Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kaza Macho Yako juu ya Jambo la Maana

Kaza Macho Yako juu ya Jambo la Maana

“Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”​—ZAB. 83:18.

NYIMBO: 46, 136

1, 2. (a) Ni jambo gani la maana lenye linahusu wanadamu wote? (b) Sababu gani jambo hilo ni la maana kwetu?

LEO, watu wengi wanaona kuwa feza ndiyo jambo la maana. Wanakaza akili yao juu ya kutafuta utajiri ao kushikamana sana na vitu vyao. Wengine wanaona kuwa jambo la maana kwao ni familia, afya, ao mambo yenye wanapenda kutimiza katika maisha yao.

2 Lakini, jambo la maana sana lenye kutuhusu sisi wote ni kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala. Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiache kukaza akili yetu juu ya jambo hilo la maana sana. Hilo linaweza kutokea namna gani? Tunaweza kuhangaikia sana mahitaji yetu ya kila siku mupaka tunasahau kuwa kutetewa kwa haki ya Mungu ya kutawala ndilo jambo la maana. Ao tunaweza kuacha magumu yetu yatuzuie kuona kuwa jambo hilo ndilo la maana. Kwa upande mwingine, ikiwa tunaendelea kuunga kabisa mukono haki ya Yehova ya kutawala, tutakuwa na uwezo zaidi wa kupiganisha magumu katika maisha yetu ya kila siku. Na kufanya hivyo kutatusaidia tumukaribie Yehova zaidi.

SABABU GANI NI JAMBO LA MAANA SANA?

3. Shetani alitoa mashitaka gani juu ya utawala wa Mungu?

3 Shetani Ibilisi alileta mashaka juu ya haki ya Yehova ya kutawala. Alisema kuwa utawala wa Mungu ni wa mubaya na kuwa Yehova ananyima viumbe wake mambo ya muzuri. Shetani alionyesha kuwa wanadamu wangekuwa na furaha na maisha ya muzuri zaidi ikiwa wangejitawala wao wenyewe. (Mwa. 3:1-5) Shetani amesema pia kuwa hakuna mwanadamu mwenye kuwa mushikamanifu kwa Mungu kwa moyo wake wote, ni kusema, ikiwa mwanadamu yeyote anapatwa na magumu makali, atakataa utawala wa Yehova. (Ayu. 2:4, 5) Ili kujibia mashitaka ya Shetani, Yehova anaachia wanadamu wakati ili waone kama maisha hayawezi kuwa mazuri bila utawala wake wenye haki.

4. Sababu gani mashitaka juu ya haki ya Mungu ya kutawala yanapaswa kujibiwa?

4 Kwa kweli, Yehova anajua kuwa mashitaka ya Shetani ni ya uongo. Sababu gani Mungu ameamua kuacha mashitaka hayo yaendelee kwa kumupatia Shetani wakati wa kujaribu kuonyesha kuwa mashitaka yake ni ya kweli? Jibu la mashitaka hayo linahusu viumbe wote wenye akili. (Soma Zaburi 83:18.) Kwa kweli, mwanaume na mwanamuke wa kwanza walikataa utawala wa Yehova, na tangu wakati huo wengine wengi wamefanya hivyo. Hilo linaweza kufanya wengine wajiulize ikiwa mashitaka ya Shetani yalikuwa ya kweli. Kadiri mashitaka ya Shetani hayajapata jibu katika akili za wanadamu ao malaika, muvurugo utaendelea kuwa kati ya mataifa, watu wa rangi mbalimbali za ngozi, makabila, familia, na watu. Lakini, kisha kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala, wote watajitiisha milele chini ya utawala wake wenye haki. Ulimwengu wote muzima utakuwa na amani.​—Efe. 1: 9, 10.

5. Namna gani jambo la kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala linatuhusu?

5 Haki ya Mungu ya kutawala itatetewa, na utawala wa Shetani na wanadamu utashindwa na kuondolewa. Utawala wa Mungu wenye kuongozwa na Masiya Mufalme utapata ushindi, na watu washikamanifu watakuwa wameonyesha kuwa wanadamu wanaweza kuunga mukono utawala wa Mungu. (Isa. 45:23, 24) Unapenda kuwa kati ya wale wenye kuonyesha ushikamanifu wao kwa kuunga mukono haki ya Yehova ya kutawala? Tunajua kuwa unapenda kabisa. Ili tukuwe washikamanifu, tunapaswa kukaza akili yetu juu ya kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala na kuelewa kuwa hilo ndilo jambo la maana.

KUTETEWA KWA HAKI YA YEHOVA YA KUTAWALA NDILO JAMBO LA MAANA ZAIDI KULIKO WOKOVU

6. Kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala ni jambo la maana kwa kadiri gani?

6 Kama vile, tumekwisha kuona, kutetewa kwa haki ya Mungu ya kutawala ni jambo la maana lenye kuhusu wanadamu. Ni jambo la maana zaidi kuliko furaha ya mwanadamu yeyote. Hilo linamaanisha kuwa wokovu wetu haiko jambo la maana ao kuwa Yehova hatuhangaikie kabisa? Hapana kabisa. Sababu gani?

7, 8. Sababu gani kutetewa kwa haki ya Mungu ya kutawala kunatia ndani kutimizwa kwa ahadi zake?

7 Yehova anawapenda sana wanadamu na anawaona kuwa wa maana. Alikuwa tayari kutoa Mwana wake ili tuweze kupata uzima wa milele. (Yoh. 3: 16; 1 Yoh. 4:9) Ikiwa Yehova angeshindwa kutimiza ahadi zake, Shetani angekuwa na sababu ya kumuita Mungu kuwa ni musema-uongo mwenye kunyima watu wake mambo ya muzuri na anatawala mubaya. Pia, hilo lingeunga mukono wapinzani wenye kuuliza hivi kwa kuchekelea ahadi za Yehova: “Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.” (2 Pet. 3:3, 4) Kwa hiyo, Yehova atahakikisha kuwa kutetewa kwa haki yake ya kutawala kunatia ndani kuokolewa kwa wanadamu wenye kumutii! (Soma Isaya 55:10, 11.) Zaidi ya hilo, utawala wa Yehova unategemea upendo. Kwa hiyo, tunaweza kuwa hakika kuwa atapenda sikuzote watumishi wake washikamanifu na kuwaona kuwa wa maana.​—Kut. 34:6.

8 Kwa sababu kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala ndilo jambo la maana, hilo halimaanishe kuwa sisi ao wokovu wetu hauna maana yoyote kwake. Tunapenda tu kuwa na mawazo yenye kufaa juu ya haki ya Mungu ya kutawala na wokovu wetu. Ni jambo la maana kuwa na mawazo hayo ya muzuri ikiwa tunapenda kukaza macho yetu juu ya jambo hilo la maana na kuunga mukono utawala wa Yehova wenye haki.

MAWAZO YENYE KUTUFUNDISHA JAMBO FULANI

9. Shetani alisema nini juu ya Ayubu? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Ni jambo la maana tukuwe na mawazo ya muzuri juu ya haki ya Yehova ya kutawala. Tunaweza kuelewa jambo hilo kwa kusoma kitabu cha Ayubu; kitabu hicho kiko kati ya vitabu vya Biblia vya kwanza-kwanza vyenye viliandikwa. Katika kitabu hicho tunajifunza juu ya mashitaka ya Shetani yenye kuonyesha kama ikiwa Ayubu angepatwa na mateso makali, angeacha kuwa mushikamanifu kwa Mungu. Shetani alimuomba Mungu yeye mwenyewe amutese Ayubu. Yehova hakufanya hivyo, lakini alimuruhusu Shetani amujaribu Ayubu. Alimuambia hivi: ‘Kila kitu alicho nacho kiko mukononi mwako.’ (Soma Ayubu 1:7-12.) Kwa muda mufupi, Ayubu alipoteza watumishi wake, mali yake yote, na watoto wake wapendwa kumi. Shetani alifanya ionekane kuwa ni Mungu ndiye alikuwa anamuletea Ayubu mateso hayo yote. (Ayu. 1:13-19) Kisha, Shetani alimuletea Ayubu ugonjwa mubaya sana na wenye maumivu. (Ayu. 2:7) Huzuni yake iliongezeka zaidi wakati bibi yake na marafiki wake wa uongo watatu walimuambia maneno yenye kuvunja moyo.​—Ayu. 2:9; 3:11; 16:2.

10. (a) Ayubu alifanya nini ili kuonyesha kuwa alikuwa mushikamanifu kwa Mungu? (b) Lakini alikosea katika njia gani?

10 Matokeo yalikuwa nini? Mashitaka ya Shetani yalionekana kuwa ya uwongo kabisa. Ayubu alikataa kumukana Mungu. (Ayu. 27:5) Lakini, wakati fulani Ayubu alikuwa na mawazo yenye hayafae. Alianza kufikiria sana uadilifu wake mwenyewe, na aliuliza hata sababu gani alikuwa anateseka. (Ayu. 7:20; 13:24) Tunaweza kufikiri kwamba hilo linaweza kueleweka kwa sababu ya mambo yote yenye yalimufikia. Lakini Mungu aliona kuwa ni lazima amusaidie Ayubu kubadilisha mawazo yake. Yehova alimuambia nini?

11, 12. Yehova alimusaidia Ayubu akuwe na mawazo gani yenye kufaa, na Ayubu aliitikia namna gani?

11 Maneno yenye Mungu aliambia Ayubu yanapatikana katika sura ine za kitabu cha Ayubu, ni kusema, sura ya 38 mupaka ya 41. Hakuna nafasi kwenye Mungu alimuambia waziwazi sababu gani alikuwa anateseka. Maneno yenye Yehova alimuambia Ayubu hayakukuwa na kusudi la kumufasiria sababu gani alikuwa anateseka; Mungu hakulazimika kufanya hivyo. Lakini Yehova alipenda kumusaidia Ayubu aelewe kama alikuwa wa hali ya chini sana kwa kulinganishwa na Mungu. Na alisaidia Ayubu aone kuwa kuko mambo yenye kuwa ya maana zaidi yenye anapaswa kuhangaikia. (Soma Ayubu 38:18-21.) Hilo lilisaidia Ayubu akuwe tena na mawazo ya muzuri.

12 Yehova alitenda kwa ukali kwa kumupatia Ayubu mashauri hayo ya moja kwa moja kisha Ayubu kuvumilia mateso makali? Mungu hakutenda kwa ukali, na Ayubu hakufikiri hivyo. Hata kama aliteseka sana, mwishowe Ayubu alianza kusema maneno ya muzuri. Alisema hata hivi: “Ninayatangua [ninayaondoa] niliyosema, nami ninatubu katika mavumbi na majivu.” Hiyo ilikuwa matokeo ya mashauri ya Yehova ya moja kwa moja lakini yenye kutia moyo. (Ayu. 42:1-6) Mbele ya hapo, Ayubu alikuwa amepata mashauri kutoka kwa kijana Elihu. (Ayu. 32:5-10) Kisha Ayubu kukubali mashauri ya Mungu na kubadilisha mawazo yake, Yehova aliambia wengine kuwa alipendezwa na Ayubu kwa sababu alibakia muaminifu wakati wa mateso.​—Ayu. 42:7, 8.

13. Namna gani mashauri ya Yehova yangeendelea kumusaidia Ayubu kisha mateso yake?

13 Mashauri ya Yehova yangeendelea kumusaidia Ayubu hata kisha mateso yake kuisha. Namna gani? ‘Yehova aliubariki mwisho wa Ayubu baadaye kuliko mwanzo wake,’ hilo lilipaswa kuchukua wakati ili akuwe tena na hali ya muzuri. Alifikia ‘kuwa na wana [watoto wanaume] saba na binti watatu.’ (Ayu. 42:12-14) Kwa kweli, Ayubu alikuwa anakumbuka watoto wake wenye Shetani alikuwa ameua. Pengine alikumbuka muzuri kwa wakati fulani mateso yenye yalimupata. Hata kama mwishowe alifikia kuelewa muzuri sababu gani alikuwa anateseka, pengine wakati fulani alifikiria sababu gani ilikuwa jambo la lazima ateseke sana hivyo. Hata iwe alikuwa na mawazo gani, angeweza kufikiria mashauri yenye Mungu alimutolea. Kufanya hivyo kungemusaidia aendelee kuwa na mawazo ya muzuri, na hilo lingemufariji.​—Zab. 94:19.

Tunaweza kuepuka kufikiria magumu yetu na kukaza akili juu ya jambo la maana zaidi? (Picha hizi inapatana na fungu la 14)

14. Mufano wa Ayubu unaweza kutufundisha nini?

14 Kitabu cha Ayubu kinaweza kutusaidia tukuwe na mawazo yenye kufaa na tupate faraja. Kwa kweli, Yehova aliandikisha kitabu hicho ‘ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tukuwe na tumaini.’ (Rom. 15:4) Hilo linatufundisha nini? Linatufundisha jambo hili la maana sana: Tusihangaikie sana maisha yetu mupaka tunakosa kukaza akili yetu juu ya jambo hilo la maana, ni kusema, kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala. Na tuendelee kuonyesha kuwa kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala ndilo jambo la maana kwa kubakia waaminifu hata wakati tunapatwa na mateso kama vile Ayubu alifanya.

15. Uaminifu wetu unatimiza nini wakati tunavumilia mateso?

15 Sababu gani ni jambo lenye kutia moyo kufikiria faida yenye tunapata wakati tunabakia waaminifu? Kwa sababu hilo linamaanisha kuwa mateso yetu yanatimiza kusudi fulani. Hayaonyeshe hata kidogo kuwa Yehova anatukasirikia, lakini yanatutolea nafasi ya kuonyesha kuwa tunaunga mukono haki ya Mungu ya kutawala. (Met. 27:11) Uvumilivu wetu unatokeza “hali yenye kukubaliwa,” na unatia nguvu tumaini letu. (Soma Waroma 5:3-5.) Habari juu ya Ayubu inaonyesha muzuri kuwa “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.” (Yak. 5:11) Kwa hiyo, tunaweza kuwa hakika kuwa atabariki wale wote wenye kuunga mukono utawala wake. Kujua jambo hilo kunatusaidia “kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.”​—Kol. 1:11.

ENDELEA KUKAZA AKILI YAKO

16. Sababu gani tunapaswa kukumbuka kuwa kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala ni jambo la maana sana?

16 Lakini, inaweza kuwa vigumu kuendelea kukaza macho yetu juu ya kutetewa kwa haki ya Yehova ya kutawala. Tunaweza kuhangaika sana kwa sababu ya magumu yetu. Hata magumu madogo-madogo yanaweza kuonekana kuwa makubwa ikiwa tunayafikiria sana. Kwa hiyo, wakati tunapatwa na magumu fulani, ni muzuri tukumbuke kila wakati kuwa ni jambo la maana sana kuunga mukono haki ya Mungu ya kutawala.

17. Namna gani kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Yehova kunatusaidia tuendelee kukaza akili yetu juu ya jambo la maana?

17 Kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Yehova kunaweza kutusaidia tuendelee kukaza macho yetu juu ya jambo la maana. Kwa mufano, dada mumoja mwenye kuitwa Renee aliteseka sana kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza na alipiganisha maumivu ya kila siku na kansere. Wakati alikuwa anatunzwa kwenye hospitali mbalimbali, alihubiria wafanyakazi, wagonjwa, na watu wenye walikuwa wanatembelea wagonjwa. Katika hospitali moja, alipitisha saa 80 katika mahubiri kwa majuma mbili na nusu tu. Hata wakati alikaribia kufa, Renee aliendelea kukaza akili yake juu ya haki ya Yehova ya kutawala. Na hilo lilipunguza huzuni yake.

18. Namna gani mufano wa dada mumoja unaonyesha faida ya kuunga mukono haki ya Yehova ya kutawala?

18 Kwa kweli, tunapenda kukaza akili juu ya haki ya Mungu ya kutawala hata wakati tunapatwa na mahangaiko na magumu ya kila siku. Jennifer alifanya siku tatu kwenye uwanja wa ndege (avion) ili kungojea ndege ya kuenda nyumbani kwao. Lakini hakuna ndege yenye ilifanya safari. Kwa sababu alijisikia kuwa peke yake na mwenye kuchoka sana, ingelikuwa mwepesi kwake kuanza kujisikilia huruma. Lakini alisali ili apate nafasi ya kuhubiria wengine wenye walikuwa katika hali kama yake. Alipata matokeo gani? Alihubiria watu wengi na aliwaachia vichapo vingi. Anasema hivi: “Niliona kuwa Yehova amenibariki hata kama nilikuwa katika hali ngumu na alinipatia nguvu ya kubeba jina lake katika njia yenye kufaa.” Kwa kweli, aliendelea kukaza macho yake juu ya kusudi la Yehova.

19. Watu wa Yehova wako na musimamo gani juu ya haki yake ya kutawala?

19 Kuunga mukono haki ya Yehova ya kutawala kumetofautisha dini ya kweli na dini ya uwongo. Kuanzia zamani watu wa Mungu wameunga mukono haki yake ya kutawala. Kwa sababu tunaunga mukono ibada ya kweli, kila mumoja wetu anapaswa kujikaza kuendelea kuwa na musimamo huo wenye kutegemea Maandiko.

20. Yehova anajisikia namna gani juu ya bidii yako ya kuunga mukono haki yake ya kutawala?

20 Ukuwe hakika kuwa Yehova anapendezwa na bidii yako ya kuunga mukono haki yake ya kutawala kwa kumutumikia kwa uaminifu na kwa kuvumilia mateso. (Zab. 18:25) Habari yenye kufuata itazungumuzia zaidi sababu gani tunapaswa kutegemeza kwa moyo wetu wote haki ya Yehova ya kutawala na namna tunaweza kuiunga mukono.