Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yakobo alikuwa babu ya Masihi kwa sababu alinunua haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza kutoka kwa Esau?

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, wazaliwa wa kwanza katika Israeli la kale ndio tu waliokuwa na haki ya kufanyiza ukoo ambao ungemtokeza Masihi?

Kuna nyakati ambazo tumesema hivyo. Ilionekana kwamba jambo hilo liliungwa mkono na yale tunayosoma katika Waebrania 12:16. Andiko hilo linasema kwamba Esau ‘hakuthamini mambo matakatifu’ na [alimpa Yakobo] haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza.” Ilionekana hilo lilidokeza kwamba Yakobo alipopokea “haki . . . za kuwa mzaliwa wa kwanza,” alipata kuwa pia babu ya Masihi.—Mt. 1:2, 16; Luka 3:23, 34.

Hata hivyo, kuchunguza upya masimulizi ya Biblia kumeonyesha kwamba mwanamume hakuhitaji kuwa mzaliwa wa kwanza ili awe katika ukoo wa Masihi. Acheni tufikirie baadhi ya mambo yanayothibitisha jambo hilo:

Mwana wa kwanza wa Yakobo (Israeli), ambaye alizaliwa na Lea, aliitwa Rubeni. Baadaye, Yosefu akazaliwa, ambaye alikuwa mwana mzaliwa wa kwanza wa Yakobo kupitia Raheli, mke aliyependwa sana na Yakobo. Rubeni alipofanya dhambi kwa kulala na suria wa baba yake, haki yake ya kuwa mzaliwa wa kwanza ilichukuliwa na Yosefu. (Mwa. 29:31-35; 30:22-25; 35:22-26; 49:22-26; 1 Nya. 5:1, 2) Lakini bado Rubeni na Yosefu hawakuwa kwenye ukoo ambao ulimtokeza Masihi. Badala yake ukoo huo ulipitia kwa Yuda, mwana wa nne wa Yakobo ambaye Lea alimzalia.—Mwa. 49:10.

Luka 3:32 inataja wanaume wengine watano ambao walifanyiza ukoo uliomtokeza Masihi. Inaonekana kila mwanamume alikuwa mzaliwa wa kwanza. Hivyo Boazi alimzaa Obedi, naye Obedi akamzaa Yese.—Rut. 4:17, 20-22; 1 Nya. 2:10-12.

Hata hivyo, Daudi hakuwa mwana wa kwanza wa Yese. Alikuwa wa mwisho kati ya wana wanane wa Yese. Ingawa hivyo ukoo wa Masihi ulikuja kupitia Daudi. (1 Sam. 16:10, 11; 17:12; Mt. 1:5, 6) Vivyo hivyo, mwanamume mwingine aliyekuwa miongoni mwa watu waliofanyiza ukoo uliomtokeza Masihi ni Sulemani, ingawa hakuwa mwana wa kwanza wa Daudi.—2 Sam. 3:2-5.

Hilo halimaanishi kwamba kuwa mzaliwa wa kwanza hakukuwa na umuhimu wowote. Lilikuwa jambo lenye kuheshimika kuwa mwana mzaliwa wa kwanza na mara nyingi mwana huyo ndiye aliyesimamia familia baada ya baba yake kufa. Pia, mwana huyo ndiye aliyepokea urithi maradufu wa mali ya baba yake.—Mwa. 43:33; Kum. 21:17; Yos. 17:1.

Hata hivyo, mtu mwingine angeweza kuchukua haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza. Abrahamu alimfukuza Ishmaeli, na hivyo haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza ikawa ya Isaka. Na kama tulivyoona, haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza iliondolewa kutoka kwa Rubeni ikawa ya Yosefu.

Acheni tusome tena Waebrania 12:16. Andiko hilo linasema hivi: “Kusiwe na mwasherati wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na mlo mmoja.” Paulo alikuwa akizungumzia nini?

Mtume Paulo hakuwa akizungumza kuhusu ukoo ambao Masihi angetokea. Alikuwa ametoka tu kuwahimiza Wakristo ‘waifanyie miguu yao mapito yaliyonyooka.’ Hilo lingewasaidia ‘wasinyimwe fadhili zisizostahiliwa za Mungu,’ jambo ambalo lingeweza kuwapata ikiwa wangefanya uasherati. (Ebr. 12:12-16) Ikiwa wangefanya hivyo, wangekuwa kama Esau. Esau ‘hakuthamini mambo matakatifu,’ na kihalisi alijiruhusu aongozwe na tamaa za mwili.

Esau aliishi nyakati za wazee wa ukoo, na huenda nyakati nyingine alikuwa na pendeleo la kutoa dhabihu. (Mwa. 8:20, 21; 12:7, 8; Ayu. 1:4, 5) Lakini kwa kuwa alikazia fikira mambo ya kimwili, Esau alitupilia mbali mapendeleo yote aliyokuwa nayo kwa sababu ya bakuli la mchuzi. Huenda alitaka kuepuka mateso yaliyotabiriwa kwamba yangewapata wazao wa Abrahamu. (Mwa. 15:13) Esau alionyesha pia kwamba alikuwa na mwelekeo wa kutanguliza tamaa zake za mwili alipooa wanawake wawili wapagani, jambo lililowahuzunisha sana wazazi wake. (Mwa. 26:34, 35) Alikuwa tofauti kabisa na Yakobo ambaye alihakikisha kwamba anaoa mwanamke aliyemwabudu Mungu wa kweli!—Mwa. 28:6, 7; 29:10-12, 18.

Hivyo basi, ni mkataa gani tunaoweza kufikia kuhusu ukoo ambao ulimtokeza Yesu, aliye Masihi? Nyakati nyingine wazaliwa wa kwanza walifanyiza ukoo ambao Masihi angetokea, lakini haikuwa hivyo nyakati zote. Wayahudi walitambua jambo hilo na kulikubali, kama walivyokiri pindi moja kwamba Kristo angekuwa mzao wa Daudi, mwana wa mwisho wa Yese.—Mt. 22:42.