Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wanadamu Wanaweza Kutuhakikishia Wakati Ujao Wenye Furaha?

Je, Wanadamu Wanaweza Kutuhakikishia Wakati Ujao Wenye Furaha?

Je, Wanadamu Wanaweza Kutuhakikishia Wakati Ujao Wenye Furaha?

Umetoka tu kuhamia nyumba imara na maridadi iliyojengwa kwa matofali. Umekuwa ukitamani sana nyumba kama hiyo. Unatazamia wakati ujao mzuri! Lakini baada ya miaka michache tu, nyumba hiyo inaharibika na lazima ibomolewe. Unahuzunika sana. Lakini si wewe tu. Nyumba nyingine katika eneo lenu zimeanza kuharibika pia. Uchunguzi unaonyesha kwamba nyumba hizo zimeharibika kwa sababu ya kasoro za ujenzi na matofali mabovu.

KAMA nyumba hiyo, ulimwengu unakabili matatizo makubwa. Licha ya majaribio mengi ya kisiasa na kijamii, na maendeleo makubwa sana katika sayansi na tekinolojia, inaonekana kwamba misingi ya jamii inabomoka. Katika nchi kadhaa, uasi-sheria na machafuko ni mambo ya kawaida. Je, hali mbaya za wanadamu zitawasukuma watatue matatizo yao, waanzishe serikali nzuri hatimaye? Fikiria yale ambayo watu fulani wamesema kuhusu historia ya wanadamu.

“Tumejaribu Kila Kitu”

Katika jitihada za kufanya ulimwengu uwe mahali bora zaidi, wasomi mbalimbali kuanzia mwanafalsafa Mgiriki Plato mpaka mwanafalsafa wa kisiasa na msoshalisti Mjerumani Karl Marx wamependekeza mifumo mingi ya utawala. Kumekuwa na matokeo gani? Makala katika gazeti New Statesman ilisema hivi: “Hatujamaliza umaskini wala kutokeza amani ulimwenguni. Badala yake, inaonekana kwamba tumepata matokeo yaliyo kinyume. Si kwamba hatujajaribu. Tumejaribu kila kitu kuanzia serikali ambazo hudhibiti uchumi mpaka zile ambazo hukubali soko huru; kuanzia Ushirika wa Mataifa hadi kurundika silaha za nyuklia. Tumepigana ‘vita [vingi] vya kukomesha vita’ hivi kwamba tunaamini hatuwezi kukomesha vita, na ni kana kwamba majiji yetu yanashambuliwa.” Makala hiyo iliongeza hivi: “Tulianza karne [ya 20] tukiwa na matumaini makubwa kwamba wanasayansi wangetuokoa na tunaimalizia bila kuamini hata neno moja wanalosema.”

Katika 2001, Eric Hobsbawm, profesa mstaafu wa uchumi na historia ya kijamii katika Chuo Kikuu cha London aliandika kwamba serikali za wanadamu “zinakabili kipindi ambapo utendaji wa wanadamu umeharibu sana mazingira na dunia yote.” Suluhisho la matatizo hayo “halitapendwa na wengi. Katika nchi nyingi, watu wanapenda vitu ambavyo kwa njia ya moja kwa moja au njia nyingine vinadhuru mazingira. Hali hiyo inaonyesha kwamba demokrasia haitafanikiwa wala hakuna tumaini kwa dunia.”

Akitazamia kwamba hivi karibuni wanadamu watapatwa na matatizo makubwa, Stephen Hawking, mwanasayansi na mwandishi aliuliza hivi: “Katika ulimwengu uliovurugika kisiasa, kijamii, na kimazingira, wanadamu wanaweza kuendeleaje kuishi kwa miaka mingine 100?”

Kwa Nini Wanadamu Hawajafaulu?

Biblia tu ndiyo inayotoa maelezo yenye kuridhisha kuhusu kwa nini wanadamu wameshindwa kabisa kujitawala. Kwanza, Biblia inatueleza waziwazi hali ya wanadamu. Kwa mfano, fikiria kweli hizi nne za msingi.

Sisi sote si wakamilifu. “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kama tu vile matofali mabovu yanavyoweza kufanya jengo liharibike hatua kwa hatua na kuporomoka, ndivyo kutokamilika kwa wanadamu kulikorithiwa kunavyoweza kudhoofisha jamii. Kutokamilika kunaonyeshwa kupitia mambo kama vile mielekeo ya ufisadi, ukosefu wa unyoofu, pupa, na kutumia mamlaka vibaya. Hayo si mambo mapya. Miaka 3,000 hivi iliyopita, mwandikaji mwenye hekima wa Biblia aliandika: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.”—Mhubiri 8:9.

Viongozi wa serikali na mahakimu wanakubali kwamba hatujakamilika na tuna udhaifu, nao hujaribu kukabiliana na hali hizo kwa kutunga sheria nyingi. Lakini wanajua kwamba hawawezi kuweka sheria za kuwalazimisha watu wapendane au watii sheria kwa hiari.

Kifo kinatupata. “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake [au nguvu za uhai] hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:3, 4) Mfalme Sulemani wa Israeli la kale ambaye anasemekana kuwa mtawala mwenye hekima zaidi, aliona matokeo ya kazi yake ngumu kuwa ubatili. Aliandika hivi: “Nami, naam mimi, nikachukia kazi yangu yote iliyo ngumu ambayo niliifanya kwa bidii chini ya jua, ambayo ningemwachia mtu ambaye angekuja baada yangu. Na ni nani anayejua kama atakuwa mwenye hekima au mpumbavu? Hata hivyo, atachukua usimamizi wa kazi yangu yote iliyo ngumu . . . Hilo pia ni ubatili.”—Mhubiri 2:18, 19.

Hatuna uwezo wa kujitawala kwa mafanikio. “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Hata ikiwa wanadamu wangekuwa wakamilifu, Biblia inafundisha kwamba kulingana na kusudi la awali la Mungu, Mungu hakuwapa haki ya kujitawala wala uwezo wa kufanya hivyo kwa mafanikio. Kwa mfano, kwa nini watu huudhiwa na wazo la mwanadamu mwingine au kikundi cha watu kuwaambia wanachopaswa kufanya au kuwawekea viwango vya maadili? Ni kwa sababu tuliumbwa ili tupate mwongozo kutoka kwa mamlaka ya juu zaidi. Mamlaka hiyo ni Mungu.—Isaya 33:22; Matendo 4:19; 5:29.

Wanadamu wanaongozwa na mtawala asiyeonekana. “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu”—Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Ikiwa wakurugenzi wa kampuni fulani ni wafisadi sana na hawawezi kuchukuliwa hatua yoyote, mfanyakazi wa kawaida angefanya nini ili kurekebisha hali? Hawezi kufanya mengi. Ndivyo ilivyo kuhusu kutatua matatizo yanayosababishwa na watawala wasioonekana wa ulimwengu huu, yaani, roho waovu wanaofanya kazi chini ya uongozi wa Shetani. Biblia inawataja watawala hao kuwa “serikali,” “mamlaka,” “watawala wa ulimwengu wa giza hili,” na “majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.”—Waefeso 6:12.

Hata hivyo, Biblia haifunui tu udhaifu wa wanadamu na watawala wa ulimwengu wasioonekana. Inatupa pia habari njema kuhusu suluhisho la matatizo yetu yote na hivyo kutupa msingi imara wa kuwa na tumaini.

Muumba Wetu Atatuokoa!

Ikiwa tungeachwa bila msaada wowote hatungeweza kusuluhisha matatizo hayo. Hata mwanadamu mwenye akili nyingi zaidi, mwenye nguvu nyingi zaidi, au tajiri zaidi hana uwezo wa kubadili yoyote kati ya mambo manne yaliyotajwa katika makala hii. * Lakini kama tutakavyoona katika makala inayofuata, Muumba wetu hajatusahau wala kutuacha. Kwa kweli, akiwa mwenye haki ya kutawala, ataondoa kipingamizi chochote kinachozuia tusiwe na furaha. (1 Yohana 4:8) Isitoshe, atafanya hivyo hivi karibuni. Tunajuaje?

Kama ilivyoelezwa katika toleo la mwezi jana la gazeti hili, matukio ya ulimwengu na hali katika jamii zinaonyesha wazi kwamba tuko ndani kabisa ya “siku za mwisho” za ulimwengu huu. (2 Timotheo 3:1; Mathayo 24:3-7) Ulimwengu huu hautaharibiwa kwa maangamizi makubwa ya nyuklia au kwa kugongana na sayari ndogo au kwa njia nyingine ambayo itawaharibu watu wazuri na wabaya bila kubagua. Badala yake, Mungu ndiye atakayeleta uharibifu huo kwa kuwaangamiza waovu, kutia ndani wale wanaosisitiza wanadamu waendelee kutawala. (Zaburi 37:10; 2 Petro 3:7) Wakati huohuo, Mungu atakomesha matatizo yote yanayosababishwa na wale wanaompinga. *2 Wathesalonike 1:6-9.

Baada ya hayo, Muumba atatatua matatizo yetu ya utawala kwa kuukabidhi utawala unaoitwa “ufalme wa Mungu” mamlaka kamili juu ya dunia. (Luka 4:43) Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, serikali hiyo ya ulimwengu wote italeta wakati ujao mzuri ajabu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Ona makala “Je, Ufadhili Ndilo Suluhisho?” kwenye ukurasa wa 19.

^ fu. 18 Swali “Kwa Nini Mungu Anawaacha Watu Wateseke?” linajibiwa kwenye ukurasa wa 106 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

“MATOFALI MABOVU” YA JAMII YA WANADAMU

▪ Sisi sote si wakamilifu.

▪ Kifo kinatupata.

▪ Hatuna uwezo wa kujitawala kwa mafanikio.

▪ Wanadamu wanaongozwa na mtawala asiyeonekana.

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

WANADAMU HAWATAIHARIBU DUNIA!

Kusudi la Muumba la kuifanya dunia iwe makao salama yenye amani kwa ajili ya wanadamu wanaomwogopa Mungu linaungwa mkono na Biblia. Fikiria maandiko yafuatayo.

“Ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.”—Zaburi 104:5.

“Umeiweka dunia imara, ili ipate kuendelea kusimama.”—Zaburi 119:90.

“Kizazi kinaenda, kizazi kinakuja; lakini dunia inasimama mpaka wakati usio na kipimo.”—Mhubiri 1:4.

“Dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

“[Yehova ndiye] Mfanyizaji wa dunia na Mtengenezaji wake, Yeye aliyeifanya imara, ambaye hakuiumba tu bila sababu, ambaye aliiumba ili ikaliwe na watu.”—Isaya 45:18.