Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Majibu ya Maswali ya Biblia

Majibu ya Maswali ya Biblia

Je, inawezekana kuishi milele?

Ni nini kinachoweza kutuweka huru kutokana na kifo?

Mwanadamu wa kwanza, Adamu, aliishi karne nyingi. Lakini baadaye alizeeka na kufa. Tangu wakati huo, watu wamejaribu njia mbalimbali za kuzuia kuzeeka. Lakini hakuna mtu ambaye amefaulu kuepuka kifo. Kwa nini? Adamu alizeeka na kufa kwa sababu alitenda dhambi kwa kutomtii Mungu. Tunazeeka kwa sababu tumerithi dhambi na kifo kutoka kwa Adamu.Soma Mwanzo 5:5; Waroma 5:12.

Ili tuishi milele, tunahitaji mtu wa kutulipia fidia. (Ayubu 33:24, 25) Fidia ni malipo yanayotolewa ili kumweka mtu huru, na sisi tunahitaji kuwekwa huru kutokana na kifo. (Kutoka 21:29, 30) Yesu alilipa fidia hiyo alipokufa kwa ajili yetu.Soma Yohana 3:16.

Tunawezaje kupata uzima wa milele?

Si kila mtu atakayewekwa huru kutokana na magonjwa na kuzeeka. Basi, wale wasiomtii Mungu kama Adamu alivyofanya, hawatapata uzima wa milele. Watu watakaosamehewa dhambi zao ndio watakaofurahia kuishi milele.Soma Isaya 33:24; 35:3-6.

Lazima tuchukue hatua fulani ili tusamehewe. Tunapaswa kumjua Mungu kwa kujifunza Biblia, Neno lake. Biblia inatufundisha jinsi ya kuwa na maisha yenye furaha na pia jinsi ya kupata kibali cha Mungu na uzima wa milele.Soma Yohana 17:3; Matendo 3:19.