Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kujifunza Kuwa Mwenye Kufanya Amani

Unaweza Kujifunza Kuwa Mwenye Kufanya Amani

Unaweza Kujifunza Kuwa Mwenye Kufanya Amani

INGAWA huenda tukazaliwa na mielekeo fulani isiyofaa, kwa kawaida mtu hujifunza jeuri. Ndivyo ilivyo na kuwa mwenye kufanya amani. Hata hivyo, ni nani anayeweza kutufundisha njia za amani ya kweli? Muumba wetu ndiye mtu mwenye kutegemeka zaidi, na hekima yake haina kifani. Fikiria mambo matano yafuatayo na uone hekima nyingi inayopatikana katika Biblia.

1 “Usimwonee wivu mtu mwenye jeuri.” (Methali 3:31) Tambua kwamba mtu aliye na sifa nzuri ni yule anayeweza kujizuia na mpole. “Asiye mwepesi wa hasira ni bora kuliko mwanamume mwenye nguvu,” inasema Methali 16:32. Kama kuta zenye nguvu za bwawa, mtu wa aina hiyo anaweza kustahimili anapochokozwa. Kwa kweli, badala ya kuonyesha hasira, anatenda kwa upole na hivyo “hugeuza ghadhabu.” (Methali 15:1) Hata hivyo, mtu mwenye mwelekeo wa kukasirika, hulipuka anapochokozwa kidogo.​—Methali 25:28.

2 Chagua marafiki wako kwa hekima. “Mtu wa jeuri atamshawishi mwenzake,” inasema Methali 16:29. Kwa upande mwingine, “anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” (Methali 13:20) Naam, tukishirikiana na watu wenye kufanya amani ambao wana sifa ya kujizuia na roho ya upole, inaelekea tutajaribu kuwaiga.

3 Sitawisha upendo wa kweli kwa wengine. Ufafanuzi bora zaidi wa upendo unapatikana kwenye 1 Wakorintho 13:​4-7. Sehemu fulani ya andiko hilo inasema hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. . . . Huhimili mambo yote, . . . huvumilia mambo yote.” Yesu alisema kwamba ikiwa tunataka kuiga upendo wa Mungu, ni lazima tuwapende adui zetu.​—Mathayo 5:​44, 45.

4 Uwe na hakika kwamba Mungu atachukua hatua dhidi ya waovu. “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu. . . . Kwa kadiri inavyowategemea ninyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote. Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe, . . . kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa, asema Yehova.’ ” (Waroma 12:​17-19) Tunapokuwa na imani katika Mungu na ahadi zake, tunafurahia amani ya akili ambayo watu wasio na imani hawawezi kuelewa.​—Zaburi 7:​14-16; Wafilipi 4:​6, 7.

5 Utegemee Ufalme wa Mungu ulete amani ya kweli duniani. Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu ambayo hivi karibuni itawaangamiza waovu wote na kutawala dunia yote. (Zaburi 37:​8-11; Danieli 2:44) Chini ya Ufalme huo, “mwadilifu atachipuka,” na kutakuwa “na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.”​—Zaburi 72:7.

Mafundisho kama hayo ya Biblia yamewasaidia mamilioni ya watu​—kutia ndani wengine waliokuwa na mwelekeo wa jeuri​—wawe wapenda amani. Soma simulizi la Salvador Garza.