Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka Katika Neno La Mungu

Je, Unaweza Kuishi Milele?

Je, Unaweza Kuishi Milele?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Kwa nini maisha yetu yanaonekana kuwa mafupi?

Baadhi ya kobe huishi miaka 150 na miti fulani huishi miaka 3,000. Kinyume cha hilo, maisha ya wanadamu ni mafupi sana. Hata hivyo, maisha yetu yanaweza kuwa yenye maana zaidi kuliko maisha ya kobe au ya mti. Yehova Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kufurahia muziki, michezo, chakula, kujifunza, kusafiri, na kukutana na watu. Mungu aliweka ndani ya mioyo yetu tamaa ya kuwa na uhai usio na kikomo.—Soma Mhubiri 3:11.

2. Je, kweli tunaweza kuishi milele?

Yehova huishi milele. Yeye hawezi kufa. Ndiye Chanzo cha uhai, na hivyo anaweza kuwapa wengine uzima wa milele. (Zaburi 36:9; Habakuki 1:12) Zaidi ya hilo, ameahidi kuwapa uzima wa milele wote wanaomtii. Atawafanya wazee wawe vijana.—Soma Ayubu 33:24, 25; Isaya 25:8; 33:24.

Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwamba tunaweza kuamini ahadi ya Mungu ya kuwa na uzima wa milele huku tukiwa na afya kamilifu. Yesu aliponya magonjwa mbalimbali na hata aliwafufua wafu.—Soma Luka 7:11-15, 18, 19, 22.

3. Tutapata uzima wa milele lini?

Mungu anataka tuishi milele, si katika ulimwengu uliojaa ukandamizaji na jeuri, bali katika dunia paradiso. Anataka tujihisi tukiwa salama. (Zaburi 37:9, 29; Isaya 65:21, 22) Dunia itakapogeuzwa na kuwa Paradiso, mamilioni ya watu waliokufa watafufuliwa. Watu watakaofufuliwa ambao watachagua kumwabudu Mungu na kumtii wataishi milele.—Soma Luka 23:42, 43; Yohana 5:28, 29.

4. Tunawezaje kupata uzima wa milele?

Mungu peke yake ndiye anayeweza kutupatia uzima wa milele. Kwa hiyo, tunapaswa kumkaribia kwa kujifunza kumhusu. Biblia inalinganisha kupata ujuzi juu ya Mungu na kula chakula. (Mathayo 4:4) Inafurahisha kula chakula, lakini tunahitaji kujitahidi ili tukipate na kukitayarisha. Vivyo hivyo, kupata chakula cha kiroho kunahitaji jitihada. Hata hivyo, ni jambo gani linaloweza kuwa na faida nyingi kuliko kumkaribia Mungu na kupata uzima wa milele?—Soma Luka 13:23, 24; Yohana 6:27; 17:3.