Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hii Habari Njema ya Ufalme Itahubiriwa”

“Hii Habari Njema ya Ufalme Itahubiriwa”

“Hii Habari Njema ya Ufalme Itahubiriwa”

“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—MATHAYO 24:14.

Inamaanisha Nini? Luka, mwandikaji wa Injili, aliripoti kwamba Yesu ‘alisafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 8:1) Yesu mwenyewe alisema: ‘Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.’ (Luka 4:43) Aliwatuma wanafunzi wake wahubiri habari njema katika miji na vijiji na baadaye akawaamuru hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Matendo 1:8; Luka 10:1.

Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Wanafunzi wa Yesu hawakusita kufanya kazi ambayo Yesu aliwapatia. “Kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo.” (Matendo 5:42) Kazi ya kuhubiri haikufanywa tu na kikundi kidogo cha watu walioheshimiwa. Mwanahistoria Neander alisema kwamba “Celsus, mwandishi wa kwanza aliyepinga Ukristo aliwadhihaki wanafunzi wa Yesu kwa kudai kuwa wafumaji wa sufu, washona-viatu, watengeneza-ngozi, watu wa kawaida wasio na elimu yoyote, walikuwa wahubiri wa injili wenye bidii.” Katika kitabu chake kinachoitwa The Early Centuries of the Church, Jean Bernardi aliandika: “[Wakristo] walipaswa kwenda kila mahali na kuzungumza na kila mtu. Kwenye barabara kuu na katika majiji, kwenye maeneo ya umma na nyumbani. Wakiwa wamekaribishwa au la. . . . Hadi miisho ya dunia.”

Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Kasisi Mwanglikana David Watson aliandika hivi: “Watu wengi leo hawako tayari kumtumikia Mungu kwa sababu kanisa limekataa kuchukua kwa uzito kazi ya kuhubiri.” Katika kitabu chake Why Are the Catholics Leaving? José Luis Pérez Guadalupe, aliandika kuhusu utendaji wa Wainjilisti, Waadventisti, na wengineo na kusema kwamba “hawahubiri nyumba kwa nyumba.” Aliandika hivi kuhusu Mashahidi wa Yehova: “Wanahubiri nyumba kwa nyumba kwa utaratibu.”

Maoni ya kweli na yenye kupendeza yaliyotolewa na Jonathan Turley yanapatikana katika kitabu Cato Supreme Court Review, 2001-2002: “Unapotaja Mashahidi wa Yehova, mara moja watu wengi wanafikiri kuhusu wahubiri wanaotutembelea nyumbani wakati usiofaa. Kwa Mashahidi wa Yehova, kuhubiri nyumba kwa nyumba si njia pekee ya kueneza imani yao bali ni sehemu muhimu ya imani yao.”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Je, Umewatambua Wakristo wa Kweli?

Kwa kutegemea ufafanuzi wa Maandiko yaliyozungumziwa katika mfululizo huu wa makala, unafikiri ni nani ambao leo wanaonyesha sifa zinazowatambulisha Wakristo wa kweli? Ingawa kuna makumi ya maelfu ya vikundi na dini zinazodai kuwa za Kikristo, kumbuka maneno ambayo Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.” (Mathayo 7:21) Kuwatambua wale wanaofanya mapenzi ya Baba—jambo linalothibitisha kwamba wao ni Wakristo wa kweli—na kushirikiana nao kunaweza kumsaidia mtu apate baraka za milele chini ya Ufalme wa Mungu. Tunakutia moyo uwaombe Mashahidi wa Yehova, yaani, watu waliokupa gazeti hili, wakufundishe mengi zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na baraka ambazo utaleta.—Luka 4:43.