Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 6

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 6

Kitabu Kinachotegemeka—Sehemu ya 6

Roma na Historia ya Biblia

Hii ni habari ya sita katika mfululizo wenye habari saba katika matoleo ya “Amkeni!” yenye kufuatana yanayozungumzia serikali saba kuu za ulimwengu zinazotajwa katika historia ya Biblia. Kusudi lake ni kuonyesha kwamba Biblia inategemeka na imeongozwa na roho ya Mungu na ujumbe wake unatoa tumaini kwamba mateso yanayosababishwa na utawala mkatili wa wanadamu yatakwisha.

YESU alianzisha Ukristo, na wafuasi wake waliueneza kotekote wakati wa utawala wa Milki ya Roma. Bado unaweza kuona barabara, mifereji ya maji, na nguzo za Roma katika nchi kama vile Uingereza na Misri. Mabaki hayo ya Roma ni halisi. Yanatukumbusha kwamba Yesu na mitume wake walikuwa watu halisi, na hata mambo waliyosema na kutenda yalikuwa halisi. Kwa mfano, unapotembea katika Njia ya Apio la kale, unatembea katika njia ileile ambayo huenda mtume Mkristo Paulo alitembea alipokuwa akienda Roma.—Matendo 28:15, 16.

Historia Inayotegemeka

Masimulizi ya Biblia kuhusu Yesu na wanafunzi wake yanatia ndani marejeo mengi kuhusu matukio ya kihistoria katika karne ya kwanza. Luka, mwandikaji wa Biblia aliandika kwa uangalifu kuhusu mwaka ambao matukio haya mawili muhimu yalitukia: mwanzo wa huduma ya Yohana Mbatizaji na kubatizwa kwa Yesu, wakati ambapo alikuwa Kristo, au Masihi. Luka aliandika kwamba matukio hayo yalitukia katika “mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwa Kaisari Tiberio [29 W.K.], Pontio Pilato alipokuwa gavana wa Yudea, na Herode alipokuwa mtawala wa wilaya ya Galilaya.” (Luka 3:1-3, 21) Luka alitaja pia maofisa wengine muhimu wanne—Filipo (ndugu ya Herode), Lisania, Anasi, na Kayafa. Majina yote saba yanatajwa na wanahistoria. Acheni tuzungumze kuhusu Tiberio, Pilato, na Herode.

Kaisari Tiberio anajulikana sana, na picha yake imechorwa na wasanii. Baraza Kuu la Roma lilimweka rasmi kuwa maliki Septemba (Mwezi wa 9) 15 mwaka wa 14 W.K., Yesu alipokuwa na umri wa miaka 15 hivi.

Jina la Pontio Pilato linatajwa pamoja na jina la Tiberio katika simulizi lililoandikwa na mwanahistoria Mroma Tasito muda mfupi tu baada ya Biblia kukamilishwa. Kuhusu neno “Mkristo,” Tasito aliandika hivi: “Christus, ambaye jina hilo lilitokana naye, aliuawa wakati wa utawala wa Tiberio mikononi mwa mmoja wa watawala wetu, Pontio Pilato.”

Herode Antipa anajulikana kuwa ndiye aliyejenga jiji la Tiberia kando ya Bahari ya Galilaya. Pia alijenga makao yake huko. Huenda Herode aliamuru Yohana Mbatizaji akatwe kichwa huko Tiberia.

Masimulizi ya Biblia yanataja pia matukio muhimu wakati wa utawala wa Roma. Biblia inasema hivi kuhusu wakati ambapo Yesu alizaliwa: “Basi katika siku hizo Kaisari Augusto alitoa amri kwamba dunia yote inayokaliwa iandikishwe; (uandikisho huu wa kwanza ulitendeka wakati Kirenio alipokuwa gavana wa Siria;) na watu wote wakaanza kusafiri kwenda kuandikishwa, kila mmoja kwenye jiji lake mwenyewe.”—Luka 2:1-3.

Tasito na mwanahistoria Yosefo wanamtaja Kirenio. Uthibitisho wa kwamba kulikuwa na uandikisho huo unapatikana katika agizo la gavana Mroma ambalo limehifadhiwa katika Maktaba ya Uingereza. Agizo hilo linasema hivi: “Kwa kuwa wakati wa kuhesabiwa kwa watu kutoka nyumba hadi nyumba umefika, watu wote wanaoishi nje ya wilaya zao kwa sababu zozote zile wanashurutishwa warudi nyumbani kwao.”

Biblia pia inataja “njaa kali . . . wakati wa [Maliki Mroma] Klaudio.” (Matendo 11:28) Yosefo, mwanahistoria wa karne ya kwanza anathibitisha simulizi hilo. Aliandika hivi: “Kulikuwa na njaa iliyowakandamiza wakati huo, na watu wengi walikufa.”

Kwa kuongezea, kwenye Matendo 18:2, Biblia inasema kwamba “Klaudio alikuwa ameagiza Wayahudi wote waondoke Roma.” Wasifu wa Klaudio ulioandikwa mwaka wa 121 W.K. na mwanahistoria Mroma Suetonius unaunga mkono jambo hilo. Suetonius anasema kwamba Klaudio “aliwafukuza Wayahudi wote kutoka Roma,” na kuongezea kwamba kwa sababu ya uhasama kuwaelekea Wakristo, Wayahudi “walikuwa wakisababisha vurugu kila mara.”

Biblia inasema kwamba karibu na wakati wa njaa ile ambayo imetoka kutajwa, Herode Agripa, akiwa amejivika “vazi la kifalme,” aliwatolea hotuba umati wa watu waliokuwa wakimhusudu, ambao walisema: “Ni sauti ya mungu, wala si ya mwanadamu!” Baada ya tukio hilo, Biblia inasema kwamba Agripa “akaliwa na wadudu akakata pumzi.” (Matendo 12:21-23) Yosefo alitaja pia tukio hilo, akiongezea mambo machache. Alisema pia kwamba Agripa alitoa hotuba yake akiwa amevalia “vazi lililokuwa limetengenezwa kwa fedha tupu.” Pia alisema kwamba ‘Agripa alipatwa na maumivu makali ya tumbo.’ Yosefo aliandika kwamba Agripa alikufa baada ya siku tano.

Unabii Unaotegemeka

Biblia pia ina unabii wa pekee ulioandikwa na kutimizwa wakati wa utawala wa Roma. Kwa mfano, Yesu alipoingia Yerusalemu akiwa amebebwa na mwana-punda, alilia na kutabiri jinsi ambavyo majeshi ya Roma yangeharibu jiji hilo. Yesu alisema: “Siku zitakuja juu yako wakati adui zako watakapojenga kukuzunguka ngome yenye miti iliyochongoka nao watakuzunguka . . . Hawataacha jiwe juu ya jiwe ndani yako, kwa sababu hukufahamu wakati wa kukaguliwa kwako.”—Luka 19:41-44.

Ingawa hivyo, wafuasi wa Yesu wangepata nafasi ya kutoroka. Jinsi gani? Yesu aliwapa maagizo hususa mapema. Aliwaonya hivi: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake [Yerusalemu] na waondoke.” (Luka 21:20, 21) Huenda wafuasi wa Yesu walijiuliza, ‘Tutatoka jinsi gani katika jiji lililozingirwa?’

Yosefo aliandika mambo yaliyotukia. Katika mwaka wa 66 W.K., gavana wa Roma alipochukua kutoka kwenye sanduku la hazina hekaluni deni la kodi ambalo Wayahudi hawakuwa wamelipa kwa Roma, Wayahudi waasi waliokuwa na hasira waliwachinja askari-jeshi wa Roma, na kujitangaza kuwa taifa huru. Baadaye mwaka huo, gavana Mroma wa Siria, Sesho Galo, akiwa na askari-jeshi 30,000 aliingia Yerusalemu kutoka upande wa kusini wakati ambapo jiji hilo lilikuwa na sherehe ya kidini. Galo aliingia vijijini na hata akaanza kuharibu ukuta wa hekalu, ambako waasi hao walikuwa wamekimbilia. Kisha, kwa ghafula, bila kutazamiwa, Galo na askari-jeshi wake wakaondoka! Wayahudi wenye hasira waliwafuata na kuwashambulia.

Wakristo waaminifu hawakupumbazwa na jambo hilo. Walitambua kwamba walikuwa wameona utimizo wa unabii wa Yesu wenye kustaajabisha: Jiji hilo lilikuwa limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi! Na sasa, kwa kuwa majeshi hayo yalikuwa yameondoka, Wakristo waaminifu walitumia nafasi hiyo kukimbia. Wengi wao walikimbilia Pela, jiji la Watu wa Mataifa lisilomilikiwa na yeyote lililokuwa milimani ng’ambo ya Yordani.

Jiji la Yerusalemu lilipatwa na nini? Majeshi ya Roma yalirudi, yakiongozwa na Vespasiani na mwana wake Tito—wakati huu majeshi hayo yalikuwa na askari-jeshi 60,000. Yaliingia kwenye jiji hilo kabla ya Pasaka ya mwaka wa 70 W.K., na kuwanasa wakaaji na wasafiri wengine kutoka maeneo mengine waliokuwa wamekuja jijini humo kwa ajili ya sherehe hiyo. Majeshi ya Roma yalikata miti yote katika wilaya hiyo ili kujenga ukuta wenye miti iliyochongoka, kama vile tu Yesu alivyokuwa ametabiri. Baada ya miezi mitano hivi, jiji hilo lilianguka.

Tito aliamuru kwamba hekalu lihifadhiwe; lakini askari-jeshi mmoja aliliteketeza, kisha likabomolewa jiwe kwa jiwe—kama Yesu alivyokuwa ametabiri. Yosefo anasema kwamba Wayahudi na wageuzwa-imani 1,100,000 hivi walikufa, wengi wao kutokana na njaa na magonjwa, na watu wengine 97,000 wakachukuliwa mateka. Wengi wao walipelekwa Roma kuwa watumwa. Ukitembelea jiji la Rome leo, unaweza kuona uwanja wa Colosseum unaojulikana sana, ambao ulijengwa na Tito baada ya kampeni yake huko Yudea. Pia unaweza kuona Tao la Tito, ambalo ni kumbukumbu la ushindi dhidi ya Yerusalemu. Kwa kweli unabii wa Biblia unategemeka hata katika mambo madogo. Kwa hiyo, tusipuuze kamwe yale ambayo inasema kuhusu wakati ujao!

Tumaini Linalotegemeka

Yesu alipokuwa mbele ya gavana Mroma Pontio Pilato, alizungumza kuhusu Ufalme, au serikali ambayo “si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Yesu hata aliwafundisha wafuasi wake kusali kwa ajili ya serikali hiyo ya kifalme. Alisema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, . . . ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Ona kwamba Ufalme wa Mungu utafanya mapenzi ya Mungu yatendeke duniani—si mapenzi ya wanadamu wenye kiburi wanaojitakia makuu.

Yesu anatawala akiwa Mfalme katika Ufalme huo wa mbinguni. Na kama Mungu alivyokusudia mwanzoni, atageuza dunia yote iwe paradiso.—Luka 23:43.

Ufalme wa Mungu utaingilia shughuli za wanadamu wakati gani? Yesu ambaye amefufuliwa alionyesha jibu la swali hilo alipozungumza na mtume Yohana, ambaye wakati huo alikuwa mfungwa katika kisiwa cha Patmosi wakati wa utawala wa Maliki Mroma Domitiani, aliyekuwa ndugu ya Tito. “Kuna wafalme saba,” Yesu alifunua. “Watano wameanguka, mmoja yuko, yule mwingine bado hajafika, lakini atakapofika lazima adumu kwa muda mfupi.”—Ufunuo 17:10.

Yohana alipoandika maneno hayo, “wafalme,” au miliki tano, zilikuwa zimeanguka: Misri, Ashuru, Babiloni, Muungano wa Umedi na Uajemi, na Ugiriki. Yule mmoja ambaye “yuko,” au alikuweko wakati wa siku za mtume Yohana, ni Roma. Kwa hiyo, ni mmoja tu aliyebaki—serikali kuu ya ulimwengu ya mwisho katika historia ya Biblia. Hiyo ilikuwa serikali gani? Itatawala kwa muda gani? Maswali hayo yatajibiwa katika toleo linalofuata la Amkeni!

[Picha katika ukurasa wa 10]

Paulo alisafiri katika Njia ya Apio

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kaisari Tiberio ni mmoja kati ya maofisa wengi Waroma wanaotajwa katika Injili ya Luka

[Picha katika ukurasa wa 11]

Maandishi yanayotaja jina la Pontio Pilato

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Picha ya Tito, mwana wa Vespasiani, kwenye sarafu ya Roma

[Hisani]

Musée de Normandie, Caen, France

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tao la Tito huko Rome ni kumbukumbu la ushindi dhidi ya Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Top, time line: Egyptian wall relief and bust of Nero: Photograph taken by courtesy of the British Museum; Persian wall relief: Musée du Louvre, Paris; bottom, bust of Tiberius Caesar: Photograph taken by courtesy of the British Museum