Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

WATU wengi wanaamini kwamba Mungu yuko kila mahali na ndani ya kila kitu. Hata hivyo, Mfalme Sulemani mwenye hekima alisali hivi kwa Yehova: “Na usikie ukiwa mbinguni, makao yako yaliyofanywa imara.” (1 Wafalme 8:30, 39) Basi, Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu ana makao. Sulemani alisema kwamba makao hayo ni “mbinguni.” Lakini hilo linamaanisha nini?

Nyakati nyingine Biblia inatumia neno “mbingu” kuwakilisha maeneo halisi ya ulimwengu yanayozunguka dunia. (Mwanzo 2:1, 4) Hata hivyo, kwa kuwa Mungu aliumba vitu vyote, makao yake lazima yawe yalikuwapo kabla ya kufanyiza ulimwengu halisi. Kwa sababu hiyo, lazima Mungu awe mahali ambapo hapajafungwa na ulimwengu halisi. Kwa hiyo, Biblia inaposema kwamba mbinguni ndiyo makao ya Yehova Mungu, inarejelea, si mahali fulani angani au kwenye anga za juu, bali kwenye makao ya kiroho.

Maono Yenye Kustaajabisha

Biblia inatuonyesha picha yenye kustaajabisha sana ya makao ya Yehova katika maono ambayo mtume Yohana alipewa. Katika maono hayo, Yohana aliona mlango uliofunguliwa mbinguni na akasikia sauti ikimwambia: “Panda uje huku.”—Ufunuo 4:1.

Kisha, Yohana alionyeshwa maono yenye kustaajabisha ya Yehova Mungu mwenyewe. Haya ni baadhi ya mambo aliyoona: “Kiti cha ufalme kilikuwa mahali pake mbinguni . . . Yule aliyeketi, kuonekana kwake ni kama jiwe la yaspi na jiwe jekundu la thamani, na upinde wa mvua ambao kuonekana kwake ni kama zumaridi unakizunguka kile kiti cha ufalme. . . . Umeme na sauti na ngurumo zinatoka katika kile kiti cha ufalme . . . Na mbele ya kile kiti cha ufalme kuna kitu mfano wa bahari kama kioo.”—Ufunuo 4:2-6.

Huo ni ufafanuzi wa wazi wa uzuri na utukufu wa Yehova usio na kifani. Ona mazingira ya kiti cha ufalme cha Yehova. Upinde unaonyesha kwamba kuna amani na utulivu. Umeme, sauti, na ngurumo zinakazia nguvu za Yehova. Bahari iliyo kama kioo inaonyesha msimamo safi wa wale walio mbele za Mungu.

Ingawa mambo yanayoonekana hapo ni ya mfano, yanatufundisha mengi kuhusu makao ya Mungu. Yehova anadumisha utaratibu kamili mbinguni. Makao yake hayana mvurugo.

Ni Kweli Yuko Kila Mahali Kila Wakati?

Kwa kuwa Yehova ana makao, hilo linaonyesha kwamba hayuko kila mahali, kila wakati. Basi, anaweza kujua jinsi gani kuhusu mambo yanayotendeka? (2 Mambo ya Nyakati 6:39) Njia moja ni kupitia roho yake takatifu, au kani ya utendaji. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Ni wapi ninapoweza kwenda mbali na roho yako, na ni wapi ninapoweza kukimbilia mbali na uso wako? Kama ningepanda mbinguni, ungekuwa huko; na kama ningetandika kitanda changu katika Kaburi, tazama! ungekuwa huko.”—Zaburi 139:7-10.

Ili kuelewa nguvu za roho takatifu, fikiria jua. Jua liko mahali fulani hususa lakini linasambaza nguvu zake kwa sehemu kubwa ya dunia. Vivyo hivyo, Yehova Mungu ana makao. Lakini anaweza kufanya chochote anachotaka popote katika ulimwengu. Isitoshe, Yehova anaweza kutumia roho yake takatifu kuelewa kinachotendeka mahali popote na wakati wowote. Kwa hiyo, 2 Mambo ya Nyakati 16:9 inasema hivi: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”

Pia, Mungu anaongoza kikundi kikubwa sana cha viumbe wa roho wanaoitwa malaika. Biblia inaonyesha kwamba kunaweza kuwa na mamia ya mamilioni ya malaika hao—labda hata mabilioni au zaidi. * (Danieli 7:10) Biblia ina masimulizi mengi yanayoonyesha malaika ambao walitenda kama wawakilishi wa Mungu wakaja duniani, wakazungumza na wanadamu, na kumrudishia Mungu ripoti. Kwa mfano, katika siku za Abrahamu, malaika walichunguza kilio cha malalamiko juu ya Sodoma na Gomora. Mungu aliamua kuharibu majiji hayo, bila shaka baada ya kupokea ripoti kutoka kwa malaika hao.—Mwanzo 18:20, 21, 33; 19:1, 13.

Kwa hiyo, Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu hahitaji kuwa kila mahali kihalisi. Kupitia utendaji wa roho yake takatifu na malaika, anaweza kutambua kabisa kile kinachotendeka kila mahali katika uumbaji wake.

Ni wazi kwamba Biblia inaweza kutusaidia kumfahamu Muumba wetu vizuri zaidi. Humo tunajifunza kwamba Mungu ana makao yake hususa, mbinguni, makao ya roho nje ya mbingu halisi. Maelfu ya viumbe wa roho wenye nguvu wanaishi pamoja naye katika makao hayo ya roho. Na makao yake yanaonyeshwa kuwa yakiwa na utulivu, nguvu, na yakiwa safi. Biblia inatuhakikishia kwamba kwa wakati unaofaa wanadamu watafurahia hali zenye amani hapa duniani kama zile zilizoko mbinguni.—Mathayo 6:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ufunuo 5:11 inaonyesha “makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu” ya malaika wakiwa wamezunguka kiti cha ufalme cha Mungu. Kumi elfu kuzidisha kumi elfu (10,000 x 10,000) ni milioni 100. Lakini andiko hilo linatumia maneno “makumi ya maelfu ya makumi ya maelfu,” hivyo kuonyesha kwamba huenda kuna mabilioni mengi ya viumbe wa roho.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, Mungu yuko kila mahali?—1 Wafalme 8:30, 39.

● Roho ya Mungu inaweza kutenda kwa kadiri gani?—Zaburi 139:7-10.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Jua liko mahali hususa, lakini nguvu zake zinafika katika sehemu kubwa. Vivyo hivyo, Mungu ana makao hususa, lakini roho yake takatifu inaweza kutenda mahali popote anapotaka katika ulimwengu