Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kupingaje Vishawishi?

Ninaweza Kupingaje Vishawishi?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kupingaje Vishawishi?

▪ Karen ameenda kwenye karamu na baada ya dakika kumi tu anawaona wavulana wawili wakiingia wakiwa na karatasi kubwa za plastiki. Kila mtu anajua kilicho katika karatasi hizo. Mapema, alikuwa amesikia wavulana hao wakisema kwamba kutakuwa na “pombe nyingi” katika karamu hiyo. Bila shaka, Karen hakuwaambia wazazi wake kuhusu jambo hilo. Alifikiria kwamba wavulana hao walikuwa wakifanya mzaha tu. Kulipaswa kuwa na watu wazima katika nyumba hiyo.

Ghafula, Karen anasikia sauti anayoifahamu nyuma yake. “Mbona unasimama hapo ukiwa umezubaa, kana kwamba unataka kutuharibia starehe?” Karen anageuka na kumwona rafiki yake Jessica akiwa ameshika chupa mbili za bia zilizofunguliwa. Jessica anamwambia Karen hivi, huku akimpa bia moja, “Usiniambie kwamba wewe ni mtoto!”

Karen anataka kukataa. Lakini anahisi kwamba amekazwa sana kuliko alivyotarajia. Tatizo si pombe. Ni kwamba tu Jessica ni rafiki yake, na Karen hataki kuonekana kuwa mtu anayewaharibia wengine starehe, kama Jessica alivyosema. Isitoshe, Jessica ni mmoja kati ya wasichana wazuri. Na ikiwa yeye anakunywa, basi shida iko wapi? ‘Ni bia moja tu,’ Karen anajiambia. ‘Si sawa na kutumia dawa za kulevya au kufanya ngono.’

UNAPOKUWA kijana, vishawishi huja katika njia nyingi. Mara nyingi, vishawishi vinahusisha watu wa jinsia tofauti. “Wasichana shuleni ni wajasiri,” anasema Ramon aliye na umri wa miaka 17. * “Wanapenda kukugusa wakitaka kuona utawaruhusu wakushike-shike kadiri gani. Hawaachi hata ukiwakataza!” Deanna, ambaye pia ana umri wa miaka 17, amepatwa na hali kama hiyo. “Mvulana mmoja alikuja na kunizungushia mkono wake,” anasema. “Niliupiga mkono wake na kumwambia, ‘Unafanya nini? Hata sikufahamu!’”

Huenda wewe pia ukawa unakabili vishawishi, na inaweza kuonekana kwamba mkazo ni mwingi sana. Kama Mkristo mmoja anavyosema, “vishawishi ni kama mtu anayeendelea kubisha mlango wako bila kujali ishara inayosema Usisumbue.” Je, wewe husikia ukisumbuliwa hivyo mara nyingi kuliko unavyotaka? Kwa mfano, je, unapatwa na vishawishi vifuatavyo?

□ Kuvuta sigara

□ Kunywa pombe

□ Kutumia dawa za kulevya

□ Kutazama ponografia

□ Kujihusisha katika uasherati

□ Mambo mengine ․․․․․

Ikiwa umetia alama katika yoyote ya mambo yaliyo juu, usiseme kwamba wewe hustahili kuwa Mkristo. Unaweza kujifunza kudhibiti tamaa mbaya na kupinga vishawishi. Jinsi gani? Ingefaa kujua chanzo cha vishawishi. Fikiria mambo haya matatu.

1. Kutokamilika. Ni kawaida kwa wanadamu wasiokamilika kuwa na mwelekeo wa kufanya dhambi. Hata mtume Paulo aliyekuwa Mkristo mkomavu, alikiri hivi kwa unyoofu: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” (Waroma 7:21) Ni wazi kwamba mara kwa mara hata mtu mnyoofu zaidi huwa na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho.” (1 Yohana 2:16) Lakini kukazia fikira vishawishi kutafanya hali iwe mbaya zaidi, kwa kuwa Biblia inasema: “Tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”—Yakobo 1:15.

2. Hali zinazotuzunguka. Vishawishi viko kila mahali. “Shuleni na kazini, watu huzungumza kuhusu ngono kila wakati,” anasema Trudy. “Kwenye televisheni na katika sinema, ngono hutukuzwa na kuonyeshwa kuwa yenye kusisimua sana. Ni mara chache sana utaonyeshwa matokeo yake mabaya!” Trudy anajua kutokana na mambo yaliyompata kwamba uvutano huo huwa na nguvu sana. “Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilifikiri kwamba mvulana fulani alikuwa mpenzi wangu,” anakumbuka. “Mama yangu aliniambia kwamba ikiwa nitaendelea kufanya jinsi nilivyokuwa nikifanya, nitapata mimba. Nilishtuka sana kwamba mama yangu angeweza kufikiri hivyo! Miezi miwili baadaye nikapata mimba.”

3. “Tamaa zinazotukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Maneno hayo yanaweza kuhusisha tamaa yoyote inayotokea mtu anapokuwa kijana, kama vile kutamani kukubaliwa au kujaribu kuonekana kuwa mtu mzima. Tamaa hizo si mbaya, lakini zisipochungwa zinaweza kufanya iwe vigumu kupinga vishawishi. Kwa mfano, kutaka kujitegemea kunaweza kukufanya ukatae kanuni nzuri ambazo umefunzwa nyumbani. Hilo ndilo lililompata Steve alipokuwa na umri wa miaka 17. Anasema, “Niliwaasi wazazi wangu na nikafanya kila kitu ambacho walikuwa wamenikataza, na yote hayo niliyafanya muda mfupi tu baada ya kubatizwa.”

Kwa kweli, uvutano ulioelezewa hapo juu una nguvu. Hata hivyo, unaweza kupinga vishawishi. Jinsi gani?

▪ Kwanza, tambua kishawishi kilicho na uvutano mkubwa zaidi kwako. (Huenda umefanya hivyo hapo juu.)

▪ Kisha, jiulize, ‘Ni wakati gani ambapo ni rahisi zaidi kupatwa na kishawishi hiki?’ Tia alama kwenye yoyote kati ya mambo yafuatayo:

□ Nikiwa shuleni

□ Nikiwa kazini

□ Nikiwa peke yangu

□ Wakati mwingine ․․․․․

Kujua ni wakati gani kishawishi kinaweza kukupata kunaweza kukusaidia kukiepuka. Kwa mfano, fikiria mfano uliotolewa mwanzoni mwa makala hii. Ni jambo gani lililopaswa kumwonyesha Karen kwamba kungekuwa na matatizo katika karamu ambayo angehudhuria? Angefanya nini ili kuepuka kishawishi hicho?

▪ Sasa kwa kuwa (1) umetambua kishawishi na (2) umejua ni wakati gani kinaweza kukupata, uko tayari kuchukua hatua zinazofaa. Jambo la kwanza unalopaswa kufanya ni kuamua jinsi ya kupunguza au kuepuka kishawishi hicho. Andika hapa chini mambo ambayo unaweza kufanya.

․․․․․

․․․․․

(Mifano: Ikiwa baada ya shule wewe hukutana na wanafunzi wenzako ambao wanakuhimiza mvute sigara, huenda ukabadili njia unayotumia ili uepuke kukutana nao. Ikiwa mara nyingi unatumiwa ponografia [picha au habari za ngono] kwenye Intaneti bila kukusudia, huenda ukataka kuweka programu za kuzuia vituo kama hivyo. Pia, unaweza kuchagua maneno hususa unapotafuta habari kwenye Intaneti.)

Bila shaka, huwezi kuepuka vishawishi vyote. Wakati fulani huenda utakabiliana na kishawishi chenye nguvu sana, na huenda kikakupata wakati usiotazamia. Unaweza kufanya nini?

Jitayarishe. Yesu alipokuwa “akijaribiwa na Shetani,” alikataa mara moja. (Marko 1:13) Kwa nini? Kwa sababu tayari alijua msimamo wake kuhusu masuala yaliyotokezwa. Hebu fikiria jambo hilo. Yesu hakuwa mashine. Angeweza kushawishika. Lakini tayari alikuwa ameazimia kumtii Baba yake nyakati zote. (Yohana 8:28, 29) Yesu hakuwa na shaka aliposema: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.”—Yohana 6:38.

Katika nafasi zilizo hapa chini, andika sababu mbili kwa nini unapaswa kupinga kishawishi ambacho wewe hukabili mara nyingi na njia mbili ambazo umeazimia kutumia kukipinga.

1. ․․․․․

2. ․․․․․

Kumbuka kwamba unapokubali kushawishika, unakuwa mtumwa wa tamaa zako. (Tito 3:3) Kwa nini uruhusu tamaa zako zikutawale? Sitawisha uwezo wa kudhibiti tamaa zako badala ya kuziacha zikutawale.—Wakolosai 3:5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Je, viumbe wakamilifu wanaweza kushawishika?—Mwanzo 6:1-3; Yohana 8:44.

▪ Unapopinga kishawishi, uaminifu wako unaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?—Methali 27:11; 1 Timotheo 4:12.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

JARIBU KUFANYA HIVI

Chukua dira na uiweke mshale wake ukielekea kaskazini. Kisha weka sumaku kando ya dira hiyo. Ni nini kinachotukia? Mshale hauonyeshi upande sahihi tena. Badala yake, unaelekea upande wa sumaku.

Dhamiri yako ni kama dira hiyo. Inapozoezwa vizuri, itaelekea upande wa “kaskazini” na kukusaidia kufanya maamuzi yenye hekima. Lakini mashirika mabaya, kama sumaku, yana uvutano unaoweza kupotosha maamuzi yako. Tunajifunza nini? Jaribu kuepuka watu na hali zinazoweza kupotosha uwezo wako wa kufanya maamuzi!—Methali 13:20.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

PENDEKEZO

Panga jinsi utakavyojibu mtu anapojaribu kukushawishi kufanya makosa. Usiogope. Huhitaji kusema jambo litakalokufanya uonekane kuwa mwadilifu sana. Mara nyingi, unahitaji tu kukataa kwa uthabiti. Kwa mfano, mwanafunzi mwenzako anapokupa sigara, unaweza kusema: “Usinipe. Mimi sivuti sigara!”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Unapokubali kushawishika, unakuwa mtumwa wa tamaa zako