Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wema​—Unaweza Kuusitawishaje?

Wema​—Unaweza Kuusitawishaje?

KIASILI, kila mmoja wetu angependa wengine wamwone kuwa mtu mwema. Hata hivyo, si rahisi kuonyesha sifa hiyo katika ulimwengu wa leo. Watu wengi ni “wasiopenda wema.” (2 Tim. 3:3) Huenda wakafuata viwango vyao wenyewe vya yaliyo sawa na yasiyo sawa, wakisema kwamba “wema ni uovu na uovu ni wema.” (Isa. 5:20) Pia, si rahisi kwetu kuonyesha sifa ya wema kwa sababu ya malezi yetu na hali yetu ya kutokamilika. Hivyo, huenda tukahisi kama Anne * ambaye, ingawa amemtumikia Yehova kwa miaka mingi, anakiri hivi: “Ni vigumu sana kwangu kuamini kwamba ninaweza kuwa mtu mwema.”

Jambo lenye kufurahisha ni kwamba sisi sote tunaweza kusitawisha sifa ya wema! Wema ni sifa ya tunda la roho takatifu ya Mungu, na roho hiyo ina nguvu kuliko hali yetu ya kutokamilika, malezi, au watu na hali zinazotuzunguka za ulimwengu huu. Acheni tuchunguze kwa undani sifa ya wema na tujifunze jinsi tunavyoweza kuonyesha sifa hiyo kwa ukamili hata zaidi.

WEMA NI NINI?

Kwa ufupi, wema ni sifa au hali ya kuwa mwema. Inahusisha kuwa na maadili mema na mwenendo bora, bila ubaya au uovu wowote. Wema huonyeshwa kupitia matendo mazuri ambayo huwanufaisha wengine. Nyakati zote, mtu mwema hutafuta fursa za kuwasaidia wengine na kuwatendea mambo mema.

Huenda umejionea kwamba watu fulani huwa tayari kuwatendea mema watu wa familia yao au rafiki zao, lakini je, ni wao tu wanaopaswa kuonyeshwa wema? Ukweli ni kwamba hakuna yeyote kati yetu anayeweza kuwa mwema kikamilifu, kwa sababu Biblia inasema kwamba “hakuna mtu mwadilifu duniani anayefanya mema sikuzote na hatendi dhambi kamwe.” (Mhu. 7:20) Mtume Paulo alikiri hivi waziwazi: “Najua kwamba ndani yangu, yaani, katika mwili wangu, halikai jambo lolote jema.” (Rom. 7:18) Hivyo basi, ni jambo linalofaa sana kwamba tujifunze jinsi ya kusitawisha sifa hiyo kutoka kwa Yehova, Chanzo cha wema.

“YEHOVA NI MWEMA”

Yehova Mungu ndiye anayeweka viwango vya mambo yaliyo mema. Biblia inasema hivi kumhusu: “Wewe ni mwema na kazi zako ni njema. Nifundishe masharti yako.” (Zab. 119:68) Acheni tuchunguze mambo mawili yanayotajwa katika mstari huo kuhusu wema wa Yehova.

Yehova ni mwema. Sifa ya wema haiwezi kamwe kutenganishwa na utu wa Yehova. Fikiria kilichotendeka Yehova alipomwambia Musa hivi: “Nitaufanya wema wangu wote upite mbele ya uso wako.” Utukufu wa Yehova kutia ndani wema wake, ulipokuwa ukipita, Musa alisikia maneno haya: “Mimi Yehova, Yehova, ni Mungu mwenye rehema na huruma, si mwepesi wa hasira, nina upendo mwingi mshikamanifu na kweli, ninawatendea maelfu kwa upendo mshikamanifu, ninasamehe makosa na uovu na dhambi, lakini sikosi kamwe kuwaadhibu wenye hatia.” (Kut. 33:19; 34:6, 7) Hivyo, ni wazi kwamba sifa ya wema huonekana katika kila sifa ya utu wa Yehova. Ingawa hakuna mwanadamu anayeweza kulinganishwa na Yesu katika kuonyesha sifa ya wema, Yesu alisema hivi: “Hakuna aliye mwema, isipokuwa mmoja, Mungu.”—Luka 18:19.

Tunajionea uthibitisho wa wema wa Yehova kupitia uumbaji

Kazi za Yehova ni njema. Wema huonekana katika kila jambo ambalo Mungu hufanya. “Yehova ni mwema kwa wote, na rehema zake zinaonekana katika kazi zake zote.” (Zab. 145:9) Yehova huonyesha wema bila upendeleo, anawapa wanadamu uhai na mambo yote wanayohitaji ili waendelee kuishi. (Mdo. 14:17) Pia, wema wake huonekana anapotusamehe. Mtunga zaburi aliandika hivi: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.” (Zab. 86:5) Tunaweza kuwa na hakika kwamba “Yehova hatawanyima jambo lolote jema wale wanaotembea kwa utimilifu.”—Zab. 84:11.

“JIFUNZENI KUTENDA MEMA”

Tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, hivyo tuna uwezo wa kuwa wema na wa kufanya mambo mema. (Mwa. 1:27) Hata hivyo, Neno la Mungu linawahimiza hivi watumishi wake: “Jifunzeni kutenda mema.” (Isa. 1:17) Lakini tunaweza kusitawishaje sifa hiyo yenye kuvutia? Fikiria njia tatu za kufanya hivyo.

Kwanza, tunaweza kusali ili tupate roho takatifu, ambayo huwasaidia Wakristo kusitawisha wema halisi. (Gal. 5:22) Naam, roho ya Mungu inaweza kutusaidia tujifunze kupenda yaliyo mema na kukataa yaliyo maovu. (Rom. 12:9) Isitoshe, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anaweza ‘kutuimarisha katika kila tendo na neno jema.’—2 The. 2:16, 17.

Pili, tunapaswa kusoma Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu. Tunapofanya hivyo, Yehova anaweza kutufundisha “njia yote ya lililo jema” na kutusaidia tuwe tayari “kwa ajili ya kila kazi njema.” (Met. 2:9; 2 Tim. 3:17) Tunaposoma Neno la Mungu na kulitafakari, tunajaza moyo wetu mambo mazuri kumhusu Mungu na mapenzi yake. Kwa kufanya hivyo, tunaongezea hazina yetu ambayo baadaye tunaweza kuingia na kuchota mambo ambayo tulijifunza.—Luka 6:45; Efe. 5:9.

Tatu, tunajitahidi kadiri tuwezavyo ‘kuiga yaliyo mema.’ (3 Yoh. 11) Biblia ina mifano tunayoweza kuiga. Bila shaka, Yehova na Yesu ndio mifano bora kabisa ya kuiga. Lakini pia tunaweza kuiga mifano ya wengine ambao walionyesha sifa ya wema. Huenda unawafikiria Tabitha na Barnaba. (Mdo. 9:36; 11:22-24) Unaweza kufaidika kwa kusoma masimulizi yao na kuchunguza mambo waliyofanya ili kuwasaidia wengine. Fikiria kuhusu hatua unayoweza kuchukua ili kuwasaidia watu wa familia yako au ndugu na dada kutanikoni. Na zingatia jinsi Tabitha na Barnaba walivyonufaika kwa sababu walisitawisha mazoea ya kuwatendea wengine wema. Wewe pia unaweza kunufaika kama wao.

Tunaweza pia kufikiria kuhusu mifano ya ndugu na dada katika siku zetu wanaotenda mema. Kwa mfano, fikiria wazee ‘wapenda mema,’ wanaofanya kazi kwa bidii kutanikoni. Hatungependa kuwasahau pia dada waaminifu ambao ni “walimu wa yaliyo mema” kupitia maneno na mfano wao. (Tito 1:8; 2:3) Dada anayeitwa Roslyn anaeleza hivi: “Rafiki yangu hujidhabihu ili awasaidie na kuwatia moyo wengine kutanikoni. Yeye hufikiria kuhusu hali zao na kwa kawaida anawapa zawadi ndogo au msaada wanaohitaji. Kwa kweli mimi humwona kuwa mtu mwema.”

Yehova huwatia moyo watu wake ‘watafute yaliyo mema.’ (Amo. 5:14) Tukifanya hivyo, hatutajifunza tu kupenda viwango vyake, bali pia tutaimarisha azimio letu la kutenda yaliyo mema.

Tunajitahidi kuwa wema na kutenda mema

Hatupaswi kuwazia kwamba ili mtu atende mema anahitaji kufanya mambo makubwa au kujidhabihu sana. Fikiria mfano huu: Mchoraji anapochora picha, je, unafikiri atatokeza mchoro mzuri kwa kupitisha brashi mara moja au mbili tu? Sivyo hata kidogo, badala yake huenda akapitisha brashi mara nyingi sana ili atokeze mchoro mzuri. Vivyo hivyo, wema wetu unaweza kuonekana kupitia matendo mengi madogo-madogo ya kuwasaidia watu.

Biblia inatuhimiza tuwe “tayari” kuwatendea wengine mema. (2 Tim. 2:21; Tito 3:1) Ikiwa tutakuwa macho kutambua hali ambazo wengine wanapitia, tunaweza kugundua njia za kumpendeza jirani yetu “kwa mema, ili kumjenga.” (Rom. 15:2) Jambo hilo linaweza kutia ndani kushiriki naye vitu tulivyo navyo. (Met. 3:27) Tunaweza kuamua kumkaribisha mtu fulani kwa ajili ya chakula chepesi au mazungumzo yenye kutia moyo. Tukipata taarifa kwamba mtu fulani ni mgonjwa, tunaweza kumtumia kadi, kumtembelea, au kumpigia simu. Naam, tunaweza kupata fursa nyingi za kusema “neno jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwanufaishe wale wanaolisikia.”—Efe. 4:29.

Tunamwiga Yehova kwa kujitahidi kuwatendea mema watu wote. Hivyo, tunawatendea wengine bila ubaguzi. Njia bora zaidi ya kufanya hivyo ni kuwahubiria watu wote habari njema ya Ufalme. Kama Yesu alivyoamuru, tunajitahidi kuwatendea mema hata wale wanaotuchukia. (Luka 6:27) Haliwezi kuwa kosa kamwe kuwaonyesha watu fadhili au kuwatendea mambo mema, kwa maana “hakuna sheria dhidi ya mambo hayo.” (Gal. 5:22, 23) Kupitia mwenendo wetu mzuri licha ya upinzani au majaribu, tunaweza kuwavuta wengine kwenye kweli na hivyo kumtukuza Mungu.—1 Pet. 3:16, 17.

THAWABU YA KUWA MWEMA

“Mtu mwema huvuna thawabu ya matendo yake.” (Met. 14:14) Baadhi ya thawabu hizo ni zipi? Tunapowatendea wengine matendo mema, kuna uwezekano mkubwa kwamba wao pia watatutendea vivyo hivyo. (Met. 14:22) Hata wasipotutendea mema, kwa kuendelea kuwatendea mema tunaweza kufanya mtazamo wao ubadilike na kuyeyusha ugumu wao.—Rom. 12:20, maelezo ya chini.

Wengi wanakiri jinsi walivyonufaika kwa kutenda mema na kujiepusha na uovu. Fikiria kisa cha Nancy. Anakiri hivi: “Nilipokuwa nikikua, nilikuwa mtu asiyejali, mwenye maadili machafu, na asiye na adabu. Hata hivyo, nilipokuwa nikijifunza na kutumia viwango vya Mungu vya mema, furaha yangu iliongezeka. Sasa ninajiheshimu.”

Sababu kuu inayotufanya tusitawishe sifa ya wema ni kwamba Yehova hufurahi tunapoisitawisha. Hata ikiwa watu wengi hawaoni mambo tunayofanya, Yehova huona. Anajua vizuri kila wazo na kila tendo jema tunalofanya. (Efe. 6:7, 8) Naye anatuthawabishaje? “Mtu mwema hupata kibali cha Yehova.” (Met. 12:2) Hivyo, acheni tuendelee kusitawisha sifa ya wema. Yehova anaahidi “utukufu na heshima na amani kwa kila mtu anayefanya mema.”—Rom. 2:10.

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.