Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilichagua kazi inayofaa

Nilichagua kazi inayofaa

Nilichagua kazi inayofaa

SIMULIZI LA SONIA ACUÑA QUEVEDO

Niliambiwa kwamba nitapandishwa cheo kwenye benki niliyokuwa nikifanya kazi. Ningepata umashuhuri na mshahara mnono. Hata hivyo, nilikuwa tu nimealikwa kutumikia katika kutaniko la mbali nikiwa painia wa wakati wote. Ninapofikiria uamuzi niliofanya miaka 32 iliyopita, najua kwamba nilifanya uamuzi wa hekima.

MAMA alilelewa katika dini ya Katoliki lakini alitilia shaka mafundisho ya kanisa hilo. Alijiuliza, ‘Kwa nini sanamu ambazo zimetengenezwa na wanadamu huabudiwa?’ Alitaka sana kujua ukweli, hivyo alienda kanisa moja hadi lingine akitafuta majibu ya maswali yake, lakini hakuyapata.

Siku moja, alipokuwa akipunga upepo nje ya nyumba yetu huko Tuxtla, Mexico, alitembelewa na Shahidi wa Yehova. Kwa kuwa alipendezwa sana na jinsi Shahidi huyo alivyojibu maswali yake kwa kutumia Biblia, alimwalika arudi tena. Aliporudi, Mama alikuwa akimngojea akiwa pamoja na mhudumu wa Kanisa la Adventisti, kasisi wa Kanisa Katoliki, na mhubiri wa Kanisa la Nazareti. Mama aliuliza kuhusu Sabato, na ni Shahidi huyo tu aliyempa jibu lenye kuridhisha kutoka katika Biblia. Kwa kweli, ni yeye tu aliyekuwa na Biblia! Mnamo 1956, miezi sita hivi baada ya Mama kuanza kujifunza Biblia, alibatizwa na akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa na umri wa miaka minane wakati huo.

Baba Apatwa na Wasiwasi

Baba hakumpinga Mama alipokuwa akijifunza Biblia. Lakini alipoanza kutufunza sisi watoto wanne—wavulana wawili na wasichana wawili—na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, Baba aliharibu vitabu vyake. Kwa kuwa alisadiki kabisa kwamba tulikuwa tukipotoshwa, Baba alijaribu kuthibitisha kutoka kwenye Biblia yake ya Kikatoliki kwamba Mashahidi waliweka kwa hila jina la Mungu, Yehova, katika tafsiri yao ya Biblia. Mama alipomwonyesha jina hilo katika Biblia hiyo ya Kikatoliki, alishangaa sana na akaanza kubadili maoni yake kuhusu Mashahidi.—Zaburi 83:18.

Nchini Mexico, siku ya kuzaliwa ya msichana ambaye amefikisha umri wa miaka 15, huwa pindi ya pekee. Nilikuwa nimeacha kusherehekea siku yangu ya kuzaliwa kwa sababu sherehe hiyo haipatani na Maandiko. * Lakini Baba alisisitiza kwamba alitaka kunipa zawadi ya pekee siku hiyo. Nilifikiria jambo hilo kisha nikamwambia: “Badala ya kunipa zawadi, ningependa uandamane nami kwenye kusanyiko lijalo la Mashahidi wa Yehova.” Alikubali, na hilo likamfanya apendezwe zaidi na Biblia.

Usiku mmoja, baada ya dhoruba kali, Baba alijeruhiwa vibaya baada ya kukanyaga waya wa umeme uliokuwa umeanguka. Alipokuwa amelazwa hospitalini, Mashahidi walimtunza saa 24. Hakusahau kamwe wonyesho huo wa upendo wa Kikristo. Baadaye alianza kuhubiri na akajiweka wakfu kwa Yehova. Kwa kuhuzunisha, alikufa Septemba 30, 1975 (30/9/1975), mwezi mmoja kabla ya ubatizo wake. Tunatamani sana kumkumbatia atakapofufuliwa!—Matendo 24:15.

Uvutano Mzuri wa Familia

Sikuzote, dada yangu mkubwa, Carmen, alithamini sana utumishi wa wakati wote. Punde tu baada ya kubatizwa mwaka wa 1967, akawa painia wa kawaida, akihubiri saa 100 hivi kwa mwezi. Baada ya muda, alihamia jiji la Toluca lililoko katikati ya Mexico. Baada ya kumaliza shule, niliajiriwa katika benki moja. Nilibatizwa Julai 18, 1970 (18/7/1970).

Utumishi wa wakati wote ulimletea Carmen furaha nyingi, naye alinitia moyo nijiunge naye huko Toluca. Nilifikiria jambo hilo siku moja nilipokuwa nikisikiliza hotuba iliyoonyesha jinsi wafuasi wa Yesu wanavyopaswa kutumia mali zao za kiroho kumtukuza Mungu. (Mathayo 25:14-30) Nilijiuliza, ‘Je, ninatumia vilivyo zawadi za kiroho nilizokabidhiwa?’ Jambo hilo lilinichochea nitamani kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova.

Kuchagua Kati ya Miradi Miwili

Mnamo 1974, nilituma ombi la kuwa mhudumu painia katika eneo lingine. Muda mfupi baadaye, nikiwa kazini, mzee mmoja Mkristo kutoka Toluca alinipigia. “Tumekuwa tukikusubiri. Mbona hauji?” akaniuliza. Kumbe! nilikuwa nimepata mgawo wa kutumikia nikiwa painia wa pekee huko Toluca, lakini inaonekana kwamba barua ya kunijulisha hilo haikunifikia. (Mapainia wa pekee huhubiri wakati wote mahali popote wanapotumwa na tengenezo la Yehova.)

Mara moja nilimjulisha msimamizi wangu katika benki kwamba nitaacha kazi. “Ngoja kidogo Sonia,” akaniambia, huku akipunga karatasi fulani. “Sasa hivi tumepata habari kwamba wewe ni kati ya wanawake saba ambao wameteuliwa kuwa mameneja wasaidizi. Kampuni yetu haijawahi kuwapa wanawake cheo hicho. Si utakubali cheo hiki?” Kama nilivyotaja mwanzoni mwa simulizi hili, ningepata umashuhuri na mshahara mnono. Licha ya hayo, nilimshukuru msimamizi wangu na kumwambia kwamba nilikuwa nimeamua kumtumikia Mungu kikamili. “Sawa basi,” akaniambia. “Lakini kumbuka, tuko tayari kukuajiri wakati wowote ukihitaji kazi.” Siku mbili baadaye, nilikuwa Toluca.

Upainia wa Pekee Huko Mexico

Carmen alikuwa tayari amekuwa painia wa pekee kwa miaka miwili nilipoungana naye huko Toluca. Tulifurahi sana kuwa pamoja tena! Lakini hatukukaa pamoja kwa muda mrefu. Miezi mitatu tu baadaye, Mama alipata aksidenti na akahitaji mtu wa kumtunza wakati wote nyumbani. Baada ya kuwasiliana na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, tulikubaliana kwamba Carmen arudi nyumbani kumtunza Mama. Alimtunza kwa miaka 17. Wakati huo wote, Carmen alitumikia akiwa painia wa kawaida, na aliwaomba wanafunzi wake wa Biblia waje kujifunza nyumbani ili awe karibu kumsaidia Mama.

Mnamo 1976, nilipewa mgawo mpya huko Tecamachalco, jiji ambalo maskini huishi upande moja wa jiji na matajiri upande ule mwingine. Nilianza kujifunza Biblia na mwanamke mmoja mzee ambaye hakuwa ameolewa. Aliishi na ndugu yake aliyekuwa tajiri. Alipomwambia ndugu yake kwamba alitaka kuwa Shahidi, ndugu yake alitisha kumfukuza kutoka nyumbani kwake. Hata hivyo, mwanamke huyo mnyenyekevu hakutishika. Alipobatizwa, ndugu yake alimfukuza. Ingawa alikuwa na umri wa miaka 86, alimtumaini Yehova kabisa. Alitunzwa na kutaniko na alikuwa mwaminifu hadi kifo chake.

Naenda Shule ya Gileadi, Kisha Bolivia

Nilifurahia sana kuwa huko Tecamachalco kwa miaka mitano. Kisha nikapokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la kwanza la Tanzu la Shule ya Gileadi huko Mexico. Kama neno tanzu linavyoonyesha, shule hiyo ilikuwa tawi la shule ya Gileadi ambayo hufanywa huko New York. Mama na Carmen walisisitiza kwamba nikubali mwaliko huo, kwa hiyo nilifunga safari hadi ofisi ya tawi huko Mexico City, ambapo nilianza mtaala wa majuma kumi. Hilo ndilo lililokuwa tukio muhimu zaidi la kiroho maishani mwangu. Darasa letu lilihitimu Februari 1, 1981 (1/2/1981), nami pamoja na Enriqueta Ayala (sasa anaitwa Fernández) tukatumwa La Paz, Bolivia.

Tulipowasili La Paz, ndugu ambao walipaswa kutulaki hawakuwa wamefika. “Kwa nini tupoteze wakati?” tukaulizana. Hivyo, tulianza kuwahubiria watu kwenye uwanja wa ndege. Baada ya kuhubiri kwa muda wa saa tatu, tulikutana na ndugu kutoka ofisi ya tawi. Walituomba radhi na kutueleza kwamba kulikuwa na msongamano wa magari kwa sababu ya sherehe fulani.

Kuhubiri Sehemu za Milimani

Mji wa La Paz uko karibu mita 3,625 juu ya usawa wa bahari, kwa hiyo mara nyingi tulifunikwa na mawingu. Kwa kuwa hewa hiyo haina oksijeni ya kutosha, tulipumua kwa shida na nilihisi nimechoka baada ya kuwa shambani kwa muda mfupi tu. Ingawa ilinichukua mwaka mzima kuzoea kuishi sehemu za milimani, baraka za Yehova zilipita matatizo yoyote niliyokabili. Kwa mfano, asubuhi moja mnamo 1984, nilipanda mlima wenye miamba hadi kwenye nyumba moja iliyokuwa kwenye kilele. Nikiwa hoi, niligonga mlango na mwanamke mmoja akatokea. Tulikuwa na mazungumzo mazuri, na nikaahidi kurudi baada ya siku chache.

“Sidhani utarudi,” akaniambia. Nilirudi, na mwanamke huyo akaniomba nimfundishe binti yake Biblia. “Hilo ni jukumu la wazazi,” nikamjibu. “Hata hivyo, ukitaka, nitakusaidia.” Alikubali nimfundishe binti yake na hata yeye mwenyewe akakubali kujifunza. Kwa kuwa hakujua kusoma wala kuandika, tulianza kwa kutumia kijitabu Kujifunza Kusoma na Kuandika, ambacho Mashahidi wa Yehova hutumia kuwafunza watu kusoma na kuandika.

Baada ya muda, familia hiyo iliongezeka na kuwa na watoto wanane. Nilipowatembelea, baadhi yao walishikana mikono na kusaidiana kunivuta juu ya mlima. Hatimaye, familia yote, yaani, baba, mama, na watoto wanane walimtumikia Yehova. Wasichana watatu ni mapainia, na kijana mmoja anatumikia akiwa mzee kutanikoni. Baba yao alitumikia akiwa mtumishi wa huduma kutanikoni hadi alipokufa mnamo 2000. Moyo wangu hufurikwa na furaha ninapoifikiria familia hiyo na uaminifu wao! Namshukuru Yehova kwa kuniruhusu kuisaidia familia hiyo.

Naungana Tena na Carmen

Baada ya Mama kufa mwaka wa 1997, Carmen alikubaliwa tena kutumikia akiwa painia wa pekee. Mnamo 1998, alitumwa Cochabamba, Bolivia, nilikokuwa nikitumikia. Naam, tuliungana tena baada ya miaka 18, na Carmen akawekwa rasmi kuwa mmishonari. Tulifurahia sana kuhubiri huko Cochabamba, ambako hali ya hewa ni nzuri hivi kwamba wenyeji husema kwamba mbayuwayu hawabanduki huko! Kwa sasa, tunatumikia huko Sucre, Bolivia, mji maridadi wenye wakazi 220,000, ulio kwenye bonde. Ingawa wakati mmoja jiji hilo liliitwa Vatikani Ndogo kwa sababu lilikuwa na makanisa mengi sana ya Katoliki, sasa lina makutaniko matano ya Mashahidi wa Yehova.

Kwa ujumla, mimi na Carmen tumekuwa mapainia kwa zaidi ya miaka 60, na tumefurahia pendeleo lisilo na kifani la kujifunza Biblia na zaidi ya watu 100 hadi wakabatizwa. Bila shaka, kumtumikia Yehova kwa nafsi yote ndiyo njia ya maisha yenye kuthawabisha kabisa!—Marko 12:30.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Biblia inataja miadhimisho miwili tu ya siku za kuzaliwa iliyofanywa na wapagani, nayo inatajwa kwa njia isiyofaa. (Mwanzo 40:20-22; Marko 6:21-28) Hata hivyo, Neno la Mungu linawatia moyo watu wapeane zawadi kwa kuchochewa kutoka moyoni wala si kwa sababu ya kulazimishwa na jamii au marafiki.—Methali 11:25; Luka 6:38; Matendo 20:35; 2 Wakorintho 9:7.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nilipanda mlima wenye miamba ili kujifunza na familia hii

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikihubiri pamoja na dada yangu, Carmen (yuko upande wa kulia)