Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unyenyekevu Ni Udhaifu au Ni Sifa Nzuri?

Je, Unyenyekevu Ni Udhaifu au Ni Sifa Nzuri?

Maoni ya Biblia

Je, Unyenyekevu Ni Udhaifu au Ni Sifa Nzuri?

KATIKA ulimwengu, mara nyingi watu wenye kiburi au majivuno, na wanaojiamini sana huonwa kuwa mifano ya kuigwa. Wanyenyekevu na wapole huonwa kuwa watu wadhaifu, waoga, au wenye kujipendekeza. Lakini, je, unyenyekevu wa kweli ni udhaifu? Na je, kiburi ni sifa nzuri? Biblia inasema nini?

Lazima tuanze kwa kusema kwamba Biblia haisemi kwamba aina zote za majivuno ni mbaya. Kwa mfano, Wakristo wanapaswa kujivunia kwamba Yehova ni Mungu wao na kwamba anawajua. (Zaburi 47:4; Yeremia 9:24; 2 Wathesalonike 1:3, 4) Wazazi wanaweza kujivunia watoto wao wanapokuwa na mwenendo mzuri wa Kikristo na kutetea kwa ujasiri ibada ya kweli. (Methali 27:11) Hata hivyo, kiburi au majivuno yana madhara.

Kuchunguza kwa Undani Kiburi na Unyenyekevu

Kamusi moja inafafanua kiburi kuwa kujiona kupita kiasi. Kiburi cha aina hiyo humfanya mtu ajihisi kuwa wa maana sana au kuwa bora kuliko wengine, labda kwa sababu ya sura, rangi, cheo, vipawa, au mali. (Yakobo 4:13-16) Biblia inasema kuhusu watu ambao ‘hujivuna kwa kiburi.’ (2 Timotheo 3:4) Yaani, wanajiona kuwa wa maana sana bila kuwa na sababu nzuri.

Kwa upande mwingine, wanyenyekevu hujiona kwa unyoofu kuwa watu wasiokamilika na duni mbele za Mungu. (1 Petro 5:6) Isitoshe, wao hutambua na hata kufurahia sifa bora za wengine. (Wafilipi 2:3) Hivyo, hawawaonei wengine uchungu kwa sababu ya wivu. (Wagalatia 5:26) Kwa hiyo, ni wazi kwamba unyenyekevu wa kweli humfanya mtu awe na uhusiano mzuri na wengine na awe mtulivu.

Fikiria mfano wa Yesu. Kabla ya kuja hapa duniani, alikuwa kiumbe mwenye nguvu huko mbinguni. Na alipokuwa hapa duniani, alikuwa mtu mkamilifu, asiye na dhambi. (Yohana 17:5; 1 Petro 2:21, 22) Alikuwa na uwezo, akili, na ujuzi usio na kifani. Hata hivyo, hakujivunia mambo hayo bali sikuzote alikuwa mnyenyekevu. (Wafilipi 2:6) Hata pindi moja aliosha miguu ya mitume wake; naye alipendezwa kikweli na watoto. (Luka 18:15, 16; Yohana 13:4, 5) Akiwa na mtoto kando yake, Yesu alisema: “Yeyote atakayejinyenyekeza mwenyewe kama mtoto huyu mchanga ndiye aliye mkuu zaidi katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:2-4) Naam, machoni pa Yesu na Baba yake, umashuhuri wa kweli hutokana na unyenyekevu wala si kiburi.—Yakobo 4:10.

Unyenyekevu Ni Sifa Nzuri

Ingawa Yesu ni kielelezo kizuri cha unyenyekevu, yeye hakuwa mtu dhaifu, mwoga au mwenye kujipendekeza. Alisema kweli kwa ujasiri na hakumwogopa mwanadamu yeyote. (Mathayo 23:1-33; Yohana 8:13, 44-47; 19:10, 11) Kwa sababu hiyo hata aliheshimiwa na baadhi ya wapinzani wake. (Marko 12:13, 17; 15:5) Lakini Yesu hakupiga ubwana kamwe. Badala yake, aliwavutia watu kwa kuwa mnyenyekevu, mwenye fadhili, na upendo. Sifa hizo zilifanya watu wampende. Watu wenye kiburi hawawezi kuwavutia watu kwa njia hiyo. (Mathayo 11:28-30; Yohana 13:1; 2 Wakorintho 5:14, 15) Hata leo, mamilioni wanajitiisha kwa ushikamanifu chini ya Kristo kwa sababu wanampenda kikweli na kumheshimu sana.—Ufunuo 7:9, 10.

Neno la Mungu linawatia moyo watu wawe wanyenyekevu kwa sababu watu walio wanyenyekevu wa akili hukubali mashauri kwa urahisi na inafurahisha kuwafundisha. (Luka 10:21; Wakolosai 3:10, 12) Kama Apolo, Mkristo wa karne ya kwanza aliyekuwa mwalimu mwenye ufasaha, wanyenyekevu huwa tayari kubadili maoni yao wakipata habari mpya zilizo sahihi. (Matendo 18:24-26) Nao hawaogopi kuuliza maswali, lakini watu wenye kiburi hawapendi kuuliza maswali kwa kuwa wanaogopa kuonekana wajinga.

Fikiria mfano wa yule towashi Mwethiopia aliyeishi katika karne ya kwanza ambaye alitatanishwa na Andiko fulani. “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Filipo, mwanafunzi Mkristo akamwuliza. Mwethiopia huyo alijibu hivi: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” Towashi huyo alionyesha unyenyekevu wa hali ya juu, hasa tukizingatia kwamba huenda alikuwa mtu mashuhuri sana nchini kwao. Kwa sababu ya unyenyekevu wake, aliweza kusaidiwa kuelewa Maandiko kwa undani.—Matendo 8:26-38.

Mwethiopia huyo ni tofauti kabisa na waandishi na Mafarisayo Wayahudi, ambao walijiona kuwa wasomi wa kidini wa wakati huo. (Mathayo 23:5-7) Badala ya kunyenyekea na kumsikiliza Yesu na wafuasi wake, waliwadharau na kujaribu kuwachambua. Kwa sababu hiyo, kiburi chao kilifanya wabaki kwenye giza la kiroho.—Yohana 7:32, 47-49; Matendo 5:29-33.

Je, Wewe Ni Udongo Laini au Udongo Mgumu?

Biblia inamfananisha Yehova na mfinyanzi na wanadamu wanafananishwa na udongo. (Isaya 64:8) Unyenyekevu humsaidia mtu kuwa kama udongo laini mikononi mwa Mungu, mtu ambaye Mungu anaweza kumfinyanga kuwa chombo kinachotamanika; ilhali wenye kiburi ni kama udongo mgumu uliokauka ambao unaweza tu kupondwa-pondwa. Farao aliyetawala Misri ya kale alikuwa na kiburi. Alimkaidi Yehova, naye akapoteza uhai wake. (Kutoka 5:2; 9:17; Zaburi 136:15) Kuangamizwa kwa Farao kunaonyesha wazi ukweli wa methali hii: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.”—Methali 16:18.

Mambo yaliyotajwa hayamaanishi kwamba watu wa Mungu hawawezi kuwa na kiburi. Kwa mfano, pindi kwa pindi, mitume wa Yesu walibishana kuhusu ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao. (Luka 22:24-27) Hata hivyo, hawakututumuka kwa kiburi bali walimsikiliza Yesu na mwishowe wakabadili mtazamo wao.

“Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima,” akaandika Sulemani. (Methali 22:4) Bila shaka, tuna sababu nzuri zinazotuchochea kusitawisha sifa ya unyenyekevu! Si kwamba tu sifa hiyo ni nzuri na inavutia, bali pia inatusaidia kupata kibali cha Mungu na zawadi ya uzima wa milele.—2 Samweli 22:28; Yakobo 4:10.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, aina zote za majivuno ni mbaya?—2 Wathesalonike 1:3, 4.

▪ Unyenyekevu humchocheaje mtu ajifunze?—Matendo 8:26-38.

▪ Je, watumishi wa Mungu wanahitaji kusitawisha sifa ya unyenyekevu?—Luka 22:24-27.

▪ Mtu mnyenyekevu anatarajia nini wakati ujao?—Methali 22:4.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Watoto walivutiwa na Yesu kwa sababu alikuwa mtu mnyenyekevu