Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upendo Ni Sifa Yenye Thamani

Upendo Ni Sifa Yenye Thamani

MTUME PAULO aliongozwa na roho kuandika kuhusu sifa tisa zinazotokana na utendaji wa roho takatifu. (Gal. 5:22, 23) Alieleza kwamba sifa hizo nzuri hutokeza tunda zima, yaani, ‘tunda la roho.’ * Tunda hilo hutokeza “utu mpya.” (Kol. 3:10) Kama ambavyo mti huzaa matunda unapotunzwa vizuri, ndivyo mtu anavyoonyesha sifa za tunda la roho, roho takatifu inapofanya kazi kwa uhuru ndani yake.​—Zab. 1:1-3.

Sifa ya kwanza ya tunda la roho ambayo Paulo alitaja ni sifa yenye thamani ya upendo. Ni yenye thamani kadiri gani? Paulo alisema kwamba bila upendo yeye “si kitu.” (1 Kor. 13:2) Lakini upendo ni nini, na tunaweza kuusitawisha na kuuonyesha jinsi gani kila siku?

JINSI UPENDO UNAVYOONYESHWA

Ingawa si rahisi kufafanua sifa ya upendo, Biblia inaeleza jinsi unavyoonyeshwa. Kwa mfano, tunasoma kwamba upendo ni “wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” Pia, “hushangilia pamoja na kweli,” na “huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” Upendo unahusisha pia hisia nyingi sana za kutoka moyoni kuelekea wengine, kuwajali kikweli, na vilevile kuwa na uhusiano wa karibu pamoja nao. Kwa upande mwingine, kutokuwa na upendo huonekana mtu anapokuwa na wivu, kiburi, mwenendo mbaya na wenye kukosa heshima, ubinafsi, na mwelekeo wa kuwa na kinyongo na kutowasamehe wengine. Tofauti na sifa hizo mbaya na zinazoonyesha ubinafsi, upendo tunaotamani kusitawisha “hautafuti faida zake wenyewe.”​—1 Kor. 13:4-8.

YEHOVA NA YESU—KIELELEZO BORA CHA UPENDO

“Mungu ni upendo.” Kwa hakika, Yehova ndiye chanzo na kielelezo bora zaidi cha upendo. (1 Yoh. 4:8) Kazi zake na matendo yake yote yanatoa ushahidi kwamba yeye ni mwenye upendo. Wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wake kwa wanadamu ulikuwa kumtuma Yesu ateseke na kufa kwa ajili yetu. Mtume Yohana alisema hivi: “Kwa hili upendo wa Mungu ulifunuliwa kwa habari yetu, kwa sababu Mungu alimtuma Mwana wake mzaliwa-pekee kuja ulimwenguni ili tupate uzima kupitia yeye. Hivi ndivyo upendo ulivyo, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yoh. 4:​9, 10) Kwa sababu ya upendo wa Mungu, tunaweza kupata msamaha, tumaini, na uzima.

Yesu alithibitisha kwamba anawapenda wanadamu kwa kutimiza mapenzi ya Mungu kwa hiari. Paulo aliandika hivi: “[Yesu] anasema: ‘Tazama! nimekuja kufanya mapenzi yako.’ . . . Kwa hayo ‘mapenzi’ yaliyosemwa sisi tumetakaswa kupitia toleo la mwili wa Yesu Kristo mara moja kwa wakati wote.” (Ebr. 10:​9, 10) Hakuna mwanadamu ambaye angeweza kuonyesha upendo mkubwa kuliko huo. Yesu alisema hivi: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yoh. 15:13) Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, je, tunaweza kuiga upendo ambao Yehova na Yesu wametuonyesha? Ndiyo! Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

“ENDELEENI KUTEMBEA KATIKA UPENDO”

Paulo anatuhimiza hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo, kama vile Kristo pia alivyowapenda ninyi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yenu.” (Efe. 5:1, 2) “[Tunaendelea] kutembea katika upendo” tunapoonyesha sifa hiyo katika mambo yote tunayofanya maishani. Tunaonyesha upendo huo kupitia matendo, si kwa maneno tu. Yohana aliandika hivi: “Watoto wadogo, acheni tupendane, si kwa neno wala kwa ulimi, bali kwa tendo na kweli.” (1 Yoh. 3:18) Kwa mfano, tunapompenda Mungu na jirani, tunachochewa kuwaambia wengine “habari njema ya ufalme.” (Mt. 24:14; Luka 10:27) Pia, tunaonyesha upendo tunapokuwa wenye ustahimilivu, wenye fadhili, na wenye kusamehe. Kwa hiyo, Biblia inatushauri hivi: “Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”​—Kol. 3:​13.

Hata hivyo, upendo halisi ni tofauti na upendo unaoongozwa na hisia. Kwa mfano, ili kumtuliza mtoto anayelia, mzazi anayeongozwa na hisia anaweza kumfanyia mtoto huyo chochote anachotaka. Lakini mzazi anayempenda mtoto wake kikweli atakuwa thabiti inapohitajika. Vivyo hivyo, ingawa Mungu ni upendo, “yeye ambaye Yehova anampenda, humtia nidhamu.” (Ebr. 12:6) Ikiwa tunawapenda wengine, sisi pia tutawashauri inapohitajiwa. (Met. 3:11, 12) Ni kweli kwamba tunapofanya hivyo tunapaswa kukumbuka kuwa sisi ni watenda dhambi pia, nasi hutenda kwa njia isiyo ya upendo nyakati fulani. Hivyo, sisi sote tuna mambo ambayo tunapaswa kufanyia kazi katika kuonyesha upendo. Tunaweza kufanyaje hivyo? Acheni tuchunguze njia tatu.

SITAWISHA SIFA YA UPENDO ​—JINSI GANI?

Kwanza, mwombe Mungu akupe roho yake, ambayo hutokeza sifa ya upendo. Yesu alisema kwamba Yehova huwapa “roho takatifu wale wanaomwomba.” (Luka 11:13) Ikiwa tunasali ili tupate roho takatifu na kujitahidi “[kuendelea] kutembea kwa roho,” tutatenda kwa njia yenye upendo zaidi na zaidi. (Gal. 5:16) Kwa mfano, ikiwa wewe ni mzee katika kutaniko la Kikristo, unaweza kumwomba Mungu akupe roho yake takatifu ili ikusaidie kuwashauri wengine kwa njia yenye upendo. Au ikiwa wewe ni mzazi, unaweza kuomba roho ya Mungu ikusaidie kuwatia nidhamu watoto wako kwa upendo, si kwa hasira.

Pili, tafakari jinsi Yesu alivyoonyesha upendo hata alipokasirishwa. (1 Pet. 2:​21, 23) Tunahitaji kufikiria mfano wa Kristo hasa tunapokosewa au kutendewa isivyo haki. Katika pindi kama hizo, inafaa tujiulize, ‘Yesu angefanya nini?’ Dada anayeitwa Leigh aligundua kwamba kujiuliza swali hilo humsaidia kufikiri kabla ya kutenda. Anaeleza hivi: “Siku moja, mfanyakazi mwenzangu alituma ujumbe kwa wafanyakazi wengine akisema mambo mabaya kunihusu na kuhusu kazi ninayofanya. Niliumia sana. Lakini nikajiuliza, ‘Ninaweza kumwigaje Yesu katika kushughulika na mtu huyu?’ Baada ya kutafakari kile ambacho Yesu angefanya, niliamua kumsamehe na kutolifikiria tena. Baadaye, niligundua kwamba mfanyakazi huyo alikuwa na ugonjwa mbaya na alikuwa na mkazo mwingi. Nilikata kauli kwamba huenda hakumaanisha mambo aliyoandika. Kutafakari mfano wa Yesu wa kuonyesha upendo hata alipokasirishwa, kulinisaidia kumwonyesha mfanyakazi mwenzangu upendo kama huo.” Naam, tukimwiga Yesu, sikuzote tutatenda kwa upendo.

Tatu, sitawisha mtazamo wa kuonyesha upendo wa kujidhabihu, sifa ambayo huwatambulisha Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:​34, 35) Kuhusiana na hilo, Maandiko yanatuhimiza tusitawishe ‘mtazamo uleule wa akili’ ambao Yesu alikuwa nao. Kwa kushuka kutoka mbinguni, “alijiondolea mwenyewe hali yake” kwa ajili yetu, hata kufikia “kifo.” (Flp. 2:​5-8) Tunapoiga upendo wake wa kujidhabihu, mawazo na hisia zetu zitakuwa kama za Kristo zaidi na zaidi, na tutachochewa kutanguliza masilahi ya wengine. Tunapata faida gani nyingine kwa kusitawisha upendo?

FAIDA ZA KUONYESHA UPENDO

Kuna faida nyingi za kuonyesha upendo. Fikiria mifano miwili:

Tunanufaikaje tunapoonyesha upendo?

  • UNDUGU WA KIMATAIFA: Kwa kuwa tunapendana, tunajua kwamba haidhuru tunatembelea kutaniko gani duniani, tutakaribishwa kwa uchangamfu na ndugu na dada zetu. Ni baraka kubwa sana kupendwa na “ushirika mzima wa ndugu [zetu] ulimwenguni”! (1 Pet. 5:9) Ni wapi pengine tunapoweza kupata upendo kama huo isipokuwa kati ya watu wa Mungu?

  • AMANI: ‘Kuvumiliana katika upendo’ kunafanya tufurahie “kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Efe. 4:2, 3) Tunajionea amani hiyo tunapohudhuria mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Je, hukubali kwamba roho hiyo ya amani ni ya pekee sana katika ulimwengu wa sasa uliogawanyika? (Zab. 119:165; Isa. 54:13) Tunapofuatia amani pamoja na wengine, tunadhihirisha kina cha upendo wetu kwao, na hilo linampendeza Baba yetu wa mbinguni.​—Zab. 133:1-3; Mt. 5:9.

“UPENDO HUJENGA”

Paulo aliandika hivi: “Upendo hujenga.” (1 Kor. 8:1) Upendo unafanyaje hivyo? Katika sura ya 13 ya barua ya kwanza ambayo Paulo aliwaandikia Wakorintho, mtume huyo anaeleza jinsi ambavyo upendo hujenga. Watu fulani huiita “Zaburi ya Upendo.” Njia moja ambayo upendo hujenga ni kwa kutuchochea kutafuta faida za wengine. (1 Kor. 10:24; 13:5) Kwa kuongezea, kwa kuwa upendo ni wenye ufikirio, wenye kujali, wenye ustahimilivu, na fadhili, unatokeza familia zenye upendo na makutaniko yenye umoja.—Kol.3:14.

Upendo tulio nao kwa Mungu tukiwa kikundi ndio upendo wenye thamani zaidi na wenye kujenga. Upendo huo huwaunganisha watu wa malezi, rangi, na lugha tofauti-tofauti na kufanya washirikiane kwa furaha wanapomtumikia Yehova “bega kwa bega.” (Sef. 3:9) Acheni tuazimie kuonyesha sifa hiyo yenye thamani ya tunda la roho takatifu ya Mungu kila siku.

^ fu. 2 Hii ni makala ya kwanza katika mfululizo wa makala tisa zitakazozungumzia kila sifa ya tunda la roho.