Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Vijana Watosheleze Mahitaji Yao

Wasaidie Vijana Watosheleze Mahitaji Yao

Wasaidie Vijana Watosheleze Mahitaji Yao

VIJANA wanahitaji watu wa kuzungumza nao kuhusu miradi, matumaini, na matatizo yao. Pia wanahitaji marafiki wazuri. Wanapokomaa, vijana wanahitaji kuhisi kwamba wana utu na sifa zinazowatofautisha na wengine. Wazazi wanapowasaidia watoto wao kutosheleza mahitaji hayo, wanawalinda kutokana na mahusiano yanayoweza kuwa hatari kutia ndani yale yanayoanzishwa kwa urahisi kupitia Intaneti.

Vijana wanahitaji kuongea. Huenda vijana wakaonekana kama hawataki kueleza hisia zao, labda kwa kunyamaza sana au kwa kuficha-ficha mambo. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba wanataka kuzungumza, naam, wanataka kuzungumza na wewe mzazi wao, kuhusu mambo mazito na yasiyo mazito. Je, wewe uko tayari kuwasikiliza?—Yakobo 1:19.

Usiache mahangaiko ya maisha yakuzuie kutumia nafasi nzuri unazopata za kuzungumza na watoto wako. Ikiwa hupati nafasi, huenda ikafaa kufikiria kwa uzito shauri hili zuri la Biblia: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Ni nini kilicho cha maana zaidi kuliko watoto wako?

Usikate kauli kwa haraka kwamba vijana hupendelea kupata mashauri kutoka kwa vijana wenzao badala ya kutoka kwa wazazi wao. Katika uchunguzi mmoja, wanafunzi zaidi ya 17,000 wa shule za msingi na sekondari waliulizwa waeleze, kwa kutumia nambari 0 hadi 5, jinsi wazazi, marafiki, watu mashuhuri, vyombo vya habari na walimu wanavyowaathiri. Nambari 0 ilionyesha hawakuwaathiri hata kidogo, na 5 ilionyesha kwamba waliwaathiri sana. Karibu nusu yao waliwapa wazazi wao alama ya 5.

Ni wazi kwamba ukiwa mzazi, una fungu muhimu sana katika maadili na miradi ambayo watoto wako wanachagua. Mzazi mmoja alisema hivi: “Huenda si kila jambo unalosema litakalokuwa na uvutano mkubwa kwao, lakini usipozungumza nao hutakuwa na uvutano wowote kwao.”

Vijana wanahitaji marafiki. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 15 anasema: “Wazazi wengi hawajui watoto wao wanawasiliana na nani kwenye Intaneti au hata hawajali.” Lakini katika siku hizi ngumu wazazi wanapaswa kujua watoto wao wanashirikiana na nani. Je, unajua watoto wako hushirikiana na nani iwe ni ana kwa ana au kupitia Intaneti? Biblia inasema: “Urafiki mbaya huharibu tabia njema.” (1 Wakorintho 15:33, Biblia Habari Njema) Naam, kuna sababu nzuri za kuchunguza marafiki wa mtoto wako.

Kuwajali vijana kunahusisha mengi zaidi ya kuwalinda na uvutano mbaya. Watoto wanahitaji marafiki wanaofaa. “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima,” Biblia inasema. (Methali 13:20) Kwa hiyo, unahitaji kuwasaidia watoto wako kupata marafiki wanaofaa, kutia ndani vijana ambao wanaweka mfano mzuri kwa kumkumbuka Muumba wao.—Mhubiri 12:1.

Yehova Mungu huchagua kwa uangalifu watu anaotaka wawe marafiki wake nasi tunapaswa kumwiga. (Zaburi 15:1-5; Waefeso 5:1) Kwa kweli, kuchagua marafiki wanaofaa ni moja kati ya mambo muhimu zaidi unayoweza kuwafundisha watoto wako kupitia maneno na mfano wako.—2 Wathesalonike 3:6, 7.

Vijana wanahitaji kuhisi kwamba wana utu wao wenyewe. Sehemu muhimu ya kukua ni kutokeza utu wa kibinafsi yaani, kuwa na sifa za kipekee zinazomtofautisha mtoto mmoja na wale wengine. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Mtoto hujulikana kwa matendo yake.” (Methali 20:11, BHN) Mojawapo ya majukumu yako ukiwa mzazi ni kukazia kanuni zinazofaa katika mioyo ya watoto wako.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Kwa mfano: Kila siku wazazi humchagulia mtoto mdogo mavazi atakayovaa, wakitarajia kwamba atajifunza kuvalia mavazi yanayofaa. Lakini je, unaweza kuwazia mtu mzima mwenye umri wa miaka 30 akiwa bado anachaguliwa mavazi na wazazi wake? Hilo ni jambo la kipumbavu! Ikitumia mfano wa mavazi, Biblia inatutia moyo hivi: “Mjivike utu mpya,” yaani utu kama wa Kristo. (Wakolosai 3:10) Unaweza kuwasaidia watoto wako wavae utu mpya kwa kutoa nidhamu kwa upendo na kuwapa “mwongozo wa akilini.” (Waefeso 6:4) Kisha wanapokuwa watu wazima na kujitegemea zaidi, wanaweza kuchagua kujivika “utu mpya,” wakiuona kuwa vazi maridadi na lenye kuvutia.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

Jiulize: “Kwa kweli watoto wangu wanahisije kuhusu kanuni za Neno la Mungu? Ninaweza kuwasaidiaje ‘kuishi kwa utimamu wa akili’?” (Tito 2:12) Lengo lako si kuwa mtoto anayetii bila kufikiri. Watoto fulani hufanya jambo lolote wanaloambiwa bila kuuliza maswali, kubishana, au kukaidi. Lakini mtoto ambaye anafuata tu kila kitu unachomwambia leo huenda akafuata yale ambayo ulimwengu utamwambia afanye kesho. Kwa hiyo, wazoeze watoto wako kusitawisha ‘nguvu zao za kufikiri.’ (Waroma 12:1) Wasaidie waone kwa nini kanuni za Biblia zinafaa na jinsi zinavyotufaidi sisi sote.—Isaya 48:17, 18.

Ni kweli kwamba jitihada nyingi zinahitajika ili kuwasaidia vijana watosheleze mahitaji yao. Lakini kuna baraka nyingi kwa wale wanaofanya hivyo! Watoto wako wakifuata kanuni bora ulizowafundisha, utasema kwa moyo wako wote kwamba kwa kweli watoto ni “urithi kutoka kwa Yehova.”—Zaburi 127:3.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wasaidie watoto wako wachague marafiki Wakristo wanaofaa