Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

“Sitamani Tena Kuubadili Ulimwengu”

“Sitamani Tena Kuubadili Ulimwengu”
  • Mwaka wa Kuzaliwa: 1966

  • NCHI: FINLAND

  • HISTORIA: MWANAHARAKATI WA MASUALA YA KIJAMII

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nimependezwa na mazingira tangu nilipokuwa mtoto. Mara kwa mara familia yetu ilitembelea misitu na maziwa maridadi yaliyo karibu na mji wetu wa nyumbani Jyväskylä, huko Finland ya Kati. Pia, ninapenda wanyama. Nilipokuwa mtoto, nilipenda kukumbatia kila mbwa na paka niliyemwona! Nilipoendelea kukua nilikasirika nilipoona jinsi watu walivyowatendea wanyama vibaya. Baadaye, nikajiunga na shirika la kutetea haki za wanyama, ambako nilikutana na watu wenye maoni kama yangu.

Tulifanya kampeni za kutetea haki za wanyama. Tulisambaza habari na kupanga maandamano ya kupinga maduka ya kuuza manyoya na maabara ya majaribio ya wanyama. Hata tulianzisha shirika jipya la kuwalinda wanyama. Kwa sababu tulichukua hatua ili kutimiza lengo letu, mara nyingi tulipambana na wenye mamlaka. Nilikamatwa na kupelekwa mahakamani mara kadhaa.

Mbali na kuwahangaikia wanyama, nilisumbuliwa na matatizo mengine yaliyo ulimwenguni. Mwishowe nikaanza kushirikiana na mashirika mengine, kutia ndani Amnesty International na Greenpeace. Nilijishughulisha sana na mashirika hayo. Niliwatetea maskini, wenye njaa, na watu wengine wanaoteseka.

Hata hivyo, pole kwa pole nilitambua singeweza kuubadili ulimwengu. Ingawa mashirika hayo yalifaulu kutatua matatizo madogo-madogo, matatizo makubwa yalizidi kuongezeka. Ni kana kwamba ulimwengu ulikuwa umejaa uovu na hakuna mtu aliyejali lolote. Nilihisi nimelemewa.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Nikiwa nimehuzunika kwa kukosa uwezo, nilianza kumfikiria Mungu na Biblia. Hapo mbeleni, nilikuwa nimejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ingawa nilitambua Mashahidi walikuwa wenye fadhili na walipendezwa nami,  sikuwa tayari kubadili maisha yangu. Hata hivyo, sasa mambo yalikuwa yamebadilika.

Nilichukua Biblia yangu, nikaanza kuisoma. Iliponya majeraha yangu yote. Nilisoma masimulizi mengi ya Biblia yanayoonyesha kuwa tunapaswa kuwatendea wanyama kwa fadhili. Kwa mfano, andiko la Methali 12:10 linasema “watu wazuri hutunza wanyama wao.” (Good News Translation) Pia, nilitambua si Mungu anayesababisha matatizo ulimwenguni. Badala yake, matatizo yetu yameongezeka kwa sababu wanadamu wengi hawamtii Mungu. Niliguswa moyo sana nilipojifunza kuhusu upendo na uvumilivu wa Yehova.—Zaburi 103:8-14.

Karibu na kipindi hicho, nilijaza na kutuma ombi la kupokea kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Muda mfupi baadaye, wenzi wa ndoa Mashahidi walinitembelea na wakajitolea kunifundisha Biblia, nami nikakubali. Pia, nilianza kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika Jumba la Ufalme. Hivyo, nikaanza kupenda mambo niliyokuwa nikijifunza katika Biblia.

Kujifunza Biblia kulinisaidia kufanya mabadiliko mengi. Niliacha kuvuta sigara na kunywa pombe kupita kiasi. Nilianza kuvalia mavazi nadhifu na kuacha kutumia lugha chafu. Nikabadili mtazamo wangu kueleka wenye mamlaka. (Waroma 13:1) Pia, niliacha maisha mapotovu, jambo nililoona kuwa la kawaida tu mwanzoni.

Badiliko gumu zaidi nililokabili ni kubadili maoni yangu kuhusu mashirika ya kijamii. Hilo lilichukua muda mrefu. Mwanzoni nilifikiri ningesaliti mashirika hayo ikiwa ningejitenga nayo. Hata hivyo, baadaye nilielewa kwamba Ufalme wa Mungu ndio tu utakaoleta mabadiliko ulimwenguni. Nikaamua kuunga mkono Ufalme huo kwa moyo wangu wote na kuwasaidia watu wajifunze kuuhusu.—Mathayo 6:33.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Nilipokuwa mwanaharakati, nilikuwa nikigawanya watu katika vikundi viwili—watu wazuri au wabaya—na nilikuwa tayari kuchukua hatua dhidi ya watu wabaya. Lakini kujifunza Biblia kumenisaidia nisiwachukie watu. Badala yake, ninajaribu kuwaonyesha watu wote upendo wa Kikristo. (Mathayo 5:44) Njia moja ninayoonyesha upendo huo ni kwa kuwahubiria watu habari njema ya Ufalme wa Mungu. Ninafurahi kuona jinsi kazi hii inavyoleta amani na furaha na kuwapa watu tumaini la kweli.

Nimepata amani na utulivu kwa kuacha Yehova aongoze mambo. Ninasadiki kwamba, akiwa Muumba hataruhusu wanyama na wanadamu wadhulumiwe milele, wala hataruhusu dunia yetu maridadi iharibiwe. Badala yake, kupitia Ufalme wake, hivi karibuni atarekebisha mambo. (Isaya 11:1-9) Ninafurahi sana kujua ukweli huu na pia kuwasaidia wengine waujue. Sitamani tena kuubadili ulimwengu.