Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Urafiki Unapokuwa wa Karibu Kupita Kiasi

Urafiki Unapokuwa wa Karibu Kupita Kiasi

KIKWAZO

Una rafiki wa jinsia tofauti ambaye hukuelewa vizuri sana. Mnaweza kuzungumza kuhusu jambo lolote. Huenda unajiambia hivi: ‘Sisi ni marafiki tu.’ Hata hivyo, huenda mwenzi wako akawa na maoni tofauti ikiwa angesikiliza mazungumzo yenu marefu.

Tayari urafiki wenu umekuwa wa karibu sana na hivyo unahitaji kushughulikia hali hiyo. Lakini kwanza, fikiria ni nini kilichokufanya ujiingize katika uhusiano wa namna hiyo.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Kutosheleza mahitaji ya kihisia. Kusema kweli, ni kawaida kujihisi vizuri mtu wa jinsia tofauti anapokujali. Tunafurahi kujua kwamba tunathaminiwa, na jambo hilo hutufanya tujihisi tunavutia. Baada ya kuwa katika ndoa kwa muda fulani, huenda ukaanza kumweleza hisia zako rafiki wa jinsia tofauti. Hata hivyo, unapaswa kutambua kwamba lazima kutakuwa na madhara ikiwa utamruhusu mtu ambaye si mwenzi wako wa ndoa atosheleze mahitaji hayo. Unapoanzisha uhusiano wa kihisia usiofaa pamoja na mtu wa jinsia tofauti, unadhoofisha uhusiano wako na mwenzi wako wa ndoa. Kwa maneno mengine, unamnyima mwenzi wako upendo ambao anastahili.

• Jiulize, ‘Urafiki huu unanitimizia mahitaji gani ambayo ingefaa yatimizwe na mwenzi wangu wa ndoa?’

Kutowasiliana. Biblia inakiri kwamba wale waliofunga ndoa watakuwa na “dhiki” kwa kiasi fulani. (1 Wakorintho 7:28) Kwa mfano, nyakati nyingine huenda ukahisi mwenzi wako anakupuuza au hakuthamini, au huenda ukawa na kinyongo kwa sababu hali fulani ya kutoelewana haikusuluhishwa. Labda mwenzi wako anaepuka kuzungumzia mambo hayo, na jambo hilo linakufanya ukate tamaa na kufanya iwe rahisi kwako kuzungumzia mambo hayo na mtu mwingine. Wataalamu fulani wa mambo ya ndoa wanasema kwamba kuepuka kuzungumzia matatizo kunaweza kufanya ndoa isiwe na furaha na hata kusababisha talaka.

• Jiulize, ‘Je, ukosefu wa mawasiliano katika ndoa yangu umenifanya nivutiwe na mtu mwingine?’

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Tambua hatari. Biblia inasema: “Je, waweza kuweka moto kifuani na nguo zako zisiungue?” (Methali 6:27, Biblia Habari Njema) Ukweli ni kwamba kuvutiwa kimahaba na mtu mwingine ukiwa umefunga ndoa kutakuletea madhara. (Yakobo 1:14, 15) Si kwa sababu tu ya mambo yanayoweza kutokea, bali pia kwa sababu ya yale ambayo tayari yametokea. Kwa kumkazia fikira mtu mwingine, umemnyima mwenzi wako upendo ambao anapaswa kupata kutoka kwako.

Usijidanganye. Urafiki wa karibu na mtu huyo unaweza kukufanya uwazie jinsi maisha yangekuwa ikiwa ungefunga ndoa pamoja naye. Kwa kufanya hivyo, unalinganisha isivyofaa udhaifu wa mwenzi wako na uwezo wa rafiki yako! Pia, kumbuka kwamba huenda msisimuko unaopata unapomfikiria rafiki yako, ni sawa tu ule uliokuwa nao mwanzoni kuelekea mwenzi wako wa ndoa.—Kanuni ya Biblia: Yeremia 17:9.

Weka mipaka. Watu huweka ving’ora kwenye magari au kwenye nyumba ili kuzuia wezi. Unaweza kufanya jambo linalofanana na hilo kwa ajili ya ndoa yako. Biblia inasema: “Linda moyo wako.” (Methali 4:23) Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Jaribu kufanya mambo yafuatayo:

  • Onyesha wazi kwamba tayari umefunga ndoa—labda kwa kuweka picha za mwenzi wako mahali pa kazi.—Kanuni ya Biblia: Mwanzo 2:24.

  • Amua mapema mambo utakayoruhusu na ambayo hutayaruhusu unaposhughulika na mtu wa jinsia tofauti. Kwa mfano, haingefaa kuzungumzia matatizo yako ya ndoa au kwenda kwenye mkahawa na mfanyakazi mwenzako wa jinsia tofauti.

  • Kama uhusiano wako na mtu wa jinsia tofauti umekuwa karibu sana, vunja uhusiano huo mara moja. Ikiwa unaona ni vigumu kuuvunja, jiulize ni kwa nini. Badala ya kujaribu kuutetea uhusiano wako na mtu huyo, mkazie fikira mwenzi wako na uchukue hatua za kuilinda ndoa yako.—Kanuni ya Biblia: Methali 5:18, 19.