya mema na mabaya? (Isa. 33:22) Leo, watu wengi wanaofikiria mambo kwa makini wanakubali kwamba hali mbaya zilizopo duniani zinathibitisha kwamba wanadamu wanahitaji msaada wa Mungu. (Soma Yeremia 10:23.) Hivyo, hatupaswi kushawishika kufikiri kwamba mtu ana uwezo kamili wa kuamua yaliyo sawa bila kuamini kwamba kuna Mungu na kushikamana na viwango vyake.—Zab. 146:3.

JE, TUNAHITAJI DINI?

6. Watu wengi wana maoni gani kuhusu dini?

6 “Unaweza kuwa na furaha bila kuwa mfuasi wa dini fulani.” Maoni haya ya ulimwengu yanawavutia watu wengi leo kwa sababu wanaona dini kuwa yenye kuchosha na isiyo na maana yoyote. Pia, dini nyingi zinawavunja watu moyo wasimtafute Mungu kwa sababu zinafundisha kuhusu moto wa mateso, zinawalazimisha watoe fungu la kumi, au kuhubiri mambo ya siasa. Haishangazi kwamba watu wanaoamini kwamba wanaweza kuwa na furaha bila kuwa wafuasi wa dini fulani wanazidi kuongezeka! Huenda watu hao wakasema, “Ninapendezwa na mambo ya Mungu, lakini sitaki kuwa mfuasi wa dini yoyote.”

7. Dini ya kweli inachangiaje furaha?

7 Je, ni kweli kwamba mtu anaweza kuwa na furaha bila kuwa mfuasi wa dini yoyote? Ni kweli kwamba mtu anaweza kuwa na furaha bila dini ya uwongo, lakini hawezi kuwa na furaha ya kweli ikiwa hana uhusiano mzuri pamoja na Yehova, ambaye anatajwa kuwa “Mungu mwenye furaha.” (1 Tim. 1:11) Mambo yote ambayo Mungu anafanya huwanufaisha wengine. Watumishi wake wana furaha kwa sababu wanapenda kuwasaidia wengine. (Mdo. 20:35) Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo ibada ya kweli huchangia furaha ya kweli katika familia. Ibada ya kweli inatufundisha tuwastahi na kuwaheshimu wenzi wetu wa ndoa, kuiona nadhiri ya ndoa kuwa takatifu, kuepuka uzinzi, kuwalea watoto wenye heshima, na kuwapenda wengine kutoka moyoni. Matokeo ni kwamba ibada hiyo imewaunganisha watu wengi katika makutaniko yenye furaha na katika undugu wa ulimwenguni pote wenye furaha.—Soma Isaya 65:13, 14.

8. Kulingana na Mathayo 5:3, ni nini hasa kinachoweza kuwafanya watu wawe na furaha ya kweli?

8 Tunaweza kuchanganuaje wazo la kwamba mtu anaweza kuwa na furaha bila kumtumikia Mungu? Fikiria swali hili, Ni nini kinachowafanya watu wawe na furaha? Baadhi ya watu hufurahia kazi wanayofanya, mchezo fulani, au mambo wanayopenda kufanya wakati wa starehe. Wengine hufurahia kutunza familia au marafiki. Mambo hayo yote yanaweza kutuletea furaha, lakini maisha yetu yana kusudi kubwa zaidi linalotupatia furaha ya kudumu. Tofauti na wanyama, tunaweza kumjua vizuri Muumba wetu na kumtumikia kwa uaminifu. Tumeumbwa katika njia ya kwamba tunapata furaha kwa kufanya hivyo. (Soma Mathayo 5:3.) Kwa mfano, waabudu wa kweli hufurahia na kutiwa moyo sana wanapokutana pamoja ili kumwabudu Yehova. (Zab. 133:1) Wanafurahia pia undugu wa ulimwenguni pote, maisha safi, na tumaini zuri.

JE, TUNAHITAJI VIWANGO VYA MAADILI?

9. (a) Watu wengi ulimwenguni wana maoni gani kuhusu ngono? (b) Kwa nini Neno la Mungu linakataza ngono nje ya ndoa?

9 “Hakuna ubaya wa kufanya ngono nje ya ndoa.” Huenda watu wakatuambia: “Tunapaswa kufurahia maisha. Hakuna ubaya wa kufanya ngono nje ya ndoa.” Maoni ya kwamba Mkristo hapaswi kushutumu ngono nje ya ndoa, si sawa. Kwa nini? Kwa sababu Neno la Mungu linakataza uasherati. * (Soma 1 Wathesalonike 4:3-8.) Yehova ana haki ya kutuwekea sheria kwa sababu alituumba. Sheria ya Mungu inayoruhusu ngono kati ya mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa ni mojawapo ya mambo yanayofanya mpango wa Mungu wa ndoa uwe tofauti na mahusiano mengine. Mungu hutuwekea sheria kwa sababu anatupenda. Sheria hizo hutunufaisha. Familia zinazotii sheria hizo huwa na upendo, heshima, na amani. Mungu hamvumilii mtu yeyote anayevunja sheria yake kimakusudi.—Ebr. 13:4.

10. Mkristo anaweza kujiepushaje na uasherati?

10 Neno la Mungu linatufundisha jinsi ya kujiepusha kabisa na uasherati. Njia moja kuu ya kufanya hivyo ni kwa kuwa waangalifu kuhusu mambo tunayotazama. Yesu alisema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake. Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe.” (Mt. 5:28, 29) Kwa hiyo, Mkristo ataepuka kutazama ponografia au kusikiliza muziki wenye maneno machafu. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wenzake: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati.” (Kol. 3:5) Zaidi ya hayo, tunahitaji kudhibiti mambo tunayofikiria na mambo tunayozungumzia.—Efe. 5:3-5.

JE, UFUATILIE SANA KAZI YA KIMWILI?

11. Kwa nini tunaweza kushawishiwa kufuatilia mradi wa kupata kazi nzuri yenye mshahara mnono?

11 “Kutafuta kazi nzuri yenye mshahara mnono ndiyo siri ya kuwa na furaha.” Watu wengi hutuhimiza tufuatilie mradi wa kupata kazi nzuri yenye mshahara mnono. Kazi kama hiyo inaweza kutufanya tuwe na cheo, mamlaka, na utajiri. Kwa kuwa watu wengi hufanya hilo kuwa jambo kuu maishani, Mkristo anaweza kuathiriwa na maoni hayo.

12. Je, kupata kazi nzuri yenye mshahara mnono ndiyo siri ya kupata furaha?

12 Je, ni kweli kwamba mtu akifaulu kupata kazi nzuri yenye mshahara mnono, inayomfanya awe na mamlaka na cheo, anaweza kupata furaha ya kudumu? Hapana. Kumbuka kwamba Shetani alinaswa na tamaa ya kuwatawala wengine na tamaa ya umashuhuri, lakini hana furaha, bali ana hasira. (Mt. 4:8, 9; Ufu. 12:12) Kuwasaidia wengine wanufaike na hekima ya Mungu inayoweza kuwafanya wapate uzima wa milele huleta shangwe ya kudumu tofauti na shangwe ya muda inayoletwa na kazi nzuri yenye mshahara mnono. Isitoshe, ulimwengu huu una roho mbaya ya mashindano. Roho hiyo inawachochea watu wajaribu kuwa bora kuliko wengine, inawachochea kuwa na wivu, na mwisho wake huwa ni “kufuatilia upepo.”—Mhu. 4:4.

13. (a) Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kazi ya kimwili? (b) Kulingana na barua ambayo Paulo aliwaandikia Wathesalonike, ni nini kilichompatia shangwe ya kweli?

13 Ni kweli kwamba ni lazima tufanye kazi ili kupata riziki, na hakuna ubaya wowote wa kuchagua kufanya kazi tunayopenda. Lakini kazi yetu ya kimwili haipaswi kuwa ndilo jambo kuu maishani mwetu. Yesu alisema: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mt. 6:24) Tunapotanguliza utumishi wetu kwa Yehova na kuwafundisha wengine Neno lake, tunapata shangwe isiyo na kifani. Mtume Paulo alijionea jambo hilo. Alipokuwa kijana, alikuwa na kazi nzuri katika dini ya Kiyahudi, lakini alipata furaha ya kweli alipowafundisha wengine kweli za Biblia na kujionea jinsi watu walivyokubali ujumbe wa Mungu na jinsi ulivyobadili maisha yao. (Soma 1 Wathesalonike 2:13, 19, 20.) Hakuna kazi nyingine inayoridhisha maishani kuliko hiyo.

Kuwasaidia wengine wanufaike na hekima ya Mungu huleta shangwe ya kudumu (Tazama fungu la 12 na 13)

JE, TUNAWEZA KUSULUHISHA MATATIZO YA WANADAMU?

14. Kwa nini huenda watu wakavutiwa na wazo la kwamba mwanadamu anaweza kusuluhisha matatizo yake mwenyewe?

14 “Wanadamu wanaweza kusuluhisha matatizo yao wenyewe.” Huenda maoni hayo ya ulimwengu yakawavutia watu wengi. Kwa nini? Ikiwa maoni hayo ni sahihi, basi inamaanisha kwamba mwanadamu hahitaji mwongozo wa Mungu na kwamba anaweza kufanya anachotaka. Pia, huenda watu wakasadiki kwamba mwanadamu anaweza kusuluhisha matatizo yake mwenyewe kwa sababu kulingana na utafiti fulani, vita, uhalifu, magonjwa, na umaskini zinazidi kupungua. Ripoti moja inasema hivi: “Maisha ya wanadamu yanazidi kuboreka kwa sababu wanadamu wameamua kufanya ulimwengu uwe mahali bora zaidi pa kuishi.” Je, maneno hayo yanaonyesha kwamba mwanadamu amefaulu kupata suluhisho la matatizo ambayo yamemkumba kwa muda mrefu? Ili kupata jibu, acheni tuchunguze matatizo hayo kwa undani zaidi.

15. Ni mambo gani ya hakika yanayoonyesha uzito wa matatizo ya wanadamu?

15 Vita: Inakadiriwa kwamba watu milioni 60 au zaidi walipoteza maisha yao katika vita viwili vikuu vya ulimwengu. Tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu viishe, kwa kweli wanadamu hawajajifunza kuepuka vita. Kufikia mwaka wa 2015, idadi ya watu waliolazimika kuhama makao yao kwa sababu ya vita au mateso ilikuwa imeongezeka hadi milioni 65. Inakadiriwa kwamba katika mwaka wa 2015 pekee, watu milioni 12.4 walilazimika kuhama makao yao. Uhalifu: Ingawa aina fulani za uhalifu zimepungua katika maeneo fulani, aina nyingine kama vile uhalifu kwa kutumia intaneti, ukatili unaotendeka nyumbani, na ugaidi zinazidi kuongezeka kwa kiwango kinachoshtua. Isitoshe, watu wengi wanaamini kwamba ufisadi umeongezeka ulimwenguni pote. Wanadamu hawawezi kukomesha uhalifu. Magonjwa: Magonjwa fulani yamedhibitiwa. Lakini ripoti moja iliyochapishwa katika mwaka wa 2013 ilisema kwamba kila mwaka watu milioni tisa walio chini ya umri wa miaka 60 hufa kutokana na magonjwa ya moyo, kiharusi, kansa, magonjwa yanayoathiri mfumo wa kupumua, na kisukari. Idadi hiyo inashtua kwelikweli! Umaskini: Kulingana na ripoti moja ya Benki ya Ulimwengu, idadi ya watu walio maskini hohehahe katika bara la Afrika pekee, imeongezeka kutoka watu milioni 280 katika mwaka wa 1990 hadi watu milioni 330 katika mwaka wa 2012.

16. (a) Kwa nini ni Ufalme wa Mungu pekee unaoweza kusuluhisha matatizo ya wanadamu? (b) Ni baraka gani za Ufalme zilizotabiriwa na Isaya na mtunga zaburi?

16 Mifumo ya kiuchumi na kisiasa iliyoko leo inachochewa na roho ya ubinafsi. Ni wazi kwamba roho hiyo haiwezi kukomesha vita, uhalifu, magonjwa, na umaskini—ni Ufalme wa Mungu tu unaoweza kufanya hivyo. Fikiria kile ambacho Yehova atawafanyia wanadamu. Vita: Ufalme wa Mungu utakomesha mambo yote yanayosababisha vita yaani, ubinafsi, ufisadi, uzalendo, dini ya uwongo, na Shetani mwenyewe. (Zab. 46:8, 9) Uhalifu: Tayari Ufalme wa Mungu unawafundisha watu kupendana na kuaminiana kwa njia ambayo hakuna serikali nyingine imefaulu kufanya. (Isa. 11:9) Magonjwa: Yehova atawabariki watu wake kwa kuwapa afya kamilifu. (Isa. 35:5, 6) Umaskini: Yehova ataondoa umaskini na kuwapa watu wake ufanisi wa kiroho na wa kimwili—ufanisi bora zaidi kuliko utajiri.—Zab. 72:12, 13.

‘MJUE JINSI MNAVYOPASWA KUJIBU’

17. Unaweza kukataa jinsi gani maoni ya ulimwengu?

17 Ukisikia maoni ya ulimwengu yanayokufanya utilie shaka imani yako, chunguza kile ambacho Neno la Mungu linasema kuhusu jambo hilo na ulizungumzie na mwabudu mwenzako mkomavu. Chunguza kwa nini huenda maoni hayo yakavutia, kwa nini maoni hayo si sahihi, na jinsi unavyoweza kuyakataa. Kwa hakika, sisi sote tunaweza kujilinda dhidi ya maoni ya ulimwengu kwa kufuata himizo ambalo Paulo alitoa kwa kutaniko la Kolosai: “Endeleeni kutembea kwa hekima kuelekea wale walio nje . . . Mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Kol. 4:5, 6.

^ fu. 9 Watu wengi hawatambui kwamba katika Biblia fulani mistari ya Yohana 7:53–8:11 haikuwa sehemu ya maandishi ya awali yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Kwa msingi wa mistari hiyo, wengine wamedai kwamba ni mtu asiye na dhambi tu ndiye anayeweza kumwona mwingine kuwa mwenye hatia ya uzinzi. Lakini sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi: “Ikiwa mwanamume atapatikana akilala na mwanamke aliye na mume, wote wawili watauawa pamoja.”—Kum. 22:22.