Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tuvunje Uhusiano Wetu?

Je, Tuvunje Uhusiano Wetu?

Vijana Huuliza

Je, Tuvunje Uhusiano Wetu?

“Miezi mitatu baada ya uhusiano wetu kuanza, tulikuwa tukisema kwamba tunafaana kabisa. Tulizungumza kuhusu kuishi pamoja milele kana kwamba ingekuwa hivyo.”—Jessica. *

“Nilivutiwa sana na kijana huyo kwa muda, kisha baada ya miaka kadhaa akaanza kupendezwa nami! Nilipenda sana kuwa na mpenzi mwenye umri mkubwa ambaye angenitunza.”—Carol.

Baada ya muda, Jessica na Carol walivunja uhusiano na marafiki wao. Kwa nini? Je, ulikuwa ujinga kuachana na vijana wazuri hivyo?

UMEKUWA rafiki yake wa karibu kwa mwaka mmoja hivi. Mwanzoni, ulikuwa na hakika kwamba yeye “ndiye.” Nyakati nyingine hata unaweza kukumbuka hisia za kimahaba ambazo ulihisi mwanzoni mwa uhusiano wenu. Lakini sasa una mashaka. Je, upuuze mawazo hayo? Utajua jinsi gani ikiwa mnapaswa kuvunja uhusiano wenu?

Kwanza kabisa, unahitaji kukubali ukweli huu: Kupuuza dalili za hatari katika uhusiano ni kama kupuuza ishara za kumwonya dereva zilizo ndani ya gari. Tatizo haliwezi kujiondoa; huenda likawa baya zaidi. Ni nini baadhi ya dalili za hatari ambazo unapaswa kutambua katika uhusiano?

Uhusiano unakuwa wa karibu haraka sana. Matatizo yanaweza kutokea wakati uhusiano wa kimahaba unapokuwa wa karibu haraka sana. “Tulikuwa tunaandikiana barua-pepe, tunawasiliana kupitia Intaneti, na kupigiana simu,” anakumbuka Carol. “Njia hizo za mawasiliano zinaweza kuwa zenye nguvu zaidi kuliko kuzungumza na mtu uso kwa uso, kwa sababu uhusiano unakuwa wa karibu haraka ajabu!” Msipoteze nafasi ya kufahamiana vizuri. Uhusiano haupaswi kuwa kama magugu yanayokua haraka-haraka na mwishowe yananyauka. Badala yake, unapaswa kuwa kama mmea wenye thamani unaokua polepole.

Anakuchambua na kukushushia heshima. “Sikuzote rafiki yangu alinishushia heshima,” anasema msichana anayeitwa Ana, “lakini nilitaka sana kuwa naye.” Anaongeza, “Nilijiruhusu kuwa katika hali ambazo sikuwahi kuwazia kwamba ningejikuta ndani yake!” Biblia inashutumu “matukano.” (Waefeso 4:31) Maneno ya kumshushia mtu heshima—hata yanaposemwa kwa upole na kwa sauti ya chini—hayapaswi kutumiwa katika uhusiano wenye upendo.—Methali 12:18.

Anakasirika haraka. Methali 17:27 inasema hivi: “Mtu mwenye utambuzi ana roho ya utulivu.” Erin aligundua kwamba rafiki yake alikuwa na tatizo la kukasirika haraka. Anasema, “Tulipokosa kuelewana, angenisukuma, na mara nyingine niliachwa na mikwaruzo.” Biblia inawaambia Wakristo: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele . . . na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Mtu ambaye hawezi kujizuia hayuko tayari kuwa na urafiki wa karibu na mtu wa jinsia tofauti.—2 Timotheo 3:1, 3, 5.

Anataka uhusiano wetu uwe wa siri. “Rafiki yangu hakutaka wengine wajue kwamba tulikuwa na urafiki wa karibu,” anakumbuka Angela. “Hata alikasirika baba yangu alipojua kuhusu jambo hilo!” Bila shaka, kunaweza kuwa na sababu zinazofaa za kutotangazia ulimwengu wote kuhusu uhusiano huo. Lakini kukataa kuwaambia wale walio na haki ya kujua kunaweza kuashiria tatizo.

Hana mpango wa kufunga ndoa. Wakristo wanatambua kwamba urafiki wa karibu kati ya watu wa jinsia tofauti umekusudiwa kumsaidia mwanamume na mwanamke wajue ikiwa wanaweza kuoana. Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba unapaswa kufanya mipango ya arusi mara tu mnapoanza urafiki. Mara nyingi, watu hawafungi ndoa na mtu wa kwanza wa jinsia tofauti wanayeanzisha urafiki naye. Hata hivyo, mtu hapaswi kuwa na urafiki wa karibu na mtu wa jinsia tofauti ikiwa hayuko tayari kukubali majukumu ya ndoa.

Urafiki wetu umevunjika mara nyingi. Methali 17:17 inasema: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote.” Hilo halimaanishi kwamba sikuzote mtakubaliana. Lakini uhusiano ambao unavunjika mara kwa mara huenda ni ishara ya kwamba kuna tatizo kubwa zaidi. Hilo ni jambo ambalo Ana alikuja kutambua baada ya muda. “Mara nyingi uhusiano wetu ulipovunjika, niliumia sana moyoni!” anasema. “Nilijitahidi kurekebisha uhusiano ambao sikuuhitaji.”

Ananishinikiza tufanye ngono. “Kama unanipenda, utakubali.” “Tunapaswa kuboresha uhusiano wetu.” “Ngono ya kweli inahusisha mahusiano ya kimwili.” Hayo yote ni baadhi maneno ambayo vijana wametumia ili kuwashinikiza wasichana wafanye ngono nao. Andiko la Yakobo 3:17 linasema: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili.” Unastahili kupata rafiki aliye safi kiadili na anayeheshimu mipaka yako ya kimahaba. Usikubali kushinikizwa hata kidogo!

Wengine wamenionya kumhusu. Biblia inasema hivi: “Tafuta mashauri kadiri unavyoweza, na utafaulu; bila hayo hautafaulu.” (Methali 15:22, Today’s English Version) “Huwezi kupuuza maoni ya watu wa familia na marafiki wako wa muda mrefu, pia huwezi kupuuza dalili zinazokuonyesha kwamba uhusiano huo si mzuri,” anasema Jessica. “Kadiri unavyopuuza kile ambacho watu wengine wanasema, ndivyo unavyofanya hali yako iwe mbaya.”

Mambo yaliyotajwa hapo juu ni baadhi ya ishara za matatizo katika uhusiano. * Ikiwa una urafiki wa karibu na mtu wa jinsia tofauti, je, ana baadhi ya matatizo yaliyotajwa? Andika hapa chini mambo ambayo huenda yakakutia wasiwasi.

․․․․․

Jinsi ya Kuvunja Uhusiano

Ikiwa umeamua ni vema kuvunja uhusiano, utafanya nini? Kuna njia mbalimbali lakini fikiria mambo yafuatayo.

Uwe jasiri. “Nilikuwa nimemtegemea sana mpenzi wangu hivi kwamba niliogopa kumwacha,” anasema msichana anayeitwa Trina. Unahitaji ujasiri ili useme uhusiano unapohitaji kuvunjwa. Lakini ni jambo linalofaa kueleza hisia zako. (Methali 22:3) Hilo litakusaidia kuweka mipaka thabiti kuhusu mambo ambayo utakubali na yale utakayokataa katika uhusiano na mtu wa jinsia tofauti na hatimaye katika ndoa.

Tenda kwa haki. Ikiwa mtu angetaka kuvunja uhusiano na wewe, ungetaka akutendee jinsi gani? (Mathayo 7:12) Ni kweli kwamba mpenzi wako anastahili mengi zaidi kuliko tu kumwandikia barua-pepe au ujumbe mfupi wa simu unaosema “Uhusiano wetu umekwisha!”

Tafuta mahali panapofaa. Je, mnapaswa kuzungumza ana kwa ana au kupitia simu? Je, unapaswa kuandika barua au kuzungumza naye? Mambo mengi yanategemea hali zenu. Hampaswi kukutana mahali ambapo utahatarisha usalama wako, wala si jambo la busara kukutana mahali pasipo na watu ambapo tamaa mbaya huenda zikaamshwa.—1 Wathesalonike 4:3.

Sema kweli. Sema waziwazi kwa nini unahisi kwamba uhusiano huo hauwezi kuendelea. Ikiwa unahisi kwamba rafiki yako amekutendea isivyofaa, mwambie. Eleza maoni yako. Kwa mfano, badala ya kusema, “Sikuzote unanishushia heshima,” mwambie, “Mimi huhisi nimeshushiwa heshima unapo . . .”

Uwe tayari kusikiliza pia. Je, kuna jambo ambalo hukuelewa vizuri kuhusu hali hiyo? Usiruhusu ushawishiwe na maneno ya ujanja, lakini wakati huohuo, uwe mwenye usawaziko na uchunguze mambo yote. Kwa hekima, Biblia inawashauri Wakristo wawe ‘wepesi kuhusu kusikia, si wepesi wa kusema.’—Yakobo 1:19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 16 Kwa habari zaidi ona Amkeni! la Mei (Mwezi wa 5) 2007, ukurasa wa 18-20.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Andika hapa chini mambo unayoona mpenzi wako anapaswa kuwa nayo. ․․․․․

▪ Ni mambo gani unayoona kuwa hapaswi kufanya? ․․․․․

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

MTU UNAYECHAGUA KUWA NA UHUSIANO NAYE ANAPASWA . . .

□ kuwa na imani kama yako.—1 Wakorintho 7:39.

□ kuheshimu mipaka yako ya kiadili.—1 Wakorintho 6:18.

□ kukujali wewe na watu wengine.—Wafilipi 2:4.

□ kuwa na sifa nzuri.—Wafilipi 2:20.

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

JIHADHARI IKIWA RAFIKI YAKO . . .

□ anasisitiza mambo yafanywe anavyotaka.

□ anakufanya uhisi una hatia, mjinga, au hufai.

□ anajaribu kukutenganisha na marafiki wako na watu wa familia.

□ anataka kujua kila wakati umeenda wapi.

□ anakushutumu bila kuwa na msingi kwamba unachezea wengine kimapenzi.

□ anatoa vitisho au anakuambia lazima utimize jambo fulani kwa wakati fulani la sivyo atakuacha.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kupuuza dalili za hatari katika uhusiano ni kama kupuuza ishara za kumwonya dereva zilizo ndani ya gari

OILI INAISHA