Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Zote Ni Barabara Mbalimbali Zinazoongoza kwa Mungu?

Je, Dini Zote Ni Barabara Mbalimbali Zinazoongoza kwa Mungu?

Maoni ya Biblia

Je, Dini Zote Ni Barabara Mbalimbali Zinazoongoza kwa Mungu?

MWANDISHI Marcus Borg alisema hivi, “siwezi kuamini kwamba Mungu wa ulimwengu wote mzima anataka kutambuliwa kupitia dini moja tu.” Desmond Tutu, mshindi wa Tuzo la Amani la Nobeli alisema: “Hakuna dini inayoweza kudai kwamba ina ukweli wote kuhusu fumbo” la imani. Usemi mmoja wa Kihindi unaopendwa ni “Jotto moth, totto poth,” ambao ukitafsiriwa kijuujuu humaanisha kwamba dini zote ni barabara mbalimbali zinazoongoza kwenye lengo moja. Wabudha wana maoni kama hayo pia. Kwa kweli, mamilioni ya watu huamini kwamba dini zote ni barabara mbalimbali zinazoongoza kwa Mungu.

Mwanahistoria Geoffrey Parrinder alisema hivi: “Nyakati nyingine inasemekana kwamba dini zote zina lengo lilelile, au ni njia zinazofanana zinazoongoza kwenye ukweli, au hata kwamba zinafundisha mafundisho yaleyale.” Ni kweli kwamba mafundisho, desturi, na miungu ya dini hufanana. Dini nyingi husema juu ya upendo na hufundisha kwamba kuua, kuiba, na kusema uwongo ni dhambi. Katika dini nyingi, watu kadhaa hujitahidi kusaidia wengine kwa moyo mweupe. Basi, ikiwa mtu anashikilia itikadi zake kwa moyo mweupe na anajaribu kuishi maisha mema, dini anayoshirikiana nayo ina ubaya gani? Au je, dini zote ni barabara mbalimbali tu zinazoongoza kwa Mungu?

Je, Inatosha Kuwa na Moyo Mweupe Tu?

Fikiria mfano wa mwanamume Myahudi wa karne ya kwanza aliyeitwa Sauli, aliyekuja kuwa mtume Mkristo aliyeitwa Paulo. Yeye alikuwa mfuasi mwenye bidii wa Dini ya Kiyahudi, na hilo lilimfanya ajaribu kufutilia mbali ibada ya wafuasi wa Kristo. Aliona kuwa ibada yao haifai. (Matendo 8:1-3; 9:1, 2) Lakini, kwa huruma za Mungu, Sauli alitambua kwamba watu wanaofuata dini sana kama yeye, wanaweza kuwa na bidii kwa ajili ya Mungu na bado wawe wanakosea kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi wa kutosha. (Waroma 10:2) Sauli alipojifunza zaidi kuhusu mapenzi na kazi za Mungu, alibadilika na akaanza kuabudu pamoja na wale aliowanyanyasa, yaani, wafuasi wa Yesu Kristo.—1 Timotheo 1:12-16.

Je, Biblia yasema kwamba twaweza kuchagua dini yoyote kati ya mamia ya dini nyingi zilizopo na kwamba yoyote ile tutakayoichagua itakubaliwa na Mungu? Yesu Kristo aliyefufuliwa alimpa Mtume Paulo maagizo yaliyopinga jambo hilo kabisa. Yesu alimtuma kwa watu wa mataifa ili “kufungua macho yao, kuwageuza kutoka kwenye giza hadi kwenye nuru na kutoka kwenye mamlaka ya Shetani hadi kwa Mungu.” (Matendo 26:17, 18) Bila shaka, uchaguzi wetu wa dini ni muhimu. Watu wengi ambao Paulo alitumwa kwao tayari walikuwa na dini zao. Lakini walikuwa “kwenye giza.” Kwa hakika, ikiwa dini zote zingekuwa tu barabara mbalimbali zinazoongoza kwenye uhai udumuo milele na kwenye kibali cha Mungu, ingekuwa kazi bure kwa Yesu kuwazoeza wafuasi wake kwa ajili ya kazi aliowaagiza ya kufanya wanafunzi.—Mathayo 28:19, 20.

Katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alisema hivi: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Biblia husema waziwazi kwamba kuna “imani moja.” (Waefeso 4:5) Bila shaka, wengi walio kwenye barabara “pana” wana dini. Lakini hawana ile “imani moja.” Kwa kuwa kuna ibada moja tu ya kweli, wale wanaotamani kuipata dini hiyo watahitaji kuitafuta mpaka waipate.

Mtafuteni Mungu wa Kweli

Tangu mwanzo wa historia ya mwanadamu, Mungu amewaambia wanadamu yale anayotaka wafanye. (Mwanzo 1:28; 2:15-17; 4:3-5) Leo, matakwa yake yanaelezwa waziwazi katika Biblia. Hiyo inatuwezesha kutofautisha ibada inayokubalika na isiyokubalika. (Mathayo 15:3-9) Watu fulani wamerithi dini yao, ilhali wengine hufuata maoni ya watu wengi katika jumuiya yao. Kwa watu wengi, kuwa katika dini fulani kunategemea wakati au mahali walipozaliwa. Hata hivyo, je, wapaswa kuacha uchaguzi wako wa dini uongozwe na nasibu au na uamuzi wa watu wengine?

Wapaswa kuchagua dini baada ya kupata habari kamili kwa kuchunguza Maandiko kwa uangalifu. Katika karne ya kwanza, watu fulani wenye elimu hawakukubali maneno ya Paulo kijuujuu tu. ‘Waliyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.’ (Matendo 17:11; 1 Yohana 4:1) Mbona usifanye hivyo?

Biblia yasema kwamba Mungu wa ulimwengu wote mzima anatafuta watu wa kumwabudu katika kweli. Kama ilivyoandikwa kwenye Yohana 4:23, 24, Yesu alieleza: “Hata hivyo, saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati waabudu wa kweli watakapomwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta wa namna hiyo wamwabudu yeye. Mungu ni Roho, na wale wanaomwabudu yeye lazima waabudu kwa roho na kweli.” “Ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba” ndiyo tu inayokubaliwa naye. (Yakobo 1:27) Mungu amebariki jitihada za mamilioni za kutafuta barabara nyembamba inayoongoza kwenye uhai. Hatawapa uhai wa milele watu wasiojali, bali atawapa wale wanaojitahidi kabisa kuipata na kuifuata ile njia nyembamba aliyoiweka.—Malaki 3:18.