Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasaidia Vijana Wakabiliane na Hali Ngumu

Kuwasaidia Vijana Wakabiliane na Hali Ngumu

Kuwasaidia Vijana Wakabiliane na Hali Ngumu

ULIMWENGU na mitindo yake hubadilika daima. Leo, mabadiliko hayo huonekana zaidi kwa sababu ya teknolojia ya kisasa. Kile kilichokuwa maarufu jana si kitu leo, na kinachopendwa leo, kesho kitakuwa kimepitwa na wakati. Mabadiliko hayo ya haraka yamewaathiri sana vijana.

Mabadiliko Makubwa ya Kijamii

Katika miaka ya karibuni, teknolojia imetokeza mabadiliko makubwa ambayo yamewaathiri sana vijana. Kwa mfano, katika nchi nyingi vijana huona simu za mkononi na kompyuta kuwa vyombo muhimu sana vya mawasiliano. Vituo vya kuwasiliana vimesababisha kuwe na mawasiliano mengi ambayo awali hayangewezekana. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 19 nchini Australia anasema hivi: “Unaweza kuwa huna marafiki wowote, kisha mara moja uwe na marafiki chungu nzima kwenye Intaneti.”

Watu wengi wanakubali kwamba simu za mkononi na Intaneti zina manufaa mengi. Hata hivyo, watu wengi huona kwamba hawawezi kuishi bila vifaa hivyo. Profesa Donald Roberts wa Chuo Kikuu anasema kwamba wanafunzi fulani “hawawezi kumaliza dakika chache za mapumziko bila kutumia simu zao za mkononi.” Anasema hivi: “Ni kana kwamba hawawezi kutulia hadi wazungumze kwenye simu, ni kama wanasema ‘mbona kuna kimya kingi sana.’”

Vijana wengine wanakiri kwamba hawawezi kuishi bila vifaa hivyo. Kijana mmoja mwenye umri wa miaka 16 aitwaye Stephanie anakiri hivi: “Mimi ni mraibu wa kutuma ujumbe wa haraka kupitia kompyuta na simu yangu ya mkononi, kwa sababu hiyo ndiyo njia kuu ya kuwasiliana na marafiki wangu. Ninaporudi nyumbani, mimi huenda moja kwa moja kwenye kompyuta na kutumia Intaneti mpaka saa tisa usiku.” Stephanie hulipa kati ya dola 100 hadi 500 kila mwezi kwa ajili ya gharama za simu. “Kufikia sasa, wazazi wangu wananidai zaidi ya dola 2,000 kwa sababu ya gharama za ziada za simu. Lakini nimezoea sana simu yangu ya mkononi hivi kwamba siwezi kufanya mambo yangu ya kawaida bila kuitumia.”

Kuna matatizo mengine zaidi ya pesa zinazotumika. Alipokuwa anafanya utafiti kuhusu maisha ya familia, Elinor Ochs, mtaalamu wa tabia na tamaduni za wanadamu aligundua kwamba mzazi aliporudi nyumbani kutoka kazini, mara nyingi mwenzi wake wa ndoa na watoto walikuwa wakijishughulisha tu na kile walichokuwa wakifanya hivi kwamba mara 2 kati ya 3 hata hawakumsalimu! Waliendelea tu kukazia fikira vifaa vyao vya elektroniki. Ochs anasema, “Tuliona pia jinsi ilivyo vigumu kwa wazazi kujihusisha katika utendaji wa watoto wao.” Anaongezea kusema kwamba utafiti huo ulipokuwa ukiendelea, wazazi walionekana wakijaribu kuepuka kuwasumbua watoto ambao walikuwa wakikazia fikira mambo waliyokuwa wakifanya.

Je, Kuna Madhara ya Kuwasiliana Kwenye Intaneti?

Wazazi na walimu wengi wanahangaishwa na muda ambao vijana wanatumia kwenye vituo vya Intaneti vya kuwasiliana. Vituo hivyo vya Intaneti humwezesha mtu kuanzisha kituo chake na kukiboresha kwa kuweka picha, video, na habari za kibinafsi.

Jambo linalowavutia watu kutumia vituo hivyo ni kwamba vinawawezesha kuwasiliana na marafiki. Vilevile kuanzisha kituo kama hicho humpa kijana nafasi ya kueleza maoni yake. Inaeleweka ni kwa nini vituo hivyo vinavutia sana vijana kwani kipindi cha kubalehe ni wakati ambapo kijana hujaribu kujielewa na kueleza hisia zake katika njia ambayo itawafikia na kuwagusa watu wengine.

Hata hivyo, tatizo moja linalozuka ni kwamba watu fulani hujifafanua kwa kutumia utu wanaotaka kuwa nao badala ya utu wao halisi. “Kuna kijana katika darasa langu ambaye anasema ana umri wa miaka 21 na anaishi Las Vegas,” anasema mvulana mmoja mwenye umri wa miaka 15. Vijana hao wawili wanaishi kilomita 1,600 hivi kutoka Las Vegas.

Ni jambo la kawaida kwa watu kutoa habari za uwongo kama hizo. “Unaweza kufanya jambo lolote kwenye Intaneti,” anasema msichana Mwaustralia mwenye umri wa miaka 18. “Unaweza kujifanya kuwa mtu tofauti kabisa kwani hakuna mtu anayekujua. Unajihisi ukiwa na ujasiri. Unaweza kubuni mambo ili uonekane kuwa mtu mwenye kupendeza zaidi. Unaweza kuingiza picha zako ukiwa umevalia mavazi ambayo kwa kawaida hungevalia au ukifanya mambo ambayo kwa kawaida hungefanya. Unaweza kuandika mambo ambayo wewe mwenyewe huwezi kusema. Unahisi kwamba huwezi kulaumiwa kwa sababu huwezi kupatikana. Hakuna mtu anayekujua vizuri.”

Kama tu njia nyingine za mawasiliano, vituo vya Intaneti vya kuwasiliana vinaweza kuwa na manufaa au madhara. Je, wewe ukiwa mzazi unajua watoto wako wanafanya nini kwenye Intaneti? Je, unahakikisha kwamba wanatumia wakati wao vizuri? * (Waefeso 5:15, 16) Isitoshe, kutumia Intaneti vibaya kunaweza kumhatarisha kijana kwa njia mbalimbali. Baadhi ya njia hizo ni zipi?

Hatari za Kutumia Intaneti

Kwa kuwa watu wanaotumia Intaneti hawajitambulishi, watu wanaowavizia watoto ili hatimaye wafanye nao ngono huona Intaneti kuwa njia rahisi ya kuwanasa. Vijana wanaweza kunaswa bila kutarajia wanapotoa habari za kibinafsi kwenye Intaneti au wanapokubali kukutana na mtu ambaye wamekuwa wakiwasiliana naye. Watu fulani hudai kwamba “watoto hukabili hatari kubwa zaidi ya kufanyiwa ujeuri au kudhulumiwa ndani ya nyumba zao au mahali wanapochezea,” kinasema kitabu Parenting 911. “Hata hivyo, jambo linalowaogopesha wazazi wengi kuhusu watu wanaowavizia watoto ili wafanye nao ngono ni kwamba wanaweza kuingia nyumbani mwao kupitia Intaneti na kuwapotosha watoto wao.”

Teknolojia ya mawasiliano imetumiwa vibaya katika njia nyingine. Vijana wengine wametumia Intaneti ili kuwaonea wengine, kwa kuwadhihaki, kutoa maoni ya kuwabagua, kuwasumbua, au kuwatisha. Vituo fulani vimeanzishwa kwa kusudi la kumwaibisha mtu fulani, ilhali barua-pepe, vituo vya maongezi, na mitandao kama hiyo imetumiwa kuwachongea wengine. Msimamizi wa kikundi fulani cha kuangalia usalama kwenye Intaneti anaamini kwamba asilimia 80 hivi ya watoto kati ya umri wa miaka 10 hadi 14, wameathiriwa kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja na uonevu unaofanywa kwenye Intaneti.

Kwa kweli, uonevu si jambo jipya. Lakini sasa, uvumi, porojo, na uchongezi zinaweza kusambazwa mbali na kwa muda mfupi zaidi. Mara nyingi uonevu huo huwa mbaya zaidi. Katika visa fulani, simu za mkononi zilizo na kamera zimetumiwa kupiga picha na video zenye kuaibisha, labda mtu akiwa ndani ya chumba cha kubadili mavazi shuleni au ndani ya bafu. Kisha picha hizo huwekwa kwenye Intaneti na kutumwa kwa watu wanaotaka kuzitazama.

Jambo Linalozidi Kuhangaisha Jamii

Tatizo hilo lilisababisha Idara ya Sheria na Usalama wa Umma huko New Jersey, Marekani, kuwatumia wazazi na walezi barua iliyokuwa na himizo hili: “Tusaidieni kukabiliana na tatizo linalozuka la matumizi yasiyofaa ya Intaneti miongoni mwa watoto wakiwa ndani au nje ya shule.” Barua hiyo ilieleza waziwazi hangaiko la idara hiyo kuhusu kuweka habari za kibinafsi na picha kwenye Intaneti. Vituo vinavyotoa habari kama hizo huwavutia walaghai wawe vijana au watu wazima. Barua hiyo ilisema hivi pia, “Wazazi mnapaswa kujua kwamba mahangaiko haya ni ya kweli na mnaweza kuchangia sana kuwalinda watoto wenu kwa kujifunza mengi kuhusu Intaneti na kujua vituo ambavyo watoto wenu hufungua.”

Hata hivyo, wazazi wengine wanajua machache sana kuhusu yale ambayo watoto wao wanafanya kwenye Intaneti. Mama mmoja ambaye hufuatilia kwa ukaribu kile ambacho binti yake mwenye umri wa miaka 16 anafanya kwenye Intaneti anasema hivi: “Wazazi wanaweza kushtuka na kuaibika sana wakijua mambo ambayo watoto wao huweka na kuzungumzia kwenye Intaneti.” Kulingana na mtaalamu mmoja wa usalama kwenye Intaneti, vijana fulani huweka picha walizopigwa wakiwa wamevalia vibaya.

Madhara

Je, malalamiko hayo yanatoka kwa watu wazima wenye wasiwasi mwingi ambao wamesahau vituko vyao vya ujanani? Takwimu zinaonyesha hilo si kweli. Fikiria hili: Katika maeneo fulani, karibu asilimia 33 hivi ya wavulana na wasichana wenye umri wa miaka kati ya 15 na 17 wamewahi kufanya ngono. Zaidi ya nusu ya vijana wenye miaka kati ya 13 na 19 wanasema kwamba wamefanya ngono ya kinywa.

Je, teknolojia imechangia takwimu hizo zenye kushtua? Bila shaka. Ripoti moja katika gazeti New York Times Magazine inasema kwamba “simu za mkononi na Intaneti, ambazo huwawezesha vijana kufanya mambo bila kujulikana, hufanya iwe rahisi kwao kukutana na kufanya ngono bila kuwajibika.” Kwa kweli, inachukua muda mfupi sana kwenye kompyuta kupanga kukutana kwa siri na mtu wa jinsia nyingine. Katika uchunguzi mmoja, zaidi ya wasichana 4 kati ya 5 walikiri kwamba hawawi waangalifu sana wanapotumia Intaneti.

Watu wengine wanaotafuta mchumba au mtu wa kufanya naye ngono bila kuwajibika wamepata zaidi ya yale waliyotarajia. ‘Tumeshuhudia ongezeko la visa vya watu kulalwa kwa nguvu,’ anasema Jennifer Welch wa Idara ya Polisi ya Novato huko California. Anasema kwamba wahasiriwa wengi huwa wamewasiliana kwanza kupitia Intaneti na kukubali kukutana na watu ambao baadaye huwadhulumu.

Jihadhari na “Hekima ya Ulimwengu”!

Makala ya kuwashauri vijana katika magazeti hayachukui msimamo thabiti inapohusu vijana na ngono. Ingawa wanawatia moyo vijana kuwa safi kiadili au kujiepusha na ngono, lengo lao kuu ni kuwatia moyo wajihusishe na ngono “salama” badala ya kutojihusisha hata kidogo na ngono. Ni kama wanasema hivi: ‘Hatuwezi kuwazuia lakini angalau tunaweza kuwafundisha wawajibike.’

Kwenye makala iliyotolewa kwenye kituo kimoja cha Intaneti kinachoheshimika ambacho hutoa ushauri kwa vijana, suala la ama mtu anapaswa au hapaswi kufanya ngono lilitegemea mambo matatu: (1) hatari za kupata mimba, (2) hatari ya kuambukizwa magonjwa ya zinaa, na (3) umuhimu wa kuamua kama msichana na mvulana wako tayari kihisia kufanya jambo hilo. “Lakini wewe ndiye utakayefanya uamuzi wa mwisho,” kinasema kituo hicho. Kilitaja kijuujuu tu kwamba mtu anapaswa pia kuzungumzia jambo hilo pamoja na mzazi wake. Makala hiyo haikutaja kama ni sawa ama si sawa kwa vijana kufanya ngono.

Ikiwa wewe ni mzazi, bila shaka ungependa watoto wako waongozwe na maoni bora zaidi kuliko “hekima ya ulimwengu” ambayo ni ya kipumbavu. (1 Wakorintho 1:20) Unaweza kuwasaidiaje wapite kipindi cha kubalehe na kuepuka hatari zilizozungumziwa katika makala hii? Jibu haliwezi kuwa tu kufunga kompyuta au kuwanyang’anya simu. Kusuluhisha mambo kijuujuu hakugusi mioyo. (Methali 4:23) Kumbuka pia kwamba huenda watoto wakawa wanatumia vifaa kama simu na Intaneti kutosheleza mahitaji fulani ambayo ukiwa mzazi unaweza kuyatosheleza kwa njia bora. Ni nini baadhi ya mahitaji hayo?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Badala ya wazazi kushutumu Intaneti, wanapaswa kujua vituo ambavyo watoto wao hupenda kuvifungua. Kwa njia hiyo, watoto wanaweza kusaidiwa ‘kuzoeza nguvu zao za ufahamu kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Mazoezi kama hayo kutoka kwa wazazi yatawasaidia watoto wanapokomaa.

 

[Blabu katika ukurasa wa 4]

“Ninaporudi nyumbani mimi huenda moja kwa moja kwenye kompyuta na kutumia Intaneti mpaka saa tisa usiku”

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Unaweza kufanya jambo lolote kwenye Intaneti. Unaweza kujifanya kuwa mtu tofauti kabisa kwani hakuna mtu anayekujua”

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Wazazi wanaweza kushtuka na kuaibika sana wakijua mambo ambayo watoto wao huweka na kuzungumzia kwenye Intaneti”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Vituo vya Kuwasiliana—Simulizi la Msichana Mmoja

“Nilianza kutumia kituo cha Intaneti cha shule yetu kuwasiliana na wanafunzi wenzangu na walimu. Nilianza kutumia saa moja kila juma kwenye kituo hicho. Baada ya muda nikaanza kukitumia kila siku. Nilikuwa nimenaswa sana hivi kwamba wakati ambapo sikuwa nikitumia Intaneti nilikuwa nikifikiria kuihusu. Sikuweza kukazia fikira kitu kingine chochote. Sikuweza kumaliza kazi yangu ya shuleni wala kukaza fikira nilipokuwa kwenye mikutano ya Kikristo, na hata niliwapuuza marafiki wangu. Mwishowe, wazazi wangu walitambua kilichokuwa kikiendelea nao wakaniwekea vizuizi. Ilikuwa vigumu kwangu kukubali vizuizi hivyo. Nilikasirika sana. Lakini sasa ninafurahi kwamba wazazi wangu walifanya hivyo nami nimefanya mabadiliko yanayofaa. Nisingependa kuhisi nimenaswa tena!”—Bianca.