Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Acheni Tulinganishe Andiko na Andiko”

“Acheni Tulinganishe Andiko na Andiko”

“Acheni Tulinganishe Andiko na Andiko”

MTU mmoja aliokota kijitabu fulani ndani ya gari-moshi lililokuwa likielekea New York City. Kijitabu hicho kilisema hivi, ‘Nafsi ya mwanadamu inaweza kufa.’ Mtu huyo, ambaye alikuwa mhubiri, alishangazwa na habari hiyo, naye akaanza kuisoma. Alishangaa kwa sababu hakuwahi kutilia shaka fundisho la kutokufa kwa nafsi. Wakati huo, hakujua ni nani aliyeandika kijitabu hicho. Lakini aliona kwamba hoja zilizotajwa zinaaminika na zinapatana na Maandiko, na kwamba zinapaswa kuchunguzwa kwa makini.

Mhubiri huyo ni George Storrs. Tukio lenyewe ni la mwaka wa 1837, mwaka ambao Charles Darwin aliandika kwa mara ya kwanza maoni ambayo baadaye yalitokeza nadharia ya mageuzi. Wakati huo, watu wengi bado walipenda mambo ya dini, na walimwamini Mungu. Wengi waliisoma Biblia na kuiheshimu.

Baadaye, Storrs aligundua kwamba kijitabu hicho kiliandikwa na Henry Grew wa Philadelphia, Pennsylvania. Grew alishikilia sana kanuni inayosema kwamba “andiko . . . ndilo hujifafanua vizuri zaidi.” Grew na washiriki wake walikuwa wamejifunza Biblia wakiwa na kusudi la kufuata mashauri yake katika maisha yao na shughuli zao. Katika uchunguzi wao, waligundua kweli za Biblia zenye kupendeza.

Storrs alichochewa na kijitabu hicho cha Grew, naye akachunguza kwa makini yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu nafsi na kuyazungumzia pamoja na wahubiri wenzake. Baada ya kufanya utafiti mwingi kwa miaka mitano, hatimaye Storrs aliamua kuchapisha kweli mpya za Biblia zenye thamani alizokuwa amepata. Kwanza, alitayarisha hotuba fulani kwa ajili ya Jumapili moja mwaka wa 1842. Hata hivyo, aliona anahitaji kutoa hotuba nyingine za ziada ili azungumzie habari hiyo kikamili. Kwa ujumla alitoa hotuba sita kuhusu kufa kwa nafsi ya mwanadamu, naye akazichapisha katika kichapo Six Sermons (Hotuba Sita). Storrs alilinganisha andiko na andiko ili kufunua kweli zenye kupendeza zilizofichwa na mafundisho yanayomvunjia Mungu heshima ya dini zinazodai kuwa za Kikristo.

Je, Biblia Inafundisha Kwamba Nafsi Haiwezi Kufa?

Biblia inasema kwamba wafuasi watiwa-mafuta wa Yesu huvaa hali ya kutoweza kufa, na hiyo ni thawabu wanayopata kwa sababu ya kuwa waaminifu. (1 Wakorintho 15:50-56) Storrs aliona kwamba ikiwa hali ya kutoweza kufa ni thawabu ambayo waaminifu wanapewa, basi si sawa kusema kwamba nafsi ya waovu haiwezi kufa. Badala ya kukisia-kisia, Storrs alichunguza Maandiko. Alichunguza andiko la Mathayo 10:28 (Zaire Swahili Bible) linalosema: “Mwogope yeye anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.” Kwa hiyo, nafsi inaweza kuharibiwa. Pia, alichunguza andiko la Ezekieli 18:4 linalosema: “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” Biblia yote ilipochunguzwa, kweli ilikuwa wazi zaidi. Storrs aliandika hivi: “Ikiwa maoni yangu kuhusu habari hii ni sahihi, basi Maandiko mengi, ambayo hayaeleweki kwa sababu ya fundisho hilo la kutokufa kwa nafsi, yatakuwa wazi, yatapendeza zaidi na kueleweka kabisa.”

Lakini namna gani maandiko kama vile Yuda 7? Andiko hilo linasema hivi: “Ndivyo pia Sodoma na Gomora na majiji yaliyoyazunguka, baada ya hayo kuwa yamefanya uasherati kwa kuzidi mno na kwenda kufuatilia mwili kwa ajili ya matumizi yasiyo ya asili, katika namna ileile kama hao waliotangulia kutajwa, yamewekwa mbele yetu kuwa kielelezo cha kuonya kwa kupatwa na adhabu ya hukumu ya moto wa milele.” Wengine wanaposoma andiko hilo, huenda wakafikiri kwamba nafsi za wale waliouawa huko Sodoma na Gomora zinateswa milele katika moto. Storrs aliandika hivi: “Acheni tulinganishe Andiko na Andiko.” Kisha akanukuu andiko la 2 Petro 2:5, 6, linalosema hivi: “Naye hakujizuia kuuadhibu ulimwengu wa kale, bali alimlinda Noa . . . , alipoleta gharika juu ya ulimwengu wa watu wasiomwogopa Mungu; na kwa kuyageuza majiji ya Sodoma na Gomora kuwa majivu aliyahukumia adhabu, akiweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.” Naam, majiji ya Sodoma na Gomora yaliteketezwa na kuwa majivu, hivyo yakaharibiwa milele pamoja na wakaaji wake.

Storrs alieleza hivi: “Petro anafafanua zaidi mambo yanayotajwa katika Yuda. Vitabu vyote viwili vinaonyesha adhabu ambazo Mungu ameleta juu ya waovu. . . . Hukumu hizo juu ya ulimwengu wa kale wa Sodoma na Gomora, ni shauri, onyo, au ‘kielelezo’ cha milele au cha kudumu kwa watu wote hadi mwisho wa ulimwengu.” Hivyo, Yuda alimaanisha kwamba moto ulioharibu Sodoma na Gomora ulikuwa na matokeo ya kudumu milele. Hilo halibadili wazo la kwamba nafsi ya mwanadamu inaweza kufa.

Storrs hakuwa akitumia tu maandiko yaliyounga mkono maoni yake huku akipuuza mengine. Alichunguza muktadha wa kila andiko na vilevile habari kuu ya Biblia. Ikiwa mstari fulani ungeonekana kuwa unapinga maandiko mengine, Storrs angechunguza sehemu nyingine za Biblia ili kupata ufafanuzi unaopatana na akili.

Uchunguzi wa Russell wa Maandiko

Mmoja wa wale waliopata kushirikiana na George Storrs ni kijana mmoja ambaye alikuwa akipanga kikundi cha kujifunza Biblia huko Pittsburgh, Pennsylvania. Kijana huyo aliitwa Charles Taze Russell. Mojawapo ya makala zake za kwanza kuhusu habari za Biblia ilichapishwa mwaka wa 1876 katika gazeti Bible Examiner, lililohaririwa na Storrs. Russell alikubali kwamba wanafunzi wa Biblia waliomtangulia walikuwa na uvutano juu ya maoni yake. Baadaye, akiwa mhariri wa gazeti Zion’s Watch Tower, alithamini jinsi Storrs alivyomsaidia sana kwa kuwasiliana naye moja kwa moja na kupitia barua.

C. T. Russell alipokuwa na umri wa miaka 18 alianzisha kikundi cha kujifunza Biblia na mpango maalumu wa kufanya hivyo. A. H. Macmillan, mwanafunzi wa Biblia aliyeshirikiana na Russell, aliufafanua mpango huo hivi: “Mtu fulani angeuliza swali. Kisha wangezungumzia swali hilo. Halafu wangechunguza maandiko yote yaliyohusiana na habari hiyo na, waliporidhika kwamba maandiko hayo yanapatana, wangekata kauli na kuiandika.”

Russell alisadiki kwamba Biblia yote inapochunguzwa inapaswa kufunua ujumbe ambao unapatana na Biblia yenyewe na utu wa Mungu, Mtungaji wake. Wakati sehemu yoyote ya Biblia ilipoonekana kuwa ngumu kueleweka, Russell aliamini kwamba inapaswa kufafanuliwa na kufasiriwa kwa kutumia sehemu nyingine za Biblia.

Desturi ya Kulinganisha Maandiko Ilianza Zamani

Hata hivyo, Russell, Storrs, na Grew hawakuwa watu wa kwanza kujaribu kuelewa Maandiko kwa kuyalinganisha. Desturi hiyo ilianzishwa na Mwanzilishi wa Ukristo, Yesu Kristo. Alitumia maandiko mbalimbali kuonyesha maana ya kweli ya andiko fulani. Kwa mfano, Mafarisayo walipowachambua wanafunzi wake kwa kukata masuke ya nafaka wakati wa Sabato, Yesu alitumia simulizi lililo katika 1 Samweli 21:6 kuonyesha jinsi sheria ya Sabato inavyopaswa kutumiwa. Viongozi hao wa kidini walijua simulizi hilo, ambapo Daudi na watu wake walikula mikate ya toleo. Kisha, Yesu alirejelea sehemu ya Sheria iliyosema kwamba makuhani wa familia ya Haruni tu ndio waliopaswa kula mkate huo wa wonyesho. (Kutoka 29:32, 33; Mambo ya Walawi 24:9) Hata hivyo, Daudi aliruhusiwa kula mikate hiyo. Yesu alimalizia hoja yake nzito kwa kunukuu kitabu cha Hosea: “Kama mngalielewa maana ya neno hili, ‘Ninataka rehema, wala si dhabihu,’ msingaliwalaumu watu wasio na hatia.” (Mathayo 12:1-8) Huo ni mfano bora kama nini wa kulinganisha andiko moja na maandiko mengine ili kulielewa kwa usahihi!

Wafuasi wa Yesu walifuata kielelezo chake cha kulinganisha maandiko ili kuelewa andiko fulani. Mtume Paulo alipokuwa akiwafundisha watu huko Thesalonike, ‘alijadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu.’ (Matendo 17:2, 3) Pia, katika barua zake zilizoandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, Paulo aliacha Biblia yenyewe ijifafanue. Kwa mfano, alipowaandikia Waebrania, alinukuu maandiko mengi ili kuthibitisha kwamba Sheria ilikuwa kivuli cha mambo mema yatakayokuja.—Waebrania 10:1-18.

Naam, wanafunzi wa Biblia wanyoofu katika karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20 walifuata tena kielelezo hicho cha Kikristo. Gazeti la Mnara wa Mlinzi lingali linafuata desturi hiyo ya kulinganisha andiko na andiko. (2 Wathesalonike 2:15) Mashahidi wa Yehova hutumia kanuni hiyo wanapochanganua andiko fulani.

Chunguza Muktadha

Tunaposoma Biblia, tunaweza kuigaje vielelezo vizuri vya Yesu na wafuasi wake waaminifu? Kwanza, tunaweza kuchunguza muktadha wa andiko tunalosoma. Muktadha unaweza kutusaidiaje kupata maana? Kwa mfano, acheni tuchunguze maneno ya Yesu katika Mathayo 16:28: “Kwa kweli ninawaambia ninyi kwamba kuna baadhi ya wale wanaosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe mpaka kwanza wamwone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” Wengine wanaweza kusema kwamba maneno hayo hayakutimia kwa sababu wanafunzi wote wa Yesu waliokuwepo wakati aliposema maneno hayo walikufa kabla ya Ufalme wa Mungu kusimamishwa mbinguni. Hata kitabu kimoja (The Interpreter’s Bible) kinasema hivi kuhusu mstari huo: “Unabii huo haukutimia, na Wakristo wa baadaye waliona ni muhimu waeleze kwamba ulikuwa mfano tu.”

Lakini, muktadha wa andiko hilo, na vilevile masimulizi ya Marko na Luka ambayo yanalingana na simulizi hilo, yanatusaidia kulielewa. Mathayo alisema nini baada tu ya kusema maneno yaliyonukuliwa juu? Aliandika hivi: “Siku sita baadaye Yesu aliwachukua Petro na Yakobo na Yohana ndugu yake akawapandisha katika mlima mrefu wakiwa peke yao. Sura yake ikageuka mbele yao.” (Mathayo 17:1, 2) Marko na Luka vilevile walihusianisha maneno ya Yesu kuhusu Ufalme na simulizi la kugeuka kwa sura yake. (Marko 9:1-8; Luka 9:27-36) Kuja kwa Yesu katika mamlaka ya Ufalme kuliwakilishwa na kugeuka kwa sura yake, yaani, wakati alipoonekana akiwa na utukufu mbele ya mitume wake watatu. Petro anathibitisha jambo hilo anapotaja “nguvu na kuwapo kwa Bwana wetu Yesu Kristo” wakati anapozungumzia jinsi alivyoshuhudia kugeuka kwa sura ya Yesu.—2 Petro 1:16-18.

Je, Wewe Huacha Biblia Ijifafanue?

Namna gani usipoelewa andiko fulani hata baada ya kuchunguza muktadha wake? Unaweza kufaidika kwa kulinganisha andiko hilo na maandiko mengine, huku ukikumbuka kichwa kikuu cha Biblia. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ambayo sasa inapatikana katika lugha 57 ikiwa nzima au katika sehemu, ni chombo bora ambacho kinaweza kukusaidia kufanya hivyo. Matoleo mengi ya tafsiri hiyo yana marejeo ya pambizoni ambayo yako katika safu ya katikati ya kila ukurasa. Kuna marejeo zaidi ya 125,000 katika tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References. “Utangulizi” wa Biblia hiyo unasema hivi: “Kuchunguza kwa makini marejeo ya pambizoni na maelezo ya chini kutaonyesha upatano mkubwa wa vile vitabu 66 vya Biblia, na kuthibitisha kwamba vyote ni kitabu kimoja, kilichoongozwa kwa roho ya Mungu.”

Acheni tuone jinsi kutumia marejeo ya pambizoni kunavyoweza kutusaidia kuelewa andiko fulani. Kwa mfano, acheni tuchunguze historia ya Abramu, au Abrahamu. Fikiria swali hili: Ni nani aliyeongoza mambo wakati Abramu na familia yake walipotoka Uru? Andiko la Mwanzo 11:31 linasema hivi: “Tera akamchukua mwana wake Abramu, na . . . Loti, . . . na binti-mkwe wake Sarai, . . . nao wakaondoka Uru la Wakaldayo pamoja naye ili kwenda katika nchi ya Kanaani. Baadaye wakaja Harani na kukaa huko.” Mtu anaposoma mstari huo, anaweza kukata kauli kwamba Tera, baba ya Abramu, ndiye aliyewaongoza. Hata hivyo, katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, kuna marejeo 11 ya pambizoni kuhusu mstari huo. Rejeo la mwisho linatuelekeza kwenye Matendo 7:2, ambapo tunasoma shauri ambalo Stefano aliwapa Wayahudi wa karne ya kwanza: “Mungu wa utukufu alimtokea babu yetu Abrahamu alipokuwa Mesopotamia, kabla ya kuanza kukaa Harani, naye akamwambia, ‘Toka katika nchi yako na kutoka kwa watu wa jamaa yako na uje mpaka katika nchi ambayo nitakuonyesha.’” (Matendo 7:2, 3) Je, Stefano alikuwa akiongea kuhusu wakati ambapo Abramu aliondoka Harani? Hapana, kwa sababu simulizi hilo ni sehemu ya Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho.—Mwanzo 12:1-3.

Basi, kwa nini andiko la Mwanzo 11:31 linasema kwamba ‘Tera alimchukua mwana wake Abramu’ na watu wengine wa familia yake na kuondoka Uru? Bado Tera ndiye aliyekuwa kichwa cha ukoo wake. Kwa kuwa alikubali kwenda pamoja na Abramu, yeye ndiye anayetajwa kuwa aliondoka pamoja na familia yake ili kwenda Harani. Tunapolinganisha na kupatanisha maandiko hayo mawili, tunaweza kuelewa mambo yaliyotukia. Kwa heshima, Abramu alimsadikisha baba yake waondoke Uru kulingana na amri ya Mungu.

Tunaposoma Maandiko, tunapaswa kufikiria muktadha na kichwa kikuu cha Biblia. Wakristo wanashauriwa hivi: “Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili. Mambo hayo tunayasema pia, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya binadamu, bali kwa yale yanayofundishwa kwa roho, tunapounganisha mambo ya kiroho pamoja na maneno ya kiroho.” (1 Wakorintho 2:11-13) Naam, tunapaswa kumwomba Yehova atusaidie kuelewa Neno lake na kujaribu ‘kuunganisha mambo ya kiroho pamoja na maneno ya kiroho.’ Tutafanya hivyo kwa kuchunguza muktadha wa andiko tunalochanganua na vilevile Maandiko mengine yanayohusiana nalo. Acheni tuendelee kupata hazina bora za kweli kwa kujifunza Neno la Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wanafunzi wa Biblia wa karne ya 19 ambao walilinganisha Andiko na andiko: George Storrs, Henry Grew, Charles Taze Russell, A. H. Macmillan

[Hisani]

Top: SIX SERMONS, by George Storrs (1855); second from top: Collection of The New-York Historical Society/69288

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mtume Paulo alithibitisha hoja yake kwa kurejelea maandiko