Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE,MWISHO UMEKARIBIA?

Wengi Wataokoka Mwisho—Wewe Pia Unaweza

Wengi Wataokoka Mwisho—Wewe Pia Unaweza

Biblia inatuambia kwamba mwisho utahusisha maangamizi: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa. Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna chochote chenye mwili ambacho kingeokolewa.’ (Mathayo 24:21, 22) Hata hivyo, Mungu anatuahidi kwamba watu wengi wataokoka: “Ulimwengu unapitilia mbali . . . , lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.

Unapaswa kufanya nini ili uokoke mwisho wa ulimwengu huu unaopitilia mbali na kisha ‘kudumu milele’? Je, unahitaji kujirundikia vitu vingi au kufanya mazoezi fulani ya mwili ili kujitayarisha? Hapana. Biblia inatuhimiza kufanya matayarisho ya aina tofauti. Tunasoma hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” (2 Petro 3:10-12) Muktadha unaonyesha kwamba “vitu vyote” vitakavyoharibiwa vitatia ndani sehemu za utawala wa ulimwengu huu na wote wanaounga mkono utawala huo badala ya utawala wa Mungu. Ni wazi kwamba, kujirundikia vitu vingi hakutaweza kutuokoa kutokana na uharibifu unaokuja.

Kwa kweli, wokovu wetu unatia ndani kumtumikia Yehova Mungu na kujifunza kuhusu aina ya mwenendo na matendo yanayompendeza. (Sefania 2:3) Badala ya kufuata maoni ya watu wengi na kupuuza ishara zinazoonyesha waziwazi kwamba tunaishi katika kipindi muhimu sana cha wakati, tunahitaji “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Mashahidi wa Yehova wanaweza kukuonyesha katika Biblia jinsi unavyoweza kuokoka siku hiyo inayokuja.