Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Nilivyoacha Kuwa Mwenye Jeuri

Jinsi Nilivyoacha Kuwa Mwenye Jeuri

Jinsi Nilivyoacha Kuwa Mwenye Jeuri

Limesimuliwa na Jose Antonio Nebrera

NI NINI humfanya mtu awe mwenye jeuri? Nilikuwa mwenye jeuri kwa sababu nililelewa katika mazingira yenye jeuri. Baba yangu alikuwa katika kikosi cha ulinzi cha serikali ya Hispania, ambacho kilitoa nidhamu kali. Alipokuwa mdogo mara nyingi baba yake alimchapa sana, hivyo baba yangu pia akawa akinichapa vivyo hivyo. Mara nyingi alitumia mshipi wake mkubwa kunicharaza. Zaidi ya hayo, alinitukana kwa kuniita mjinga, huku akimpendelea sana dada yangu mdogo. Kwa kuwa mama yangu alihofu sana ghadhabu ya baba, hakunisaidia wala kunionyesha upendo niliohitaji.

Nilipokuwa shuleni pamoja na watoto wengine, niliishi katika ulimwengu wa kuwaziwa tu, ambako nilionekana kana kwamba nilikuwa na furaha. Na huenda watu walifikiri kuwa mimi ni mtoto mchangamfu na mwenye mtazamo mzuri. Lakini hayo yalikuwa mambo ya kijuujuu tu. Nilificha tu hisia zangu za woga na hasira. Nilirudiwa na fahamu jioni nilipokuwa nikitembea polepole kuelekea nyumbani, kwani niliogopa ningekutana na matusi zaidi au ningechapwa kikatili.

Nilipokuwa na umri wa miaka 13, niliamua kuyatoroka maisha hayo ya jeuri na hivyo nikajiandikisha katika shule moja ya bweni ya Kijesuti. Kwa kipindi fulani nilitaka kuwa kasisi. Lakini shule hiyo haikunisaidia kuona kusudi la maisha yangu. Tulilazimika kuamka saa kumi na moja asubuhi na kuoga kwa maji baridi. Kisha tulifuata programu ngumu iliyotia ndani masomo, sala, na ibada tukipumzika kwa muda mfupi tu mara kwa mara.

Ingawa tulipaswa kusoma hadithi za “watakatifu,” hatukutumia Biblia katika masomo yetu. Kulikuwa na Biblia moja tu ambayo ilihifadhiwa kwenye kasha la kioo, na mtu alihitaji kupewa ruhusa ya pekee ikiwa alitaka kuisoma.

Katika mwaka wangu wa tatu kwenye shule hiyo ya bweni tulikuwa na vipindi vya kujipiga mijeledi, ambavyo vilijulikana kama “mazoezi ya kiroho.” Nilijaribu kumeza chakula kingi kwa wakati mmoja niwe mgonjwa ili niepuke vipindi hivyo. Lakini sikufua dafu. Baada ya miaka mitatu hivi, singeweza kuvumilia ukatili huo. Hivyo, nilitoroka shule hiyo ya Wajesuti na kurudi nyumbani. Nilikuwa na umri wa miaka 16.

Kutafuta Maisha Yenye Kusisimua

Niliporudi nyumbani, nilijifunza ndondi na pia kupigana mweleka. Nilipofaulu katika michezo hiyo ya jeuri nilihisi kuwa ninaheshimika, lakini ustadi wangu wa kupigana ulinifanya nitumie nguvu kupata chochote nilichohitaji, kama vile tu baba yangu alivyofanya.

Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka 19, badiliko fulani maishani mwangu lilinifanya niwe mpole kwa kiasi fulani. Nilikutana na Encarnita, na baada ya miezi tisa tulifunga ndoa. Aliona jinsi nilivyokuwa kwa nje tu mtu mwenye adabu, fadhili, na furaha. Lakini hakujua jinsi nilivyokuwa na hasira kali ndani yangu. Hasira hiyo ilianza kuonekana nilipoagizwa nijiunge na jeshi punde tu baada ya mwana wetu wa kwanza kuzaliwa.

Kwa kuwa nilitaka kukwepa kunyolewa kama mwanajeshi na pia nilitaka maisha yenye kusisimua, nilijitolea kujiunga na Kikosi cha Kigeni cha Hispania. Niliwazia kwamba ningepata uhuru zaidi katika jangwa la Morocco na pia kwa kushiriki katika kikosi cha pekee cha kijeshi. Pia, hilo lilinipa nafasi nzuri ya kuepuka kushughulikia madaraka yangu ya familia. Hata hivyo, hilo lilifanya sifa zangu mbaya zionekane waziwazi.

Upesi niliingia mashakani kwani kulikuwa na sajini mkatili aliyefurahia sana kutesa wanajeshi wapya. Nilichukia sana ukosefu wa haki na nilikuwa tayari kupigania yale niliyoona kuwa haki. Asubuhi moja tulipokuwa tukiitwa majina, nilifanya mzaha na sajini huyo akanielewa vibaya. Alipoinua mkono wake kunipiga, mara moja niliushika, nikaupinda, na kumpiga mweleka hadi akaanguka. Nilihakikisha kwamba alibaki akiwa chini yangu kwani nilihofu kwamba ikiwa ningempa nafasi, angenipiga risasi.

Tendo hilo lilifanya nipelekwe kwa miezi mitatu katika kikosi cha wanajeshi waliokuwa wakitiwa nidhamu. Nilijipata nikiishi katika chumba kidogo kilichokuwa na wanaume 30 hivi. Kwa muda huo wote, sikuweza hata kubadilisha nguo zangu. Kikosi hicho kilikuwa na sajini aliyefurahia kuwachapa watu mijeledi. Lakini wakati mmoja nilitisha kumwua ikiwa angenipiga, hivyo akapunguza adhabu yangu kutoka viboko 30 hadi 3. Nilikuwa nimejifunza kuwa sugu kama walionitesa.

Kikosi cha Siri

Nilipokuwa nikizoezwa katika kikosi hicho cha kigeni, nilijitolea bila kufikiri kwa ajili ya migawo yenye “kusisimua.” Kwa mara nyingine, sikujua migawo hiyo ingekuwa na matokeo gani. Nilipokea mazoezi ya pekee ya kupigana kama komando, ambayo yalitia ndani kupata uzoefu wa kutumia vifaa vyote vya kijeshi pamoja na makombora. Nilipomaliza mazoezi hayo, nilitumwa huko Langley, Virginia, Marekani, ambako nilipata mafunzo katika Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA).

Upesi nikaanza kushirikiana na kikundi cha wanajeshi wa kikosi cha siri. Katika miaka ya 1960, nilishiriki katika uvamizi mbalimbali wa siri. Nilisaidia kukabiliana na walanguzi wa dawa za kulevya na pia wasafirishaji wa silaha haramu katika nchi za Amerika ya Kati na Amerika Kusini. Tulipowakamata, tulipewa amri ya kuwaua mara moja. Ninasikitika kusema kwamba nilishiriki katika mauaji hayo. Tuliwaua maadui wote isipokuwa wale ambao wangehojiwa ili tupate habari zaidi.

Baadaye nilipewa mgawo wa kuwapeleleza viongozi wa jeshi la Hispania ili kufahamu ni nani ambao hawakuunga mkono utawala wa kimabavu wa Jenerali Franco. Pia tuliwapeleleza wapinzani wa utawala wa Franco ambao walikuwa wakiishi nchini Ufaransa. Lengo lilikuwa kuwateka nyara wapinzani hao wakuu na kuwapeleka hadi nchini Hispania, na kuwaua huko.

Mgawo wangu wa mwisho ulikuwa kupanga askari-jeshi wa kukodiwa ili wapindue serikali moja katika nchi ndogo ya Afrika. Tuliagizwa tushambulie kambi ya wanajeshi iliyo kwenye mji mkuu wa nchi hiyo kisha tuteke makao ya rais. Tulifanya kama tulivyoagizwa, tukavamia nchi hiyo katikati ya usiku na kumaliza mashambulizi yetu kwa muda wa saa nne pekee. Wanajeshi wenzangu watatu waliuawa katika mapigano hayo, pamoja na “adui” zetu wengi sana. Mimi pia nilishiriki katika mauaji hayo.

Kisa hicho cha kutisha kiliumiza sana dhamiri yangu. Singeweza kulala usiku kwa kuwa niliota nikiwaua adui zangu kwa kutumia mikono. Katika ndoto hizo niliona nyuso za watu walionitazama kwa hofu kubwa kabla ya kuwaua.

Niliazimia kutoshiriki tena katika uvamizi mwingine. Kwa hiyo, nilirudisha stakabadhi zangu zote na nikaruhusiwa kutoka jeshini. Hata hivyo, baada ya miezi mitatu wasimamizi wangu waliniita tena kwa ajili ya mgawo mwingine wa upelelezi. Nilitorokea nchini Uswisi, na baada ya miezi kadhaa, mke wangu Encarnita—ambaye hakujua lolote kuhusu kazi yangu kama jasusi—alijiunga nami huko Basel.

Mazoea Mabaya Hayaishi Haraka

Katika muda wa miaka mitatu niliyotumikia jeshini, Encarnita alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova alipokuwa huko Hispania. Alinieleza kwamba alikuwa amepata kweli kumhusu Mungu, na shauku yake ilinichochea nitake kujua mengi kuhusu kweli hiyo. Mara moja tuliwatafuta Mashahidi wa Yehova nchini Uswisi na tukaanza kujifunza Biblia pamoja.

Nilifurahi sana kujifunza kuhusu makusudi ya Mungu. Ingawa nilitaka kufuata kanuni za Biblia maishani mwangu, haikuwa rahisi kufanya mabadiliko—hasa ya utu wangu uliokuwa wenye jeuri. Hata hivyo, bado nilipenda mambo mapya niliyokuwa nikijifunza. Baada ya kujifunza kwa miezi michache, nilisisitiza kwamba nilikuwa tayari kushiriki katika kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri nyumba kwa nyumba.

Kwa msaada wa Yehova, hatimaye nilijifunza kujizuia, na baada ya muda, mimi na Encarnita tukabatizwa. Nilipokuwa na umri wa miaka 29, niliwekwa rasmi kutumika nikiwa mwangalizi wa kutaniko.

Mnamo 1975 tuliamua kurudi Hispania. Lakini wenye mamlaka jeshini hawakuwa wamenisahau, kwa hiyo niliitwa nishiriki katika mgawo mwingine wa pekee. Ili kuepuka matatizo, nilikimbilia tena Uswisi mara moja. Tuliishi huko hadi mwaka wa 1996 wakati ambapo tulirudi Hispania tena.

Sasa mwana na binti yangu tayari wamefunga ndoa, na nina wajukuu wawili, na wote hao wanamtumikia Yehova. Pia katika miaka hiyo yote, nimesaidia watu 16 hivi kumjua Yehova, kutia ndani kijana mmoja ambaye zamani alihusika katika maandamano yenye jeuri kaskazini mwa Hispania. Mambo hayo yameniletea uradhi wa kweli.

Nimemwomba Mungu mara nyingi anisaidie nisahau maisha yangu ya jeuri na pia niache kuota ndoto mbaya ambazo hunisumbua. Katika pigano langu la kufanya yaliyo mema, nimefuata shauri la Zaburi 37:5: “Mkabidhi Yehova njia yako, na kumtegemea, naye mwenyewe atatenda.” Yehova ametimiza ahadi hiyo. Amenisaidia niache maisha yenye jeuri. Hilo limekuwa baraka kubwa kwangu na pia kwa familia yangu.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nilipojiandikisha katika shule ya bweni ya Wajesuti nikiwa na umri wa miaka 13

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mnamo 1968 kwenye ofisi ya kikosi cha kigeni baada ya kuruhusiwa kuondoka

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu Encarnita, leo