Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Huu Ndio Uriti Wetu wa Kiroho

Huu Ndio Uriti Wetu wa Kiroho

‘Huu ndio uriti wa watumishi wa [Yehova’].​—ISA. 54:17, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo.

1. Kwa upendo, Yehova amelinda nini kwa faida ya wanadamu?

 YEHOVA, “Mungu aliye hai na anayedumu,” ameulinda ujumbe wake wenye kutoa uzima kwa ajili ya wanadamu. Bila shaka, ujumbe huo utadumu kwa sababu “neno la Yehova linadumu milele.” (1 Pet. 1:23-25) Sisi ni wenye furaha kabisa kwa sababu kwa upendo Yehova ameulinda ujumbe huo wa maana katika Neno lake, Biblia.

2. Mungu amelinda nini katika Neno lake kwa faida ya watumishi wake?

2 Mungu alijipatia jina na kulinda jina hilo katika Neno lake ili watumishi wake walitumie. Maandiko yanataja kwa mara ya kwanza maneno “Yehova Mungu” yanapozungumuzia “historia ya mbingu na dunia.” (Mwa. 2:4) Jina la Mungu liliandikwa kimuujiza kwenye mabamba ya majiwe yaliyokuwa na Amri Kumi mara nyingi. Kwa mufano, amri ya kwanza inaanza hivi: “Mimi ni Yehova Mungu wako.” (Kut. 20:1-17) Shetani amefanya yake yote ili jina la Yehova lisionekane tena na pia amefanya yake yote ili kuliharibu Neno la Yehova, lakini jina la Mungu linaendelea kudumu, kwa sababu Yehova, Mutawala Mukubwa wa Ulimwengu Wote, amelinda jina lake na Neno lake.​—Zab. 73:28.

3. Hata ikiwa mafundisho mengi ya uongo yameenea duniani pote, Mungu amelinda jambo gani?

3 Yehova ameilinda pia kweli katika Neno lake. Hata ikiwa mafundisho mengi ya uongo yameenea duniani pote, sisi ni wenye furaha kwa sababu Mungu ametupatia mwangaza wa kiroho na kweli. (Soma Zaburi 43:3, 4.) Watu wengi leo wanatembea katika giza la kiroho, lakini sisi tunaendelea kutembea kwa furaha katika mwangaza wa kiroho unaotoka kwa Mungu.​—1 Yoh. 1:6, 7.

TUFURAHIE URITI WETU

4, 5. Tumekuwa na pendeleo gani la pekee kuanzia mwaka wa 1931?

4 Sisi Wakristo tuna uriti wa maana sana. Kitabu kimoja kinasema kwamba “Uriti wa inchi fulani ni sifa zote, desturi zote, ao namna yote ya kuishi ao ya kufikiri ya watu wa inchi hiyo ambayo imeendelea kwa muda wa miaka mingi, kizazi kwa kizazi.” Uriti wetu wa kiroho ni ujuzi sahihi tulio nao wa Neno la Mungu na kuelewa vizuri ukweli juu ya Mungu na makusudi yake. Unatia ndani pia pendeleo la pekee kabisa tulilo nalo.

5 Tulipata pendeleo hilo la pekee kwenye mukusanyiko uliofanywa katika muji wa Columbus, Ohio, États-Unis katika mwaka wa 1931. Herufi mbili “JW” ziliandikwa kwenye karatasi ya programu ya mukusanyiko huo. Dada mumoja alisema hivi: “Watu wengi walijiuliza kama herufi JW zilimaanisha nini.” Hapo mbele tuliitwa Wanafunzi wa Biblia, lakini Siku ya Yenga tarehe 26 Mwezi wa 7, 1931, tulikubali kuitwa Mashahidi wa Yehova (Jehovah’s Witnesses, maana ya herufi zile mbili). Ilikuwa furaha kubwa kupokea jina hilo linalopatana na Biblia. (Soma Isaya 43:12.) Ndugu mumoja alisema hivi: “Sitasahau hata kidogo namna watu walivyoshangilia kwa muda murefu na kupiga mikono wakati tangazo hilo lilitolewa.” Katika dunia watu wengine hawakupenda jina hilo, lakini Mungu ametubariki kwa kulitumia kwa muda wa miaka zaidi ya 80. Bila shaka, kuwa Mashahidi wa Yehova ni pendeleo la pekee kabisa.

Tulikubali kwa furaha jina Mashahidi wa Yehova kwenye mukusanyiko wetu wa 1931

6. Uriti wetu wa kiroho una habari gani za kweli?

6 Uriti wetu wa kiroho unatia ndani pia habari nyingi za kweli na za maana kuhusu watumishi wa Yehova wa zamani. Tuchukue mufano wa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Bila shaka, mababu hao wa zamani walielezea watu wa familia zao mambo ya kufanya ili kumupendeza Yehova. Kwa hiyo, si jambo la kushangaza ikiwa Yosefu alikataa kufanya uasherati ili ‘asimutendee Mungu zambi.’ (Mwa. 39:7-9) Wakristo wa kwanza pia walikuwa na mapokeo fulani yasiyoandikwa, walifundishana pia kwa mwenendo. Kwa mufano, mutume Paulo alitolea makutaniko maagizo kuhusu Ukumbusho wa Kifo cha Yesu. (1 Kor. 11:2, 23) Leo, mambo tunayohitaji ili kumuabudu Mungu ‘kwa roho na kweli’ yanapatikana katika Neno lake, Biblia. (Soma Yohana 4:23, 24.) Biblia iliandikwa kwa ajili ya watu wote, lakini sisi watumishi wa Yehova tunaisamini zaidi.

7. Uriti wetu wa kiroho una pia ahadi gani yenye kutia moyo?

7 Sehemu ingine ya uriti wetu wa kiroho ni habari nyingi zilizochapishwa hivi karibuni zinazoonyesha kwamba ‘Yehova iko upande wetu.’ (Zab. 118:7) Habari hizo zinatufanya tujisikie salama, hata wakati ambapo tunateswa kwa sababu ya imani yetu. Kati ya mambo yanayozidi kuongezeka ya uriti wetu wa kiroho ni ahadi hii yenye kutia moyo: “‘Silaha yoyote itakayofanywa juu yako haitafanikiwa, na ulimi wowote utakaoinuka juu yako katika hukumu wewe utauhukumu. Hilo ndilo fungu la uriti la [ao, huu ndio uriti wa] watumishi wa Yehova, na uadilifu wao ni kutoka kwangu,’ asema Yehova.” (Isa. 54:17) Kwa hiyo, hakuna silaha ya Shetani inayoweza kutuangamiza milele.

8. Tutajifunza nini katika habari hii na ile inayofuata?

8 Shetani amejaribu kuzima jina Yehova, kuangamiza Neno la Mungu, na kuficha kweli. Lakini ameshindwa kabisa kwa sababu Yehova amezuia mipango yake yote. Katika habari hii na ile inayofuata, tutajifunza (1) namna gani Mungu amelinda Neno lake; (2) namna gani amelinda jina lake; na (3) namna gani Baba wetu wa mbinguni ametupa kweli na kulinda kweli hiyo.

YEHOVA AMELINDA NENO LAKE

9-11. Ni mifano gani inayoonyesha kama Biblia imeshambuliwa katika njia mbalimbali na imeokoka?

9 Yehova amezuia maadui wa Neno lake wasiliharibu kabisa. Kitabu Enciclopedia Cattolica kinasema hivi: “Ili kupiganisha Waalbijwa na wafuasi wa Waldo katika mwaka wa 1229, Baraza la Toulouse lilikataza watu wa hali ya chini kusoma [Biblia zilizotafsiriwa katika luga za watu hao] . . . Mukutano uliofanywa katika mwaka wa 1234 katika muji wa Tarragona, Espanye, ulioongozwa na James wa Kwanza, ulikataza pia watu kufanya hivyo. . . . Katika mwaka wa 1559, papa wa Roma, Paul wa Ine, aliingilia kati kwa mara ya kwanza kwa kukataza watu kuchapisha na kuwa na Biblia zilizotafsiriwa katika luga za watu wa hali ya chini bila ruhusa yake.

10 Mungu amelinda Biblia hata ikiwa ilishambuliwa katika njia mbalimbali. Karibu na mwaka wa 1382, John Wycliffe na rafiki zake walitafsiri Biblia ya kwanza katika Kiingereza. Mutafsiri mwengine wa Biblia aliitwa William Tyndale, aliyeuawa na maadui wa Neno la Mungu katika mwaka 1536; alifungwa juu ya muti, na inasemekana kuwa alipokuwa hapo juu ya muti, mbele ya kufa alilia hivi kwa sauti: “Ee Bwana, fungua macho ya mufalme wa Angleterre.” Kisha alinyongwa na kuchomwa.

11 Biblia imeokoka ijapokuwa maadui walifanya juu chini ili waiangamize. Kwa mufano, katika mwaka wa 1535, Biblia ya Kiingereza iliyotafsiriwa na Miles Coverdale ilitokea. Coverdale alitumia tafsiri ya Tyndale ya “Agano Jipya” nzima na pia “Agano la Kale” kuanzia kitabu cha Mwanzo mupaka Mambo ya Nyakati. Alitafsiri sehemu zingine za Biblia kutoka Kilatini. Alitumia pia Biblia ya Kialemand ya Martin Luther. Leo, Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni Biblia inayopendwa kwa sababu inaeleweka waziwazi, imetafsiriwa kwa usahihi kwa kufuata Maandishi ya zamani, na inasaidia sana katika mahubiri. Sisi ni wenye furaha kwa sababu iwe wanadamu wala Shetani na mashetani wake, hakuna anayeweza kuangamiza Neno la Yehova.

YEHOVA AMELINDA JINA LAKE

Wanaume wengi kama vile Tyndale walitoa maisha yao kwa ajili ya Neno la Mungu

12. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imesaidia namna gani kulinda jina la Mungu?

12 Yehova Mungu amehakikisha kwamba jina lake linaendelea kulindwa katika Biblia. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imesaidia sana kulinda jina hilo. Katika maneno yake ya utangulizi, halmashauri ya watafsiri wa Biblia hiyo, ambao ni Wakristo waliojitoa kwa Mungu, iliandika hivi: “Jambo linalopendeza zaidi katika tafsiri hii ni kule kulirudisha jina la Mungu mahali pake panapofaa katika maandishi ya Kiingereza. Jambo hilo limefanywa kwa kutumia jina ‘Yehova’ mara 6 973 katika Maandiko ya Kiebrania na mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki.” Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana sasa ikiwa nzima ao sehemu katika luga zaidi ya 116, na zaidi ya Biblia 178 545 862 zimechapishwa.

13. Sababu gani tunaweza kusema kama tangu kuumbwa kwa mwanadamu, watu wamejua jina la Mungu?

13 Tangu kuumbwa kwa mwanadamu, watu wamejua jina la Mungu. Adamu na Eva walijua jina hilo, na walijua kulitamka vizuri. Kisha Garika, Hamu alipomukosea adabu Noa baba yake, yeye [Noa] alisema hivi: ‘Abarikiwe Yehova, Mungu wa Shemu, Kanaani [mwana wa Hamu] na awe mutumwa wake.’ (Mwa. 4:1; 9:26) Mungu mwenyewe alisema: ‘Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitamupa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe.’ Tena akasema: “Mimi ni Yehova, na hakuna mwingine yeyote. Zaidi ya mimi hakuna Mungu.” (Isa. 42:8; 45:5) Yehova amefanya jina lake liendelee kulindwa na lijulikane duniani pote. Sisi tuna pendeleo kabisa la kutumia jina Yehova na kuwa Mashahidi wake. Kwa hiyo, tunasema hivi kwa sauti: “Tutainua bendera zetu katika jina la Mungu wetu.”​—Zab. 20:5.

14. Zaidi ya Biblia, jina la Mungu linaweza tena kupatikana wapi?

14 Jina la Mungu halipatikane tu katika Biblia. Tuchukue mufano wa Jiwe la Moabu, lililopatikana huko Dibon kwenye umbali wa kilometre 21 mashariki mwa Bahari ya Chumvi. Maandishi yaliyo kwenye jiwe hilo yanamutaja Mufalme Omri wa Israeli na yanazungumuzia uasi wa Mufalme Mesha wa Moabu juu ya Israeli. (1 Fal. 16:28; 2 Fal. 1:1; 3:4, 5) Lakini tunapendezwa zaidi na Jiwe hilo la Moabu kwa sababu lina herufi ine zinazounda jina la Mungu, ni kusema, YHWH. Herufi hizo zinapatikana pia mara nyingi kwenye vipande vya vyombo vya udongo vilivyopatikana Israeli, vinavyoitwa Barua za Lakishi.

15. Tafsiri ya Septante ni nini, na ilipatikana namna gani?

15 Watafsiri wa kwanza-kwanza wa Biblia walisaidia sana ili jina la Mungu lilindwe. Kisha kupelekwa Babiloni katika mwaka wa 607 mupaka mwaka wa 537 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Wayahudi wengi hawakurudi Yuda na Israeli. Katika miaka ya 200 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Wayahudi wengi walikaa katika muji wa Alexandrie huko Misri. Wao walihitaji Maandiko ya Kiebrania yatafsiriwe katika Kigiriki, ambayo ilikuwa luga ya kimataifa wakati huo. Tafsiri hiyo ilimalizika katika miaka ya 100 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, na iliitwa Septante. Kopi fulani za Tafsiri hiyo zilikuwa na jina Yehova katika Kiebrania.

16. Ni kitabu gani cha kwanza kutafsiriwa katika mwaka wa 1640 ambacho kilikuwa na jina la Mungu?

16 Kitabu cha kwanza kutafsiriwa katika inchi za Amerika zilizotawaliwa na Uingereza ni Zaburi na kilikuwa na jina la Mungu. Kilitafsiriwa katika Kiingereza kutoka Kiebrania, na kiliitwa kitabu cha Zaburi cha Guba. Kilichapishwa kwa mara ya kwanza katika mwaka wa 1640. Kilitumia jina la Mungu katika maandiko kama vile Zaburi 1:1, 2, inayosema kwamba “mwenye furaha” hatembee katika shauri la waovu, ‘lakini mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova.’ Ili kupata habari zaidi juu ya jina la Mungu, soma broshua Jina la Mungu Litakalodumu Milele.

YEHOVA AMELINDA KWELI

17, 18. (a) Kweli ni nini? (b) Taja mafundisho ambayo ni sehemu ya “kweli ya habari njema.”

17 Tunamutumikia “Yehova Mungu wa ukweli” kwa furaha. (Zab. 31:5) Kitabu kimoja kinasema kwamba “kweli” ni mambo ya hakika juu ya jambo fulani, si mambo ya kuwaziawazia ao kutungwa. Katika Kiebrania cha Biblia, neno linalotumiwa ili kutafsiri neno “kweli” ni neno linaloonyesha jambo fulani la kweli, lenye kutegemeka ao lenye kuaminika. Katika Kigiriki, neno linalotumiwa ili kutafsiri neno “kweli” linamaanisha mambo yanayopatana kabisa na ukweli ao mambo mazuri na yaliyo sawa.

18 Yehova amelinda kweli na anatusaidia tuwe na ujuzi wa kweli hiyo ambao unaendelea kuongezeka. (2 Yoh. 1, 2) Tunaelewa kweli hatua kwa hatua kwa sababu ‘njia ya waadilifu ni kama nuru inayongaa, inayozidi kuongezeka mupaka muchana mukamilifu.’ (Met. 4:18) Bila shaka, tunakubaliana kabisa na Yesu aliyesali kwa Mungu hivi: “Neno lako ni Kweli.” (Yoh. 17:17) Biblia ina “kweli ya habari njema,” ambayo ni musingi wa mafundisho yote ya Kikristo. (Gal. 2:14) Mafundisho kuhusu jina la Yehova, utawala wake, zabihu ya ukombozi ya Yesu, tumaini la ufufuo, na Ufalme wa Mungu ni sehemu tu ya kweli hiyo. Acheni tuone sasa namna Mungu amelinda kweli hata ikiwa Shetani amefanya yake yote ili kuificha.

YEHOVA AMEZUIA MIPANGO YA SHETANI YA KUANGAMIZA KWELI

19, 20. Nimrodi alikuwa nani na alikuwa na mupango gani ulioshindwa kabisa?

19 Kisha Garika, watu walizoea kusema hivi: ‘Kama tu Nimrodi, mwindaji mwenye nguvu kwa kumupinga Yehova.’ (Mwa. 10:9) Kwa kuwa Nimrodi alikuwa mupinzani wa Yehova, basi, alikuwa anamuabudu Shetani na alifanana na wale wapinzani ambao Yesu alisema hivi juu yao: ‘Ninyi mumetoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi munataka kufanya tamaa za baba yenu. Huyo hakusimama imara katika kweli.’—Yoh. 8:44.

20 Nimrodi alitawala Babeli na miji mingine iliyokuwa kati ya mito Tigri na Efrati. (Mwa. 10:10) Inawezekana Babeli na munara wake, vilianza kujengwa karibu na mwaka wa 2269 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, wakati wa utawala wa Nimrodi. Mapenzi ya Yehova yalikuwa kwamba watu watawanyike katika dunia yote, lakini wajengaji hao walienda kinyume na mapenzi ya Yehova na walisema hivi: ‘Haya! Na tujijengee jiji na pia munara na kilele chake kiwe mbinguni, na tujifanyie jina maarufu [ao lenye kujulikana], tusije tukatawanyika juu ya uso wote wa dunia.’ Lakini mupango wao haukuendelea kwa sababu Mungu ‘alikuwa amevuruga luga ya dunia yote’ na kuwatawanya wale waliodai kwamba wangejenga munara huo. (Mwa. 11:1-4, 8, 9) Ikiwa mupango wa Shetani ulikuwa ni kuanzisha dini moja ambamo kila mutu atamuabudu, mupango huo ulishindwa kabisa. Katika historia yote ya wanadamu, watu wanaomuabudu Yehova wanaongezeka kila siku na ibada yake inazidi kusonga mbele siku baada ya siku.

21, 22. (a) Sababu gani dini ya uongo imeshindwa kuangamiza ibada ya kweli? (b) Tutajifunza nini katika habari inayofuata?

21 Dini ya uongo haiweze hata kidogo kuangamiza ibada ya kweli. Sababu gani? Kwa sababu Mufundishaji wetu Mukubwa amefanya mipango ya kulinda Neno lake, amefanya jina lake liendelee kujulikana na wanadamu na ameendelea kuwapa watumishi wake kweli. (Isa. 30:20, 21) Kumuabudu Mungu katika kweli kunatuletea furaha, lakini ili kuendelea kufanya hivyo, tunapaswa kubaki macho kiroho, kumutegemea Yehova na kufuata muongozo wa roho yake takatifu.

22 Katika habari inayofuata, tutaona namna gani mafundisho fulani ya uongo yalianza kufundishwa. Tutaona kwamba mafundisho hayo hayapatane na Maandiko. Zaidi ya hayo, tutaona namna gani Yehova, Mulindaji mukubwa wa kweli, ametubariki kwa kututolea mafundisho ya kweli tunayofurahia na ambayo ni sehemu ya uriti wetu wa kiroho.