Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nitapata Wapi Marafiki Tunaopatana?

Nitapata Wapi Marafiki Tunaopatana?

Vijana Huuliza

Nitapata Wapi Marafiki Tunaopatana?

“Nina umri wa miaka 21. Katika eneo hili hakuna vijana wengi wa rika langu, kwa hiyo ninalazimika kushirikiana na vijana wenye umri mdogo kuliko umri wangu au wenzi wa ndoa. Kikundi cha kwanza huzungumza sana kuhusu mitihani, na kile cha pili huhangaikia tu mahitaji ya familia zao. Mambo hayo si muhimu sana kwangu. Ningefurahi sana ikiwa ningepata watu wenye mapendezi kama yangu!”—Carmen. *

KARIBU kila mtu, hata awe na umri gani, anataka kukubaliwa na wengine. Bila shaka wewe pia unataka kukubaliwa. Hiyo ndiyo sababu wakati mtu anapotengwa na kupuuzwa kana kwamba haonekani, yeye huumizwa hisia—“yaani ni kama hata siko,” hivyo ndivyo Michaela mwenye umri wa miaka 15 anavyohisi.

Bila shaka, ikiwa wewe ni Mkristo, una “ushirika mzima wa akina ndugu” unaoweza kushirikiana nao. (1 Petro 2:17) Hata hivyo, huenda wakati mwingine ukahisi kana kwamba hakuna mtu aliye na mapendezi kama yako. Helena, mwenye umri wa miaka 20 anasema, “Nilipokuwa nikirudi nyumbani baada ya mikutano, niliketi kwenye kiti cha nyuma ndani ya gari na kulia. Kadiri nilivyojitahidi nikubaliwe na wengine, ndivyo nilivyohisi kwamba nimekata tamaa.”

Unaweza kufanya nini unapohisi kwamba hupati marafiki wenye mapendezi kama yako? Ili tujibu swali hilo, acheni kwanza tuchunguze kuhusu (1) watu ambao wewe huona ni vigumu sana kuanzisha urafiki nao na (2) jinsi unavyojiendesha unapokuwa nao.

Weka alama ya ✔ kando ya kikundi cha watu ambacho unahisi kwamba ni vigumu sana kuanzisha urafiki nao.

1. Umri

□ marika □ vijana wenye umri mkubwa □ watu wazima

2. Utendaji

Watu ambao

□ ni stadi katika michezo □ wenye vipawa fulani □ wenye akili

3. Utu

Watu

□ wajasiri □ maarufu □ walio katika kikundi

Sasa weka alama ya ✔ kando ya sentensi inayoonyesha jinsi unavyotenda unapokuwa na watu uliotaja hapo juu.

□ mimi hujifanya kwamba nina mapendezi na vipawa kama vyao.

□ mimi hupuuza mapendezi yao na kuzungumza kuhusu mapendezi yangu.

□ mimi hukaa kimya na kutafuta nafasi ya kuondoka.

Kwa sababu umetambua kikundi cha watu ambacho wewe huona vigumu kushirikiana nao na pia umetambua jinsi ambavyo umekabiliana na hali hiyo, sasa tuko tayari kuona jinsi unavyoweza kurekebisha hali hiyo. Kwanza kabisa, unapaswa kujua na kuepuka vizuizi fulani ambavyo vinaweza kufanya usikubaliwe.

KIZUIZI cha 1: Kujitenga

Changamoto. Unapokuwa pamoja na watu ambao mapendezi au vipawa vyao vinatofautiana na vile vyako, ni rahisi kuhisi kwamba hufai—hasa ikiwa wewe ni mwenye haya. Anita aliye na umri wa miaka 18 anasema, “Mimi huchukia kuanzisha mazungumzo, kwa sababu ninahofu kwamba nitasema jambo lisilofaa.”

Biblia inasema nini? “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Ni wazi kwamba kujitenga na wengine kutafanya hali iwe mbaya hata zaidi. Unapojitenga na wengine, utanaswa katika hali mbaya yenye kujirudia: Upweke unakuambia kwamba hakuna aliye na mapendezi kama yako, na hilo linakufanya ujitenge na wengine, na hivyo unakuwa mpweke, na upweke unakuambia kwamba hakuna aliye na mapendezi kama yako. Na hivyo unabaki umenaswa katika hali hiyo inayojirudia, hadi utakapoirekebisha!

“Watu hawawezi kusoma akili yako. Usiposema kile unachotaka, hutakipata. Usiposhirikiana na watu wengine, hutakuwa na marafiki. Lazima utie bidii. Si vizuri kufikiri eti ni daraka la yule mtu mwingine. Kila mtu anapaswa kutia bidii katika urafiki.”—Melinda, 19.

KIZUIZI cha 2: Kujitahidi kupita kiasi

Changamoto. Watu fulani huwa tayari kufanya lolote ili tu wakubaliwe hivi kwamba wanajiingiza katika mashirika mabaya—wakifikiri kwamba kuwa na rafiki yeyote ni bora kuliko kuwa bila rafiki. “Nilihisi vibaya kwa sababu sikuwa katika kikundi cha vijana waliokuwa maarufu sana shuleni kwa hiyo nilitamani kufanya makosa ili wanikubali,” anasema René, mwenye umri wa miaka 15.

Biblia inasema nini? “Anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya”—au kama vile tafsiri ya Union Version inavyosema, “rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Methali 13:20) Usielewe kimakosa maneno “wajinga” au “wapumbavu” yanayotumiwa katika mstari huo kumaanisha watu wasiojua jambo lolote. Tofauti na hilo, huenda vijana hao wawe werevu sana shuleni. Lakini ikiwa hawaheshimu viwango vya Biblia, basi machoni pa Mungu wao ni wapumbavu. Kwa hiyo, utajiumiza mwenyewe ikiwa utakuwa kama kinyonga, ukijaribu kubadilisha rangi yako kila mara ili ufaane nao.—1 Wakorintho 15:33.

“Hupaswi kuamini kwamba mtu yeyote tu ni rafiki mzuri. Hungependa kuwa na marafiki ambao watafanya ujihisi kwamba ni lazima ujibadili ili ufanane nao. Ungependa kuwa na rafiki ambao wanakupenda kwelikweli na ambao watashikamana nawe.”—Paula, 21.

Chukua Hatua ya Kwanza

Usingoje watu wengine wakufikie na kukukaribisha katika kikundi chao cha marafiki. Gene, mwenye umri wa miaka 21 anasema, “Si vizuri kungoja kila mara watu wengine waje wajijulishe kwetu. Tunahitaji kuchukua hatua ya kwanza kuwajua.” Madokezo mawili yafuatayo yatakusaidia kufanya hivyo:

Tafuta marafiki ambao si wa umri wako. Inaonekana kwamba ingawa Yonathani na Daudi walikuwa na tofauti ya miaka 30, walikuwa “marafiki wakubwa.” * (1 Samweli 18:1, Contemporary English Version) Tunajifunza nini? Inawezekana kuanzisha urafiki na watu wenye umri mkubwa! Fikiria hili, Kuna haja gani kuwa na marafiki wa umri wako tu halafu ulalamike kwamba huwezi kupata marafiki wapya? Kufanya hivyo ni kama kufa njaa ukiwa kwenye kisiwa kilichozungukwa na samaki! Ukweli wa mambo ni kwamba kuna watu wenye tabia nzuri ambao unaweza kuanzisha urafiki nao. Na njia moja ya kufanya hivyo ni kutafuta watu wenye umri tofauti na wako.

“Mama yangu alinitia moyo niwe nikizungumza na watu wenye umri mkubwa katika kutaniko letu. Alisema ningeshangaa kuona kwamba walikuwa na mapendezi kama yangu. Hakuwa amekosea, na sasa nina marafiki wengi sana!”—Helena, 20.

Sitawisha mbinu za kuwasiliana. Si rahisi kuanzisha mazungumzo—hasa ikiwa wewe ni mwenye haya. Lakini unaweza kufaulu. Jambo kuu ni (1) kusikiliza, (2) kuuliza maswali, na (3) kuwajali wengine kikweli.

“Mimi hujaribu kusikiliza badala ya kuongea zaidi. Na ninapozungumza, ninajaribu kuepuka kuzungumza sana kujihusu au kuzungumza kwa njia isiyofaa kuhusu watu wengine.”—Serena, 18.

“Ikiwa mtu anazungumza kuhusu jambo fulani ambalo silijui vizuri, mimi humwomba anieleze zaidi kulihusu, na huenda hilo linaweza kumfanya azungumze hata zaidi.”—Jared, 21.

Huenda ikawa kwamba kwa kawaida wewe ni mnyamavu, na hakuna ubaya wowote na hilo. Haimaanishi unapaswa kuwa kama kasuku! Lakini ikiwa unahisi kwamba hukubaliki na watu wengine, jaribu madokezo yaliyoonyeshwa katika habari hii. Huenda ukahisi jinsi Leah anavyohisi. Anasema hivi: “Mimi ni mwenye haya, kwa hiyo, mimi hujilazimisha kuzungumza. Lakini ili uwe na marafiki, lazima uwe mwenye urafiki. Kwa hiyo, ninajitahidi kuanzisha mazungumzo.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 31 Inaelekea Daudi alikuwa kijana sana alipoanzisha urafiki pamoja na Yonathani.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 19]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Mimi hujaribu kuzungumza angalau na mtu mmoja ambaye sijawahi kuzungumza naye katika mkutano wa Kikristo. Nimegundua kwamba unaweza kuanzisha urafiki kwa kumsalimu mtu!”

“Ilikuwa rahisi kwangu kuketi tu na kusema kwamba watu wengine hawanipendi na kwamba siwezi kuanzisha urafiki nao. Lakini ilibidi nitie bidii sana ili nibadili hali hiyo. Hatimaye, kufanya hivyo kulikuwa na matokeo mazuri, na niliboresha utu wangu.”

“Pole kwa pole nilianza kuzungumza na watu wazima. Mwanzoni ilikuwa vigumu sana! Lakini hatimaye nilifaidika sana, kwa sababu nikiwa mwenye umri mdogo nilianzisha urafiki na watu ambao wameshikamana nami hadi sasa.”

[Picha]

Lauren

Reyon

Carissa

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Je, ilikuwa vigumu kwenu kuanzisha urafiki mlipokuwa na umri kama wangu? Ni kikundi gani cha watu ambacho ilikuwa vigumu zaidi kwenu kuanzisha urafiki? Mlifanya nini ili kubadili hali hiyo?

․․․․․

[Mchoro katika ukurasa wa 20]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

HALI MBAYA YA UPWEKE YENYE KUJIRUDIA

Mimi ni MPWEKE,

na hilo hunifanya

nihisi . . . ↓

. . . NIMETENGWA,

na hilo hunifanya

↑ nitake . . .

. . . KUJITENGA,

na hilo hunifanya

nihisi kwamba . . .