Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Watoto Wenye Matatizo ya Kujifunza

Kuwasaidia Watoto Wenye Matatizo ya Kujifunza

Kuwasaidia Watoto Wenye Matatizo ya Kujifunza

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI MEXICO

Steven ana tatizo la kusoma. Kila mara anapojua kwamba ataombwa asome kwa sauti darasani, yeye huanza kuumwa na tumbo.

Ingawa mwalimu wake anamtia moyo, Maria ana tatizo la kuandika kwa mwandiko wenye kusomeka vizuri. Anatumia saa nyingi ili kumaliza kazi ya shuleni.

Ingawa Noah anasoma migawo aliyopewa shuleni kwa kurudia-rudia, bado anasahau yale ambayo amesoma. Kwa sababu hiyo, mara nyingi yeye huanguka mitihani.

STEVEN, Maria, na Noah wana matatizo ya kujifunza, na tatizo linalowapata watoto wengi ni kushindwa kusoma vizuri. Kwa mfano, tatizo moja ni kutatanishwa na herufi zinazokaribia kufanana linaloitwa dyslexia. Tatizo lingine ni kutoweza kuandika kwa mwandiko unaosomeka vizuri linaloitwa dysgraphia, na tatizo la kushindwa kuelewa mawazo ya hesabu linaloitwa dyscalculia. Hata hivyo, wengi walio na matatizo ya kujifunza ni werevu kwa kadiri fulani.

Dalili za matatizo ya kujifunza zinatia ndani kuchelewa kuanza kuzungumza, tatizo la kutamka maneno yaliyo na miisho inayofanana, kutamka maneno vibaya kwa kawaida, kuzungumza kama mtoto kwa muda mrefu, tatizo la kujifunza herufi na namba, kushindwa kutamka herufi katika maneno rahisi, kutatanishwa na maneno yaliyo karibu kufanana, na kushindwa kufuata maagizo. *

Kumsaidia Mtoto Wako Akabiliane na Tatizo

Unaweza kufanya nini ikiwa mtoto wako anaonekana ana tatizo la kujifunza? Kwanza mpeleke ili achunguzwe uwezo wake wa kusikia na kuona ili hilo lisiwe ndilo tatizo. * Kisha afanyiwe uchunguzi wa kitiba. Ikiwa mtoto wako ana tatizo la kujifunza, atahitaji umtegemeze kihisia. Kumbuka kwamba tatizo la kujifunza halihusiani na werevu wa mtoto wako.

Tumia vizuri nafasi za pekee za kujifunza ambazo mtoto wako anaweza kupata kama vile mafunzo baada ya shule. Omba msaada wa mwalimu wake. Huenda mtoto wako anaweza kuruhusiwa kuketi mbele darasani na kupewa wakati wa ziada kumaliza kazi za shule. Mwalimu wake anaweza kumpa maagizo akitumia maandishi na maneno na amruhusu afanye mtihani kwa kuzungumza badala ya kuandika. Kwa kawaida, watoto wenye matatizo ya kujifunza ni wasahaulifu na hawafanyi mambo kwa mpango, hivyo, inafaa kuwa na vitabu vingine vya kusoma nyumbani. Kompyuta yenye mfumo wa kumsaidia kutambua maandishi yenye makosa inaweza kutumiwa darasani na nyumbani.

Panga vipindi vifupi vya kusoma kila siku. Ni vizuri mtoto aliye na tatizo la kusoma asome kwa sauti ili mzazi atoe madokezo na kumsahihisha. Kwanza, soma kwa sauti, huku mtoto wako akifuatana nawe. Kisha, someni sehemu hiyohiyo pamoja kwa sauti. Halafu mwache mtoto wako asome peke yake kwa sauti. Mwambie atumie rula chini ya kila sentensi na atie alama maneno magumu. Huenda ukatumia dakika 15 tu kila siku kufanya hivyo.

Unaweza kumsaidia aboreshe uwezo wake wa hesabu kupitia kazi za kawaida kama vile kupima kiasi cha viungo katika upishi, kutumia rula kutengeneza vitu vya mbao, au kununua bidhaa. Karatasi zenye visanduku vidogo na michoro zinaweza kumsaidia kutatua maswali ya hesabu. Ikiwa ana tatizo la kuandika kwa mwandiko usiosomeka vizuri, jaribu kutumia karatasi yenye mistari yenye nafasi kubwa na penseli yenye risasi pana. Herufi zenye sumaku inayoziwezesha kushikiliwa kwenye ubao wa chuma zinaweza kumsaidia mtoto wako ajue kufuatanisha herufi.

Pia kuna mbinu zinazofaa za kushughulikia watoto wenye ADHD. Kabla ya kuzungumza na mtoto mwenye matatizo ya kukaza fikira, mtazame ana kwa ana. Tafuta mahali patulivu ambapo anaweza kufanyia kazi za shule, na mruhusu mtoto wako apumzike mara nyingi. Tumia umachachari wake kwa kumpa kazi zinazomfanya afanye kazi kwa bidii, kama kumtembeza mbwa.

Unaweza Kufanikiwa

Sitawisha sifa za mtoto wako, na umtie moyo kukuza uwezo au kipawa chochote alicho nacho. Msifu na kumpa zawadi kwa jambo lolote analofanya, hata jambo dogo. Gawa mradi mkubwa katika sehemu kadhaa ndogondogo ili afurahie kuzitimiza. Tumia picha au michoro ya kuonyesha hatua anazopaswa kufuata ili amalize mradi fulani.

Maishani, ni muhimu kwa vijana kujua kusoma, kuandika, na kuelewa mawazo ya hesabu. Uwe na hakika kwamba mtoto wako akichochewa inavyofaa na kusaidiwa anaweza kujifunza lakini huenda akajifunza kwa njia tofauti na wengine na akachukua muda mrefu zaidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Mara nyingi, matatizo ya kujifunza huambatana na Tatizo la Upungufu wa Makini Kutokana na Utendaji wa Kupita Kiasi (ADHD), tatizo ambalo huonekana mtoto anapokuwa mwenye umachachari, kufanya mambo haraka-haraka, na kutokuwa na uwezo wa kukaza fikira. Ona Amkeni! la Februari 22, 1997 (22/2/1997), ukurasa wa 5-10.

^ fu. 9 Ni rahisi zaidi kwa wavulana kupatwa na tatizo la dyslexia na umachachari kuliko wasichana.

[Picha katika ukurasa wa 11]

NAFAIDIKA KUTOKANA NA TATIZO LA KUJIFUNZA

“Nilipotazama maandishi kwenye ukurasa, yalionekana kama michoro isiyo na maana yoyote. Ni kama tu nilikuwa nikitazama maneno ya lugha nyingine. Sikuelewa maneno yoyote hadi mtu mwingine alipoyasoma kwa sauti. Walimu walifikiri nilikuwa mvivu au nilikosa heshima au sikuwa na bidii au sikuwa nikisikiliza masomo. Walikuwa wamekosea sana. Nilikuwa nikisikiliza na nilikuwa na bidii sana, lakini sikuweza kuelewa jinsi ya kusoma na kuandika. Masomo mengine kama hesabu, hayakuwa magumu kwangu. Nilipokuwa mtoto nilijifunza haraka kukazia fikira michezo, kazi za ufundi, sanaa, na kitu chochote kilichohusisha kutumia mikono yangu, maadamu tu hakikuhusu kusoma na kuandika.

“Baadaye, niliamua kufanya kazi ya mikono, kwa hiyo, nikawa fundi. Kwa sababu hiyo, nimepata pendeleo la kushiriki katika miradi mitano ya ujenzi wa kimataifa ya Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu ninahitaji kutia jitihada nyingi sana kusoma, inakuwa rahisi zaidi kwangu kukumbuka mambo mengi niliyosoma. Jambo hilo linanisaidia sana hasa katika huduma yangu ya Kikristo, kwa kuwa mimi ni mwanafunzi wa Biblia. Hivyo, badala ya kuona tatizo langu kuwa udhaifu, ninaliona kuwa jambo linalonifaidi.”—Peter, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova mwenye tatizo la “dyslexia.”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Watoto wanaweza “kupiga picha akilini” wanaposikiliza kwa makini