Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Kushuka Moyo

Kushuka Moyo

Mtu aliye na ugonjwa wa kushuka moyo huhisije?

“Nimeingiwa na wasiwasi, nimeinama kupita kiasi; nimetembea huku na huku kwa huzuni mchana kutwa.”Zaburi 38:6.

WATAFITI WANASEMA NINI?

Mara kwa mara sisi sote huhuzunika, lakini kushuka moyo ni ugonjwa wenye kufadhaisha ambao huendelea kwa muda mrefu na humzuia mtu kufanya shughuli zake za kila siku. Ni muhimu kuzingatia kwamba watafiti wana maoni yanayotofautiana kuhusu huzuni ya kawaida na ugonjwa wa kushuka moyo. Lakini tunaweza kusema kwamba watu fulani huwa na hisia nyingi za huzuni, na nyakati nyingine hisia hizo humfanya mtu ajihisi hafai na mwenye hatia.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inazungumza kuhusu wanaume na wanawake wengi ambao walikuwa na huzuni nyingi. Kwa mfano, Hana alihisi “uchungu katika nafsi”—maneno ambayo yamefafanuliwa kuwa “kuvunjika moyo” na “kufadhaika sana.” (1 Samweli 1:10) Pindi moja, nabii Eliya alihuzunika sana hivi kwamba alimwomba Mungu amwue!1 Wafalme 19:4.

Wakristo wa karne ya kwanza walihimizwa ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14) Kulingana na kitabu kimoja, maneno “nafsi zilizohuzunika” yanaweza kurejelea wale ambao “kwa muda fulani wamelemewa na taabu za maisha.” Ni wazi kwamba hata wanaume na wanawake waaminifu wanaotajwa katika Biblia walishuka moyo pindi fulani.

 Je, kushuka moyo ni tatizo la kujiletea?

“Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.”Waroma 8:22.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inafundisha kwamba ugonjwa ni matokeo ya uasi wa wanadamu wawili wa kwanza. Kwa mfano, Zaburi 51:5 inasema hivi: “Nilizaliwa kwa maumivu nikiwa na kosa, na mama yangu alinichukua mimba katika dhambi.” Na Waroma 5:12 inaeleza kwamba “kupitia mtu mmoja [mwanadamu wa kwanza, Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” Kwa sababu tumerithi kutokamilika kutoka kwa Adamu, kila mmoja wetu anaweza kuwa mgonjwa kimwili au kihisia. Ndiyo sababu Biblia inasema kwamba “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Hata hivyo, Biblia inatoa tumaini ambalo hakuna tabibu anayeweza kutoa, yaani, ahadi ya Mungu ya kuleta ulimwengu mpya wenye amani ambamo hakutakuwa na magonjwa yoyote, kutia ndani kushuka moyo.Ufunuo 21:4.

Unaweza kukabilianaje na kushuka moyo?

“Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”Zaburi 34:18.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU

Huwezi kudhibiti hali zako siku zote, na huenda ukapatwa na mambo mabaya nyakati nyingine. (Mhubiri 9:11, 12) Hata hivyo, kuna mambo unayoweza kufanya ili huzuni nyingi isitawale maisha yako.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inasema wazi kwamba wagonjwa wanahitaji tabibu. (Luka 5:31) Kwa hiyo, ikiwa unaugua ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia, hakuna ubaya wowote kutafuta msaada wa daktari. Biblia pia inakazia umuhimu wa sala. Kwa mfano, Zaburi 55:22 inasema: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” Sala haipaswi kuonwa kuwa njia ya kutuliza hisia; ni njia ya kuzungumza waziwazi na Yehova Mungu, ambaye “yuko karibu na wale waliovunjika moyo.”Zaburi 34:18.

Unaweza pia kufaidika kwa kumweleza rafiki wa karibu hisia zako. (Methali 17:17) “Mwamini mwenzangu alinitia moyo nimweleze kuhusu ugonjwa wangu wa kushuka moyo,” anasema Daniela, ambaye ni Shahidi wa Yehova. “Ingawa kwa miaka mingi sikutaka kuzungumzia tatizo langu, nilitambua kwamba kwa kweli nilihitaji kufanya hivyo. Nilifurahi sana kwamba kufanya hivyo kuliniletea kitulizo.”