Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Ninaweza Kueleza kwa Njia Gani Maoni ya Biblia Kuhusu Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Ninaweza Kueleza kwa Njia Gani Maoni ya Biblia Kuhusu Ngono Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Wakati wa sherehe ya kupewa tuzo, wanawake wawili ambao ni waigizaji maarufu wanasalimiana kwa kubusiana kimahaba! Kwanza watazamaji wanaachwa vinywa wazi kwa mshangao, kisha wanashangilia kwa vigelegele! Mashoga wanasema huo ni ushindi. Wachambuzi wanasema hiyo ni mbinu ya kuvutia umati ili kupata umaarufu. Vyovyote vile, video kuhusu busu hilo zitaonyeshwa tena na tena kwenye televisheni na kusambazwa kwa wingi sana kwenye Intaneti.

KAMA kisa kilichosimuliwa hapo juu kinavyoonyesha, mtu mashuhuri anaposema waziwazi kwamba yeye ni shoga wa kiume au wa kike, au anavutiwa kingono na watu wa jinsia zote mbili, habari hiyo huzungumziwa sana katika vyombo vya habari. Watu fulani huwasifu watu hao kwa ujasiri wao; wengine huwashutumu kwa mwenendo wao mpotovu. Mbali na maoni hayo yanayotofautiana sana, watu wengi huona ngono kati ya watu wa jinsia moja kuwa mtindo mwingine tu wa maisha. “Nilipokuwa shuleni, hata watoto ambao si mashoga walihisi kwamba ikiwa ungechukizwa na mashoga, basi ungeonwa kuwa na ubaguzi na mwenye kuhukumu,” anasema Daniel, mwenye umri wa miaka 21. *

Maoni kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja hutofautiana kati ya watu wa umri na nchi mbalimbali. Lakini Wakristo ‘hawachukuliwi huku na huku na kila upepo wa fundisho.’ (Waefeso 4:14) Badala yake, wao hufuata maoni ya Biblia.

Biblia ina maoni gani kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja? Ikiwa unafuata viwango wa Biblia vya maadili, utawajibu namna gani watu wanaokuona kuwa mwenye ubaguzi, mwenye kuhukumu, au hata anayewachukia mashoga? Chunguza maswali yanayofuata na majibu unayoweza kutoa.

Biblia inasema nini kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?

Biblia inaeleza waziwazi kwamba Mungu alikusudia ngono ifanywe tu na mwanamume na mwanamke ambao wamefunga ndoa. (Mwanzo 1:27, 28; Mambo ya Walawi 18:22; Methali 5:18, 19) Biblia inaposhutumu uasherati, inatia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja na pia kati ya watu wa jinsia tofauti. *Wagalatia 5:19-21.

Mtu akikuuliza: “Una maoni gani kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?”

Unaweza kumjibu: “Mimi siwachukii mashoga, lakini siungi mkono mwenendo wao.”

✔ Kumbuka: Ikiwa unaongozwa na viwango vya Biblia vya maadili, basi huo ndio mtindo wa maisha ambao umechagua, na una haki ya kuufuata. (Yoshua 24:15) Usiaibikie maoni yako.—Zaburi 119:46.

Je, si Wakristo wanapaswa kuwaheshimu watu wote, haidhuru wanavutiwa kingono na watu wa jinsia gani?

Bila shaka. Biblia inasema hivi: “Waheshimuni watu wa namna zote” au kama tafsiri ya Union Version inavyosema, “Waheshimuni watu wote.” (1 Petro 2:17) Kwa hiyo, Wakristo hawawachukii mashoga. Wao huwaonyesha watu wote fadhili kutia ndani mashoga.—Mathayo 7:12.

Mtu akikuuliza: “Je, maoni yako kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja hayakufanyi uwabague mashoga?”

Unaweza kumjibu: “Hapana. Ninachukia mwenendo wao, si wao wenyewe.”

✔ Unaweza kuongezea hivi: “Kwa mfano, mimi sivuti sigara. Zoea hilo hunichukiza sana. Lakini tuseme wewe ni mvutaji-sigara na maoni yako yanatofautiana na yangu. Singekubagua kwa sababu ya maoni yako, na nina hakika hungenibagua kwa sababu ya maoni yangu, sivyo? Tunaweza kutumia kanuni hiyohiyo kuhusu maoni yetu yanayotofautiana kuelekea ngono kati ya watu wa jinsia moja.”

Si Yesu alifundisha kwamba tunapaswa kuwakubali watu wengine? Ikiwa ndivyo, je, Wakristo hawapaswi kulegeza msimamo wao kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja?

Yesu hakuwatia moyo wafuasi wake wakubali mitindo yote ya maisha. Badala yake, aliwafundisha kwamba njia ya kupata wokovu imefunguliwa kwa “kila mtu anayemwamini.” (Yohana 3:16) Kumwamini Yesu kunatia ndani kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya maadili, ambavyo hushutumu mienendo fulani, kutia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja.—Waroma 1:26, 27.

Mtu akisema: “Mashoga hawawezi kubadili mwenendo wao; walizaliwa na mwelekeo huo.”

Unaweza kumjibu: “Biblia haizungumzi kuhusu maumbile ya mashoga, ingawa inakubali kwamba mazoea fulani yamekita mizizi ndani yetu. (2 Wakorintho 10:4, 5) Hata ingawa watu fulani wana mwelekeo wa kupendezwa kingono na watu wa jinsia yao, Biblia inawaambia Wakristo waepuke ngono kati ya watu wa jinsia moja.”

✔ Dokezo: Badala ya kujihusisha katika mjadala wa kwa nini watu hutamani kufanya ngono na watu wa jinsia yao, kazia kwamba Biblia inakataza ngono kati ya watu wa jinsia moja. Unaweza kutoa mfano na kusema: “Unajua kwamba watu wengi husema ujeuri hutokana na chembe za urithi na kwa sababu hiyo, watu fulani wana mwelekeo wa kuwa wajeuri. (Methali 29:22) Vipi ikiwa maoni hayo yangekuwa ya kweli? Kama unavyojua, Biblia hushutumu milipuko ya hasira. (Zaburi 37:8; Waefeso 4:31) Je, viwango hivyo vinawabagua watu fulani kwa sababu huenda wakawa na mwelekeo wa kuwa wajeuri?”

Kwa nini Mungu amwambie mtu anayevutiwa kingono na mtu wa jinsia yake aepuke ngono ya aina hiyo? Kufanya hivyo ni kumtesa.

Kufikiri kwa njia hiyo kunategemea wazo la kwamba lazima mwanadamu atosheleze tamaa zake za ngono. Biblia inawaheshimu wanadamu kwa kuwahakikishia kwamba wanaweza kuchagua kutotosheleza tamaa zisizofaa za ngono ikiwa wanataka.—Wakolosai 3:5.

Mtu akisema: “Hata kama wewe si shoga, unapaswa kubadili maoni yako kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja.”

Unaweza kumjibu: “Tuseme mimi siungi mkono kucheza kamari lakini wewe unaunga mkono. Je, lingekuwa jambo la hekima usisitize kwamba nibadili maoni yangu kwa sababu tu mamilioni ya watu hucheza kamari?”

✔ Kumbuka: Watu wengi (kutia ndani mashoga) hufuata maadili fulani ambayo huwafanya wachukizwe na mambo kama vile ulaghai, ukosefu wa haki, au vita. Biblia inakataza matendo hayo; pia inashutumu matendo fulani ya kingono, kutia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja.—1 Wakorintho 6:9-11.

Biblia haikosi usawaziko wala haibagui. Inawaagiza watu wanaovutiwa kingono na watu wa jinsia yao waepuke kile ambacho wale wanaovutiwa na watu wa jinsia tofauti wanahimizwa kufanya, yaani, ‘waukimbie uasherati.’—1 Wakorintho 6:18.

Wakristo huwa na ujasiri wa kukataa maoni yanayofuatwa na wengi

Ukweli wa mambo ni kwamba ili waishi kupatana na viwango vya Biblia, mamilioni ya watu wanaovutiwa kingono na watu wa jinsia tofauti hujizuia licha ya vishawishi ambavyo huenda wakakabili. Idadi hiyo inatia ndani waseja wengi ambao hawana matumaini ya kufunga ndoa na pia wale ambao wamefunga ndoa na mtu asiyeweza kufanya ngono kwa sababu ya ulemavu fulani. Watu hao huishi kwa furaha bila kutosheleza tamaa zao za ngono. Watu walio na mwelekeo wa kuvutiwa kingono na watu wa jinsia yao wanaweza kufanya vivyo hivyo ikiwa wanataka kweli kumpendeza Mungu.—Kumbukumbu la Torati 30:19.

^ fu. 4 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 7 Katika Biblia, neno “uasherati” halimaanishi tu kufanya ngono bali pia matendo kama vile kumpiga mtu mwingine punyeto, ngono ya mdomo au ya mkundu.

MAMBO YA KUFIKIRIA

  • Kwa nini Mungu amewawekea wanadamu sheria za maadili?

  • Unafaidika kwa njia gani kwa kufuata sheria za Biblia za maadili?