Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Singeweza Kuacha Kukisoma!”

“Singeweza Kuacha Kukisoma!”

“Singeweza Kuacha Kukisoma!”

● Vijana ulimwenguni pote wameshukuru sana kwa ajili ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2. * Hebu ona mifano ifuatayo:

“Nimependezwa sana jinsi kitabu hiki kinavyotutia moyo tuwasiliane na wazazi wetu. Nilitumia madokezo hayo, na sasa ninaweza kusema kwamba mimi na wazazi wangu tumeboresha mawasiliano kati yetu.”—Roberto, Mexico.

“Mara tu nilipoanza kusoma kitabu hicho, singeweza kuacha kukisoma! Ninapenda sehemu, ‘Hatua za Kuchukua!’ inayopatikana mwishoni mwa kila sura na pia ukurasa wa ‘Daftari’ unaopatikana mwishoni mwa kila sehemu. Kitabu hiki kimenisaidia niitetee imani yangu shuleni.”—Joelah, Marekani.

“Kadiri nilivyokisoma, ndivyo kitabu hicho kilivyonigusa moyo. Nilipendezwa na manukuu ya vijana wengi, na pia sehemu yenye kichwa ‘Je Wajua?’ na ‘Pendekezo.’ Kitabu hiki kimenihakikishia kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linapendezwa sana na vijana!”—Hui-won, Korea Kusini.

“Kati ya vitabu vyote vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova, hiki ndicho ninachofurahia zaidi kusoma. Kwa kweli, mnajua yale ambayo vijana wanafikiria na pia matatizo wanayokabili nyumbani, shuleni, na wanapokuwa na marafiki.”—Shana, Kanada.

“Kila mara wazazi wangu walipogombana, nilienda chumbani mwangu na kulia. Lakini baada ya kusoma sura ya 24, ‘Nifanye Nini Wazazi Wangu Wanapogombana?,’ nilizungumza na wazazi wangu kuhusu jambo hilo. Walishangaa sana kujua kwamba mabishano yao yaliniathiri vibaya sana. Wao pia walisoma sura hiyo. Sasa wanaelewa hisia zangu vizuri zaidi, na hawabishani sana.”—Mariana, Jamhuri ya Cheki.

“Kurasa zenye kichwa ‘Mfano wa Kuigwa’ zimenigusa sana na pia zimenisaidia nifanyie kazi udhaifu wangu. Kwa mfano, ni vigumu sana kwangu kuanzisha urafiki katika kutaniko la Kikristo na watu nisiowajua. Lakini ukurasa wa 97 unaonyesha jinsi Lidia alivyokuja kumfahamu Paulo na waandamani wake vizuri zaidi kwa sababu aliwakaribisha nyumbani. Sasa ninajaribu kuiga mfano wake.”—Mónika, Hungaria.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

“KWA NINI NI VIBAYA KUFANYA NGONO KABLA ya NDOA?”

Katrina, msichana mwenye umri wa miaka 16 kutoka Marekani, alipewa mgawo wa kutoa hotuba mbele ya darasa lake kuhusu kichwa chochote ambacho angechagua. Akitumia kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, alichagua kuzungumzia kichwa “Kwa Nini Ni Vibaya Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa?” Wazazi wake wanaeleza hivi: “Katika hotuba yake, Katrina alieleza maana ya ‘kujiepusha kabisa na ngono,’ akaeleza hatari za kufanya ngono kabla ya ndoa, na pia matokeo mabaya ya kuvunja viwango vya maadili vya Mungu. Katrina pia alisoma manukuu yaliyo kwenye kitabu hicho, yanayoonyesha jinsi vijana fulani walivyohisi baada ya kuvunja viwango vya Mungu. Kisha akawapa wanafunzi wenzake nafasi ya kumwuliza maswali, naye akawajibu. Baada ya hotuba yake, mwalimu alimwandikia ujumbe ambao kwa sehemu ulisema hivi: ‘Asante kwa kusema ukweli na kwa kuleta nuru katika ulimwengu uliojaa giza. Endelea kuwa imara katika imani.’”