Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana na Uzee Vizuri

Kukabiliana na Uzee Vizuri

UNAHISIJE wazo la kuzeeka linapokuja akilini? Wengi hukosa furaha, huwa na wasiwasi, na hata huogopa. Hii ni kwa sababu uzee unahusisha matatizo mbalimbali kama vile ngozi kusinyaa, mwili kuwa dhaifu, kupoteza kumbukumbu, na magonjwa ya kudumu.

Hata hivyo, hali ya kuzeeka hutofautiana kutoka mmoja na mwingine. Wengine wanapozeeka huendelea kwa kadiri fulani kuwa na afya nzuri kimwili na kiakili. Maendeleo ya kitiba yamewawezesha wengine kutibu au kupambana na magonjwa ya kudumu. Hii ndiyo sababu katika nchi nyingi watu wengi wanaishi miaka mingi na wana afya bora.

Hata hivyo, iwe unakabili matatizo yanayotokana na uzee au la, watu wengi wangependa kuzeeka katika hali inayofaa. Hilo linawezekanaje? Kwa sehemu, kufanya hivyo kunategemea mtazamo, utayari na uwezo wetu wa kubadilikana kulingana na hali hiyo mpya maishani. Ili kutusaidia kufanya hivyo, acheni tuchunguze baadhi ya kanuni za Biblia zenye kufaa.

UWE NA KIASI: “Wenye kiasi wana hekima.” (Methali 11:2) Katika muktadha huo, “wenye kiasi” wanaweza kurejelea wazee wanaotambua na kukubali kwamba hawawezi kutimiza mambo fulani kwa sababu ya umri wao. Charles, mwenye umri wa miaka 93 kutoka Brazili, anasema hivi: “Kama utaishi muda mrefu, lazima utazeeka. Huwezi kurudisha wakati nyuma.”

Hata hivyo, kuwa na kiasi hakumaanishi kuwa na mtazamo huu usiofaa: “Nimezeeka, siwezi kufanya jambo lolote.” Mtazamo huo unaweza kudhoofisha shangwe ya mtu. Methali 24:10 inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Badala yake, mtu mwenye kiasi anaonyesha hekima kwa kufanya mambo anayoweza.

Corrado, mwenye umri wa miaka 77 kutoka Italia, anasema hivi kwa busara: “Unapoendesha gari kupanda mlima, unahitaji kubadili gia na kuepuka kuzima injini.” Kwa kweli, mtu anapozeeka anahitaji kufanya mabadiliko. Corrado na mke wake wamepanga ratiba yenye usawaziko ya kufanya kazi za nyumbani inayowasaidia kutochoka kabisa ifikapo jioni. Marian, mwenye umri wa miaka 81 kutoka Brazili, anasema hivi kuhusu jinsi ya kukabiliana na uzee: “Nimejifunza jinsi ya kujiongoza. Mimi hupumzika kidogo kila mara ninapohitaji kufanya hivyo kwa sababu ya kuhisi uchovu ninapofanya kazi. Mimi hukaa au kulala ili kusoma au kusikiliza muziki. Nimejifunza kutambua na kuheshimu kile ninachoweza kutimiza.”

Uwe na Usawaziko

UWE NA USAWAZIKO: “Wanawake wajipambe kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.” (1 Timotheo 2:9) Maneno “mavazi yenye mpangilio mzuri” yanaonyesha kuwa yana usawaziko na yanayofaa. Barbara, mwenye umri wa miaka 74 kutoka Kanada, anasema hivi: “Ninajitahidi kuwa msafi na nadhifu. Nisingependa kuwa mtu anayevalia ovyo eti kwa sababu ya mtazamo wa kwamba ‘mimi ni mzee; na sijali jinsi ninavyoonekana.’” Fern, mwenye umri wa miaka 91 kutoka Brazili, anasema hivi: “Ninanunua nguo mpya kila baada ya kipindi fulani ili kujisikia vizuri.” Wanaume waliozeeka wana maoni gani? Antônio, mwenye umri wa miaka 73 kutoka Brazili, anasema hivi: “Ninajitahidi kupendeza kwa kuvaa nguo safi na zinazofaa.” Kuhusu usafi wa kimwili, anaongeza hivi: “Ninaoga na kunyoa ndevu kila siku.”

Kwa upande mwingine, ni muhimu kuepuka kuhangaikia kupita kiasi kuhusu mwonekano wako kufikia hatua ya kupoteza “utimamu wa akili.” Bok-im, mwenye umri wa miaka 69 kutoka Korea Kusini, ana maoni yaliyosawazika kuhusu mavazi. Anasema hivi: “Ninaona kuwa jambo lisilofaa kuvaa baadhi mavazi niliyovaa nilipokuwa kijana.”

Uwe na Mtazamo Unaofaa

UWE NA MTAZAMO UNAOFAA: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” (Methali 15:15) Kadiri unavyozeeka, unaweza kuhisi vibaya unapokumbuka nguvu zako za ujana na mambo uliyoweza kutimiza. Hali hiyo inaeleweka. Hata hivyo, jitahidi kutozidiwa na hisia hizo zisizofaa. Kuendelea kufikiria mambo ya zamani kunaweza kufanya maisha yako yasiwe na furaha na kukuvunja moyo ushindwe kufanya yale unayoweza kutimiza. Joseph, mwenye umri wa miaka 79 kutoka Kanada, ana mtazamo huu unaofaa: “Ninajaribu kufurahia kufanya mambo ninayoweza na kuepuka kuhuzunika kuhusu mambo niliyoweza kutimiza nilipokuwa kijana ambayo sasa siwezi kutimiza.”

Kusoma na kujifunza kunaweza pia kukusaidia kuwa na mtazamo unaofaa na kukusaidia kujifunza mambo mapya. Hivyo, jitahidi kwa kadiri uwezavyo kutafuta fursa za kusoma na kujifunza mambo mapya. Ernesto, mwenye umri wa miaka 74 kutoka Filipino, hutembelea maktaba ili kutafuta kitabu chenye habari nzuri anazoweza kusoma. Anasema hivi: “Ninafurahia kusoma kuhusu matukio yenye kusisimua, na kusafiri kimawazo kwa kusoma vitabu.” Lennart, mwenye umri wa miaka 75 kutoka Sweden hata aliamua kujifunza lugha mpya.

Uwe Mkarimu

UWE MKARIMU: “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi.” (Luka 6:38) Uwe na kawaida ya kushiriki na wengine wakati na mali zako. Hilo litakufanya uhisi kwamba umetimiza jambo na kukupa furaha. Hosa, mwenye umri wa miaka 85 kutoka Brazili, hujitahidi kuwasaidia wengine licha ya kuwa dhaifu kimwili. Anasema hivi: “Mimi huwapigia simu na kuwaandikia barua rafiki zangu ambao ni wagonjwa au waliovunjika moyo. Pindi nyingine mimi huwatumia zawadi. Ninapenda pia kuwapikia wagonjwa chakula.”

Tunapokuwa wakarimu tunawachochea wengine pia kuwa wakarimu. Jan, mwenye umri wa miaka 66 kutoka Sweden, anasema hivi: “Unapowaonyesha wengine upendo, wao pia watakuonyesha upendo na urafiki.” Kwa kweli, mtu mkarimu huwafanya wengine wahisi kwamba wanathaminiwa.

UWE MWENYE URAFIKI: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Ingawa kuna pindi ambazo huenda ungependa kuwa peke yako, epuka kujitenga na wengine. Innocent, mwenye umri wa miaka 72 kutoka Nigeria, anapenda kushirikiana na marafiki. Anasema hivi: “Ninafurahia kushirikiana na watu wenye umri mbalimbali.” Börje, mwenye umri wa miaka 85 kutoka Sweden, anasema hivi: “Mimi hujitahidi kushirikiana na vijana. Nguvu zao hunifanya nijihisi kijana—angalau moyoni.” Chukua hatua ya kwanza kwa kuwaalika marafiki kila unapopata nafasi. Han-sik, mwenye umri wa miaka 72 kutoka Korea Kusini, anasema hivi: “Mimi na mke wangu tunapenda kuwaalika marafiki wenye umri tofauti-tofauti—wazee na vijana—ili kufurahia mazungumzo au kushiriki mlo pamoja.”

Uwe Mwenye Urafiki

Marafiki huwasiliana. Hata hivyo, kwa kuwa mawasiliano yanahusisha kuzungumza na kusikiliza wengine, jitahidi kufanya hivyo ili uwe rafiki mzuri. Pendezwa kibinafsi na wengine. Helena, mwenye umri wa miaka 71 kutoka Msumbiji, anasema hivi: “Mimi ni mwenye urafiki na ninawaheshimu wengine. Ninawasikiliza wanapozungumza ili kujua wanachofikiri na mambo wanayopenda.” José, mwenye umri wa miaka 73 kutoka Brazili, anasema hivi: “Watu hufurahia kushirikiana na wasikilizaji wazuri—wanaoonyesha hisia-mwenzi na wanaopendezwa na wengine, wanaotoa pongezi inayostahili, na wacheshi.”

Unapozungumza, hakikisha kwamba ‘maneno yako yanakuwa yenye kukolezwa chumvi.’ (Wakolosai 4:6) Uwe mwenye ufikirio na mwenye kutia moyo.

UWE MWENYE SHUKRANI: “Mjionyeshe kuwa wenye shukrani.” (Wakolosai 3:15) Unapopokea msaada, onyesha kwamba unathamini jambo hilo. Maneno yanayoonyesha shukrani yanasaidia kusitawisha mahusiano mazuri. Marie-Paule, mwenye umri wa miaka 74 kutoka Kanada, anasema hivi: “Hivi karibuni mimi na mume wangu tulihama kutoka kwenye nyumba yetu. Tulikuwa na marafiki wengi waliotusaidia. Tuliwashukuru sana. Tulimtumia kila mmoja wao kadi ya shukrani na baadhi yao tuliwaalika kula chakula pamoja nasi.” Jae-won, mwenye umri wa miaka 76 kutoka Korea Kusini, anathamini msaada anaopata wa kusafirishwa na gari kwenda Jumba la Ufalme. Anasema hivi: “Ninashukuru sana kwa msaada huo hivi kwamba mimi huchangia kiasi fulani cha pesa kwa ajili ya mafuta. Mara nyingine mimi hutoa zawadi na kadi za shukrani.”

Zaidi ya yote, onyesha shukrani kuelekea uhai. Mfalme mwenye hekima, Sulemani, anatukumbusha hivi: “Mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa.” (Mhubiri 9:4) Kwa kweli, unaweza kukabiliana na uzee vizuri ukiwa na mtazamo unaofaa na ukiwa tayari kubadilikana kulingana na hali.

Uwe Mwenye Shukrani