Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Asanteni kwa Kuwapenda Watu Sana”

“Asanteni kwa Kuwapenda Watu Sana”

“Asanteni kwa Kuwapenda Watu Sana”

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI URUSI

▪ Katika jiji la Chita lililoko mashariki mwa Siberia, kutaniko la Mashahidi wa Yehova lilikutana katika darasa la shule moja kwa ajili ya mikutano ya Kikristo hadi lilipohamia Jumba lao jipya la Ufalme. Kwa sababu Mashahidi walisafisha darasa hilo na kulirekebisha, na walikuwa wenye fadhili na heshima, wasimamizi wa shule hiyo waliandikia kutaniko hilo barua ya shukrani.

Sehemu fulani ya barua hiyo ilisema hivi: “Asanteni kwa kuwapenda watu sana. Upendo huo huonekana wazi na kila mtu mnayekutana naye na asanteni pia kwa kazi zenu za umishonari na kuwasaidia watu wote. Hatutasahau kamwe mambo tuliyojifunza kutoka kwenu kwa miaka tuliyoshirikiana ambayo yanaonyesha kwamba wale wanaomwamini Mungu ni wenye adabu, wanaongozwa na dhamiri, wenye fadhili na, zaidi ya yote, wana miradi, imani, na kusudi maishani.” Mashahidi wa Yehova wanathamini maneno hayo.

▪ Kilomita 5,500 hivi magharibi ya Chita, mwakilishi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Urusi alikaribishwa kwenye sherehe ya pekee iliyoandaliwa na wasimamizi wa wilaya ya St. Petersburg. Kwa nini? Kila mwaka, baada ya theluji kuyeyuka, Mashahidi wa eneo hilo husaidia kuondoa takataka ambazo zimejikusanya kwenye barabara yenye urefu wa kilomita 60 iliyo karibu na ofisi ya tawi. Ili kuonyesha shukrani kwa roho hiyo ya ushirikiano, ofisa mmoja alimpa mwakilishi wa ofisi ya tawi cheti cha sifa njema. Wahudhuriaji walipiga makofi kwa furaha. Inapendeza kwamba msemaji mmoja katika sherehe hiyo alipotamka vibaya jina la Mungu, Yehova, watu kadhaa ambao si Mashahidi walimsahihisha haraka, wakionyesha kwamba wanafahamu jina la Mungu na watu wanaoitwa kwa jina hilo.

Sababu kuu inayowafanya watu walifahamu jina la Mungu ni kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova wapatao 150,000 nchini Urusi. Lengo lao ni kuendelea “kuwapenda watu sana” kwa kuwaambia ujumbe wenye kufariji wa Biblia watu wote watakaosikiliza.—Mathayo 22:39.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ofisi ya tawi ya Urusi ilipata cheti cha sifa njema