Hamia kwenye habari

Unawezaje kuielewa Biblia?

Unawezaje kuielewa Biblia?

Jibu la Biblia

 Biblia yenyewe inaonyesha njia nyingi za kuielewa. Bila kujali malezi yako, ujumbe wa Mungu ulio katika Biblia ‘si ngumu mno kwako, wala hauko mbali.’—Kumbukumbu la Torati 30:11.

Njia za kuielewa Biblia

  1.   Uwe na mtazamo unaofaa. Kubali kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Uwe mnyenyekevu, kwa kuwa Mungu anawapinga wenye kiburi. (1 Wathesalonike 2:13; Yakobo 4:6) Hata hivyo, usiamini tu bila kufikiri, Mungu anataka utumie ‘nguvu zako za kufikiri.’—Waroma 12:1, 2.

  2.   Sali ili upate hekima. Biblia inasema hivi katika Methali 3:5: “Usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Badala yake, ‘endelea kumwomba Mungu’ ili akupe hekima ya kuielewa Biblia.—Yakobo 1:5.

  3.   Jifunze kwa ukawaida. Utafaidika hata zaidi ukiendelea kujifunza Biblia kwa ukawaida badala ya kuisoma mara kwa mara tu.—Yoshua 1:8.

  4.   Jifunze kwa kuchagua wazo. Funzo linalotegemea vichwa mbalimbali, yaani, kujifunza habari fulani hususa, ni njia nzuri sana ya kujifunza mafundisho ya Maandiko. Anza na “masomo ya msingi,” na kisha “endelea na mafundisho makomavu zaidi (mazito zaidi).’ (Waebrania 6:1, 2, Easy-to-Read Version) Utaona kwamba unaweza kulinganisha andiko moja na andiko lingine na kugundua kwamba sehemu mbalimbali za Biblia zinafafanua sehemu nyingine, hata zile zilizo ‘ngumu kueleweka.’—2 Petro 3:16.

  5.   Waombe wengine msaada. Biblia inatutia moyo tukubali msaada kutoka kwa wengine wanaoielewa Biblia. (Matendo 8:30, 31) Mashahidi wa Yehova huandaa programu ya kujifunza Biblia bila malipo kwa kutumia njia iliyotumiwa na Wakristo wa mapema. Wanatumia marejeo ya Kimaandiko kuwasaidia wengine kujua yale ambayo Biblia inafundisha hasa.—Matendo 17:2, 3.

Ili kuijua Biblia huhitaji kuwa na mambo yafuatayo

  1.   Akili au elimu ya juu. Kwa mfano, mitume 12 wa Yesu walielewa Maandiko na kuwafundisha wengine, hata ingawa mitume walionwa na wengine kuwa “wasio na elimu na wa kawaida tu.”—Matendo 4:13.

  2.   Pesa. Unaweza kujifunza Biblia bila malipo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:8.