Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Lazima Uende Kwenye Jengo la Ibada ili Usali kwa Mungu?

Je, Ni Lazima Uende Kwenye Jengo la Ibada ili Usali kwa Mungu?

Maoni Ya Biblia

Je, Ni Lazima Uende Kwenye Jengo la Ibada ili Usali kwa Mungu?

WATU wengi huenda kwa ukawaida kwenye majengo ya kidini ili wasali kwa Mungu. Wengine hufunga safari ndefu ili wafike sehemu kama hizo. Je, unahisi ni lazima uende kwenye hekalu, madhabahu, au kanisani ili usali kwa Mungu? Au unahisi kwamba unaweza kuzungumza naye wakati wowote na mahali popote? Biblia inasema nini?

Mwanzoni mwa historia ya wanadamu, hakukuwa na majengo yoyote ya kidini. Wazazi wetu wa kwanza waliishi katika bustani maridadi. (Mwanzo 2:8) Walizungumza na Muumba wao, Yehova Mungu, kutoka katika bustani hiyo. Baadaye, wanadamu walipoongezeka duniani, wanaume waadilifu, kama vile Noa, ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli’​—bila kwenda kwenye majengo ya kidini. (Mwanzo 6:9) Walimpenda Mungu na walisali kwake na wakapata kibali chake.

Mungu Hakai Katika Majengo Yaliyofanywa kwa Mikono

Wanaume waaminifu wa kale walijua kwamba Muumba wa dunia na ulimwengu huu mkubwa hakai katika majengo yaliyofanywa kwa mikono. “Je, kweli Mungu atakaa pamoja na wanadamu duniani? ” akauliza Mfalme Sulemani mwenye hekima. Kisha akakiri hivi waziwazi: “Tazama! Mbingu, ndiyo, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha.” (2 Mambo ya Nyakati 6:18) Ni kweli kwamba Waisraeli wa kale walikuwa na maskani na baadaye hekalu ambapo walikusanyika kwa ajili ya sherehe za kidini za kila mwaka kulingana na Sheria ya Mungu. (Kutoka 23:​14-17) Hata hivyo, wangeweza kusali kwa Mungu wakati wowote​—walipokuwa wakichunga mifugo yao, wakifanya kazi katika mashamba yao, wakiwa pamoja kama familia, au wakiwa peke yao faraghani.​—Zaburi 65:2; Mathayo 6:6.

Sisi pia tunaweza kusali kwa Mungu mahali popote na wakati wowote. Yesu Kristo, kielelezo chetu, mara nyingi alienda mahali patulivu, penye faragha ili asali. (Marko 1:35) Kwa mfano, pindi moja “alienda mlimani kusali, naye akaendelea kusali kwa Mungu usiku wote.”​—Luka 6:12.

Bila shaka, akiwa Myahudi, Yesu alihudhuria kwa ukawaida sherehe za kidini katika hekalu huko Yerusalemu. (Yohana 2:​13, 14) Hata hivyo, alitabiri wakati ambapo hekalu halingekuwa tena kitovu cha ibada ya kweli. Alipokuwa akizungumza na mwanamke fulani Msamaria karibu na mlima mmoja uliokuwa na hekalu la Wasamaria, Yesu alisema: “Saa inakuja wakati ambapo mtamwabudu Baba si katika mlima huu wala kule Yerusalemu.” Kisha akaongezea kwamba waabudu wa kweli “watamwabudu Baba kwa roho na kweli.”​—Yohana 4:​21, 23.

Ndiyo, Yesu hakukazia fikira majengo yaliyojengwa kwa matofali na saruji, bali alikazia fikira ibada ya kweli inayofanywa kwa moyo mnyoofu. Lakini je, hilo lilimaanisha kwamba wafuasi wa Yesu, ambao baadaye walikuja kuitwa Wakristo, hawangewahi kutumia majengo ya ibada kumwabudu Mungu? (Matendo 11:26) La, na kuna sababu nzuri za kujibu hivyo.

Watu wa Mungu Ni Familia ya Kiroho

Watumishi wa kweli wa Mungu ni familia​—familia ya kiroho. (Luka 8:21) Familia nzuri hufanya mambo mengi pamoja kama vile kula pamoja, na hilo huimarisha vifungo vya familia. Ndivyo ilivyo na familia ya kiroho. Mikutano ya Kikristo ni kama karamu ya kiroho kwa kuwa kupitia hiyo, yule mtu wa ndani analishwa na vifungo vya kiroho vinaimarishwa. Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo.”​—Waebrania 10:​24, 25.

Hivyo, waabudu wa kweli wanatambua kwamba kutaniko lina fungu muhimu, kwa kuwa linamwezesha kila mshiriki asitawishe sifa za kiroho ambazo haziwezi kukuzwa kikamili ikiwa mtu amejitenga. Sifa hizo zinatia ndani upendo, kusamehe, fadhili, upole, na amani.​—2 Wakorintho 2:7; Wagalatia 5:​19-23.

Wakristo wa karne ya kwanza walikutanika wapi kwa ajili ya ushirika na ibada? Mara nyingi, walikutana katika nyumba za watu. (Waroma 16:5; Wakolosai 4:15) Kwa mfano, alipokuwa akimwandikia barua Mkristo mwenzake, mtume Paulo pia aliliandikia ‘kutaniko lililo katika nyumba yake.’ *​—Filemoni 1, 2.

Vivyo hivyo leo, watu wa Mungu hawahitaji majengo ya kidini yenye madoido mengi, bali wao hutumia majengo yanayofaa ambayo yanaweza kutoshea wote wanaohudhuria. Mashahidi wa Yehova wana majengo kama hayo, ambayo wanayaita Majumba ya Ufalme. Kuna uwezekano mkubwa kwamba kuna Jumba la Ufalme katika eneo unamoishi. Majengo hayo ni yenye kiasi na hutimiza kusudi lake, na mikutano inafanywa kwa njia rahisi​—inatia ndani wimbo, sala, na mazungumzo ya Biblia.

Mashahidi wa Yehova wanathamini sana pindi wanazokuwa nazo za kuzungumza na Mungu kwa undani faraghani. Kwa hiyo, wao hutumia muda fulani kila siku kusali, wakiwa familia na pia faraghani wakiwa mtu mmojammoja. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi,” inasema Yakobo 4:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Biblia fulani za Kiswahili zinatafsiri neno la awali la Kigiriki “kutaniko” kuwa “kanisa.”

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, Mungu anakaa katika majengo yaliyofanywa kwa mikono?​—2 Mambo ya Nyakati 6:18.

● Yesu alisali usiku wote akiwa wapi?​—Luka 6:12.

● Kwa nini waabudu wa kweli hukutanika pamoja?​—Waebrania 10:​24, 25.

[Blabu katika ukurasa wa 15]

Je, sala zako zitasikiwa tu ukiwa mahali fulani?